Uchaguzi wa Kenya 2022: Je hatua ya Rais Kenyatta kumuunga mkono Raila Odinga itamsaidia au kumharibia?

Uhuru Kenyatta na Raila Odinga

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Uhuru Kenyatta na Raila Odinga
    • Author, Joseph Kioko
    • Nafasi, Mchambuzi Kenya

Msemo 'kikombe chenye sumu' hutumika mara kwa mara katika Siasa kuelezea kazi au usaidizi anaopewa mtu, ambapo mwanzoni, mtu huyo hufikiri kuwa ameheshimiwa lakini baadaye akagundua msaada huo aliopewa ni, mzigo, ambao huenda ukaharibu sifa yake au matarajio yake.

Msemo huo unajiri siku chache tu baada ya rais Uhuru Kenyatta kumuunga mkono rasmi kiongozi wa ODM Raila Odinga , hatua inayotarajiwa kuzua hisia tofauti miongoni mwa Wakenya wapipga kura katika mkutano uliofanyika katika Ikulu ya Sagana mjini Nyeri.

Katika hatua ya rais Uhuru Kenyatta kumuunga mkono aliyekuwa waziri mkuu Raila Odinga, ni rahisi mtu kushawishika kwamba ni hatua itakayomuwezesha kiongozi huyo kuafikia azma yake ya kuwania urais na upande mwengine kuna wale ambao huenda wakafikiria kwamba hatua hiyo huenda ikamharibia.

Ujio wa 'Handshake'

Uamuzi wa mahakama ya juu zaidi ya Kenya kubatilisha matokeo ya uchaguzi wa Rais wa 2017 na kuamuru uchaguzi mpya ufanyike, ambao ulisusiwa na muungano wa upinzani wa NASA, ulizua mazingira ya mgawanyiko ndani ya nchi.

Kulikuwa na hisia kwamba kura halisi zilizopigwa hazikuhesabiwa na badala yake kulikuwa na watu binafsi au "mifumo" ilioamua mshindi hali ambayo ingewatenga watu wa jamii fulani na viongozi mgao wa rasilimali za nchi.

Ni nia ya kushughulikia mapungufu haya miongoni mwa mengine, kwamba Rais Uhuru na Waziri Mkuu Raila Odinga walifanya Handshake Machi 2018, ambayo iliashiria mwanzo wa ushirikiano wa kisiasa kati ya wahusika wawili wakuu wa kisiasa.

Katika jitihada za kutatua changamoto za kihistoria zilizokuwa zikiikabili nchi, wakuu hao wawili waliunda kamati ya watu mashuhuri iliyozunguka nchi nzima kukusanya na kukusanya maoni kutoka kwa wananchi, maoni hayo yalifupishwa na kuwa waraka wa kisiasa unaoitwa Ripoti ya Ujenzi wa Madaraja BBI ambayo ilibadilika na kuwa Mswada wa marekebisho ya katiba "mpango maarufu" ambao ulipaswa kuwasilishwa kwa umma kupitia kura ya maoni.

Mpango huu maarufu wa BBI hatahivyo ulitangazwa kuwa "batili na Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa na kwa sasa unasubiri uamuzi wa Mahakama ya Juu zaidi ya Kenya.

Kando na mpango wa BBI, mshikamano wa kisiasa kati ya viongozi hao wawili umesababisha ishara nyingi kwamba Waziri Mkuu Raila Odinga ndiye mgombea urais anayependekezwa zaidi ra Rais Uhuru.

Kenyatta kumuunga mkono Odinga

Rais amejitokeza waziwazi kuonyesha mshikamano na kuunga mkono muungano wa Azimio ambao ni gari la muungano ambalo Raila Odinga atatumia kuwania urais katika uchaguzi Mkuu ujao wa Agosti, rais pia amekuwa mwenyeji wa ujumbe katika ikulu ya Nairobi kuwa mgombeaji wa muungano wa Azimio (Raila Odinga) ndiye anayempendelea zaidi.

Nani yuko kwenye kinyang'anyiro cha kuiongoza Kenya ?

Fahamu zaidi kuwahusu wagombea urais wa Kenya

Chagua mgombea ili kutazama wasifu wake

Raila Amollo Odinga

Muungano wa Azimio la Umoja

  • Mgombea huyo mwenye umri wa miaka 77 ni mhandisi aliyesomea Chuo Kikuu cha Ufundi cha Magdeburg (sasa kinajulikana kama Chuo Kikuu cha Otto-von-Guericke Magdeburg) nchini Ujerumani.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya Azimio la Umoja One Kenya Coalition Party.
  • Hili litakuwa jaribio lake la tano baada ya kugombea katika: 1997, 2007, 2013 na 2017.
  • Bw Odinga alikuwa mmoja wa wapiganiaji wa demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya. Alikamatwa, akafungwa na wakati fulani akaenda uhamishoni kwa sababu ya kupigania haki hiyo
  • Aliwahi kuwa Waziri Mkuu, kuanzia 2008-2013.
  • Odinga alihusika kufanikisha miradi mikubwa iliyotekelezwa na serikali ya Kibaki, kama vile miradi ya umeme vijijini na barabara.
  • Kuafikia ukuaji wa uchumi wa tarakimu mbili kupitia uwekezaji katika biashara ndogo ndogo na sekta ya viwanda.
  • Utoaji wa huduma bora za afya kwa wote.
  • Utoaji wa vifaa vya michezo na burudani kwa ukuaji wa kimwili, kiakili, kijamii, kimaadili na maendeleo ya watu.
  • Kufuatia jaribio la mapinduzi ya Agosti 1, 1982, Raila Odinga alikamatwa na kukabiliwa na mashtaka kadhaa, yakiwemo ya uhaini ambayo alizuiliwa bila kufunguliwa mashtaka. Tume ya Ukweli ya Haki na Maridhiano iliambiwa mwaka 2011 kwamba Odinga alikuwa na mawasiliano na mpangaji mkuu wa mapinduzi hayo. Odinga amekana kuhusika kila mara. - Makavazi ya Kitaifa ya Kenya.

William Samoei Ruto

Muungano wa Kenya Kwanza

  • Mgombea huyu mwenye umri wa miaka 55 ana Shahada ya Uzamifu/PhD katika Ikolojia ya Mimea na BSc katika Botany na Zoology kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya chama cha United Democratic Alliance ( chenye mafungamano na Kenya Kwanza).
  • Aliongoza Vuguvugu la vijana la Youth for Kanu '92 (YK'(92).
  • Wizara yake iliorodheshwa kama inayofanya bora zaidi serikalini alipokuwa Waziri wa Kilimo.
  • Alihudumu kama Naibu Rais wa kwanza wa Kenya chini ya katiba mpya ya 2010.
  • Alihudumu kama mbunge wa eneo bunge la Eldoret Kaskazini kuanzia 1997-2007.
  • Kutenga $424 milioni kila mwaka kwa biashara ndogo ndogo za kati.
  • Kuanzisha mfuko wa elimu wa kitaifa ili kukidhi gharama zisizo za masomo.
  • Tekeleza kikamilifu sheria ya usawa wa kijinsia ya thuluthi mbili katika uteuzi wa kisiasa na kutenga nusu ya baraza lake la mawaziri kwa wanawake.
  • Mnamo 2008, Mahakama Kuu ya Kenya iliamuru Naibu Rais William Ruto kusalimisha shamba la ekari 100 na kulipa $ 62,500 kwa Adrian Muteshi, mkulima ambaye alimshtaki kwa kuchukua mali hiyo baada ya uchaguzi wa 2007. - Kenya Law
  • Mnamo 2011, Bw Ruto alikabiliwa na kesi kwa makosa matatu dhidi ya binadamu: Mauaji, uhamisho wa watu kwa lazima na mateso ya watu katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu. Miaka mitano baadaye mahakama ilisitisha kesi hiyo kwa msingi kwamba - ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa dhaifu. -ICC

George Wajackoyah

Chama cha Roots

  • Profesa huyo mwenye umri wa miaka 61 ana shahada ya uzamili katika sheria kuhusu maendeleo kutoka Chuo Kikuu cha Warwick na shahada ya uzamili , sheria (sheria za Marekani kutoka Chuo Kikuu cha Baltimore.
  • Bw Wajackoyah anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Roots Party.
  • Alihudumu kama Inspekta katika idara ya usalama ya Special branch wakati wa utawala wa marehemu Rais Daniel Moi kabla ya kulazimika kutorokea ng'ambo ili kuepuka kufunguliwa mashtaka na mamlaka.
  • Yeye ni mshirika katika kampuni ya mawakili aliyoianzisha mwaka wa 2018.
  • Alifunnza somo la sheria na uchumi katika vyuo vikuu vya Marekani, Uingereza na Kenya.
  • Kuhalalisha matumizi ya kiviwanda ya bangi
  • Badilisha siku za kazi hadi Jumatatu hadi Alhamisi.
  • Huduma ya afya ya bure na msaada kwa wazee, walio hatarini na wajawazito

David Mwaure Waihiga

Chama cha Agano

  • David Mwaure anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Agano.
  • Ni kiongozi wa Chama cha Agano.
  • Alihitimu na shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi na ana Shahada ya Uzamili katika masomo ya uongozi.
  • Yeye ni wakili mkuu na amehudumu kama mwanasheria kwa zaidi ya miongo mitatu.
  • Ana kampuni ya uwakili na amewania viti mbalimbali vya kisiasa.
  • Ilianzishwa chama cha Agano mwaka 2006.
  • Kupambana na ufisadi uliokithiri.
  • kuunda nafasi za ajira.
  • Kurejesha mali ya Kenya iliyofichwa nje ya nchi.

Pata maelezo zaidi kuhusu sera za wagombea urais hapa

Naibu wa rais William Ruto, rais Uhuru kenyatta na kionozi wa upinzani Raila Odinga
Maelezo ya picha, Naibu wa rais William Ruto, rais Uhuru kenyatta na kionozi wa upinzani Raila Odinga

Kando na kuwa mwenyeji wa wajumbe na pia kutumia rasilimali za serikali kushinikiza uongozi wa Raila Odinga, Rais pia amewasiliana na wanasiasa wengine wakuu na Magavana katika juhudi za kuwavutia kujiunga na muungano wa Azimio na kumuunga mkono Raila Odinga.

Muungano wao na hatua ya kumuunga mkono Raila Odinga inahitaji pia kuonekana katika mtazamo wa kihistoria, ambapo baba za mabwana hawa wawili walikuwa Rais na Makamu wa rais mtawalia. Wakakti taifa hili lilipojipatia uhuru.

Baadaye walitofautiana kimawazo na mzozo mkubwa wa kisiasa ukatokea ambao sio tu ulikumba familia hizo mbili bali pia ulipanda mbegu za kutoaminiana miongoni mwa makabila yao.

Huku watu wa kabila la mkoa wa kati nchini Kenya wakifurahia uongozi wa nchi kupitia Rais Jomo Kenyatta, Rais Mwai Kibaki na kwa sasa Rais Uhuru Kenyatta, Jamii ya watu wa eneo la uliokuwa mkoa wa Nyanza hawajabahatika katika masuala ya uongozi wa nchi. ni mitazamo hii ya kutaka kurekebisha "ukosefu" huu wa usawa wa kihistoria ambao unaonekana kumsukuma Rais Uhuru Kenyatta kutaka kuunga mkono uonozi wa Raila Odinga.

Na ili kuleta usawa huo wa uongozi , Rais Uhuru Kenyatta amekuwa akitofautiana na naibu wake William Ruto kuhusu uongozi wa taifa la Kenya kuzunguka kati ya watu wamakabila mawili , lile la watu wa uliokuwa mkoa wa kati na ule wa mkoa wa Bonde La Ufa, hali ambayo anadai huenda imesababisha usawa wa kushirikishwa kwa jamii nyingine katika uongozi wa taifa hilo - na ndio sababu ameamua kumuunga mkono Raila Odinga.

'Miradi ya kisiasa'

Ni muhimu kuelewa kwamba uchaguzi Mkuu ujao wa Agosti 9 nchini Kenya utakuwa uchaguzi wa 3 tangu kuanzishwa kwa siasa za vyama vingi na kupitishwa kwa ukomo wa mihula miwili kwa wahudumu wa kiti cha urais. Uchaguzi Mkuu wa 2002 uliwakilisha mwisho wa ukomo wa mihula miwili ya Rais Moi na katika jaribio la kusimamia mrithi wake KANU ilishindwa.

Rais Uhuru Kenyatta na ndugu yake Raila Odinga

Chanzo cha picha, AFP

Maelezo ya picha, Rais Uhuru Kenyatta na ndugu yake Raila Odinga

Wakati wa uchaguzi huo, Rais Moi alimpendekeza mwanasiasa kijana Uhuru Kenyatta kuwa mrithi wake mbele ya wanasiasa wengine wakuu wa KANU, ambao wakiongozwa na Raila Odinga waliasi na kujiunga na Mwai Kibaki katika muungano wa upinzani wa National Rainbow Coalition (NARC).

Uhuru Kenyatta wa KANU alishindwa na Rais Mwai Kibaki wa NARC, licha ya kuhusika sana katika kampeni na serikali ya wakati huo ya KANU kumuunga mkono. Uchaguzi Mkuu wa 2013 uliwakilisha mpito wa 2 ambapo rais aliye madarakani alizuiwa na sheria kugombea wadhifa huo.

Kwa upande wake Rais Mwai Kibaki hakuonyesha kwa njia yoyote upendeleo kwa wagombeaji wowote waliokuwa na nia ya kuwania Urais.

Kwa vyovyote vile wagombea wakuu wote katika uchaguzi walikuwa wajumbe wa baraza lake la mawaziri wakihudumu nyadhifa tofauti wakati huo. Katika uchaguzi wa 2013, muungano wa Uhuru Kenyatta na William Ruto (TNA/URP) ulishinda muungano wa Waziri Mkuu wa wakati huo Raila Odinga na Makamu wa Rais Kalonzo Musyoka (CORD), hali ambayo ilirudiwa tena 2017.

Kwa hivyo uchaguzi huu ujao utashuhudia uhamishaji wa 3 wa mamlaka kwa mujibu wa katiba ya Kenya. Jinsi marais hao wa zamani walivyofanya na kusimamia mabadiliko yao itakuwa muhimu katika kutathmini iwapo kweli uungwaji mkono wa Rais Uhuru kwa Waziri Mkuu Raila Odinga ni kikombe chenye sumu au ubabe wa kisiasa.

Ni historia pekee ndiyo itakayotuhukumu.