'Mtego wa kundi la Hamas' wanasa wanajeshi wa Israel

Chanzo cha picha, IDF
Vyombo vya usalama vya Israeli vimegundua kuwa wanamgambo wa Palestina wamekuwa wakitumia majina feki na utambulisho bandia kwenye mitandao, kuwadanganya wanajeshi wa Israeli kwamba ni wapenzi wanaotaka uhusiano nao huku wakiwa na lengo la kupata taarifa za kijasusi.
Kundi la wanamgambo la Hamas ndilo linalodaiwa kupanga njama hiyo iliyowanasa baadhi ya wanajeshi hao wa Israel.
Lengo la mbinu hiyo ni kuhakikisha mahusiano hayo yanaimarika halafu wanabembelezwa waingie kwenye tovuti mahsusi ambazo kisha wanapoteza kabisa udhibiti wa simu zao.
Huku wakifanikiwa kurekodiwa na picha za wanajeshi hao kuchukuliwa bila wao kujua.
Hata hivyo duru za kiusalama za Israel zimefafanua kuwa, ingawa visa hivyo vinatishia usalama, hali imedhibitiwa punde tu ujanja huo ulipogunduliwa.

Chanzo cha picha, IDF
Baadhi ya wanajeshi walioingia katika mtego huo ni wale wa vyeo vya chini na kwamba wadukuzi walilenga kupata habari kuhusu jeshi la Israel, silaha katika eneo linaloshikiliwa na Hamas katika ukanda wa Gaza.
Afisa ambaye jina lake halikutajwa anasema kuwa picha hizo zilizotumika katika njama hiyo ni za wanawake ambao picha zao ziliibwa katika mitandao.








