Makombora ya Iran yazuiwa Uturuki, UAE na Qatar huku bei ya mafuta ikipita $100 kwa pipa

Israel inasema kuwa inafanya mashambulizi kote Iran na Lebanon huku mawaziri wa fedha wa G7 wakitarajiwa kufanya mkutano wa dharura kuhusu bei ya mafuta.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma & Ambia Hirsi

  1. Na kufikia hapo tunakamilisha matangazo ya moja kwa moja. Kwaheri.

  2. India ilitoa hifadhi kwa meli ya Iran siku tatu kabla ya Marekani kuizamisha

    Meli ya kivita ya Iran Iris Dena ilizama baada ya kushambuliwa na manowari ya Marekani tarehe 4 Machi

    Chanzo cha picha, AP

    Maelezo ya picha, Meli ya kivita ya Iran Iris Dena ilizama baada ya kushambuliwa na manowari ya Marekani tarehe 4 Machi

    Meli ya kivita ya Iran Iris Dena ilipewa ruhusa na India kutia nanga siku tatu kabla ya kushambuliwa na manowari ya Marekani, India imesema.

    Waziri wa Mambo ya Nje S Jaishankar anasema Iran iliomba ruhusa kwa meli zake tatu kutia nanga katika bandari za India tarehe 28 Februari - siku ambayo Marekani na Israel zilianza vita dhidi ya Iran - na idhini ilitolewa na India tarehe 1 Machi.

    Mwenendo wa meli kati ya 1 na 4 Machi hauko wazi na haijabainika kwa nini ni mmoja tu ndio aliyofika India.

    Kuzama kwa Iris Dena, ikiwa mabaharia 130, katika maji ya kimataifa karibu na pwani ya kusini mwa Sri Lanka tarehe 4 Machi kulionyesha kuongezeka kwa vita - na kuibua maswali kuhusu mamlaka ya India nyumbani.

    Lilikuwa ni shambulio la kwanza la kijeshi nje ya Mashariki ya Kati tangu Marekani na Israel kuanzisha vita vyao dhidi ya Iran.

    Rais Donald Trump amesema kuharibu jeshi la wanamaji la Iran ni lengo moja la shambulio hilo.

    Meli hizo tatu za Iran - Iris Dena, Iris Bushehr na Iris Lavan -zote zilishiriki mazoezi ya kijeshi yaliyoandaliwa na India kati ya 15 na 25 Februari katika mji wa pwani wa Visakhapatnam.

    Pia unaweza kusoma:

  3. Habari za hivi punde, Qatar yazuia makombora 17 ya balistiki na droni sita za Iran

    Wizara ya Ulinzi ya Qatar inaripoti kuwa imeshambuliwa kwa makombora 17 ya balistiki na droni sita za Iran.

    Inasema kuwa vikosi vyake vya ulinzi vimefanikiwa kuzuia mashambulio hayo bila mtu yeyote kujeruhiwa.

    Wkati huo huo wanajeshi wawili wa Umoja wa Falme za Kiarabu wameuawa katika ajali ya helikopta iliyosababishwa na hitilafu ya kiufundi, kulingana na wizara ya ulinzi ya nchi hiyo.

    Haijabainika ikiwa tukio hilo linahusiana na vita vya Marekani na Israel dhidhi ya Iran.

    Wizara ya Ulinzi ya UAE inasema maafisa wawili waliouawa walikuwa "wakitekeleza wajibu wao wa kitaifa" wakati wa tukio hilo siku ya Jumatatu, na "ikutoa rambirambi zake kwa familia wawili hao".

    .
  4. Maelfu washerehekea uteuzi wa kiongozi mkuu mpya wa Iran mjini Tehran

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Nchini Iran, wafuasi wa utawala huo wameingia katika mitaa ya Tehran kusherehekea uteuzi wa Mojtaba Khamenei kkuwa kiongozi mkuu mpya.

    Picha zinaonyesha watu wakinyanyua picha za Khamenei na babake Ayatollah Ali Khamenei, aliyeuawa katika mashambulizi ya Marekani na Israel wiki iliyopita.

    Katika tukio moja, mwanamume mmoja anaonekana akishikilia bango linaloonyesha picha ya Ayatollah Ali Khamenei akipitisha bendera kwa mwanawe.

    Shirika la habari la AFP limeripoti kuwa maelfu ya watu walimiminika katika uwanja wa katikati mwa mji mkuu wa Iran leo asubuhi kuahidi utiifu wao kwa kiongozi mpya wa nchi hiyo.

    Ingawa wengine wamesherehekea hadharani, wengine wameiambia BBC Idhaa ya Kiajemi kwamba Mojtaba ni "mbaya zaidi kuliko baba yake" na kwamba wanatumai hatma yake itakuwa sawa na ya baba yake.

    Angalizo: Mashirika ya habari ya kimataifa mara nyingi huzuiwa viza ya kuingia Iran, jambo ambalo kwa kiasi kikubwa hudhibiti uwezo wao wa kukusanya taarifa ndani ya nchi hiyo.

    .

    Chanzo cha picha, EPA

  5. Habari za hivi punde, Marekani yawataka raia wake kuondoka kusini mashariki mwa Uturuki

    Wizara ya mambo ya nje ya Marekani imewataka raia wake walioko kusini mashariki mwa Uturuki kuondoka.

    Washington pia imewashauri wafanyakazi wasio na shughuli zisizo maalum katika ubalozi wake mdogo karibu na Adana kusini mwa Uturuki kuondoka, kulingana na taarifa kutoka kwa ubalozi wa Marekani mjini Ankara.

    Ubalozi huo wa Marekani uko karibu na kituo cha NATO.

    Soma zaidi:

  6. Watanzania waliokwama Dubai warejea nyumbani

    abiria wakichuka kutoka kwenye ndege

    Watanzania 236 mchana wa hii leo wamerejea nyumbani kwa ndege maalumu ya shirika la ndege la Tanzania baada ya kukwama Dubai kwa muda kutokana na vita vinavyondelea kati ya Marekani Israel na Iran.

    ATCL wanasema si kawaida wao kutuma ndege kubwa Dubai lakini kutokana uhitaji mkubwa imebidi wao kufanya hivyo na huenda wakatuma tena ndege nyingine siku za karibuni.

    Afisa uendeshaji mkuu Captain Arif Jinnah amesema ndege hii ilikuwa ni ya gharama nafuu sio bure na abiria wote waliopangwa kuja wamekuja licha ya kwamba wamelazimika pia kuacha mizigo.

    Mashirika ya ndege ya kimataifa yaliahirisha safari za kuelekea Mashariki ya Kati tangu Iran ilipoanza kulipiza kisasi hatua ya Marekani na Israel dhidi yake kwa kushambulia kambi za jeshi la Marekani zilizo katika mataifa ya Kiarabu katika eneo hilo.

    Ndege zinazoingia na kutoka katika viwanja vya ndege vya Tel Aviv, Dubai, Doha na vituo vingine vya kimataifa katika eneo hilo zimesitishwa.

    Iran imefanya mashambulizi katika mataifa ya Ghuba kama sehemu ya kulipiza kisasi mashambulizi ya Marekani na Israel yaliyoanza mapema Jumamosi tarehe 28 mwezi Februari.

    Maelezo zaidi:

  7. Ghana yaitaka Jumuiya ya Madola kulaani shambulio dhidi ya walinda amani wa UN Lebanon

    .

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Ghana imetoa wito kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola kulaani shambulio la makombora la hivi karibuni dhidi ya ujumbe wake wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa kusini mwa Lebanon.

    Akizungumza katika Mkutano wa 26 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Jumuiya ya Madola huko London Jumapili, Waziri wa Mambo ya Nje Samuel wa Ghana Okudzeto Ablakwa, alionya kuwa vitendo kama hivyo vinajumuisha "uvunjifu wa kila kanuni ambayo inatetewa na Mkataba wa Umoja wa Mataifa."

    "Tukiwa njiani kuelekea kwenye mkutano huu, walinda amani wetu nchini Lebanon walishambuliwa. Tunapozungumza, watatu kati yao wamefanyiwa upasuaji ... Tunahimiza Jumuiya ya Madola kulaani vikali shambulio hili na kudai uchunguzi wa haraka," aliongeza.

    Wanajeshi hao wa Ghana walikuwa wakihudumu katika Kikosi cha Muda cha Umoja wa Mataifa nchini Lebanon (UNIFIL) wakati kituo chao kilipopigwa na makombora baada ya uhasama kungezeka katika eneo hilo Ijumaa iliyopita kati ya saa kumi na moja na dakika arobaini na tano ma saa kumi na mbili kasoro dakika nane 5:45 na 5:52 kwa saa za huko.

    Wizara ya Ulinzi ya Ghana ilisema kuwa mmoja wa askari ambaye alipata majeraha mabaya ya miguu yote miwili na nyonga amefanyiwa upasuaji baada ya kupelekwa Beirut na kwa sasa anaendelea kupata nafuu.

    Mitandao ya kijamii ilijaa video zinazoonyesha uharibifu mkubwa wa vifaa vya vikosi hivyo vya kulinda amani vya Ghana.

    Tukio hilo linakuja wakati mvutano katika Mashariki ya Kati ukiendelea kuongezeka, na kuzua wasiwasi kuhusu usalama wa wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa waliotumwa kusaidia kudumisha utulivu kwenye mpaka wa Israel-Lebanon.

    Wizara ya Mambo ya Nje ya Ghana pia imewasilisha malalamiko rasmi kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, kuhusu shambulio lililotokea kusini mwa Lebanon.

    Ghana ni mojawapo ya nchi zinazochangia kwa muda mrefu askari katika operesheni za ulinzi wa amani za Umoja wa Mataifa nchini Lebanon, ambapo wanajeshi wake wanatumika kama sehemu ya kikosi kazi cha kimataifa cha kudumisha utulivu kwenye mpaka wa Israel na Lebanon.

    Soma zaidi:

  8. Putin ampongeza kiongozi mkuu mpya na kusisitiza 'uungaji mkono usioyumba' kwa Iran

    Putin

    Chanzo cha picha, Sputnik

    Rais wa Urusi Vladimir Putin amempongeza Mojtaba Khamenei kwa kuwa kiongozi mkuu mpya wa Iran na kusisitiza uungaji mkono wa Moscow kwa Tehran.

    "Naomba upokee pongezi zangu za dhati kwa kuteuliwa kuwa kiongozi mkuu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran," Putin anasema katika ujumbe uliochapishwa kwenye tovuti ya Kremlin.

    Kiongozi huyo wa Urusi pia anasema "anathibitisha tena uungaji mkono [wa Urusi] usioyumba kwa Tehran na mshikamano na marafiki zetu wa Iran" na kuahidi kuwa "atasalia mshirika anayetegemewa".

    "Wakati ambapo Iran inakabiliana na mashambulizi, hatua zako katika nafasi hii ya juu bila shaka zitahitaji ujasiri mkubwa na kujitolea. Nina imani kwamba utaendeleza kwa heshima kazi ya baba yako na kuwaunganisha watu wa Iran katika kukabiliana na majaribu haya makubwa," anasema.

    Soma zaidi:

  9. Wachezaji 23 wapewa kadi nyekundu baada ya rabsha kuzuka Brazil

    Mshambuliaji wa zamani wa Brazil na FC Porto Hulk alikuwa miongoni mwa wachezaji waliopewa kadi nyekundu

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Mshambuliaji wa zamani wa Brazil na FC Porto Hulk alikuwa miongoni mwa wachezaji waliopewa kadi nyekundu

    Wachezaji 23 wamepewa kadi nyekundu baada ya vurugu kubwa kuzuka kati ya vilabu vya Brazil Cruzeiro na Atletico Mineiro wakati wa fainali ya Campeonato Mineiro.

    Kaio Jorge alifunga bao la ushindi huko Belo Horizonte huku Cruzeiro, inayonolewa na kocha wa zamani wa Brazil, Tite, ilipowalaza wapinzani wao Atletico 1-0 na kuwa mabingwa wa jimbo la Minas Gerais kwa mara ya kwanza tangu 2019.

    Lakini mechi hiyo ilikumbwa na vurumai kali ndani ya sekunde hizo, hali iliyowalazimu maafisa wa usalama na polisi wa kijeshi kuingilia kati na kusababisha wachezaji 23, akiwemo mshambuliaji wa zamani wa Atletico wa Brazil, Hulk, kutolewa uwanjani kwa kadi nyekundu.

    Makabiliano hayo makubwa yalianza pale kipa wa Atletico, Everson, alipomsukuma Christian na kumuangusha chini, kuweka goti lake kwenye kifua cha kiungo huyo wa Cruzeiro, ambaye aligongana naye wakati akifukuzia mpira.

    Wenzake Christian mara moja walikabiliana na Everson, na kumsukuma kipa kwenye nguzo ya goli, jambo lililozua maswali huku wachezaji wengi wakijiunga na vurumai hilo, wafanyakazi wa usalama wakijaribu kutenganisha timu hizo.

    Ingawa hakuna kadi nyekundu iliyotolewa na mwamuzi Matheus Delgado Candancan wakati wa mchezo, chombo cha habari cha Brazil Globo kiliripoti, wachezaji 23 walitolewa nje baadaye kwa sababu pambano lilimzuia afisa wa mechi kuonyesha kadi uwanjani.

    Soma pia:

  10. Habari za hivi punde, Milipuko mikubwa yasikika Tehran - ripoti

    Milipuko mikubwa imesikika katika mji mkuu wa Iran wa Tehran, kulingana na shirika la habari la AFP.

    Haijabainika ni nini kililcholengwa mjini Tehran lakini milipuko hiyo ilisikika katika maeneo kadhaa ya mji huo, shirika hilo linaripoti.

    Huku hayo yakijiri mtu mmoja ameuawa na mwingine kujeruhiwa vibaya baada ya kombora kugonga eneo la ujenzi katikati mwa Israel, kwa mujibu wa msemaji wa huduma za dharura za Israel.

    Mwanamume aliye na umri wa miaka 30 amekimbizwa hospitalini akiwa na majeraha mabaya katika eneo lingine.

  11. Trump 'hajafurahishwa' na uteuzi wa kiongozi mpya wa Iran - Fox News

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais Donald Trump wa Marekani amesema "hajafurahishwa" na uteuzi wa Iran wa Mojtaba Khamenei kama kiongozi wake mkuu mpya, kulingana na kipindi cha Fox News.

    Mtangazaji Brian Kilmeade amesema alizungumza na rais baada ya tangazo hilo, ambaye alimwambia: "Sijafurahia."

    Kilmeade hakutoa maelezo zaidi kuhusu mazungumzo hayo na Trump bado hajatoa maoni yake hadharani.

    Iran yaanzisha wimbi jipya la mashambulizi dhidi ya Israel na mataifa ya Kiarabu

    Wakati huo huo, Bahrain inaripoti idadi kubwa zaidi ya vifo katika shambulizi moja dhidi ya nchi za Ghuba tangu vita kuanza.

    Wizara yake ya Afya inasema shambulizi lililotokea nchini humo la ndege zisizo na rubani liliwajeruhi raia 32, wakiwemo watoto wanne, mdogo wao akiwa na umri wa miezi miwili.

    Takriban watu 10 wameuawa kote eneo la Ghuba hadi kufikia sasa, wengi wao wakiwa wafanyakazi wa usalama au wafanyakazi wa kigeni. Qatar, Kuwait, Falme za Kiarabu na Saudi Arabia pia ziliripoti mashambulizi mapya usiku kucha.

    Soma zaidi:

  12. Faini za makosa ya barabarani Kenya sasa kutozwa papo hapo

    .

    Chanzo cha picha, File photo/AFP

    Mamlaka ya Kitaifa ya Uchukuzi na Usalama (NTSA) Kenya imeanzisha Mfumo wa Usafiri wa utoaji Faini za Papo Hapo kukabiliana na ukiukaji wa Sheria za Trafiki.

    Kupitia mfumo huu, makosa ya ukiukaji yatanakilia hapo hapo na kutuma ujumbe mfupi kwa njia ya simu kwa madereva.

    "Mchakato huu unajiendesha wenyewe na unafanya kazi bila uingiliaji kati wa binadamu, kuhakikisha uwazi zaidi, ufanisi, na uwajibikaji katika utekelezaji wa sheria za trafiki," NTSA ilisema katika taarifa Jumatatu.

    Malipo ya makosa yote yatafanywa ndani ya siku saba vyinginevyo, adhabu zingine zitajumuishwa.

    "Kukosa kulipa faini inayodaiwa ndani ya muda wa siku saba kutasababisha nyongeza ya riba. Isitoshe, gari au dereva ambaye anasubiri kutozwa faini hataweza kufanya miamala kwenye majukwaa ya huduma ya NTSA hadi faini hiyo itakapolipwa," ilani hiyo ilisema.

    NTSA pia iliwataka madereva kuzingatia kanuni zote za trafiki na kujibu mara moja arifa zozote rasmi zinazopokelewa.

    Hatua hiyo ni sehemu ya mipango endelevu ya serikali kuimarisha usalama barabarani na kuongeza uzingatiaji wa sheria za trafiki.

    Utekelezaji wa hatua hiyo kunafuatia agizo lililotolewa na Rais William Ruto mnamo Machi 2 kwamba Wizara ya Barabara na Uchukuzi na NTSA zitekeleze mpango wa kutoza faini za papo hapo ndani ya mwezi mmoja.

  13. Mjumbe wa China yuko Saudia kusuluhisha vita vya Iran

    .

    Chanzo cha picha, Charly Triballeau via Getty Images

    Mjumbe maalum wa serikali ya China anayeshughulikia masuala ya Mashariki ya Kati Zhai Jun ametembelea Saudi Arabia kama sehemu ya upatanishi wake kutokana na vita kati ya Marekani na Israeli dhidi ya Iran, akisema Beijing iko tayari kushirikiana na Riyadh katika "juhudi endelevu za kudumisha amani na utulivu katika eneo la Ghuba".

    Zhai, ambaye aliielezea China kama "rafiki mzuri na mshirika wa Saudi Arabia", anafanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudi Arabia Faisal bin Farhan Al Saud na Katibu Mkuu wa Baraza la Ushirikiano la Ghuba (GCC) Jasem al-Budaiwi.

    Katika mkutano na mwana mfalme Faisal siku ya Jumatatu, Zhai alielezea "wasiwasi mkubwa kuhusu mvutano wa sasa katika eneo hilo" na akasema kwamba uhuru, usalama, na uadilifu wa eneo la mataifa ya Ghuba haupaswi kukiukwa na "shambulio lolote dhidi ya raia wasio na hatia linapaswa kulaaniwa".

    Zhai pia alirejelelea wito wa Beijing wa "kusitishwa mara moja kwa shughuli za kijeshi".

    Wakati huo huo, G7 kujadili kutolewa kwa pamoja kwa akiba ya mafuta ya dharura

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Kama tulivyokufahamisha awali, bei ya mafuta imepanda na kufikia kiwango $100 kwa pipa moja kwa mara ya kwanza tangu 2022, ingawa bei hiyo imeshuka kidogo tu tangu wakati huo.

    Sasa, Financial Times inaripoti kwamba mawaziri wa fedha wa G7 watafanya mkutano wa dharura leo Jumatatu kujadili uwezekano wa kutolewa kwa pamoja kwa akiba ya mafuta ili kukabiliana na ongezeko la bei.

    Akiba ya mafuta inaratibiwa na Shirika la Nishati la Kimataifa (IEA), huku wanachama 32 wa kundi hilo wakishikilia akiba muhimu kama sehemu ya mfumo wa kukabiliana na dharura wa pamoja ulioundwa kwa ajili ya migogoro ya bei ya mafuta.

    Nchi tatu za G7, ikiwa ni pamoja na Marekani, hadi sasa zimeonyesha kuunga mkono uwezekano wa kutolewa kwa pamoja mafuta hayo, kulingana na watu wanaofahamu mazungumzo hayo, FT inaripoti.

    Soma zaidi:

  14. Bei ya mafuta yapanda huku hisa zikishuka kutokana na vita vya Iran

    .

    Chanzo cha picha, Anadolu via Getty Images

    Bei ya mafuta duniani imepanda zaidi ya dola 110 (£82.74) kwa pipa na masoko ya hisa yameshuka huku vita vinavyoendelea kati ya Marekani na Israel dhidi ya Iran vikizidi kuongeza hofu ya kukatizwa kwa muda mrefu kwa usafirishaji kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz.

    Iran imemtaja Mojtaba Khamenei kumrithi baba yake Ali Khamenei kama Kiongozi Mkuu, ikiashiria kwamba wiki moja ya mapigano hayo ambayo bado yanaendelea, viongozi wenye msimamo mkali bado wanaongoza nchi hiyo.

    Marekani na Israel zilianzisha mawimbi mapya ya mashambulizi ya anga kote Iran mwishoni mwa juma, zikishambulia maeneo mengi ikiwemo maghala ya mafuta.

    Usumbufu mkubwa wa usambazaji wa nishati kutoka eneo hilo unatishia bei kupanda kwa watumiaji na biashara kote ulimwenguni.

    Kupanda kwa bei ya mafuta kunaweza pia kuongeza gharama ya bidhaa muhimu zinazotokana na mafuta kama vile mafuta ya ndege na nyenzo muhimu katika uzalishaji wa mbolea.

    Rais wa Marekani Donald Trump alijibu ongezeko la bei kwa kusema kwamba ongezeko la muda mfupi lilikuwa "gharama ndogo ya kulipa" kwa kuondoa tishio la nyuklia la Iran.

    Soma zaidi:

  15. Nyumba ya Rihanna yashambuliwa kwa risasi - Polisi

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Polisi wanasema nyumba ya nyota wa muziki wa pop, Rihanna huko Beverly Hills imeshambuliwa kwa risasi.

    Maafisa kutoka Idara ya Polisi ya Los Angeles walijibu ripoti za milio ya risasi saa 13:15 saa za eneo hilo (21:15 GMT) siku ya Jumapili. Mshukiwa alipatikana na kukamatwa.

    Afisa wa polisi alimwambia mshirika wa BBC nchini Marekani, CBS News, kwamba nyumba iliyolengwa ilikuwa ya Rihanna na kwamba maganda ya risasi yalipatikana katika eneo la tukio.

    Hakuna mtu aliyejeruhiwa katika tukio hilo. Rihanna alikuwa katika jumba hilo la kifahari wakati huo, chanzo cha afisa wa usalama kiliambia Los Angeles Times.

    Polisi wanasema mshukiwa, mwanamke mwenye umri wa miaka 30, alisimamisha gari nje ya nyumba hiyo na kufyatua risasi saba kabla ya kuondoka kwa kasi.

    Gari lake lilipatikana umbali wa maili nane (kilomita 12) kutoka nyumbani kwa mwimbaji huyo, ambapo mwanamke huyo alikamatwa. Bado hajatambuliwa hadharani.

    Septemba mwaka jana, nyota huyo alijifungua mtoto wake wa tatu, msichana, na mpenzi wake A$AP Rocky.

    Wawili hao, ambao pia wana watoto wawili wa kiume Riot na RZA, walitangaza ujauzito wa hivi karibuni wa Rihanna katika tamasha la Met Gala mwaka jana.

    Pia unaweza kusoma:

  16. IRGC iko 'tayari kumtii kikamilifu' Kiongozi Mpya Mkuu - vyombo vya habari vya Iran

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Shirika la Utangazaji la serikali ya Iran (Irib) na shirika la habari la Tasnim, linaloungwa mkono na IRGC, yote yametoa taarifa iliyotolewa kwa Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya kukaribisha uteuzi wa Mojtaba Khamenei.

    Taarifa hiyo inamuelezea Khamenei kama "mwanasheria mwenye ujuzi, mtaalamu na mwenye ufahamu mzuri zaidi katika masuala ya kisiasa na kijamii".

    Jeshi la Iran( IRGC) pia limetangaza "kuheshima, kujitolea na kutii" kiongozi wake mpya Khamenei, likisema kwamba wanachama wake "wako tayari kumtii kikamilifu na kujitolea katika kutekeleza amri takatifu za Mwanasheria Kiongozi".

    IRGC ni kikosi cha jeshi chenye jukumu la kulinda na kuhifadhi Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, na lina ushawishi katika masuala yote kuanzia usalama hadi uchumi.

    Soma zaidi:

  17. Marekani na Israeli huenda zikapinga uteuzi wa Mojtaba Khamenei

    .

    Chanzo cha picha, IRINN

    Katika wiki iliyopita, na tena mapema hii leo, Rais wa Marekani Donald Trump amesema alitaka kuchangia katika uteuzi wa kiongozi mpya mkuu wa Iran.

    Ingawa aliashiria kwamba angekuwa wazi kwa mtu anayehusishwa na uongozi wa zamani kuchukua madaraka, alipinga peupe mtu huyo kuwa Mojtaba Khamenei - ambaye amethibitishwa tu kuwa mrithi wa baba yake.

    "Mtoto wa Khamenei simkubali," Trump alisema mapema wiki hii. Na saa chache tu zilizopita, alisema kwamba, bila idhini yake, Yeyote atakayechukua nafasi hiyo "hatadumu kwa muda mrefu".

    Israeli ilitoa onyo kabla ya mtoto wa pili wa Khamenei kuthibitishwa kuwa kiongozi mkuu mpya - ikisema kwamba "itaendelea kumfuatilia kila mrithi" wa marehemu Ayatollah.

    Soma zaidi:

  18. Mojtaba Khamenei achaguliwa kuwa kiongozi mkuu mpya wa Iran

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Baraza la Wataalamu la Iran limemchagua Mojtaba Khamenei kuchukua nafasi ya baba yake, Ayatollah Ali Khamenei, kama kiongozi mkuu mpya wa nchi hiyo, vyombo vya habari vya serikali vinaripoti.

    Jinsi uteuzi wa Khamenei ulivyotangazwa

    Taarifa kutoka kwa Bunge la Wataalamu ilisomwa kwa sauti na mtangazaji kwenye Televisheni ya serikali:

    "Licha ya hali mbaya ya wakati wa vita na vitisho vya moja kwa moja vya maadui dhidi ya taasisi hii maarufu, na licha ya kulipuliwa kwa ofisi za Sekretarieti ya Baraza la Wataalamu, na kusababisha vifo vya wafanyakazi kadhaa na wanachama wa timu yake ya usalama, hawakusita hata kidogo katika mchakato wa kumchagua na kuanzisha uongozi wa mfumo wa Kiislamu."

    Mtangazaji alipaza sauti “Allahu Akbar, Allahu Akbar, Khamenei ndiye kiongozi.”

    Kiongozi mpya aliyechaguliwa licha ya vitisho - Mkuu wa Usalama wa Iran

    Katibu wa Baraza Kuu la Usalama la Taifa la Iran amelishukuru Baraza la Wataalamu kwa kumchagua mrithi wa Ali Khamenei licha ya "tishio la Trump kulishambulia kwa bomu", kulingana na mashirika mengi ya habari ya Iran.

    Ali Larijani anasema "maadui" wa Tehran walidhani nchi "itakuwa katika hali ya mkwamo" kufuatia kifo cha Ali Khamenei lakini hatimaye Bunge limeendelea na uteuzi wa Mojtaba Khamenei.

    Soma zaidi:

  19. Hujambo na karibu katika matangazo yetu mubashara ya tarehe 09/03/2026.