Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Afrika Kusini yamtimua Balozi wa Israel nchini humo
Ariel Siedman amepewa saa 72 kuondoka Afrika Kusini, kwa mujibu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya nchi hiyo.
Muhtasari
- Afrika Kusini yamtimua Balozi wa Israel nchini humo
- Trump: Ni 'hatari' kwa Uingereza kushirikiana na China kibiashara
- Mwanamke azirai kwa kupigwa viboko 140 kisa kushiriki mapenzi nje ya ndoa Indonesia
- Umoja wa Afrika wataka vikosi vinavyozozana eneo la Tigray 'kujidhibiti'
- Fela Kuti awa Mwafrika wa kwanza kutunukiwa Tuzo ya Mafanikio ya Maisha ya Grammy
- Viongozi wa Chad na Ufaransa wakubaliana kuimarisha uhusiano wao
- Jeshi la Uganda lazua mjadala kwa madai dhidi ya Ubalozi wa Marekani
- Tanzania yapanga kuuza sehemu ya akiba ya dhahabu kusaidia kufadhili miradi ya miundombinu
- Shambulio baya la wanajihadi laua makumi ya watu Nigeria, wakiwemo wanajeshi
- Jenerali Kainerugaba akiri kumshinikiza mke wa Bobi Wine kuwafahamisha alipo mumewe
- Waziri wa Ulinzi wa Marekani asema jeshi lipo tayari kutekeleza uamuzi wowote wa Trump kuhusu Iran
- Trump asema Putin hatashambulia miji ya Ukraine kipindi hiki cha baridi
- Iran yafanya mazoezi ya kijeshi kwenye mkono wa bahari wa Hormuz
- Trump atishia kutoza ushuru kwa mataifa yanayouza mafuta kwa Cuba
- Trump aonya kuwa ni "hatari sana" kwa Uingereza kushirikiana na China
- Rais Traoré 'afuta' vyama vyote vya siasa Burkina Faso
Moja kwa moja
Na Mariam Mjahid & Beldeen Waliaula
Trump amteua Kevin Warsh kusimamia Benki Kuu ya Marekani
Rais wa Marekani Donald Trump, amemteua Kevin Warsh, kuwa Mwenyekiti wa Benki Kuu ya Marekani.
Trump amekuwa akimtafuta mrithi wa mwenyekiti wa benki hiyo Jerome Powell, ambaye amemshambulia marakwa mara kwa kushindwa kupunguza viwango vya riba kwa haraka.
''Nimemjua Kevin kwa muda mrefu, na sina shaka kuwa atakuwa mweyekiti mzuri wa Benki Kuu kuwahi kutokea',' Trump aliandika kwenye mtandao wake wa kijamii wa Truth Social.
Hatamu ya uongozi wa Powell unakamilika mwezi Mei.
Warsh atahitajika kuchunguzwa na kuidhinishwa na bunge la Senate kabla ya kuanza kuhudumu katika nafasi hiyo.
Trump awali alikuwa amejaribu kumuondoa gavana wa benki kuu Lisa Cook na utawala wake kuanza kumchunguza Powell kwa ubadhirifu wa fedha alizotumia kukarabati benki hiyo na kuzua maswali kuhusu uhuru wa kujisimamia kwa benki hiyo kuu.
Syria yafikia makubaliano na vikosi vinavyoongozwa na Wakurdi
Wapiganaji wa Kikurdi wamekubali kujiunga na jeshi la Syria na asasi zao za kiraia kugeuzwa kuwa za serikali.
Washington kupitia mjumbe wake Tom Barrack, imesema makubaliano hayo ni ya kihistoria.
Katika wiki za hivi karibuni vikosi vya Syrian Democratic Forces (SDF) vilikuwa vimeachia maeneo kadhaa wanayodhibiti kwa jeshi la serikali ya Syria.
Vikosi vya SDF vilikuwa na ukaribu na Marekani, ila tangu kuondolewa madarakani kwa Bashar al- Assad mwaka wa 2024, Marekani imeanza kupendelea serikali ya Syria mjini Damascus.
Mapema mwezi huu baada ya jeshi la SDF kupoteza udhibiti wa maeneo mengi kwa jeshi la Syria, walikubali kusitisha makabiliano na kujiunga na serikali ya taifa hilo.
Katika makubaliano hayo yenye vipengele14, SDF watajiondoa kabisa kutoka maeneo wanayodhibiti na kujiunga na serikali huku asasi za raia zikigeuzwa kuwa za serikali.
Jeshi la Syria pia litazindua vitengo tofauti vitakavyoongozwa na vikosi vya SDF.
Katika ujumbe uliochapishwa kwenye mtandao wa X, haki za kiraia na elimu za jamii ya waKurdi zitaheshimiwa, na wale waliokimbia makwao wanauhuru wa kurejea nyumbani.
Magereza, na mapipa ya mafuta na gesi ambayo yalikuwa chini ya SDF, sasa yataongozwa na serikali ya Syria.
Katika makabiliano yao ya awali, jeshi la Syria lilichukua udhibiti wa mapipa ya mafuta ya Omar na Tabqa karibu na mto Euphrates.
Wakurdi walikuwa wanatawala zaidi ya theluji moja ya Syria na walikuwa wakiungwa mkono na Marekani, baada ya kuwasaidia kukabiliana na kundi la kigaidi la Islamic State (IS).
Makubaliano haya yameleta mabadiliko makubwa katika uongozi wa Syria tangu kuondolewa madarakani kwa Bashar al-Assad mwaka wa 2024, na kumaliza vita vya wenyewe kwa wenyewe ambavyo vilikuwa vimedumu kwa takriban miaka kumi na tatu.
Soma:
Afrika Kusini yamtimua Balozi wa Israel nchini humo
Serikali ya Afrika Kusini imempa balozi wa Israel nchini humo makataa ya saa 72 kuondoka.
Idara ya mambo ya kigeni ya Afrika Kusini, imesema hatua hiyo imetokana na ‘'ukiukwaji wa kanuni za kidiplomasia ambazo zinatishia uhuru wa taifa la Afrika Kusini.’'
Katika taarifa iliyotelewa na idara hiyo, Afrika Kusini inaishtumu Israel kwa kutumia mitandao yake ya kijamii kumshambulia rais wa taifa hilo Cyril Ramaphosa.
Aidha taarifa hiyo pia inasema, ubalozi huo wa Israel, haukuwafahamisha serikali ya Afrika kusini kuhusu ziara ya maafisa wakuu wa Israel nchini humo.
Afrika Kusini inasema hatua hiyo inakiuka uhuru wa kidiplomasia na kukandamiza uaminifu walionao katika uhusiano wao wa kimataifa.
Balozi wa Israel nchini Afrika Kusini Ariel Seidman, amepewa siku tatu kuhama nchi hiyo.
Uhusiano kati ya Israel na Afrika Kusini umekuwa ukiyumbayumba baada ya taifa hilo kuishtaki Israel katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ), mwaka wa 2023, kwa tuhuma za kutekeleza mauji ya kimbari katika eneo la Gaza madai ambayo Israel ilikanusha.
Pia unaweza kusoma:
Trump: Ni ‘hatari’ kwa Uingereza kushirikiana na China kibiashara
Rais wa Marekani Donald Trump amesema kuwa ni ‘hatari’ kwa Uingereza kuwa na ushirikiano wa kibiashara na China.
Hii inajiri wakati ambapo waziri mkuu wa Uingereza yuko katika siku ya tatu ya ziara yake nchini China.
China na Uingereza zilitangaza kuimarisha ushirikiano wao baada ya Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer kukutana na rais wa China Xi Jinping.
Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa filamu ya mkewe Melania Trump, Trump alisema Rais Xi ni rafiki yake na anamfahamu vyema.
Waziri wa biashara wa Uingereza Bwana Chris Bryant, alisema itakuwa makosa kwa Uingereza kupuuza nafasi ya China katika jukwaa la kimataifa.
'‘Tumeingia katika mkataba na China tukiwa macho,’' alisema Waziri huyo akiongeza kuwa Rais Trump anatarajiwa kuzuru China mwezi Aprili.Starmer yuko mjini Shanghai hii leo kabla ya kuelekea nchini Japan kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa Japan Sanae Takaichi.
Maelezo zaidi:
Mwanamke azirai kwa kupigwa viboko 140 Indonesia- Kunani?
Wanandoa wawili nchini Indonesia wamepigwa viboko mara 140 kwa kufanya mapenzi nje ya ndoa ambayo ni makosa au haram katika sheria za dini ya kiislamu.
Mwanaume na mwanamke hao walipigwa viboko hivyo hadharani.
Mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 21, alizirai baada ya kupigwa viboko hivyo katika wilaya ya Aceh.
Maafisa watatu wa polisi walimpiga viboko kwa zamu mwanamke huyo, aliyekuwa akilia kwa maumivu.
Baada ya kuzirai, polisi walimsafirisha kwa kutumia ambulensi na kumuondoa katika eneo hilo.
Wawili hao walaidhibiwa siku ya Alhamishi pamoja na wengine wanne ikiwemo afisa mmoja wa polisi na mchumba wake ambao walipigwa viboko 23, baada ya kupatikana na hatia ya kuvunja sheria za dini ya Kiislamu maarufu Sharia.
Kupigwa viboko ni moja ya adhabu ambazo hupewa mtu anayevunja sheria za dini ya kiislamu katika wilaya ya Aceh, nchini Indonesia, ingawa adhabu hiyo inakoselewa sana kutokana na ukatili wake.
Katika sheria za dini ya Kiislamu wilaya ya Aceh, kufanya mapenzi nje ya ndoa, mtu hupewa adhabu ya viboko 100, na viboko 40 kwa kunywa pombe.
Wilaya ya Aceh, ndiyo wilaya pekee nchini Indonesia ambayo inashurutisha utiifu wa sheria za dini ya kiislamu na huwaadhibu wanaovunja sheria hizo kwa kuwapiga viboko mbele ya umati wa watu.
Maelezo zaidi:
Umoja wa Afrika wataka vikosi vinavyozozana eneo la Tigray ‘kujidhibiti’
Umoja wa Africa AU, umetoa wito kwa wapiganaji wa Tigray People’s Liberation Front (TPLF) na vikosi vya Ethiopia kujiepusha na matukio yatakayozua vita vingine katika eneo la Tigray.
Hali ya usalama inaripotiwa kudorora Tigray, baada ya vikosi vya serikali na na vile vya eneo hilo kuzozana kaskazini mwa Ethiopia.
Safari za ndege zilisitishwa siku ya alhamisi baada ya utovu wa usalama kuripotiwa eneo hilo karibu na mpaka wa Amhara.Katika taarifa, mwenyekiti wa tume ya umoja wa Africa (AUC) amezitaka pande zinazozozana eneo la Tigray nchini Ethopia kujizuia kupigana.
'‘Mwenyekiti wa AUC Mahmoud Ali Youssouf, anafuatilia kwa karibu jinsi hali ilivyo eneo la Tigray nchini Ethiopia, na ana wasiwasi kuhusu vurugu za hivi karibuni.’' ilisema taarifa iliyotolewa na AUS.
Mwenyekiti wa AUC alisisitiza umuhimu wa kuheshimu mikataba iliyofikiwa awali kuhusu kudumisha amani Eneo hilo.Mwaka wa 2022, umoja wa Africa uliwapatanisha serikali ya Ethiopia na wapiganaji wa TPLF na kutia saini mkataba wa kudumisha amani mjini Pretoria, Afrika Kusini.
Umoja wa Afrika unasema bado una imani na mkataba huo maarufu kama COHA na kusema iko tayari kuendelea kuunga mkono pande hizo mbili katika jitahada zao za kudumisha amani, na kuongezea kuwa iko tayari kufanya mazungumzo ili kuhakikisha amani inadumu eneo hilo.
Vita eneo la Tigray vilizuka mwaka wa 2020, na kuwauwa maelfu ya watu na wengine kuyakimbia makazi yao. Vita hivyo vilimalizika mwaka wa 2022.
Soma pia:
Fela Kuti awa Mwafrika wa kwanza kutunukiwa Tuzo ya Mafanikio ya Maisha ya Grammy
Gwiji wa muziki wa Nigeria, marehemu Fela Anikulapo Kuti—aliyetawazwa kwa muda mrefu na mashabiki wake kama mfalme wa Afrobeat—hatimaye anatambuliwa rasmi na tasnia ya muziki ya kimataifa.
Fela Kuti atatunukiwa Tuzo ya Mafanikio ya Maisha ya Grammy baada ya kifo chake, takribani miongo mitatu tangu alipofariki dunia akiwa na umri wa miaka 58.
“Fela amekuwa mioyoni mwa watu kwa muda mrefu sana. Sasa Grammys wametambua hilo, na huu ni ushindi maradufu,” anasema mwanawe, mwanamuziki Seun Kuti, alipolizungumza shirika la BBC.
Anaongeza kuwa hatua hiyo “inakamilisha simulizi la maisha ya Fela”.
Rikki Stein, rafiki wa karibu na meneja wa muda mrefu wa marehemu Fela Kuti, anasema kutambuliwa huko ni “bora kuchelewa kuliko kutofanyika kabisa”.
Kulingana naye, Afrika kwa muda mrefu haikuwa ikipewa uzito unaostahili katika vipaumbele vya tuzo hizo, ingawa hali hiyo sasa inaonekana kubadilika.
Kufuatia mafanikio ya kimataifa ya Afrobeats—mtindo wa kisasa uliovutiwa na sauti na falsafa ya Fela—Grammys zilianzisha kipengele cha Tuzo ya Uigizaji Bora wa Kiafrika (Best African Performance) mwaka 2024.
Mwaka huu pia, nyota wa Nigeria Burna Boy amepata uteuzi katika kipengele cha Albamu Bora ya Muziki wa Dunia (Best Global Music Album).
Hata hivyo, Fela Kuti ataweka historia kwa kuwa Mwafrika wa kwanza kabisa kupokea Tuzo ya Mafanikio ya Maisha ya Grammys, ingawa baada ya kifo chake.
Tuzo hiyo ilianza kutolewa mwaka 1963, ikianza na mwimbaji na muigizaji wa Marekani, Bing Crosby.
Wasanii wengine watakaotunukiwa tuzo hiyo mwaka huu ni pamoja na mpiga gitaa maarufu wa Marekani mwenye asili ya Mexico, Carlos Santana, Chaka Khan—anayefahamika kama Malkia wa Funk—pamoja na Paul Simon.
Familia ya Fela Kuti, pamoja na marafiki na washirika wake wa karibu, watakuwepo katika hafla ya Grammys kupokea tuzo hiyo kwa niaba yake. Kwa hakika, Fela Anikulapo Kuti hakuwa mwanamuziki tu.
Alikuwa mwanafikra wa kitamaduni, mpambanaji wa kisiasa na mbunifu mkuu wa muziki wa Afrobeat—mtindo ulio tofauti na Afrobeats ya kisasa, lakini ambao hatimaye uliweka msingi wake.
Akiungana na mpiga ngoma Tony Allen, Fela alianzisha Afrobeat kwa kuchanganya midundo ya Afrika Magharibi, jazz, funk, highlife, uimbaji wa maswali na majibu, ubunifu wa uchezaji mrefu wa ala, pamoja na mashairi yenye msimamo mkali wa kisiasa.
Katika taaluma yake iliyodumu kwa takribani miongo mitatu hadi alipofariki mwaka 1997, Fela Kuti alitoa zaidi ya albamu 50, akijenga urithi wa kazi uliounganisha muziki na itikadi, midundo na upinzani, na jukwaa la burudani na harakati za kijamii.
Hata hivyo, muziki wake pia ulimuingiza katika migogoro mikali na tawala za kijeshi zilizotawala Nigeria wakati huo—uthibitisho wa nafasi yake kama msanii aliyesimama bila kuyumba katika kutetea haki na uhuru wa watu.
Viongozi wa Chad na Ufaransa wakubaliana kuimarisha uhusiano wao
Mataifa ya Chad na Ufaransa yamekubaliana kuimarisha ushurikiano wao kwa kuheshimu maslahi ya kila mmoja, hii ikiashiria mwamko mpya wa uhusiano wao.
Uamuzi huo unafuatia kile wachambuzi wanakitaja kuwa '‘uhusiano baridi’' kati ya mataifa hayo mawili, baada ya Chad kujiondoa kwenye mkataba wa kiusalama kati yake na Ufaransa mwaka wa 2024.
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron alimualika kiongozi wa Chad Mahamat Deby, katika ziara ya kikazi na baadaye kufanya mazungumzo naye mjini Paris siku ya Alhamisi.
Katika taarifa ya pamoja, viongozi hao wawili walisema wamezungumzia maswala tofauti na wamekubaliana kuimarisha uhusiano wao haswa kiuchumi.
'‘Mazungumzo kati ya Ufaransa na Chad yataendelea, kuhakikisha tunatekeleza yale tuliokubaliana na kila upande unatimiza ahadi zake”
Wawili hao pia waliakubaliana kuhusu njia muafaka ya kufufua uhusiano wao wa awali, wakikuwa na matumaini na mkakati huu mpya.
Lakini bado haijabainika jinsi viongozi hao wawili watatatua kuvunjika kwa mkataba wao wa muda mrefu wa kiusalama, kwani swala la usalama halikuangaziwa katika taarifa ya pamoja walioitoa.
Viongozi hao wawili aidha walizungumzia kuhusu vita vya wenyewe kwa wenyewe vinavyoendelea nchini Sudan, wakitoa wito kwa pande mbili zinazozozana kusitisha vita hivyo.
Awali baada ya Chad kuvunja mkataba wa kiusalama waliokuwa nao na Ufaransa, wanajeshi wa Ufaransa waliokuwa nchini humo walitakiwa kuondoka mara moja, na kuzua wasiwasi kuhusu uhusiano kati ya mataifa hayo mawili.
Pia unaweza kusoma:
Jeshi la Uganda lazua mjadala kwa madai dhidi ya Ubalozi wa Marekani
Mwana wa Rais Yoweri Museveni na Kiongozi wa Majeshi ya Ulinzi ya Wananchi wa Uganda (UPDF), Jenerali Muhoozi Kainerugaba, usiku wa kuamkia leo amezua mjadala mpana katika mitandao ya kijamii baada ya kuchapisha mfululizo wa ujumbe akilaumu Ubalozi wa Marekani nchini Uganda kwa madai ya kumficha kiongozi wa upinzani, Robert Kyagulanyi Ssentamu, maarufu kama Bobi Wine.
Kyagulanyi alishika nafasi ya pili katika uchaguzi mkuu wa Januari 15, baada ya Rais Museveni, baba yake Jenerali Muhoozi, kutangazwa mshindi kwa ushindi mkubwa.
Jenerali Muhoozi, ambaye pia ni mshauri mkuu wa Rais Museveni kuhusu oparesheni maalumu za kijeshi, alidai kuwa uongozi wa sasa wa Ubalozi wa Marekani nchini Uganda ulihusika kusaidia Kyagulanyi kuondoka nyumbani kwake Magere, Wilaya ya Wakiso, wakati wa operesheni ya kijeshi iliyofanyika usiku wa Januari 16, 2026.
Katika ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wa X (zamani Twitter), Jenerali Muhoozi alisema:
“Wananchi wenzangu wa Uganda, kutokana na hali ya sasa ambapo kiongozi wa upinzani amejiteka mwenyewe na kutoweka, na kwa mujibu wa taarifa zetu bora za kijasusi, vitendo hivi vilifanyika kwa ushirikiano na uongozi wa sasa wa Ubalozi wa Marekani nchini mwetu. Kwa sababu hiyo, UPDF imesitisha ushirikiano wote na uongozi wa sasa wa Ubalozi wa Marekani jijini Kampala. Hii inajumuisha pia ushirikiano wetu nchini Somalia. Ushirikiano wa kiusalama uliokuwa wa thamani kubwa kati ya Uganda na Marekani umeathiriwa vibaya tangu mwaka 2015 na watendaji wa urasimu wasio na ubunifu katika ubalozi huo.”
Baadaye, Jenerali Muhoozi alifuta ujumbe huo na kutoa radhi kwa kauli zake.
Aidha, alionya kuwa nguvu yoyote ya kigeni itakayojaribu kumtorosha Kyagulanyi nje ya nchi italeta mgawanyiko mkubwa wa kidiplomasia kati ya Uganda na mataifa husika.
Hata hivyo, tarehe 24 Januari 2026, Robert Kyagulanyi alidai kuwa wanajeshi waliivamia makazi yake usiku, kuwashambulia wafanyakazi wake na kumkaba mke wake, Barbara Kyagulanyi, hali iliyomlazimu kutafuta matibabu.
Tukio hilo limezidi kuchochea mvutano wa kisiasa na kidiplomasia nchini Uganda, huku likizua maswali mapya kuhusu haki za kiraia, usalama na nafasi ya wahusika wa kimataifa katika siasa za ndani za taifa hilo.
Soma pia:
Tanzania yapanga kuuza sehemu ya akiba ya dhahabu kusaidia kufadhili miradi ya miundombinu
Serikali ya Tanzania imepanga kuuza sehemu ya akiba yake ya dhahabu ili kupata fedha za kusaidia kufadhili miradi mbalimbali ya miundombinu, hatua ambayo inajiri huku msaada wa wafadhili wa maendeleo ukipungua duniani.
Akizungumza jijini London, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uwekezaji), Prof. Kitila Mkumbo, alisema uamuzi huo umetokana na maagizo ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuchukua hatua ya kuuza sehemu ya hazina ya dhahabu.
Waziri Mkumbo alisema kuwa kwa kuzingatia kupungua kwa misaada ya nje, Tanzania inahitaji kutafuta njia mbadala za kupata fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo na miundombinu, na hivyo kutumia rasilimali za ndani kama dhahabu.
Benki Kuu ya Tanzania imepewa jukumu la kutekeleza mauzo ya dhahabu hizo, ingawa bado haijafahamishwa kwa umma kiasi au ratiba ya utekelezaji wa muamala huo.
Akiba ya dhahabu ya taifa ilikuwa na thamani takriban dola bilioni 1.3 (takriban shilingi trilioni nyingi) mwishoni mwa Desemba 2025, kulingana na takwimu za benki.
Uamuzi wa kuuza dhahabu unajitokeza wakati misaada ya maendeleo kwa nchi za Afrika ikipungua kutokana na mabadiliko ya sera za wafadhili wakuu wa kigeni, ambao sasa wanabadilisha mtazamo wao wa kugharamia miradi ya nje huku wakielekeza rasilimali zao kwa vipaumbele vya ndani kama ulinzi na huduma za kijamii.
Tanzania ni miongoni mwa watengenezaji wakubwa wa dhahabu barani Afrika, na dhahabu imekuwa chachu muhimu ya mapato ya nje kupitia mauzo ya kuuza nje; sekta hii pia inachangia asilimia kubwa ya Pato la Taifa na mapato ya kodi.
Uamuzi huu umevutia mijadala ya kitaifa kuhusu njia bora za kusimamia rasilimali za asili ili kuimarisha uchumi na chanzo cha fedha za maendeleo, bila kutegemea kabisa misaada kutoka nje.
Soma pia:
Shambulio baya la wanajihadi laua makumi ya watu Nigeria, wakiwemo wanajeshi
Jeshi la Nigeria limesema wanamgambo wameshambulia kambi ya kijeshi iliyoko katika jimbo la Borno, kaskazini mwa nchi hiyo.
Wanajeshi na wanamgambo kumi na mmoja wameuawa katika shambulizi hilo.
Jeshi limesema washambuliaji walitumia droni kushambulia kambi ya Sabon Gari.
Msemaji wa Jeshi la Nigeria amesema wameshuhudia kuongezeka kwa matumizi ya droni katika mashambulizi yanayofanywa na waasi.
Soma pia:
Jenerali Kainerugaba akiri kumshinikiza mke wa Bobi Wine kuwafahamisha alipo mumewe
Jeshi la Uganda limekiri kuwa wanajeshi walimkamata kwa muda mfupi Barbara “Barbie” Kyagulanyi, mke wa kiongozi wa upinzani Robert Kyagulanyi Ssentamu maarufu kama Bobi Wine, na baadaye kumuachilia huru, huku wakiashiria kuwa alisaidia katika jitihada za kumtafuta mumewe.
Katika chapisho kwenye mtandao wa X, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, Kiongozi wa Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Uganda, aliweka picha ya Barbie wakati wanajeshi walipochukua hatua hiyo usiku wa Januari 23 katika eneo la Magere, Wilaya ya Wakiso.
Jenerali Kainerugaba alisema: “Walimkamata na kisha kumuachilia huru Kabobi wake, Barbie. Alikuwa msaada mkubwa katika kutupatia taarifa za mumewe.”
Hata hivyo, Jenerali Kainerugaba ameikana madai ya kudhalilishwa kwa mke huyo. Ameashiria kuwa jeshi halimdhalilishi wanawake na lengo kuu ni kumtafuta Bobi Wine, sio kuwadhalilisha wanafamilia wake.
''Ikiwa askari yeyote alijaribu kumgusa Barbie. Ataadhibiwa vikali sana! Wanajeshi wetu wote wanafahamishwa jinsi ya kushughulikia wanawake'', aliandika kwa mtandao wa X.
Tukio hili linatokea katika hali ya utafutaji mkali wa Bobi Wine, ambaye amekuwa mafichoni kufuatia uchaguzi wa rais uliofanyika Januari 15, ambapo matokeo rasmi yalionyesha Rais wa sasa Yoweri Museveni kuibuka na ushindi wa muhula wa saba.
Bobi Wine amekanusha matokeo hayo akidai uchaguzi haukuwa wazi na haki.
Naye, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Uongozi wa Kitaifa, Dkt. Chris Baryomunsi, ameweka bayana kwamba kuwepo kwa vikosi vya usalama kwenye nyumba ya kiongozi wa upinzani ni kwa lengo la kuzuia machafuko, si kuharibu familia.
Alisema Kyagulanyi ana uhuru wa kurudi nyumbani na usalama huo ni wa kuhakikisha hakutokei makundi makubwa ya wananchi.
Tukio hili limevutia ukosoaji kutoka kwa wanaharakati wa haki za binadamu, wakiashiria kuwa hatua kali za usalama dhidi ya viongozi wa upinzani na wafuasi wake zinaashiria hatari kwa uhuru wa kiraia na hofu ya ukandamizaji wa kisiasa.
Soma pia:
Waziri wa Ulinzi wa Marekani asema jeshi lipo tayari kutekeleza uamuzi wowote wa Trump kuhusu Iran
Waziri wa Ulinzi wa Marekani amesema kuwa jeshi la nchi hiyo lipo tayari kutekeleza uamuzi wowote utakaochukuliwa na Rais Donald Trump kuhusu Iran, ili kuzuia nchi hiyo kupata silaha za nyuklia.
Katika mkutano wa Baraza la Mawaziri, Bw. Trump aliomba maoni ya Pete Hegsett kuhusu uwekaji wa wanajeshi wa Marekani katika Ghuba ya Uajemi (Persian Gulf).
Bw. Hegsett alisema: “Iran haiwezi kutafuta nguvu za nyuklia. Tupo tayari kufanya yale Rais anayoyatarajia kutoka Wizara ya Ulinzi.”
Maafisa wa Marekani wamesema kuwa Trump bado anapitia chaguzi mbalimbali, lakini bado hajafikia uamuzi wa mwisho kuhusu shambulio dhidi ya Iran.
Mvutano kati ya Marekani na Iran umeongezeka katika wiki za hivi karibuni kufuatia hatua kali za Iran dhidi ya maandamano yenye vurugu.
Rais Trump amesema kuwa Marekani itachukua hatua iwapo Tehran itaendelea na mpango wake wa nyuklia, hasa baada ya mashambulio ya anga ya Israel na Marekani yaliyozingatia maeneo muhimu ya nyuklia.
Unaweza pia kusoma:
Trump asema Putin hatashambulia miji ya Ukraine kipindi hiki cha baridi
Rais wa Ukraine Volodomyr Zelensky amesema anatumai Marekani ingeweza kusitisha mashambulizi ya Urusi yanayolenga miundo mbinu nchini mwake.
Rais Trump alikuwa amesema Rais wa Urusi Vladimir Putin alikubali ombi la kusitisha mashamblizi dhidi ya mji mkuu wa Ukraine Kyiv na miji mingine kwa angalau wiki moja katika kipindi hiki cha msimu wa baridi kali.
"Ilikuwa na ufanisi kubwa. Watu wengi walisema, 'Usipoteze muda wa kumpigia simu, hatokubali.' Na yeye [Putin] alinikubalia," Trump aliongeza.
Hata hivyo, Ikulu ya Rais wa Urusi ya Kremlin bado haijathibitisha iwapo imeridhia kusitisha kwa muda mashambulizi dhidi ya Ukraine.
Mamilioni ya watu Ukraine hawana huduma ya umeme na maji katika msimu huu wa baridi kali kutokana na mashambulizi makali ya mara kwa mara kutoka Urusi yanayoilenga miundo mbinu ya Ukraine.
Soma Pia:
Iran yafanya mazoezi ya kijeshi kwenye mkono wa bahari wa Hormuz
Press TV, kituo cha televisheni cha Iran cha lugha ya Kiingereza, kiliripoti kwamba Jeshi la Wanamaji la Walinzi wa Mapinduzi ya Iran litafanya mazoezi ya kuzima moto katika Mlango wa bahari wa Hormuz katika siku zijazo.
Al Jazeera, ikinukuu chanzo cha Iran ambacho hakikutajwa jina, pia ilisema kuwa Urusi na China ni sehemu ya mazoezi hayo.
Mamlaka za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran bado hazijajibu kuwepo kwa nchi hizo mbili katika mafunzo hayo.
Shirika la habari la Associated Press pia liliripoti kuwa Iran ilitangaza siku ya Alhamisi, katika notisi kwa makampuni ya meli, kwamba mazoezi ya majini yangefanyika katika Mlango-Bahari wa Hormuz.
Ukanda huu ndio njia kuu ya usafirishaji wa mafuta duniani, inayounganisha wazalishaji wakubwa wa mafuta katika Ghuba ya Uajemi, ikiwa ni pamoja na Saudi Arabia, Iran, na Iraq.
Unaweza kusoma pia:
Trump atishia kutoza ushuru kwa mataifa yanayouza mafuta kwa Cuba
Rais wa Marekani Donald Trump ameitangaza Cuba kuwa kitisho cha usalama wa taifa dhidi ya taifa lake.
Ametia saini amri ya Rais ambapo nchi yoyote itakayoiuzia au kuipa Cuba mafuta kuongezewa ushuru.
Marekani inaishutumu Cuba kwa kuunga mkono na kuyasaidia makundi ya kigaidi kama Hamas na Hezbollah na nchi ambazo ni hasimu wa Marekani zikiwemo Urusi,China na Iran.
Utawala wa Trump umekuwa ukijaribu kuzuia bidhaa muhimu ya mafuta kutoifikia Cuba kutoka kwa wasambazaji wake wakuu kama Venezuela na muuzaji wake mwingine mkuu Mexico mapema wiki hii ilitangaza kuwa inasitisha kwa muda kuiuzia Cuba mafuta.
Siku ya Jumanne, Trump alisema Cuba "itaanguka hivi karibuni", kwani mshirika wa muda mrefu Venezuela haipeleki tena mafuta au pesa nchini humo baada ya Rais Nicolás Maduro kutekwa na majeshi ya Marekani tarehe 3 Januari.
Hapo awali, taifa hilo la Amerika Kusini liliaminika kutuma takriban mapipa 35,000 ya mafuta kwa siku nchini Cuba.
Trump aliwahi kuamuru Cuba "kufanya makubaliano, kabla ya kuchelewa", ingawa hajataja masharti ya mpango huo au matokeo ambayo taifa hilo la kisiwa linaweza kukabili.
Wakati huo, Rais wa Cuba Miguel Díaz-Canel alisema Washington haikuwa na mamlaka ya kimaadili kulazimisha makubaliano juu ya nchi yake.
Mbinu ya utawala wa Trump ya kutwaa meli za mafuta za Venezuela zilizowekewa vikwazo tayari imeanza kuzidisha tatizo la mafuta na umeme nchini Cuba.
Nchi hiyo imekabiliwa na kukatika kwa umeme, huku Wacuba wakijitahidi kustahimili bila umeme wa kutegemea.
Waziri wa mambo ya nje wa Cuba Bruno Rodriguez hivi majuzi alisema kuwa taifa hilo la kisiwa cha Karibean lilikuwa na "haki kamili ya kuagiza mafuta" kutoka kwa msafirishaji yeyote aliye tayari "bila kuingiliwa au kutii hatua za upande mmoja za Marekani".
BBC imewasiliana na Wizara ya Mambo ya Nje ya Cuba kwa maoni.
Trump aonya kuwa ni “hatari sana” kwa Uingereza kushirikiana na China
Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema kuwa ni “hatari sana” kwa Uingereza kuimarisha mahusiano yake na China, kauli aliyotoa wakati Waziri Mkuu wa Uingereza, Sir Keir Starmer, akiendelea na ziara yake rasmi mjini Beijing.
Trump alikuwa akijibu makubaliano yaliyotangazwa baada ya Sir Keir kukutana na Rais wa China, Xi Jinping, katika ziara ya siku tatu iliyolenga kufufua na kurekebisha upya uhusiano kati ya mataifa hayo mawili.
Makubaliano hayo yanalenga kuongeza biashara na uwekezaji kati ya Uingereza na China.
Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa filamu ya maandishi kuhusu mke wake, Melania Trump, alisema: “Ni hatari sana kwao kufanya hivyo,” alipoulizwa maoni yake kuhusu Uingereza kuimarisha uhusiano wa kibiashara na China.
Kauli hiyo ilitolewa kufuatia matamshi ya Sir Keir kwamba uhusiano wa Uingereza na China uko katika “hali nzuri na imara” baada ya mkutano wake na Rais Xi katika Ukumbi Mkuu wa Watu, siku ya Alhamisi.
Waziri Mkuu huyo aliongeza kuwa mikutano aliyofanya ilikuwa “ya mafanikio makubwa” na ilifikia kiwango cha ushirikiano ambacho Uingereza ilikuwa inakitarajia.
“Tulizungumza kwa uwazi na kwa heshima, na tumepiga hatua muhimu, kwani Uingereza ina mchango mkubwa wa kutoa,” alisema Sir Keir alipohutubia Jukwaa la Biashara la Uingereza na China katika Benki ya China mjini Beijing.
Miongoni mwa matokeo ya ziara hiyo ni makubaliano ya kusafiri bila visa, kupunguzwa kwa ushuru wa whiski, pamoja na uwekezaji wa pauni bilioni 10.9 kutoka kampuni ya AstraZeneca kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vya uzalishaji nchini China.
Aidha, makubaliano ya kuimarisha ushirikiano katika maeneo mengine, yakiwemo mapambano dhidi ya uhalifu uliopangwa na uhamiaji haramu, yalitangazwa.
Mwenyekiti wa Chama cha Biashara cha Uingereza nchini China, Chris Torrens, aliitaja ziara hiyo kuwa “ya mafanikio” na kusema kuwa ni jambo la msingi kwa Uingereza kuendelea kushirikiana na China, mmoja wa washirika wake wakubwa wa kibiashara.
Bw Torrens alieleza kuwa, ingawa Marekani mara nyingine huweka vikwazo au kutoza ushuru kwa mataifa yanayofanya biashara na China, bado kuna uwezekano mkubwa kwa Marekani yenyewe kuingia makubaliano ya kiuchumi na China, jambo analosema linatarajiwa kutokea mwaka huu mwezi April.
Awali wiki hii, Trump alitishia kuiwekea Canada ushuru iwapo ingetimiza makubaliano ya kiuchumi iliyoafikiana na China kufuatia ziara ya kiongozi wake, Mark Carney, mjini Beijing.
Kwa mujibu wa takwimu za Idara ya Biashara na Biashara ya Kimataifa ya Uingereza, Marekani ilikuwa mshirika mkubwa zaidi wa kibiashara wa nchi hiyo mwaka 2025, huku China ikishika nafasi ya nne.
Soma Pia:
Rais Traoré 'afuta' vyama vyote vya siasa Burkina Faso
Serikali ya kijeshi ya Burkina Faso imefuta vyama vyote vya siasa na kufuta mfumo wa kisheria uliokuwa unasimamia uendeshaji wake, kwa mujibu wa amri iliyoidhinishwa na baraza la mawaziri la taifa hilo la Afrika Magharibi siku ya Alhamisi.
Hatua hiyo, iliyochukuliwa na utawala huo wa kijeshi chini ya Rais Ibrahim Traoré aliyeingia madaraka kupitia mapinduzi ya Septemba 2022, ni hatua ya hivi karibuni ya kuimarisha udhibiti wa mamlaka baada ya kusimamishwa kwa shughuli za kisiasa kufuatia mapinduzi hayo.
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Burkina Faso, Emile Zerbo, alisema uamuzi huo ni sehemu ya juhudi pana za “kuijenga upya dola”, akidai kuwa mfumo wa vyama vingi ulikuwa unatumika vibaya na kushindwa kufanya kazi ipasavyo.
Alisema tathmini ya serikali imebaini kuwa kuongezeka kwa idadi ya vyama vya siasa kulichochea migawanyiko na kudhoofisha mshikamano wa kijamii.
Kabla ya mapinduzi, Burkina Faso ilikuwa na zaidi ya vyama vya siasa 100 vilivyosajiliwa, huku 15 kati ya hivyo vikiwa na uwakilishi katika bunge baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.
Amri hiyo inafuta vyama vyote vya siasa na miungano ya kisiasa. Sheria ya kufuta kanuni zilizokuwa zinasimamia vyama, ufadhili wake, pamoja na hadhi ya kiongozi wa upinzani, itapelekwa kwenye baraza la mpito kwa ajili ya kuidhinishwa, kulingana na kumbukumbu za kikao cha baraza la mawaziri.
Mali zote za vyama vilivyovunjwa ama kufutwa zitahamishiwa mikononi mwa serikali.
Taifa hilo la ukanda wa Sahel, kama zilivyo nchi jirani za Mali na Niger, limekuwa likipambana na mashambulizi ya makundi ya wanamgambo wa Kiislamu yanayohusishwa na al-Qaeda na Islamic State, ambayo yamesababisha vifo vya maelfu ya watu na kuwafanya mamilioni kukimbia makazi yao katika kipindi cha zaidi ya muongo mmoja.
Habari na karibu katika matangazo yetu ya habari za moja kwa moja