Uchaguzi wa Kenya 2022: Ghadhabu baada IEBC kusitisha uchaguzi wa ugavana Mombasa na Kakamega

Chebukati

Chanzo cha picha, Getty Images

    • Author, Ambia Hirsi
    • Nafasi, BBC Swahili

Vyama vya kisiasa nchini Kenya vimepinga uamuzi wa Tume ya Uchaguzi kusitisha uchaguzi katika viti vinne vya uchaguzi kabla ya uchaguzi wa Jumanne.

Miungano miwili mikuu ya Azimio One Kenya na United Democratic Alliance-chama tanzu cha Muungano wa Kenya Kwanza imeelezea kusikitishwa na uamuzi huo ikidai kuna hila na ufisadi katika mpango huo mzima.

Maafisa wa chama wanahofia hitilafu hiyo inaweza kuathiri matokeo ya uchaguzi.

Mamlaka ya uchaguzi ilisimamisha uchaguzi wa ugavana katika kaunti za Mombasa na Kakamega baada ya karatasi za kura kubainika kuwa na makosa- maelezo na picha za wagombea hazikuwa sahihi.

Wapiga kura katika maeneo bunge mengine mawili ya Pokot Kusini na Kacheliba hawatampigia kura mbunge wao.

Katika taarifa kwa vyombo vya habari Katibu Mkuu wa Muungano wa Azimio One Kenya Junet Mohamed ameelezea kusikitishwa na hatua hiyo akidai kuna mpango fiche kwani maeneo yaliyoathiriwa wanayazingatia kama ngome yao.

''Sisi hatujafurahishwa na hatua ya kamati ya uchaguzi kuahirisha uchaguzi wa ugavana katika kaunti ya Mombasa na Kakamega. Tunaona kama kuna mpango fiche ambayo bado tunachunguza kwa nini ni hizo kaunti mbili ambayo ni ngome ya Azimio peke yake uchaguzi umeahirishwa na sio kaunti zingine'', alisema Bw Junet

Kwa upande wake mgombea wa ugavana wa United Democratic Alliance (UDA), Hassan Omar alisema yeye na mgombea mwenza wake waligutushwa na taarifa za kuahirisha uchaguzi wa ugavana wa Mombasa.

''Naona kuna njama mbaya katika uahirishaji huu uliyokusudiwa'',alisema Bw Hassan akiongeza kuwa timu yake inajadiliana na mamlaka ya chama na kwamba kauli rasmi itatolewa kuhusiana na suala hilo.

Hata hivyo pande zote mbili zimewaomba wafuasi wao kujitokeza kwa wingi na kuwampigia kura wagombeaji wanaowania nyadhifa nyingine tano za uchaguzi.

A Senior Independent Electoral and Boundaries Commission (IEBC) official shows a sample ballot paper after the opening of a container with official electoral material to be deployed in different polling stations at a tallying centre in Nairobi, Kenya.

Chanzo cha picha, AFP

IEBC imetetea uamuzi wake ikisema dosari hiyo haikutokana na wao ikiongeza kuwa kampuni iliyopewa kandarasi ya kuchapisha makaratasi ya kupiga kura ndio ilichanganya makaratasi hayo.

Tume hiyo aidha imesema kuwa imeanza uchapishaji wa karatasi za kupigia kura na hivi karibuni watatangaza tarehe za chaguzi katika maeneo hayo.

Upigaji kura kwa nyadhifa nyingine tano za kuchaguliwa ambazo ni Urais, Seneta, Mbunge, Mwakilishi wa Wanawake na Mbunge wa Kaunti utaendelea kama ilivyopangwa.

Awali tume hiyo iliwafuta kazi wafanyikazi saba wa uchaguzi baada ya kupatikana nyumbani kwa mgombeaji kwa kile kinachoaminika kuwa mpango wa kushawishi matokeo ya uchaguzi huo.

Maandalizi ya uchaguzi wa Jumanne yamekumbwa na hofu ya wizi wa kura huku wanasiasa kutoka pande zote wakidai kulikuwa na mipango ya kushawishi matokeo ya uchaguzi huu.

Nani yuko kwenye kinyang'anyiro cha kuiongoza Kenya ?

Fahamu zaidi kuwahusu wagombea urais wa Kenya

Chagua mgombea ili kutazama wasifu wake

Raila Amollo Odinga

Muungano wa Azimio la Umoja

  • Mgombea huyo mwenye umri wa miaka 77 ni mhandisi aliyesomea Chuo Kikuu cha Ufundi cha Magdeburg (sasa kinajulikana kama Chuo Kikuu cha Otto-von-Guericke Magdeburg) nchini Ujerumani.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya Azimio la Umoja One Kenya Coalition Party.
  • Hili litakuwa jaribio lake la tano baada ya kugombea katika: 1997, 2007, 2013 na 2017.
  • Bw Odinga alikuwa mmoja wa wapiganiaji wa demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya. Alikamatwa, akafungwa na wakati fulani akaenda uhamishoni kwa sababu ya kupigania haki hiyo
  • Aliwahi kuwa Waziri Mkuu, kuanzia 2008-2013.
  • Odinga alihusika kufanikisha miradi mikubwa iliyotekelezwa na serikali ya Kibaki, kama vile miradi ya umeme vijijini na barabara.
  • Kuafikia ukuaji wa uchumi wa tarakimu mbili kupitia uwekezaji katika biashara ndogo ndogo na sekta ya viwanda.
  • Utoaji wa huduma bora za afya kwa wote.
  • Utoaji wa vifaa vya michezo na burudani kwa ukuaji wa kimwili, kiakili, kijamii, kimaadili na maendeleo ya watu.
  • Kufuatia jaribio la mapinduzi ya Agosti 1, 1982, Raila Odinga alikamatwa na kukabiliwa na mashtaka kadhaa, yakiwemo ya uhaini ambayo alizuiliwa bila kufunguliwa mashtaka. Tume ya Ukweli ya Haki na Maridhiano iliambiwa mwaka 2011 kwamba Odinga alikuwa na mawasiliano na mpangaji mkuu wa mapinduzi hayo. Odinga amekana kuhusika kila mara. - Makavazi ya Kitaifa ya Kenya.

William Samoei Ruto

Muungano wa Kenya Kwanza

  • Mgombea huyu mwenye umri wa miaka 55 ana Shahada ya Uzamifu/PhD katika Ikolojia ya Mimea na BSc katika Botany na Zoology kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya chama cha United Democratic Alliance ( chenye mafungamano na Kenya Kwanza).
  • Aliongoza Vuguvugu la vijana la Youth for Kanu '92 (YK'(92).
  • Wizara yake iliorodheshwa kama inayofanya bora zaidi serikalini alipokuwa Waziri wa Kilimo.
  • Alihudumu kama Naibu Rais wa kwanza wa Kenya chini ya katiba mpya ya 2010.
  • Alihudumu kama mbunge wa eneo bunge la Eldoret Kaskazini kuanzia 1997-2007.
  • Kutenga $424 milioni kila mwaka kwa biashara ndogo ndogo za kati.
  • Kuanzisha mfuko wa elimu wa kitaifa ili kukidhi gharama zisizo za masomo.
  • Tekeleza kikamilifu sheria ya usawa wa kijinsia ya thuluthi mbili katika uteuzi wa kisiasa na kutenga nusu ya baraza lake la mawaziri kwa wanawake.
  • Mnamo 2008, Mahakama Kuu ya Kenya iliamuru Naibu Rais William Ruto kusalimisha shamba la ekari 100 na kulipa $ 62,500 kwa Adrian Muteshi, mkulima ambaye alimshtaki kwa kuchukua mali hiyo baada ya uchaguzi wa 2007. - Kenya Law
  • Mnamo 2011, Bw Ruto alikabiliwa na kesi kwa makosa matatu dhidi ya binadamu: Mauaji, uhamisho wa watu kwa lazima na mateso ya watu katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu. Miaka mitano baadaye mahakama ilisitisha kesi hiyo kwa msingi kwamba - ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa dhaifu. -ICC

George Wajackoyah

Chama cha Roots

  • Profesa huyo mwenye umri wa miaka 61 ana shahada ya uzamili katika sheria kuhusu maendeleo kutoka Chuo Kikuu cha Warwick na shahada ya uzamili , sheria (sheria za Marekani kutoka Chuo Kikuu cha Baltimore.
  • Bw Wajackoyah anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Roots Party.
  • Alihudumu kama Inspekta katika idara ya usalama ya Special branch wakati wa utawala wa marehemu Rais Daniel Moi kabla ya kulazimika kutorokea ng'ambo ili kuepuka kufunguliwa mashtaka na mamlaka.
  • Yeye ni mshirika katika kampuni ya mawakili aliyoianzisha mwaka wa 2018.
  • Alifunnza somo la sheria na uchumi katika vyuo vikuu vya Marekani, Uingereza na Kenya.
  • Kuhalalisha matumizi ya kiviwanda ya bangi
  • Badilisha siku za kazi hadi Jumatatu hadi Alhamisi.
  • Huduma ya afya ya bure na msaada kwa wazee, walio hatarini na wajawazito

David Mwaure Waihiga

Chama cha Agano

  • David Mwaure anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Agano.
  • Ni kiongozi wa Chama cha Agano.
  • Alihitimu na shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi na ana Shahada ya Uzamili katika masomo ya uongozi.
  • Yeye ni wakili mkuu na amehudumu kama mwanasheria kwa zaidi ya miongo mitatu.
  • Ana kampuni ya uwakili na amewania viti mbalimbali vya kisiasa.
  • Ilianzishwa chama cha Agano mwaka 2006.
  • Kupambana na ufisadi uliokithiri.
  • kuunda nafasi za ajira.
  • Kurejesha mali ya Kenya iliyofichwa nje ya nchi.

Pata maelezo zaidi kuhusu sera za wagombea urais hapa

Huku hayo yakiarifiwa Tume ya IEBC imesema sasa itategemea vifaa vya elektroniki kuwatambua wapiga kura ili kutii uamuzi wa mahakama ya Rufaa ambao umebatilisha uamuzi wa mahakama kuu uliokuwa umeitaka IEBC kutumia sajili ya daftari kuwatambua wapiga kura.

Mwenyekiti wa Tume hiyo Wafula Chebukati amesema hawana budi ila kufuta maagizo ya mahakama ya Rufaa .

Chama cha UDA kilikuwa kimewasilisha pingamizi kortini dhidi ya uamuzi wa hapo awali wa mahakama Kuu kuhusu matumizi ya sajili ya daftari.

Uchaguzi wa Kenya 2022: Vyama vinakuahidi nini?

Chagua suala ambalo linakuvutia

Sera za kila chama

  • Azimio La Umoja One Kenya Coalition

  • Roots Party of Kenya

  • Chama cha Agano

  • Kenya Kwanza Alliance

Mwongozo huu ni muhtasari wa sera kuu zinazotolewa na kila chama.

Pata maelezo zaidi kuhusu wagombea urais wa Kenya hapa

End of Uchaguzi wa Kenya 2022: Vyama vinakuahidi nini?

Jopo la majaji watatu lilisema kuwa tume ya uchaguzi itatumia maelekezo katika kesi ya NASA ya mwaka 2017 ambapo mahakama iliamuru IEBC kutumia sajili iliyochapishwa ya wapiga kura pekee katika hali ambapo vifaa vya elektroniki KIEMS vinafeli kabisa bila uwezekano wa kukarabatiwa au kubadilishwa.

Uchambuzi

Dickens Olewe-BBC News, Nairobi

Taarifa ya kusimamisha upigaji kura katika maeneo manne, ikiwa ni pamoja na kinyang'anyiro cha ugavana kinachofuatiliwa kwa karibu, ni habari ambayo mwenyekiti wa tume ya uchaguzi hangetaka kutangazasaa chache kabla ya uchaguzi mkuu wa Kenya.

Wafula Chebukati tayari kibarua cha kuwaregeshea imani Wakenya baada ya uchaguzi wa urais aliokuwa akisimamia miaka mitano iliyopita kubatilishwa na kurudiwa tena.

Uchaguzi wa Jumanne ulikusudiwa kumkomboa, lakini kufuatia msururu wa visa vilivyoshuhudiwa Jumatatu, kazi yake ilizidi kuwa ngumu.

Katika saa chache zilizopita Bw Chebukati amelazimika kuwatimua maafisa kadhaa wa uchaguzi kwa sababu ya madai ya mikutano isiyofaa na wagombeaji, gari lililobeba vifaa vya kupigia kura lilishambuliwa na umma na vitu kuharibiwa, kifaa ambacho kilipaswa kutumiwa kuthibitisha wapiga kura na kutuma matokeo kimeripotiwa kupotea katika mkoa mwingine.

Amejaribu kuwahakikishia Wakenya kwamba tume hiyo ilikuwa tayari kuendesha uchaguzi lakini maneno hayo yanayumba.

Ikiwa matatizo ya kiusimamizi yataendelea kuongezeka katika saa chache zijazo na kuwa mbaya zaidi uchaguzi utakapofanyika Jumanne, basi tume ya uchaguzi itakuwa na mgogoro mkubwa mkononi mwake.

Kwa sasa, Wakenya wengi wanatumai kuwa matukio ya Jumatatu hayakukusudiwa na kwamba tume itakuwa na jukumu la kuendesha uchaguzi wa haki na wa kuaminika.

th

Pia unawezakusoma:

th