Uchaguzi wa Kenya 2022: Kwanini kura za Wakikuyu zinapiganiwa katika uchaguzi?

Composite photo of Martha Karua and Rigathi Gachagua

Chanzo cha picha, AFP

Maelezo ya picha, Wagombea wa naibu rais, Martha Karua (Kushoto) na Rigathi Gachagua (Kulia), wanatokea jamii ya Wakikuyu
    • Author, Na Evelyne Musambi
    • Nafasi, BBC News

Wagombea wawili wakuu katika uchaguzi wa urais nchini Kenya wamechagua wagombea wenza kutoka kabila la Wakikuyu ambalo lina kura nyingi ili kuongeza nafasi yao ya kushinda katika uchaguzi wa mwezi Agosti unaosubiriwa kwa hamu.

Naibu wa Rais William Ruto amemteua mfanyabiashara na mbunge Rigathi Gachagua huku Waziri Mkuu wa zamani Raila Odinga akimteua Waziri wa zamani wa Sheria Martha Karua.

"Wawili hao wanatoka ulimwengu mbili tufauti, ijapokuwa wanatoka eneo la mlima Kenya," mchambuzi Javas Bigambo aliambia BBC.

Eneo la Mlima Kenya ni nyumbani kwa jamii ya Wakikuyu, ambayo inaweza kuwa muhimu katika kuamua matokeo ya uchaguzi.

Bw. Gachagua ni mhamasishaji hodari na ana ushawishi mkubwa miongoni mwa Wakikuyu wanaohangaika, ambao wamekuwa wakimuunga mkono Bw Ruto kuhusu mipango yake ya kushughulikia malalamishi ya kiuchumi.

Bi Karua ni gwiji wa kisiasa anayetambuliwa nje ya jamii ya Wakikuyu - na anajulikana kwa shauku yake ya mageuzi ya mahakama na kampeni dhidi ya ufisadi.

Wachambuzi wanasema kwamba wakati wasomi wanaweza kumuunga mkono mwanaharakati wa kupinga ufisadi, uchaguzi huu zaidi unahusu mageuzi ya kiuchumi.

"Pande zote mbili zimegubikwa na tuhuma za ufisadi na ndiyo maana hakuna anayenyooshewa vidole. Ufisadi si suala la msingi tena. Inaonekana kuwa mtindo wetu wa maisha na imekuwa vigumu kuonyesha kiongozi shupavu ambaye hajachafuliwa na ufisadi," mchambuzi Bobby Mkangi aliambia BBC.

Bw. Gachagua anakabiliwa na mashtaka ya ufisadi na utakatishaji fedha za thamani ya dola milioni 65 (£53m). Amepinga mashataka, na kusema kuwa anateswa na serikali kwa kumuunga mkono Naibu wa Rais William Ruto.

Naibu Rais wa Kenya, William Ruto (Kulia) ameketi karibu na mgombea mwenza wake Rigathi Gachagua, katika makao rasmi ya Naibu Karen, Nairobi, Mei 15, 2022.

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Mfanyabiashara Rigathi Gachagua (Kulia) anawania kwa tiketi ya William Ruto (Kulia)

Rais anayeondoka madarakani Uhuru Kenyatta anamuunga mkono Bw. Odinga, ambaye alisalimiana naye 2018 katika kile kilichofahamika kama ''Hand Shake'' kuashiria maridhiano kati yao baada ya uhasama wa kisiasa wa miaka kadhaa.

Wachambuzi wanasema kuanzia wakati huo, Bw. Odinga, kiongozi mkongwe wa upinzani ambaye amejaribu mara nne kugombea urais wa Kenya na kushindwa, kwa kiasi kikubwa amepuuza uozo wote serikalini.

Uamuzi wake wakumteua Bi Karua kama mgombea mwenza pia ni jaribio la kuvutia kura ya wanawake, lakini Bw. Bigambo hana uhakika atapata ufanisi kiasi gani.

"Anawavutia wananawake kielimu sio kivitendo. Anavutia sehemu ya tabaka la kati na jumuiya ya mashirika yasiyo ya kiserikali ambayo hayana mchango mkubwa katika matokeo ya uchaguzi," Bw Bigambo anasema.

Nani yuko kwenye kinyang'anyiro cha kuiongoza Kenya ?

Fahamu zaidi kuwahusu wagombea urais wa Kenya

Chagua mgombea ili kutazama wasifu wake

Raila Amollo Odinga

Muungano wa Azimio la Umoja

  • Mgombea huyo mwenye umri wa miaka 77 ni mhandisi aliyesomea Chuo Kikuu cha Ufundi cha Magdeburg (sasa kinajulikana kama Chuo Kikuu cha Otto-von-Guericke Magdeburg) nchini Ujerumani.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya Azimio la Umoja One Kenya Coalition Party.
  • Hili litakuwa jaribio lake la tano baada ya kugombea katika: 1997, 2007, 2013 na 2017.
  • Bw Odinga alikuwa mmoja wa wapiganiaji wa demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya. Alikamatwa, akafungwa na wakati fulani akaenda uhamishoni kwa sababu ya kupigania haki hiyo
  • Aliwahi kuwa Waziri Mkuu, kuanzia 2008-2013.
  • Odinga alihusika kufanikisha miradi mikubwa iliyotekelezwa na serikali ya Kibaki, kama vile miradi ya umeme vijijini na barabara.
  • Kuafikia ukuaji wa uchumi wa tarakimu mbili kupitia uwekezaji katika biashara ndogo ndogo na sekta ya viwanda.
  • Utoaji wa huduma bora za afya kwa wote.
  • Utoaji wa vifaa vya michezo na burudani kwa ukuaji wa kimwili, kiakili, kijamii, kimaadili na maendeleo ya watu.
  • Kufuatia jaribio la mapinduzi ya Agosti 1, 1982, Raila Odinga alikamatwa na kukabiliwa na mashtaka kadhaa, yakiwemo ya uhaini ambayo alizuiliwa bila kufunguliwa mashtaka. Tume ya Ukweli ya Haki na Maridhiano iliambiwa mwaka 2011 kwamba Odinga alikuwa na mawasiliano na mpangaji mkuu wa mapinduzi hayo. Odinga amekana kuhusika kila mara. - Makavazi ya Kitaifa ya Kenya.

William Samoei Ruto

Muungano wa Kenya Kwanza

  • Mgombea huyu mwenye umri wa miaka 55 ana Shahada ya Uzamifu/PhD katika Ikolojia ya Mimea na BSc katika Botany na Zoology kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya chama cha United Democratic Alliance ( chenye mafungamano na Kenya Kwanza).
  • Aliongoza Vuguvugu la vijana la Youth for Kanu '92 (YK'(92).
  • Wizara yake iliorodheshwa kama inayofanya bora zaidi serikalini alipokuwa Waziri wa Kilimo.
  • Alihudumu kama Naibu Rais wa kwanza wa Kenya chini ya katiba mpya ya 2010.
  • Alihudumu kama mbunge wa eneo bunge la Eldoret Kaskazini kuanzia 1997-2007.
  • Kutenga $424 milioni kila mwaka kwa biashara ndogo ndogo za kati.
  • Kuanzisha mfuko wa elimu wa kitaifa ili kukidhi gharama zisizo za masomo.
  • Tekeleza kikamilifu sheria ya usawa wa kijinsia ya thuluthi mbili katika uteuzi wa kisiasa na kutenga nusu ya baraza lake la mawaziri kwa wanawake.
  • Mnamo 2008, Mahakama Kuu ya Kenya iliamuru Naibu Rais William Ruto kusalimisha shamba la ekari 100 na kulipa $ 62,500 kwa Adrian Muteshi, mkulima ambaye alimshtaki kwa kuchukua mali hiyo baada ya uchaguzi wa 2007. - Kenya Law
  • Mnamo 2011, Bw Ruto alikabiliwa na kesi kwa makosa matatu dhidi ya binadamu: Mauaji, uhamisho wa watu kwa lazima na mateso ya watu katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu. Miaka mitano baadaye mahakama ilisitisha kesi hiyo kwa msingi kwamba - ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa dhaifu. -ICC

George Wajackoyah

Chama cha Roots

  • Profesa huyo mwenye umri wa miaka 61 ana shahada ya uzamili katika sheria kuhusu maendeleo kutoka Chuo Kikuu cha Warwick na shahada ya uzamili , sheria (sheria za Marekani kutoka Chuo Kikuu cha Baltimore.
  • Bw Wajackoyah anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Roots Party.
  • Alihudumu kama Inspekta katika idara ya usalama ya Special branch wakati wa utawala wa marehemu Rais Daniel Moi kabla ya kulazimika kutorokea ng'ambo ili kuepuka kufunguliwa mashtaka na mamlaka.
  • Yeye ni mshirika katika kampuni ya mawakili aliyoianzisha mwaka wa 2018.
  • Alifunnza somo la sheria na uchumi katika vyuo vikuu vya Marekani, Uingereza na Kenya.
  • Kuhalalisha matumizi ya kiviwanda ya bangi
  • Badilisha siku za kazi hadi Jumatatu hadi Alhamisi.
  • Huduma ya afya ya bure na msaada kwa wazee, walio hatarini na wajawazito

David Mwaure Waihiga

Chama cha Agano

  • David Mwaure anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Agano.
  • Ni kiongozi wa Chama cha Agano.
  • Alihitimu na shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi na ana Shahada ya Uzamili katika masomo ya uongozi.
  • Yeye ni wakili mkuu na amehudumu kama mwanasheria kwa zaidi ya miongo mitatu.
  • Ana kampuni ya uwakili na amewania viti mbalimbali vya kisiasa.
  • Ilianzishwa chama cha Agano mwaka 2006.
  • Kupambana na ufisadi uliokithiri.
  • kuunda nafasi za ajira.
  • Kurejesha mali ya Kenya iliyofichwa nje ya nchi.

Pata maelezo zaidi kuhusu sera za wagombea urais hapa

Raila Odinga (Kulia) amemteua Martha Karua (Kushoto) kama mgombea mwenza

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Raila Odinga (Kulia) amemteua Martha Karua (Kushoto) kama mgombea mwenza

Bi Karua aligombea urais mwaka wa 2013 na kupata kura 43,881 - au 0.36% ya jumla ya kura ziliyopigwa.

Lakini anafahamika kwa kuwa jasiri na mpigania demokrasia ya vyama vingi.

Ametofautiana na marais wawili wa zamani kiasi cha kuondoka kwa hasira katika mikutano yao.

Mwaka 2001 aliondoka katika mkutano uliokuwa ukuhudhuriwa na rais wa wakati huo hayati Daniel arap Moi, kupinga kauli iliyotolewa dhidi ya aliyekuwa mkuu wa chama chake wakati huo Mwai Kibaki.

Bi Karua alijiuzulu wadhifa wa waziri wa sheria mwaka wa 2009 akitaja hali ya kufadhaika baada ya Bw Kibaki, rais wakati huo kuwateua majaji bila yeye kujua.

"Swali kuu ni iwapo ana uwezo wa kung'atuka kama kinara wa Mlima Kenya kwa sasa Rais Uhuru anapostaafu. Je, atakumbatiwa kikamilifu miongoni mwa nyadhifa za chini za Mlima Kenya?" Bwana Bigambo anauliza.

Uhuru Kenyatta anaondoka madarakani baada ya kuhudumu kwa mihula miwili

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Uhuru Kenyatta anaondoka madarakani baada ya kuhudumu kwa mihula miwili

Bw Gachagua kwa upande mwingine amesifiwa na wachanganuzi kwa uwezo wake wa kuingia katika mtandao wa kisiasa aliokuwa sehemu yake alipokuwa akifanya kazi kama msaidizi wa kibinafsi wa Rais Kenyatta na afisa wa wilaya katika maeneo tofauti.

"Uwezo wake wa kutumia fursa aliyopata kufikia wadhifa huu ukizingatia majina ya watu wengine walijulikana kitaifa ni kitu cha ajabu," Bw Mkangi anasema.

Bw. Gachagua ni Mbunge wa eneo bunge la Mathira kati kati mwa Kenya, ambalo linajivunia kutoa Marais watatu wa Kenya - Jomo Kenyatta, Mwai Kibaki na Uhuru Kenyatta.

Ni mfanyabiashara ambaye hotuba zake katika majukwaa ya kampeni zinaashiria anaelewa masuala yanayowaathiri Wakikuyu.

"Ni mbwa mwitu wa kisiasa anayeogopwa ambaye Ruto alihitaji ili kuweza kukabiliana na Rais Uhuru katika eneo la kati," Bw Bigambo anasema.

Licha ya masuala ya kiuchumi kujitokeza katika uchaguzi huu kama kigezo kinachowezekana cha jinsi watu watakavyopiga kura, ukabila bado una ushawishi mkubwa kwa wapiga kura.

Hii ni mara ya kwanza tangu Kenya ipate uhuru ambapo Mkikuyu hajajitokeza kuwa mgombeaji mkuu wa urais - Bw Ruto ni Mkalenjin, kabila la tatu kwa ukubwa, na Bw Odinga ni Mjaluo, kabila la nne kwa ukubwa.

Kwa hivyo wawili hao wamependekeza Wakikuyu - kabila kubwa zaidi - kama wagombea wenza katika uchaguzi wa Agosti 9, uamuzi ambao unaweza kuimarisha au kuvunja kampeni zao za urais.

"Chaguo la wagombea wenza kutoka jamii ya Wakikuyu ndiyo ilikuwa njia pekee ya kuhamasisha jamii hiyo kujitokeza kupiga kura," Bw Mkangi anasema.

Uchaguzi Kenya 2022:Unaweza pia kusoma