Jinsi vita vya Iran vinavyovuruga malengo ya kimkakati ya China

Chanzo cha picha, AFP via Getty Images
China bado haijahisi mtikisiko wa vita Mashariki ya Kati, lakini tayari inahisi athari zake za awali.
Kwa muda mfupi, China ina akiba ya mafuta ya kutosha kwa miezi kadhaa.
Baada ya hapo, inaweza kugeukia jirani yake Urusi kwa msaada wa mafuta. Hata hivyo, China inafikiria kwa makini athari za muda mrefu za hali hii, si tu kwa uwekezaji wake Mashariki ya Kati, bali pia kwa malengo yake ya kimkakati duniani.
Wiki hii, maelfu ya wajumbe wa Chama cha Kikomunisti wanakutana Beijing kujadili ramani ya maendeleo ya uchumi wa pili kwa ukubwa duniani, wakati China ikiendelea kukabiliana na changamoto kadhaa: matumizi ya ndani yaliyopungua, mgogoro wa muda mrefu katika sekta ya mali isiyohamishika, na madeni makubwa ya serikali za mitaa.
Siku ya Alhamisi, China ilipunguza lengo lake la ukuaji wa uchumi wa mwaka hadi kiwango cha chini zaidi tangu mwaka 1991, hata wakati Beijing ikiendelea kuendeleza kwa kasi sekta za teknolojia ya juu na nishati jadidifu.
China huenda ilitarajia kuongeza mauzo ya bidhaa nje ya nchi ili kujinasua kutoka katika matatizo ya kiuchumi.
Lakini kwa mwaka mmoja sasa imekuwa ikipambana na vita vya kibiashara na Marekani, na sasa inakabiliwa pia na uwezekano wa msukosuko Mashariki ya Kati, eneo ambalo lina njia muhimu za usafirishaji wa bidhaa pamoja na sehemu kubwa ya mahitaji yake ya nishati.
Kadiri vita vitakavyoendelea kwa muda mrefu, ndivyo madhara yatakavyoweza kuongezeka, hasa ikiwa usafiri kupitia Mlango wa Bahari wa Hormuz utaendelea kuzuiwa.
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
Philip Shetler-Jones kutoka Taasisi ya Royal United Services Institute anasema:
"Kipindi kirefu cha vurugu na ukosefu wa usalama Mashariki ya Kati kitavuruga pia maeneo mengine muhimu kwa China. Uchumi wa Afrika, kwa mfano, umefaidika kwa muda mrefu kutokana na uwekezaji mkubwa kutoka nchi za Ghuba.
Ikiwa uwekezaji huo utapungua, kuna hatari ya kutokea kwa hali ya kukosa utulivu ambayo inaweza kudhoofisha maslahi ya China kwa muda mrefu."
Kwa maneno mengine, kutokana na uwepo mkubwa wa China duniani, uwekezaji wake na masoko yake nje ya Mashariki ya Kati pia yako katika hatari iwapo vita vitaendelea kwa muda mrefu.
Na kama ilivyo kwa nchi nyingine nyingi, China pia ina wasiwasi kuhusu hali hii mpya ya kutotabirika duniani.
Profesa Kerry Brown, mkurugenzi wa Taasisi ya China Lau katika Chuo cha King's London, anasema:
"Nafikiri China inawaza sawa na wengine wote: mpango wa mwisho ni upi? Hakika Wamarekani hawakuingia katika hali hii bila kuwa na mpango."
Lakini anaongeza:
"Pengine, kama ilivyo kwa wengine, pia wanafikiri: Mungu wangu, inaonekana kweli waliingia bila mpango wowote. Sasa hatutaki kuvutwa katika mgogoro huu kama ambavyo hatutaki kuvutwa katika migogoro mingine, lakini pia tunahitaji kufanya jambo fulani."
Washirika wasio imara sana
Iran mara nyingi imekuwa ikitajwa na wengi katika nchi za Magharibi kama "mshirika" wa China.
Kwa hakika, nchi hizi mbili zimekuwa na uhusiano wa kirafiki kwa muda mrefu. Safari ya mwisho ya kigeni iliyofanywa na Kiongozi Mkuu wa Iran, Ali Khamenei, ilikuwa kwenda Beijing mwaka 1989.
Wakati wa ziara hiyo alipigwa picha akiwa kwenye Ukuta Mkubwa wa China.

Chanzo cha picha, Getty Images
Ushirikiano kati yao uliimarika zaidi wakati Xi Jinping alipotembelea Tehran mwaka 2016, na hatimaye nchi hizo mbili zilisaini ushirikiano wa kimkakati wa miaka 25 mwaka 2021.
China iliahidi kuwekeza dola bilioni 400 nchini Iran katika kipindi cha miaka 25, na kwa upande wake Iran iliahidi kuendelea kusambaza mafuta.
Hata hivyo, wachambuzi wanaamini kuwa sehemu ndogo tu ya fedha hizo imewafikia Wairani, lakini usambazaji wa mafuta uliendelea.
Mwaka 2025, China iliagiza mapipa milioni 1.38 ya mafuta ghafi kwa siku kutoka Iran, kulingana na Center on Global Energy Policy, kiasi ambacho ni takribani asilimia 12 ya jumla ya mafuta ghafi yanayoingizwa China. Inadaiwa kuwa mapipa mengi ya mafuta hayo yalibadilishiwa lebo na kuoneshwa kama mafuta ya Malaysia ili kuficha asili yake.
Kituo cha utafiti cha Chuo Kikuu cha Columbia kilitoa ripoti ikidai kuwa kuna zaidi ya mapipa milioni 46 ya mafuta ya Iran yaliyohifadhiwa kwenye meli katika Asia, na mengine zaidi katika maghala maalumu ambayo bado hayajapitishwa na forodha katika bandari za China za Dalian na Zhoushan, ambako Kampuni ya Taifa ya Mafuta ya Iran hukodisha matangi ya kuhifadhia mafuta.
Kumekuwa pia na madai kuhusu uuzaji wa silaha kati ya nchi hizi mbili. China imekanusha kuuza Iran makombora ya baharini ya cruise yanayolenga meli, lakini ujasusi wa Marekani umeishutumu Beijing kwa kusaidia mpango wa makombora ya balistiki wa Iran kwa kuwafundisha wahandisi na kusambaza ujuzi wa teknolojia.
Makundi ya kutetea haki za binadamu pia yamedai kuwa ukandamizaji mkali wa Iran dhidi ya waandamanaji na wakosoaji wa serikali umewezeshwa na teknolojia ya China ya utambuzi wa sura na ufuatiliaji wa kidijitali, inayodaiwa kutolewa na Beijing.
Haya yote yanaweza kufanya ionekane kana kwamba nchi hizi mbili ni marafiki wa karibu sana.
Ni kweli kwamba nchi zote nne zinataka kuipinga au kubadilisha mfumo wa dunia unaoongozwa na Marekani, lakini kwa kweli, uhusiano wao ulikuwa wa kimaslahi zaidi kuliko urafiki wa kweli.
"Kwa kweli hakuna sababu ya kiitikadi au kitamaduni inayofanya China iwe karibu na Iran," anasema Profesa Brown.
"Mkakati wa China unaofanana na 'utawala wa kuwagawa watu' wakati mwingine uliwanufaisha kwa sababu Iran ilikuwa ikibaki kuwa kero ya kudumu kwa Marekani.
Kwa hiyo nadhani sababu za China kutaka kuwa na uhusiano na Iran ni zaidi sababu za kuepuka au kupunguza shinikizo, badala ya sababu chanya."
"Huo ni msingi dhaifu sana wa uhusiano, na ulifanya kazi, lakini kwa kiwango fulani tu. Haukuwa uhusiano wa kina sana."
China pia haiangalii 'ushirika' kwa namna ile ile ambayo nchi za Magharibi zinautazama. Kwa kawaida haisaini mikataba ya pamoja ya ulinzi wa kijeshi, na haitakimbilia mara moja kumsaidia mshirika wake wakati wa vita.
Badala yake, Beijing hupendelea kujiepusha na kuhusika moja kwa moja katika migogoro au vita.
Kuongoza harakati
Lakini hilo halimaanishi kwamba China haijali sana kuhusu kile kinachotokea Mashariki ya Kati.
Beijing ilitoa tamko la kulaani kwa upole na kwa njia inayotarajiwa, na ikatoa wito wa kusitishwa kwa mapigano,
Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Wang Yi, alisema kuwa "haikubaliki kwa Marekani na Israel kufanya mashambulizi dhidi ya Iran… na zaidi kabisa kumuua waziwazi kiongozi wa nchi huru na kujaribu kubadilisha serikali."
Ukweli ni kwamba hatua za Washington, kwanza Venezuela mwezi Januari, na sasa Iran zimeonesha mipaka ya ushirikiano wa nchi hizo na China.
Katika matukio yote mawili, Beijing imeachwa pembeni kama mtazamaji tu, bila uwezo wa kuwasaidia wale walio ndani ya mzunguko wake wa kisiasa au kiuchumi.
China inajaribu kujionesha kama nguvu ya dunia yenye uwajibikaji inayoweza kuwa mizani dhidi ya Marekani, anasema Philip Shetler-Jones kutoka Taasisi ya Royal United Services .
Lakini kwa upande wa nguvu za kijeshi, anasema Marekani inaonesha maana halisi ya kuwa dola kubwa, uwezo wa kulazimisha matokeo ya kisiasa au kijeshi katika maeneo mbalimbali duniani.
Kwa hoja yake, Beijing bado si "yenye nguvu zaidi" katika kiwango sawa, licha ya nguvu yake kubwa ya kiuchumi.
"China haina uwezo wa kuwalinda marafiki zake dhidi ya aina hii ya hatua, hata kama ingetaka kufanya hivyo."
Ili kukabiliana na wasiwasi huo, Xi Jinping ataendelea kujiweka kama kiongozi wa dunia aliye thabiti na anayetabirika, tofauti na Donald Trump.
"Kile China itasema ni kwamba Donald Trump ameonesha tena waziwazi unafiki wa nchi za Magharibi na madai yao kuhusu mfumo wa kimataifa wa kiliberali," anasema Profesa Steve Tsang, mkurugenzi wa Taasisi ya China ya SOAS.

Chanzo cha picha, Getty Images
Anaongeza kwamba usumbufu katika usambazaji wa nishati na safari za ndege unaotokana na mgogoro huu utakuwa na athari kubwa zaidi kiuchumi katika nchi za Global South kuliko katika nchi za Magharibi.
"Baadhi ya nchi zinaweza kukabiliwa na uhaba wa chakula katika miezi michache ijayo, na nchi hizo nyingi ni za Global South. Pia tayari tunaona mipasuko katika muungano wa nchi za Magharibi, huku Uingereza na Hispania zikitengwa na kushambuliwa kisiasa," anasema.
Beijing inaweza pia kuona fursa ya kusaidia kupatanisha mazungumzo ya amani pamoja na nchi nyingine. Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Wang Yi, tayari amezungumza na mawaziri wenzake kutoka Oman na Ufaransa, na China imetangaza kuwa itatuma mjumbe maalum Mashariki ya Kati kusaidia juhudi za kidiplomasia.
Ziara inayokuja ya Trump
Hata hivyo, China inafanya mambo kwa tahadhari kubwa, kwa sababu moja ya mambo muhimu wanayoyazingatia ni rais wa Marekani ambaye tabia yake hubadilika haraka, ambaye anatarajiwa kuwasili kwenye mkutano uliokuwa unasubiriwa kwa muda mrefu baadaye mwezi huu.
Hakuna hata moja ya ukosoaji wa China kuhusu mashambulizi ya Marekani na Israel dhidi ya Iran uliomlenga moja kwa moja rais huyo, jambo ambalo linaweza kufanya salamu ya mkono wakati wa mkutano iwe rahisi kidogo.
Baadhi ya watu wamekuwa wakijiuliza kama ziara hiyo bado inaweza kufanyika. Lakini kuna dalili kuwa bado inaendelea kama ilivyopangwa. Maafisa kutoka pande zote mbili wanatarajiwa kukutana kujadili maandalizi ya safari hiyo, kulingana na ripoti ya Reuters.
China inaweza kuona mkutano huo kama nafasi ya "kutafuta ishara" au dalili, anasema Shetler-Jones, kuhusu jinsi rais wa Marekani anaweza kujibu migogoro mingine kama vile suala la Taiwan, kisiwa kinachojitawala ambacho China inadai kuwa sehemu ya eneo lake.
"Ama kwa kiwango ambacho vita hivi havitapendwa na watu, vinaweza kuchangia kuongezeka kwa mwelekeo wa kujizuia katika sera za nje na usalama za Marekani.
Na ikiwa hali hiyo itatekelezwa na serikali ya baadaye, inaweza kuipa China uhuru mkubwa zaidi kufuatilia maslahi yake katika eneo lake na duniani kwa ujumla."
Mgogoro huu pia unatoa nafasi kwa baadhi ya watu nchini China kuichora Washington kama wachochezi wa vita, jambo ambalo Jeshi la Ukombozi wa Watu wa China (PLA) limekuwa likifanya kwenye mitandao ya kijamii.
Lakini kuwa na mhusika ambaye hatabiriki na ambaye mara nyingi anaonekana kutofanya kazi kwa utaratibu pia kunaweza kuwa chanzo cha wasiwasi kwa Beijing, anasema Profesa Brown.
"Sidhani kama China inataka dunia inayotawaliwa na Marekani," anasema.
"Lakini pia hawataki dunia ambayo Marekani ni mhusika asiye na utulivu kabisa."















