Bayern yaibebesha Arsenal 5

Bayern Munich imeichapa Arsenal kwa mabao 5-1 katika duru ya kwanza ya UEFA Klabu Bingwa Ulaya nchini Ujerumani.

UEFA

Chanzo cha picha, Matthias Schrader

Maelezo ya picha, Thiago alin'gara katika mchezo huo

Arjen Robben aliiandikia Bayern Munich bao la kwanza katika dakika ya 11 tu ya mchezo baada ya kuvunja ngome ya Arsenal na kuachia mkwaju mkali.

Arsenal walipigana kufa na kupona, huku Alexis Sanchez akijituma, na kupata matunda katika dakika ya 30, baada ya kufunga bao la kusawazisha. Bao hilo limefungwa baada ya kukosa mkwaju wa penati.

Sanchez

Chanzo cha picha, Reuters / Michaela Rehle Livepic

Maelezo ya picha, Alexis Sanches, alipachika bao pekee la Arsenal

Bayern Munich walirejea kwa kasi katika kipindi cha pili na kufunga mabao manne. Mabao hayo yote yalipatikana baada ya beki Laurent Koschielnly wa Arsenal kutoka akiwa majeruhi.

Robert Lewandowski alifunga bao la pili katika dakika ya 53. Thiago akifunga mabao mawili katika dakika za 56 na 63. Thomas Muler aliyeanzia benchi, aliingia na kupiga msumari wa mwisho katika dakika ya 88.

Arsenal sasa wana mlima mkubwa wa kupanda katika mchezo wa marudiano utakaochezwa kwenye dimba la Emirates.

REAL MADRID YASHINDA

Katika mchezo mwingine, Real Madrid waliojikuta wamefungwa bao katika dakika ya 8 tu wakicheza na Napoli.

Real Madrid

Chanzo cha picha, Reuters / Juan Medina Livepic

Maelezo ya picha, Pepe Reina wa Napoli akitazama baada ya Casemiro kufunga bao la tatu

Hata hivyo vijana wa Zinedine Zidane walizinduka na kupata ushindi wa mabao 3-1 baada ya kipyenga cha mwisho. Mabao ya Karim Benzima, Toni Kroos na Casemiro yaliipa Real matumaini ya kucheza robo fainali.