Uchaguzi wa Kenya 2022: Wanaotarajiwa kuwa Mama taifa wa Kenya

    • Author, Ambia Hirsi
    • Nafasi, BBC Swahili

Kenya inapoelekea kwa uchaguzi mkuu macho yanaelekezwa kwa wanawake walio katika maisha ya wagombea wanne wa urais.

Je ni nani kati ya wanawake hawa wanne atachukua mkoba kutoka kwa Margaret Kenyatta kama Mama Taifa wa Kenya?

Tunawaangazia kwa ufupi ili uwajue kwani mmoja wao ndiye atakayekuwa mama wa taifa wa nchi endapo mume wake atachaguliwa kuwa rais wa Kenya .

Ida Odinga

ida Odinga

Chanzo cha picha, Ida Odinga Twitter

Ni mke wa mwanasiasa mkongwe na kiongozi wa upinzani Raila Odinga.

Ida Anyango Oyoo, alizaliwa tarehe 27 Agosti, 1950, katika kaunti ya Migori Magharibi mwa Kenya.

Ida alikutana kwa mara ya kwanza na mume wake Raila Amollo Odinga alipokuwa akisoma katika Chuo Kikuu cha Nairobi.

Aliolewa na Bw Odinga tarehe 1 Septemba 1973 na katika ndoa yao walijaaliwa watoto wanne, Fidel Odinga, Winnie Odinga, Raila Odinga Jr na Rosemary Odinga.

Japo kitaaluma Mama Odinga ni mfanyabiashara, mwanaharakati na mwalimu, lakini umaarufu wake zaidi umetokana na jinsi anavyosimama kidete katika harakati za kumuunga mkono bwana Raila Amollo Odinga katika siasa na azma yake ya kuongoza taifa la Kenya.

Kwa miaka mingi, amekuwa akijihusisha katika miradi tofauti ikiwa ni pamoja na kampeni dhidi ya uelewa kuhusu saratani ya matiti na fistula.

Pia amekuwa mshauri wa wanafunzi kadhaa wa kike na pia mdhamini mkubwa katika kujenga maktaba ya kisasa katika shule yake ya zamani ya sekondari.

Mwaka 2021, alipewa tuzo ya kutambua uungaji mkono wake mkubwa katika masuala ya afya, elimu, wanawake, amani, pamoja na uwezeshwaji wa watoto wavulana na wasichana.

Rachel Ruto

Rachel Ruto

Chanzo cha picha, RACHEL/TWITTER

Rachel Chebet Ruto ni mke wa Naibu wa Rais wa Kenya William Ruto.

Alizaliwa tarehe 20 mwezi Novemba 1968 mjini Kakamega magharibi mwa Kenya na kupata masomo yake ya sekondari katika shule ya wasichana ya Butere hadi kidato cha sita.

Baadaye alijiunga na Chuo Kikuu cha Kenyatta na kusomea shahada ya Elimu.

Bi Rachel na William Ruto walikutana mwanzoni mwa miaka ya tisini na wawili hao walianza kuchumbiana wakiwa chuo kikuu.

Alifunga pingu za maisha na mume wake William Ruto na kuanza familia yao mwaka wa 1991.

Rachel alijaaliwa watoto sita-mabinti watatu na wavulana watatu mkubwa wao akiwa Nick Ruto.

Amekuwa mstari wa mbele kupigania haki za wanawake na harakati za kuwawezesha katika jamii.

Nani yuko kwenye kinyang'anyiro cha kuiongoza Kenya ?

Fahamu zaidi kuwahusu wagombea urais wa Kenya

Chagua mgombea ili kutazama wasifu wake

Raila Amollo Odinga

Muungano wa Azimio la Umoja

  • Mgombea huyo mwenye umri wa miaka 77 ni mhandisi aliyesomea Chuo Kikuu cha Ufundi cha Magdeburg (sasa kinajulikana kama Chuo Kikuu cha Otto-von-Guericke Magdeburg) nchini Ujerumani.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya Azimio la Umoja One Kenya Coalition Party.
  • Hili litakuwa jaribio lake la tano baada ya kugombea katika: 1997, 2007, 2013 na 2017.
  • Bw Odinga alikuwa mmoja wa wapiganiaji wa demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya. Alikamatwa, akafungwa na wakati fulani akaenda uhamishoni kwa sababu ya kupigania haki hiyo
  • Aliwahi kuwa Waziri Mkuu, kuanzia 2008-2013.
  • Odinga alihusika kufanikisha miradi mikubwa iliyotekelezwa na serikali ya Kibaki, kama vile miradi ya umeme vijijini na barabara.
  • Kuafikia ukuaji wa uchumi wa tarakimu mbili kupitia uwekezaji katika biashara ndogo ndogo na sekta ya viwanda.
  • Utoaji wa huduma bora za afya kwa wote.
  • Utoaji wa vifaa vya michezo na burudani kwa ukuaji wa kimwili, kiakili, kijamii, kimaadili na maendeleo ya watu.
  • Kufuatia jaribio la mapinduzi ya Agosti 1, 1982, Raila Odinga alikamatwa na kukabiliwa na mashtaka kadhaa, yakiwemo ya uhaini ambayo alizuiliwa bila kufunguliwa mashtaka. Tume ya Ukweli ya Haki na Maridhiano iliambiwa mwaka 2011 kwamba Odinga alikuwa na mawasiliano na mpangaji mkuu wa mapinduzi hayo. Odinga amekana kuhusika kila mara. - Makavazi ya Kitaifa ya Kenya.

William Samoei Ruto

Muungano wa Kenya Kwanza

  • Mgombea huyu mwenye umri wa miaka 55 ana Shahada ya Uzamifu/PhD katika Ikolojia ya Mimea na BSc katika Botany na Zoology kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya chama cha United Democratic Alliance ( chenye mafungamano na Kenya Kwanza).
  • Aliongoza Vuguvugu la vijana la Youth for Kanu '92 (YK'(92).
  • Wizara yake iliorodheshwa kama inayofanya bora zaidi serikalini alipokuwa Waziri wa Kilimo.
  • Alihudumu kama Naibu Rais wa kwanza wa Kenya chini ya katiba mpya ya 2010.
  • Alihudumu kama mbunge wa eneo bunge la Eldoret Kaskazini kuanzia 1997-2007.
  • Kutenga $424 milioni kila mwaka kwa biashara ndogo ndogo za kati.
  • Kuanzisha mfuko wa elimu wa kitaifa ili kukidhi gharama zisizo za masomo.
  • Tekeleza kikamilifu sheria ya usawa wa kijinsia ya thuluthi mbili katika uteuzi wa kisiasa na kutenga nusu ya baraza lake la mawaziri kwa wanawake.
  • Mnamo 2008, Mahakama Kuu ya Kenya iliamuru Naibu Rais William Ruto kusalimisha shamba la ekari 100 na kulipa $ 62,500 kwa Adrian Muteshi, mkulima ambaye alimshtaki kwa kuchukua mali hiyo baada ya uchaguzi wa 2007. - Kenya Law
  • Mnamo 2011, Bw Ruto alikabiliwa na kesi kwa makosa matatu dhidi ya binadamu: Mauaji, uhamisho wa watu kwa lazima na mateso ya watu katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu. Miaka mitano baadaye mahakama ilisitisha kesi hiyo kwa msingi kwamba - ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa dhaifu. -ICC

George Wajackoyah

Chama cha Roots

  • Profesa huyo mwenye umri wa miaka 61 ana shahada ya uzamili katika sheria kuhusu maendeleo kutoka Chuo Kikuu cha Warwick na shahada ya uzamili , sheria (sheria za Marekani kutoka Chuo Kikuu cha Baltimore.
  • Bw Wajackoyah anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Roots Party.
  • Alihudumu kama Inspekta katika idara ya usalama ya Special branch wakati wa utawala wa marehemu Rais Daniel Moi kabla ya kulazimika kutorokea ng'ambo ili kuepuka kufunguliwa mashtaka na mamlaka.
  • Yeye ni mshirika katika kampuni ya mawakili aliyoianzisha mwaka wa 2018.
  • Alifunnza somo la sheria na uchumi katika vyuo vikuu vya Marekani, Uingereza na Kenya.
  • Kuhalalisha matumizi ya kiviwanda ya bangi
  • Badilisha siku za kazi hadi Jumatatu hadi Alhamisi.
  • Huduma ya afya ya bure na msaada kwa wazee, walio hatarini na wajawazito

David Mwaure Waihiga

Chama cha Agano

  • David Mwaure anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Agano.
  • Ni kiongozi wa Chama cha Agano.
  • Alihitimu na shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi na ana Shahada ya Uzamili katika masomo ya uongozi.
  • Yeye ni wakili mkuu na amehudumu kama mwanasheria kwa zaidi ya miongo mitatu.
  • Ana kampuni ya uwakili na amewania viti mbalimbali vya kisiasa.
  • Ilianzishwa chama cha Agano mwaka 2006.
  • Kupambana na ufisadi uliokithiri.
  • kuunda nafasi za ajira.
  • Kurejesha mali ya Kenya iliyofichwa nje ya nchi.

Pata maelezo zaidi kuhusu sera za wagombea urais hapa

Anna Ngibuini Mwaure

Anna Ngibuini Mwaure

Chanzo cha picha, Anne Mwaure/FB

Anna Ngibuini Mwaure ni mke wa mgombea wa Urais wa chama cha Agano David Mwaura Waihiga.

Mengi hayajulikani kumhusu kwa sababu ameishi maisha yake kimya kimya, na ni nadra sana kumpata kwenye mijadala ya umma.

Mnamo Juni 2021, alikula kiapo kama jaji wa Mahakama ya Ajira na Mahusiano ya Kazi.

Uteuzi wake ulijiri wakati ambapo Rais Uhuru Kenyatta alichapisha kwenye gazeti rasmi la serikali majaji 34 na kuondoa sita waliopendekezwa na Tume ya Huduma za Mahakama.

Kabla ya uteuzi wake kama jaji alifanya kazi kama mpatanishi.

Katika taarifa zilizopita zilizochapishwa katika vyombo vya habari nchini humo, Anne amekuwa mtetezi mkali wa kutumia mbinu ya upatanishi wa mizozo baina ya wahusika bila kuwaingiza wahusika zaidi. Alibainisha kuwa njia hii ni nzuri na ya gharama nafuu kinyume na kesi za madai.

Meller Lee Chatham

th

Chanzo cha picha, Meller Lee Cheatham/Facebook

Bi Chatham ni mke wa mgombea urais George Wajackoyah.

Mengi hayajulikani kumhusu lakini taarifa zilizoangaziwa mtandaoni nchini Kenya zinaonyesha kwamba aliwahi kufanya kazi katika tasnia ya usafiri wa anga.

Alionekana hadharani maajuzi akiwa na mume wake wakati wa mdahalo wa wagombea wa urais ambao Wajackoyah hakushiriki licha ya kufika katika eneo la mdahalo huo na kisha kuondoka .

Katika mahojiano yaliyopita na vyombo vya habari nchini Kenya mume wake Bw Wajackoyah alisema mke wake anaishi Marekani na watoto wao watatu - mabinti wao wawili na mwana wao wa kiume.

Uchaguzi wa Kenya 2022: Vyama vinakuahidi nini?

Chagua suala ambalo linakuvutia

Sera za kila chama

  • Azimio La Umoja One Kenya Coalition

  • Roots Party of Kenya

  • Chama cha Agano

  • Kenya Kwanza Alliance

Mwongozo huu ni muhtasari wa sera kuu zinazotolewa na kila chama.

Pata maelezo zaidi kuhusu wagombea urais wa Kenya hapa

End of Uchaguzi wa Kenya 2022: Vyama vinakuahidi nini?
th

Pia unaweza pia kusoma

th