Maelezo ya picha, Wagombea wa Urais Kennya, kutoka kushoto, William Samwei Ruto, Mwaihiga Mwaure, Raila Odinga na George WajackoyahMaelezo kuhusu taarifa
Author, Na Mohammed AbdulRahman.
Nafasi, Mchambuzi
Uchaguzi mkuu wa Kenya uliopangwa kufanyika Agosti 9, 2022 ni suala linalofuatiliiwa kwa karibu na kwa kuzingatia kwamba matokeo yatakuwa na athari kubwa. Kenya ambalo ni Taifa kubwa kubwa zaidi kiuchumi miongoni mwa mataifa ya Afrika Mashariki, litamchagua rais mpya wa tano na viongozi wengine wa uwakilishi huku mafanikio ya uchaguzi huo yakitarajiwa kuwa dira ya demokrasia, ambayo imezorota katika nchi kadhaa jirani.
Viongozi wa baadhi ya mataifa katika kanda ya AfrikaMashariki wamezifanyia marekebisho katiba zao zilizokuwa awali na ukomo wa utawala wa miaka kumi na kuondoa kikomo hicho ili kujifungulia njia ya kuwawezeshaa kubakia madarakani kwa muda mrefu zaidi. Hao ni Pamoja na viongozi wa Uganda na Rwanda. Rais Kagame wa Rwanda aliwahi kusema wakati wa mabadiliko ya katiba yaliyomruhusu kuongoa zaidi ya miwili kuwa uamuzi huo ni kuzingatia matakwa ya Wanyarwanda walimuomba kufanya hivyo.
Kenya ni nchi iliyoheshimu katiba yake na Rais Uhuru Kenyatta anasubiri kumkabidhi madaraka yule atakayekuwa mrithi wake, mshindi wa uchaguzi huo. Washindani wawili wakuu ni Wazri mkuu wa zamani, Rais Odinga, aiyeteuliwa na Muungano wa Azimio la Umoja, akiungwa mkono na Uhuru Kenyatta awe mrithi wake. Chama cha Jubilee cha Kenyatta ni sehemu ya Azimio la Umoja. Mpinzani wake ni Makamu wa Rais William Ruto, mgombea wa Muungano wa Kenya Kwanza, aliyehitilafiana na Kenyatta.
Uamuzi wa Kenyatta wa kuheshimu katiba ni jambo la kupongezwa, lakini sababu kubwa ni uhuru wa mahakama ambayo ni taasisi ya kusimamia sheria. Itakumbukwa yaliotokea katika uchaguzi wa 2017, wakati Jaji mkuu wa wakati ule, David Maraga alipotangaza kwamba matokeo ya uchaguzi ni batili kufuatia dosari zilizotokea katika uchaguzi huo hilo. Hatua ya mahakama kuu ilitokana na malalamiko yaliowasilishwa na mgombea wa upinzani Raila Odinga. Pia pamoja na kampeni kali ya uchaguzi wagombea wote wakuu Raila Odinga na William Ruto wametoa wito wa amani kuliepusha taifa na janga la machafuko ya uchaguzi wa 2007/2008.
Ujumbe kwa Tanzania
Mafanikio ya uchaguzi ujao nchini Kenya yatakuwa na ujumbe mahsusi kwa jirani yake mkubwa Tanzania ambayo tangu iliporudi kwenye mfuo wa vyama vingi vya siasa 1992 na kufuatiwa na uchaguzi wa kwanza 1995, mchakato wa uchaguzi umedhibitiwa na serikali ya Chama cha Mapinduzi (CCM). Matokeo yake ni kushindwa kuimarika kwa taasisi muhimu katika ujenzi wa demokrasia imara, huku nguzo kuu ikiwa ni mahakama.
Wanaharakati wamekuwa wakitaja sababu za kutopatikana mafanikio kuwani Pamoja na Rais kuwa na madaraka ya kupita kiasi yakimpa nguvu miongoni mwa mengine kuteua Tume ya Uchaguzi, inayoangaliwa kuwa ni mzizi wa kutopatikana haki katika uchaguzi. Tume ya Uchaguzi huteuliwa na Rais na matokeo ya uchaguzi wa Rais yanapotangazwa hayawezi kupigwa kama ilivotokea Kenya 2017.
Wanaharakati wanadai dawa mjarab ni kuwepo Katiba mpya itakayofungua njia ya kupatikana Tume Huru ya Uchaguzi itakayosimamia uchaguzi huru na wa haki. Tanzana ilishuhudia uamuzi wa mpiga kura kutoheshimiwa, baada ya nguvu ya dola kutumika kuhakikisha matokeo ya uchaguzi yanakipa ushindi mkubwa chama tawala CCM na kuvikandamiza vyama vya upinzani. Wadadisi wanaueleza uchaguzi wa 2020 wakati wa uongozi wa Rais John Pombe Magufuli aliyefariki Machi 2021 kuwa ndiyo uliokuwa mbaya kabisa kuwahi kuonekana tangu Tanzania irejeshe mfumo demokrasia ya vyama vingi vyama siasa.
Haya hivyo, viongozi kadhaa wa serikali ya chama tawala CCM mara kadhaa wamekuwa wakisema kuwa uchaguzi ulifanyika kwa kufuata taratibu zote na kwamba wanaolalamika wafungue mashauri mahkamani.
Mrithi wa Magufuli, Rais Samia Suluhu Hassan aliyeingia madarakani Machi 19, 2021 baada ya kifo cha mtangulizi wake, sasa anaonekana kubadili dira. Wakati Magufuli aliondoa uwezekano wa kuwa na Katiba mpya akisisitiza sio kipaumbele bali muhimu ni maendeleo, Rais Samia Suluhu Hassan ameonesha ishara ya kulizungumzia suala la katiba mpya na kupata baraka za chama chake tawala.
Wengi wanaashira kuwa pindi uchaguzi wa Kenya utafanyika katika hali iliyo shwari, utakuwa chachu katika mchakato wa kuimarishwa demokrasia nchini Tanzania. Wakisifia mafanikio yaliopatikana chini ya uongozi wa Rais Samia katika kipindi kifupi, katika sekta mbali mbali, raia wa kawaida nchini humo wamekuja na msemo " Mama anaupiga mwingi" wakilinganisha na mchezo maridadi wa kandanda.
Swali linalosalia ni je kweli atahakikisha anamaliza kiu ya Watanzania kutaka katiba mpya itakayowafungulia mlango wa kuwa na demokrasia imara zaidi?
Miongoni mwa mafanikio yake mengine ni kurekebisha haraka uhusiano wa kidugu na Kenya ambao ulizorota kipindi cha Rais Magufuli. Hatua yake imeipa msukumo mkubwa biashara ya nchi hizi mbili, na pasina shaka anatarajia kuendeleaa ushirikiano huo na yeyote atakayeibuka kuwa mshindi.
Nani yuko kwenye kinyang'anyiro cha kuiongoza Kenya ?
Fahamu zaidi kuwahusu wagombea urais wa Kenya
Chagua mgombea ili kutazama wasifu wake
Raila Amollo Odinga
Muungano wa Azimio la Umoja
Mgombea huyo mwenye umri wa miaka 77 ni mhandisi aliyesomea Chuo Kikuu cha Ufundi cha Magdeburg (sasa kinajulikana kama Chuo Kikuu cha Otto-von-Guericke Magdeburg) nchini Ujerumani.
Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya Azimio la Umoja One Kenya Coalition Party.
Hili litakuwa jaribio lake la tano baada ya kugombea katika: 1997, 2007, 2013 na 2017.
Bw Odinga alikuwa mmoja wa wapiganiaji wa demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya. Alikamatwa, akafungwa na wakati fulani akaenda uhamishoni kwa sababu ya kupigania haki hiyo
Aliwahi kuwa Waziri Mkuu, kuanzia 2008-2013.
Odinga alihusika kufanikisha miradi mikubwa iliyotekelezwa na serikali ya Kibaki, kama vile miradi ya umeme vijijini na barabara.
Kuafikia ukuaji wa uchumi wa tarakimu mbili kupitia uwekezaji katika biashara ndogo ndogo na sekta ya viwanda.
Utoaji wa huduma bora za afya kwa wote.
Utoaji wa vifaa vya michezo na burudani kwa ukuaji wa kimwili, kiakili, kijamii, kimaadili na maendeleo ya watu.
Kufuatia jaribio la mapinduzi ya Agosti 1, 1982, Raila Odinga alikamatwa na kukabiliwa na mashtaka kadhaa, yakiwemo ya uhaini ambayo alizuiliwa bila kufunguliwa mashtaka. Tume ya Ukweli ya Haki na Maridhiano iliambiwa mwaka 2011 kwamba Odinga alikuwa na mawasiliano na mpangaji mkuu wa mapinduzi hayo. Odinga amekana kuhusika kila mara. - Makavazi ya Kitaifa ya Kenya.
William Samoei Ruto
Muungano wa Kenya Kwanza
Mgombea huyu mwenye umri wa miaka 55 ana Shahada ya Uzamifu/PhD katika Ikolojia ya Mimea na BSc katika Botany na Zoology kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi.
Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya chama cha United Democratic Alliance ( chenye mafungamano na Kenya Kwanza).
Aliongoza Vuguvugu la vijana la Youth for Kanu '92 (YK'(92).
Wizara yake iliorodheshwa kama inayofanya bora zaidi serikalini alipokuwa Waziri wa Kilimo.
Alihudumu kama Naibu Rais wa kwanza wa Kenya chini ya katiba mpya ya 2010.
Alihudumu kama mbunge wa eneo bunge la Eldoret Kaskazini kuanzia 1997-2007.
Kutenga $424 milioni kila mwaka kwa biashara ndogo ndogo za kati.
Kuanzisha mfuko wa elimu wa kitaifa ili kukidhi gharama zisizo za masomo.
Tekeleza kikamilifu sheria ya usawa wa kijinsia ya thuluthi mbili katika uteuzi wa kisiasa na kutenga nusu ya baraza lake la mawaziri kwa wanawake.
Mnamo 2008, Mahakama Kuu ya Kenya iliamuru Naibu Rais William Ruto kusalimisha shamba la ekari 100 na kulipa $ 62,500 kwa Adrian Muteshi, mkulima ambaye alimshtaki kwa kuchukua mali hiyo baada ya uchaguzi wa 2007. - Kenya Law
Mnamo 2011, Bw Ruto alikabiliwa na kesi kwa makosa matatu dhidi ya binadamu: Mauaji, uhamisho wa watu kwa lazima na mateso ya watu katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu. Miaka mitano baadaye mahakama ilisitisha kesi hiyo kwa msingi kwamba - ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa dhaifu. -ICC
George Wajackoyah
Chama cha Roots
Profesa huyo mwenye umri wa miaka 61 ana shahada ya uzamili katika sheria kuhusu maendeleo kutoka Chuo Kikuu cha Warwick na shahada ya uzamili , sheria (sheria za Marekani kutoka Chuo Kikuu cha Baltimore.
Bw Wajackoyah anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Roots Party.
Alihudumu kama Inspekta katika idara ya usalama ya Special branch wakati wa utawala wa marehemu Rais Daniel Moi kabla ya kulazimika kutorokea ng'ambo ili kuepuka kufunguliwa mashtaka na mamlaka.
Yeye ni mshirika katika kampuni ya mawakili aliyoianzisha mwaka wa 2018.
Alifunnza somo la sheria na uchumi katika vyuo vikuu vya Marekani, Uingereza na Kenya.
Kuhalalisha matumizi ya kiviwanda ya bangi
Badilisha siku za kazi hadi Jumatatu hadi Alhamisi.
Huduma ya afya ya bure na msaada kwa wazee, walio hatarini na wajawazito
David Mwaure Waihiga
Chama cha Agano
David Mwaure anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Agano.
Ni kiongozi wa Chama cha Agano.
Alihitimu na shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi na ana Shahada ya Uzamili katika masomo ya uongozi.
Yeye ni wakili mkuu na amehudumu kama mwanasheria kwa zaidi ya miongo mitatu.
Ana kampuni ya uwakili na amewania viti mbalimbali vya kisiasa.
Ilianzishwa chama cha Agano mwaka 2006.
Kupambana na ufisadi uliokithiri.
kuunda nafasi za ajira.
Kurejesha mali ya Kenya iliyofichwa nje ya nchi.
Pata maelezo zaidi kuhusu sera za wagombea urais hapa
Matumaini ya nchi nyingine za Kanda
Kenya ni nchi muhimu panapohusika biashara ya kanda, kwa sababu ya kutumiwa kwa bandari yake ya Mombasa na wengi wa majirani zake. Kwa mfano Uganda isiyo na bahari inategemea kwa kiwango kikubwa bandari ya Mombasa kwa usafirishaji wa bidhaa inazosafirisha kwenda nje na zile inazoagiza kutoka ng'ambo. Kenya ni mshirika mkubwa wa biashara wa Uganda na Wagombea wote wawili wakuu; Raila ana Ruto walikwenda Kampala kwa nyakati tafauti kuonana na Rais Museveni, tukio linaloashiria kila mmoja anatafuta kuungwa mkono na kiongozi huyo jirani na mkongwe.
Rwanda ni nchi nyingine ambayo inategemea kwa upana mkubwa uagizaji bidhaa kutoka Kenya. Kwa mujibu wa takwimu za 2019, Rwanda iliagiza bidhaa za thamani za dola milioni 278.45 za Marekani kutoka Kenya.
2021 Burundi mwanachama mwengine wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ilisaini mkataba wa kuimarisha ushirikiano wa biashara na maendeleo Kenyatta. Tangu ilipojiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki Aprili 2022, Jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo (DRC) imeonesha ishara ya kufungua zaidi milango ya kiuchumi kwa wawekezaji.
Kenya imekuwa kipaumbele kwa kwa serikali ya Rais Felix Tshisekedi. Mwishoni mwa 2021 ujumbe wa wafanya biashara wa nchi hizo mbili ulikutana nchini Kongo kutathmini nafasi za uwekezaji na kibiashara.
Sambamba na Kongo inaizingatia Kenya kuwa mshirika wa kuaminika katika kusimamia amani nchini humo. Mbali ya wanajeshi wa Kenya kushiriki katika ujumbe wa amani wa Umoja wa Mataifa (MONUSCO), Rais Uhuru Kenya alianzisha juhudi mwezi Aprili za kuundwa kikosi cha mataifa ya Jumuiya ya Afrika Masharki, kulisaidia jeshi la Kongo, kufuatia mashambulio mapya ya kijeshi ya waasi wa M23.
Lakini hadi sasa kuundwa kwa kikosi hicho kunakabiliwa na kizingiti kutokana na Kongo kukataa kabisa Rwanda isiwemo katika kikosi hicho ikiishutumu kuwaunga mkono waasi hao, madai ambayo Rwanda inaendelea kuyakanusha.
Kenya kwa hivyo inabakia mshirika muhimu wa kanda kibiashara na kiuchumi na yeyote Hapana shaka yeyote atakayemrithi Rais Uhuru Kenyata, iwe ni Raila Odinga au William Ruto atakuwa na wajibu wa kuendeleza ushirika. Matumaini ya wakaazi katika kanda hii sawa na wakenya kwa jumla, ni kwamba uchaguzi wa Agosti 9, 2022 utakuwa wa amani na utulivu.
Kwa wanaharakati katika nchi jirani wana matarajio kwamba Kenya itakuwa pia na nafasi kubwa ya kuwa usukukani sio tu wa kiuchumi lakini wa kisiasa, panapohusika na vuguvugu lao la kupigania demokrasia na haki za binadamu katika nchi zao.