Urusi yakataa baadhi ya masharti ya mpango wa amani ya Ukraine

Msemaji wa Urusi amesema mkutano wa Moscow ulikuwa "wenye tija," lakini baadhi ya sehemu za mpango wa amani hazikubaliki kwa Urusi.

Muhtasari

Moja kwa moja

Rashid Abdallah & Asha Juma

  1. UN yashutumu kuongezeka kwa ukandamizaji dhidi ya upinzani Uganda

    .

    Chanzo cha picha, Bobi Wine/X

    Umoja wa Mataifa umeshutumu Jumatano kuongezeka kwa ukandamizaji dhidi ya upinzani na vyombo vya habari nchini Uganda kabla ya uchaguzi mkuu mwezi ujao, na kutaka uchunguzi ufanyike bila upendeleo kuhusu madai ya kukamatwa kiholela, kutoweka na "mateso".

    Ofisi ya haki za Umoja wa Mataifa iliangazia "ripoti za kuaminika" zinazoonyesha kuwa takriban watu 550, wakiwemo wanachama na wafuasi wa chama kikuu cha upinzani cha National Unity Platform (NUP) na mgombea urais Bobi Wine, wamekamatwa na kuzuiliwa tangu mwanzoni mwa mwaka huu.

    Zaidi ya 300 kati yao walikuwa wamekamatwa tangu kampeni za uchaguzi zilipoanza mwezi Septemba kabla ya kura ya urais ya Januari 15.

    "Wengi wa waliokamatwa wamesalia rumande, wakikabiliwa na mashtaka kuanzia kero ya umma na kutotii amri hadi kushambulia, kuzuia na kuchochea vurugu," ilisema taarifa ya tume ya umoja wa mataifa ya haki za binadamu.

    Ofisi ya tume hiyo pia ilionyesha jinsi vikosi vya usalama vilivyojihami vilikuwa vimetumwa katika maeneo ambayo NUP ilipanga kufanya mikutano.

    "Pia wametumia mabomu ya machozi, mijeledi, marungu, maji ya kuwasha na virutubishi vya kemikali miongoni mwa silaha nyingine wakati wa maandamano ya kuwatawanya wafuasi wa NUP, na kujeruhi watu wengi," ilisema, ikiongeza kuwa wiki iliyopita pia waliripotiwa kutumia "risasi za moto" katika mkutano wa hadhara wa Bobi Wine mashariki mwa mji wa Iganga, ambapo angalau mtu mmoja aliuawa.

    Inasikitisha sana kwamba kampeni za uchaguzi kwa mara nyingine tena zimekuwa na matukio mengi ya kukamatwa kiholela, kuwekwa kizuizini na matumizi ya nguvu zisizo za lazima dhidi ya upinzani," mkuu wa haki za Umoja wa Mataifa Volker Turk alisema katika taarifa hiyo. Huku akisisitiza "Ninaziomba mamlaka za Uganda kusitisha matumizi ya mbinu hizo za ukandamizaji."

    Turk alitoa wito kwa mamlaka ya Uganda "kuchunguza kikamilifu na bila upendeleo" madai yote kama hayo, kuwaachilia wale "waliozuiliwa kiholela, na "kuadhibu wanaowajibika na kutoa fidia kamili kwa waathiriwa".

    Taarifa ya Jumatano pia ilipinga vizuizi vya uhuru wa wanahabari, ikiangazia kesi za hivi majuzi ambapo wanahabari waliondolewa kibali chao kwa sababu ya ripoti muhimu.

    Kwa mjibu wa ripoti hiyo ya tume ya umoja wa mataifa ya haki za binadamu- Makumi ya waandishi wa habari pia walivamiwa au kupokonywa vifaa vyao au kuharibiwa na maafisa wa usalama wakati wa uchaguzi mdogo wa ubunge katika eneo bunge la Kawempe Kaskazini mnamo mwezi Machi.

    "Mamlaka za Uganda lazima zisitishe vurugu zote dhidi ya vyombo vya habari na upinzani na kuchukua hatua kikamilifu kulingana na wajibu wao chini ya sheria za kimataifa za haki za binadamu," Turk alisema.

    Pia unaweza kusoma:

  2. Putin hajakataa mpango wote wa amani wa Marekani kwa Ukraine - Urusi

    .

    Chanzo cha picha, Alexander Kazakov/Sputnik/Kremlin Pool/EPA/Shutterstock

    Msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov anasema "haitakuwa sahihi" kusema kwamba Rais Putin amekataa mapendekezo ya Marekani ya amani wakati wa mazungumzo na Steve Witkoff na Jared Kushner hapo jana.

    Akijibu swali katika mkutano wa waandishi wa habari wa kila siku, Peskov anasema: "Jana ilikuwa mara ya kwanza kubadilishana moja kwa moja maoni. Kuna kitu kilikubaliwa, na kuna lile ambalo halikukubalika. Huu ni mchakato wa kawaida wa kufanya kazi na utafutaji wa maelewano."

    Peskov pia alikataa kufichua maelezo yoyote ya mazungumzo ya saa tano huko Kremlin: "Kuna uelewa kwamba kadiri mazungumzo haya yakiwa ya utulivu zaidi, ndivyo yanakuwa na tija zaidi. Tutashikamana na kanuni hii na tunatumai kuwa wenzetu wa Marekani watafanya hivyo pia."

    Wiki iliyopita kulikuwa na msururu wa uvujaji wa vyombo vya habari ukipendekeza kwamba Wamarekani walijaribu kuwasilisha orodha ya matakwa yenye kupendelea Urusi kama "mpango wao wa amani", kwamba Marekani imekuwa ikihusika katika mazungumzo ya siri ya kibiashara na Urusi, na kwamba Witkoff aliwashauri Warusi jinsi ya kuzungumza na Donald Trump.

    Soma zaidi:

  3. Mwanamume ashtakiwa kwa madai kuwa alimeza kito chenye thamani ya $19k

    .

    Chanzo cha picha, Fabergé

    Mwanamume mmoja wa New Zealand ameshtakiwa kwa wizi baada ya kudaiwa kuiba kito cha almasi kwa njia isiyo ya kawaida - kwa kuimeza.

    Kito kilichomezwa - chenye thamani ya NZ$33,585 ($19,300; £14,600) - bado hakijapatikana, polisi waliviambia vyombo vya habari vya ndani.

    Polisi waliitwa Ijumaa alasiri na mwanamume huyo mwenye umri wa miaka 32 akakamatwa dukani dakika chache baadaye.

    Amefanyiwa uchunguzi wa kimatibabu na bado yuko kizuizini, polisi wanasema.

    Kito cha thamani kinachodaiwa kuibwa kina almasi 60 nyeupe na yakuti 15 ya samawati, kulingana na tovuti ya sonara, na dhahabu ya karati 18.

    Soma zaidi:

  4. Wabunge Kenya wabaini 'mwenendo wa utovu wa nidhamu' wa wanajeshi wa Uingereza

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Uchunguzi wa bunge nchini Kenya umeshutumu wanajeshi wa Uingereza wanaofanya mazoezi yao nchini humo kwa kuwa na utovu wa nidhamu wa kingono na uharibifu wa mazingira..

    Matokeo ya uchunguzi wa kamati ya bunge ulioangazia ulinzi na uhusiano wa kigeni yanaangazia kuongezeka kwa hali ya kutatanisha nchini humo kutokana na mienendo ya wanajeshi wa Kitengo cha Mafunzo ya Jeshi la Uingereza (BATUK), ambao wamekabiliwa na lawama nyingi katika miaka ya hivi karibuni.

    Msemaji wa wizara ya ulinzi ya Uingereza alisema katika taarifa yake kwa shirika la habari la Reuters kwamba wizara hiyo inajutia sana "changamoto ambazo zimejitokeza kuhusiana na uwepo wetu wa ulinzi nchini Kenya" na kusema kuwa iko tayari kuchunguza madai mapya katika ripoti hiyo punde ushahidi utakapotolewa.

    Madai yanayojulikana zaidi yakiwa yenye kuhusiana na mauaji ya mwaka 2012 ya Agnes Wanjiru mwenye umri wa miaka 21 karibu na kambi ya mafunzo ya wanajeshi wa Uingereza katika mji wa Nanyuki.

    Mshukiwa huyo, mwanajeshi wa Uingereza aitwaye Robert Purkiss, alikamatwa nchini Uingereza mwezi uliopita baada ya jitihada za miaka mingi za familia ya Wanjiru na mashirika ya kutetea haki za binadamu Kenya, ambayo yalisema wauaji wake wanalindwa na makubaliano ya ushirikiano wa ulinzi kati ya nchi hizo mbili.

    Soma zaidi:

  5. Marekani yasitisha upataji uraia kwa wahamiaji kutoka nchi zilizopigwa marufuku kusafiri

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Marekani imesitisha mchakato wa maombi yote ya uhamiaji yanayohusishwa na nchi 19 ambazo tayari zimepigwa marufuku ya kusafiri, kwa mujibu wa taarifa rasmi ya ndani iliyoonekana na mshirika wa BBC CBS News.

    Mawakala wa uhamiaji wamearifiwa "kusitisha shughuli za mwisho mwisho kwa maombi yote", na kusimamisha hatua hizo kwa wahamiaji wanaokaribia kupata uraia.

    Hili linawadia huku kukiwa na ripoti kwamba Donald Trump anafikiria kupanua amri ya Juni inayozuia usafiri kwa nchi 19 hadi 30.

    Huu ni uimarishaji wa hivi punde wa sheria za uhamiaji baada ya shambulizi la wiki jana huko Washington DC, ambalo lilisababisha kifo cha mwanajeshi mmoja wa Jeshi la Ulinzi na mwingine akiwa katika hali mbaya.

    Mshukiwa wa shambulizi hilo ni raia wa Afghanistan anayeishi Marekani.

    Soma zaidi:

  6. Israel yasema mabaki iliyokabidhiwa na Hamas sio ya mateka wao

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Idara za uchunguzi wa Israel zilihitimisha kuwa mabaki iliyokabidhiwa na Hamas siku ya Jumanne hayakuwa ya mateka wawili wa mwisho walioko Gaza, ofisi ya waziri mkuu wa Israel ilisema.

    Hamas ilikuwa imekabidhi mabaki yaliyoelezewa na Shirika la Msalaba Mwekundu kama yale ya mmoja wa mateka wawili wa mwisho waliofariki Gaza, kulingana na ahadi zilizotolewa chini ya makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyoungwa mkono na Marekani mnamo mwezi Oktoba.

    Vikosi vya Israel vilisema viliagiza uchunguzi wa kitaalamu kwa mabaki waliyoyaelezea "matokeo" yake.

    "Matokeo yaliyoletwa jana kwa uchunguzi wa mabaki kutoka Ukanda wa Gaza hayahusiani na mateka yeyote," ofisi ya Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu ilisema katika taarifa Jumatano.

    Utambulisho huo ulifanywa katika Kituo cha Kitaifa cha Tiba ya Uchunguzi, iliongeza.

    Vikosi vya Al Quds - tawi la wanaharakati wa Jihad ya Kiislamu ya Palestina inayoshirikiana na Hamas - walisema baadaye Jumatano walikuwa wakitafuta mwili wa mateka kaskazini mwa Gaza, pamoja na timu ya Msalaba Mwekundu.

    Haikusema ni mateka yupi kati ya wawili waliosalia ilikuwa ikimtafuta.

    Wawili hao ni afisa wa polisi wa Israel Ran Gvili na raia wa Thailand Sudthisak Rinthalak, wote walitekwa nyara wakati wa shambulizi la Hamas la Oktoba 7, 2023 dhidi ya Israel ambalo lilipelekea miaka miwili ya vita vikali huko Gaza.

    Pia unaweza kusoma:

  7. Mawaziri wa kigeni wa NATO wakutana

    .

    Chanzo cha picha, AFP

    Mkutano wa pande zote wa mawaziri wa kigeni wa Nato umeanza, ambapo wanatarajiwa kuzungumza kuhusu amani pamoja na masuala ya ulinzi.

    Katika hotuba yake ya ufunguzi katika meza ya mazungumzo, mkuu wa Nato Mark Rutte anasema Urusi "inaendelea kujaribu imani yetu", na "tunakabiliwa na hatari za kweli na za kudumu".

    Rutte anaendelea kusema kuwa Urusi imekiuka anga yake kwa ndege na ndege zisizo na rubani, kufanya hujuma na kutuma meli za kijasusi kwenye maji yake.

    Vitendo hivi ni "vya kizembe na hatari", anaongeza.

    .

    Chanzo cha picha, Alexander Kazakov/Sputnik/Kremlin Pool/EPA/Shutterstock

    Urusi "inashirikiana kwa karibu" na China, Korea Kaskazini na Iran "kuvuruga jamii zetu na kuvunja sheria za kimataifa", anasema, na "kujiandaa kwa makabiliano ya muda mrefu".

    Rutte anasema nchi za Nato "zinaimarisha ulinzi wetu lakini sote tunahitaji kujitahidi".

    Aliongeza kuwa Ukraine "inahitaji msaada wetu zaidi sasa hivi kuliko hapo awali", kwani msimu wa baridi unawadia na mashambulizi ya Urusi yanaendelea.

  8. Mfanyabiashara Niffer afutiwa kesi ya uhaini, aachiliwa huru

    dx

    Chanzo cha picha, Habari Leo

    Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) amefuta mashtaka na kumwachia huru mfanyabiashara wa vipodozi Jenifer Jovin (26) maarufu Niffer na Mika Lucas Chavala, waliokuwa na kesi ya uhaini.

    Kwa mujibu wa gazeti la Mwananchi, uamuzi huo umetolewa leo Jumatano Desemba 3, 2025 na Hakimu Mkazi Mkuu Dr es Salaam, baada wakili wa Serikali, kuileleza Mahakama hiyo kuwa DPP hana nia ya kuendelea na mashtaka

    Jeniffer Jovin pamoja na Mika Chavala walikuwa wanakabiliwa na mashtaka ya uhaini.

    Ikumbukwe Novemba 25, 2025 washtakiwa 20 kati ya 22 ambao walikuwa wanashtakiwa pamoja na Niffer waliachiwa baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), kueleza kuwa hana nia ya kuendelea na mashtaka yao.

    Pia unaweza kusoma:

  9. Amnesty inawatuhumu wanamgambo wa Sudan kwa uhalifu wa kivita

    dfc

    Chanzo cha picha, AP

    Maelezo ya picha, Wanamgambo wa Sudan wa Rapid Support Forces wakipiga doria katika mji wa Garawee, kaskazini mwa Sudan, Jumamosi, Juni 15, 2019.

    Kundi la kimataifa la kutetea haki za binadamu linalishutumu kundi la wanamgambo linalopigana dhidi ya jeshi la Sudan kwa kufanya uhalifu wa kivita wakati wa shambulio lao mapema mwaka huu kwenye kambi kubwa zaidi ya wakimbizi nchini humo katika eneo la Darfur.

    Vikosi vya Rapid Support Forces, ambavyo viko vitani dhidi ya jeshi la Sudan, vilivamia kambi ya Zamzam mwezi Aprili kama sehemu ya kuzingira mji wa el-Fasher, mji mkuu wa jimbo la Darfur Kaskazini. RSF iliteka jiji, ngome ya mwisho ya jeshi huko Darfur, mwezi Oktoba.

    Amnesty International ilisema katika ripoti iliyotolewa leo kwamba mashambulizi ya siku kadhaa ya RSF dhidi ya Zamzam yalihusisha mauaji ya raia, utekaji nyara na uharibifu wa misikiti, shule na kliniki za afya, na lazima hayo yachunguzwe kama uhalifu wa kivita.

    "Shambulio la kutisha na la makusudi la RSF dhidi ya raia waliokata tamaa na wenye njaa katika kambi ya Zamzam lilifichua kwa mara nyingine tena kutojali kwao na maisha ya binadamu," amesema Agnès Callamard, katibu mkuu wa Amnesty International.

    Ripoti ya Amnesty ni ya hivi punde zaidi ya shirika la kimataifa la kutetea haki za binadamu kushutumu RSF kwa ukatili katika vita vya Sudan. Shutuma hizo zikijumuisha mauaji ya halaiki na ubakaji katika mashambulizi katika miji na vijiji, hasa katika Darfur.

    Jeshi la Sudan pia limeshutumiwa kwa ukatili katika vita hivyo.

    Mapambano ya kuwania madaraka kati ya jeshi na RSF yalizuka katika vita mwezi Aprili 2023. Mgogoro huo umesababisha vifo vya watu 40,000 - ingawa baadhi ya mashirika ya haki za binadamu yanasema idadi ya vifo ni kubwa zaidi - na imesababisha mgogoro mbaya zaidi wa kibinadamu duniani huku zaidi ya milioni 14 wakikimbia makazi yao. Maeneo mengi yamekumbwa na njaa, ikiwa ni pamoja na katika kambi ya Zamzam.

    Pia unaweza kusoma:

  10. Waziri wa Marekani ajitetea kutokana na shambulio dhidi ya boti katika pwani ya Caribbea

    [

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth anasema alitazama tu shambulio la kwanza kati ya mawili dhidi ya boti inayodaiwa kuwa ya dawa za kulevya tarehe 2 Septemba.

    Waziri wa Ulinzi wa Marekani Pete Hegseth amesema "hakuona manusura" kabla ya shambulio la pili katika boti inayodaiwa kuwa ya madawa ya kulevya katika visiwa vya Caribbea.

    Shambulio la awali linaripotiwa kuwaacha watu wawili walionusurika waking’ang’ania boti hilo lililokuwa linawaka moto, kabla ya shambulio la pili kudaiwa kuamriwa na kusababisha vifo vyao.

    Shambulio la Septemba 2 limezua wasiwasi kwamba huenda vikosi vya Marekani vimekiuka sheria zinazosimamia mizozo ya kivita.

    Ikulu ya White House imesema kamanda mkuu wa Jeshi la Wanamaji la Marekani, Frank Bradley, aliidhinisha shambulio la pili.

    Gazeti la Washington Post liliripoti maelezo kuhusu shambulio la pili, ripoti ambayo imesababisha wasiwasi kutoka kwa wabunge wa Democrat na Republican.

    Akijibu swali la mwandishi wa habari wakati wa mkutano wa baraza la mawaziri siku ya Jumanne, Hegseth alisema alitazama shambulio la kwanza "moja kwa moja" lakini haraka akahamia kwenye mkutano mwingine.

    "Binafsi sikuwaona walionusurika," Hegseth alisema kuhusu shambulio la kwanza. "Boti iliwaka moto na kulilipuka ... huwezi kuona chochote. Huu unaitwa ukungu wa vita."

    Aliongeza kuwa alijuzwa kuhusu "uamuzi sahihi" wa Admiral Bradley wa kuizamisha boto hiyo "saa chache baadaye."

    "Tunamuunga mkono," Hegseth alisema kuhusu Bradley.

    Rais Trump, kwa upande wake, pia alimtetea Adm Bradley, ingawa alijitenga na uamuzi wake wa kushambulia boti kwa mara ya pili, akisema "hatukujua" kuhusu shambulio lililofuata.

    "Na nasema hivi: nataka boti hizo zipotee," Trump aliongeza.

    Zaidi ya watu 80 wameuawa katika wimbi la mashambulio kama hayo katika eneo la Caribea na Mashariki mwa Pasifiki tangu mapema Septemba.

    Utawala wa Trump umerudia kutetea mashambulizi hayo na kusema ni hatua muhimu ya kujilinda ili kuokoa maisha ya Wamarekani kutokana na dawa haramu.

    Adm Bradley - ambaye alikuwa kamanda wa Kamandi Maalum ya Operesheni Maalum ya jeshi la Marekani wakati wa shambulio - anatarajiwa kwenda Capitol Hill wiki hii kwa ajili ya mahojiano.

    Mkataba wa Geneva unakataza kuwashambulia kwa makusudi wapiganaji waliojeruhiwa, ukisema kwamba wanapaswa kukamatwa na kupewa msaada wa matibabu.

    Wataalamu kadhaa waliozungumza na BBC walionyesha mashaka kwamba shambulio hilo huenda sio halali chini ya sheria za kimataifa.

  11. Msako wa ndege ya Malaysia iliyopotea 2014 kuanza tena

    df

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Haya yanajiri zaidi ya muongo mmoja baada ya ndege hiyo kutoweka katika kile ambacho kimesalia kuwa moja ya kitendawili kikubwa katika usafiri wa anga

    Shughuli ya kutafuta mabaki ya ndege ya Malaysia MH370 itaanza tena tarehe 30 Disemba, zaidi ya muongo mmoja baada ya ndege hiyo iliyokuwa na watu 239 kutoweka, imesema serikali ya Malaysia.

    Utafutaji huu mpya, ambao utaendelea kwa siku 55, ulianza Machi lakini ukasitishwa muda mfupi baadaye kwa sababu ya hali mbaya ya hewa.

    Ndege ya MH370, Boeing 777, ilitoweka mwaka 2014 ilipokuwa ikisafiri kutoka Kuala Lumpur kuelekea Beijing na kusababisha msako mkubwa zaidi katika historia ya usafiri wa anga.

    Kampuni ya utafutaji Ocean Infinity inaongoza utafutaji wa sasa chini ya mkataba wa "usipoipata, hulipwi.” Itapokea dola milioni 70 (£56m) ikiwa mabaki hayo yatapatikana, Waziri wa Uchukuzi Loke Siew Fook alisema.

    Majaribio ya awali ni pamoja na utafutaji uliohusisha meli 60 na ndege 50 kutoka nchi 26, ambao ulimalizika mwaka 2017, na jitihada za 2018 za Ocean Infinity zilimalizika baada ya miezi mitatu.

    Ndege ya MH370 ilipoteza mawasiliano chini ya saa moja baada ya kupaa tarehe 8 Machi 2014, na rada ilionyesha kuwa ilikuwa imetoka kwenye njia yake ya awali ya ndege.

    Katika uchunguzi wa mwaka 2018, wachunguzi walisema "majibu kamili yatapatikana ikiwa mabaki yatapatikana."

    Pia unaweza kusoma:

  12. Papa Leo ameitaka Marekani kutotumia nguvu kumwondoa rais wa Venezuela

    xc

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Papa Leo XIV akiongoza Misa Takatifu huko Waterfront, wakati wa safari yake ya kwanza Beirut, Lebanon Desemba 2, 2025.

    Papa Leo ameutaka utawala wa Rais wa Marekani Donald Trump siku ya Jumanne kutojaribu kumwondoa madarakani Rais wa Venezuela Nicolas Maduro kwa kutumia nguvu za kijeshi.

    Leo, Papa wa kwanza raia wa Marekani, alisema itakuwa bora kujaribu mazungumzo au kuweka shinikizo la kiuchumi kwa Venezuela ikiwa Washington inataka kuona mabadiliko huko.

    Alipoulizwa wakati wa mkutano wa waandishi wa habari kuhusu vitisho vya Trump vya kumuondoa Maduro kwa nguvu, Leo alisema: "Ni bora kutafuta njia za mazungumzo, au labda shinikizo, ikiwa ni pamoja na shinikizo la kiuchumi."

    Papa, akizungumza wakati akirudi nyumbani kutoka ziara ya Uturuki na Lebanon, safari yake ya kwanza nje ya nchi, aliongeza kuwa Washington inapaswa kutafuta njia nyingine za kufikia mabadiliko "ikiwa ndio wanataka mabadiliko."

    Shirika la habari la Reuters liliripoti mwezi uliopita kwamba Marekani inafikiria kufanya jaribio la kumpindua kiongozi huyo wa Venezuela, na jeshi la Marekani liko tayari kwa awamu mpya ya operesheni baada ya kuongeza wanajeshi katika Caribiani na karibu miezi mitatu ya mashambulizi dhidi ya boti zinazoshukiwa za biashara ya madawa ya kulevya katika pwani ya Venezuela.

    Leo, akijibu swali la mwandishi wa habari, pia alisema ishara zinazotoka kwa utawala wa Trump kuhusu sera yake kuelekea Venezuela haziko wazi.

    Papa, aliyechaguliwa mwezi Mei kutoka Chicago, anaifahamu Amerika ya Kusini kwa sababu alikaa miaka mingi kama kasisi nchini Peru.

    Pia unaweza kusoma:

  13. Maelfu ya risasi za jeshi la Ujerumani zaibwa katika lori

    l

    Chanzo cha picha, Reuters

    Shehena ya risasi za Ujerumani imeibwa kutoka katika lori la mizigo katika mji wa mashariki wa Burg, wizara ya ulinzi ya nchi hiyo imesema.

    Wakizungumza na shirika la habari la Ujerumani DPA, maafisa hawakutaja ni kiasi gani kilichukuliwa. Lakini, ripoti zingine zikimtaja msemaji wa wizara ya ulinzi akisema ni karibu risasi 20,000.

    Wizi huo unakisiwa kufanyika baada ya dereva wa kampuni ya uchukuzi wa kiraia - iliyopewa kandarasi na jeshi - kuliacha lori lake katika sehemu ya kuegesha isiyokuwa na ulinzi usiku wa tarehe 25 Novemba.

    Siku iliyofuata, wakati wa uwasilishaji kwenye kambi ya Clausewitz, risasi zikawa hazipo. Jeshi limeanzisha uchunguzi pamoja na polisi.

    Der Spiegel, chombo cha habari cha Ujerumani, kiliripoti kuwa shehena hiyo ilikuwa na risasi 10,000 za bastola, risasi 9,900 za bunduki, na mabomu ya moshi.

    Serikali haijathibitisha ikiwa kuna mtu yeyote amekamatwa au kutambuliwa kuhusiana na tukio hilo, jambo ambalo limezua wasiwasi wa usalama.

    "Tunauchukulia wizi huu kwa uzito mkubwa - aina hii ya risasi lazima zisianguke katika mikono isiyofaa," wizara ya ulinzi iliviambia vyombo vya habari vya Ujerumani.

    Kiini cha uchunguzi wa Bundeswehr (jeshi la Ujerumani) itakuwa ni kwa nini dereva alishindwa kutambua eneo salama la kusimama, kulingana na shirika la utangazaji la umma la Ujerumani MDR.

    Inaripoti kuwa kuna nambari maalum ya simu kwa madereva wanaohitaji usaidizi na vikosi vya jeshi na vinaweza kutoa msindikizaji ikihitajika.

    Dereva aliliacha gari hilo katika sehemu ya kuegesha isiyokuwa na ulinzi na kulala usiku huo katika hoteli iliyo karibu.

    Hili ni tukio la hivi punde zaidi katika mfululizo wa matukio kama haya katika eneo la Saxony-Anhalt.

    Mwezi Agosti, polisi wa eneo la Bernburg waliripoti risasi 90 zilizopotea. Wiki moja kabla, maafisa huko Eisleben waliripoti kuwa walipoteza risasi 180.

    Pia unaweza kusoma:

  14. Trump asema hataki Wasomali Marekani

    sd

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema hataki wahamiaji wa Kisomali nchini Marekani, na kuwaambia waandishi wa habari wanapaswa "kurejea walikotoka."

    "Siwataki katika nchi yetu, nitakuwa mkweli," amesema wakati wa mkutano wa baraza la mawaziri siku ya Jumanne. Trump amesema Marekani "itaharibika ikiwa tutaendelea kuchukua takataka katika nchi yetu."

    Maoni yake ya kudhalilisha yanakuja wakati maafisa wa uhamiaji wakiripotiwa kupanga operesheni katika jamii kubwa ya Wasomali ya Minnesota.

    Maafisa katika jimbo hilo wamekosoa mpango huo, wakisema unaweza kuwaondoa isivyo haki raia wa Marekani ambao wanatoka katika taifa hilo la Afrika Mashariki.

    Minneapolis na St Paul, ambazo kwa pamoja zinajulikana kama Twin Cities, ni nyumbani kwa mojawapo ya jumuiya kubwa zaidi za Wasomali duniani na kubwa zaidi nchini Marekani.

    Maoni yake ya siku ya Jumanne, ambayo yalikuja mwishoni mwa mkutano wa baraza la mawaziri, Trump alisema: "Siwataki katika nchi yetu. Nitakuwa mkweli kwa hilo. Mtu atasema, 'Loo, hiyo si sahihi kisiasa.' Sijali siwataki katika nchi yetu."

    "Nchi yao ya Somalia unajua hawana chochote. Wanakimbia huku na huko kuuana," Trump alisema.

    Kisha akageukia kumkosoa Mbunge Ilhan Omar, wa chama cha Democratic, ambaye ni Mmarekani mwenye asili ya Somalia, ambaye amekuwa akigombana naye mara kwa mara.

    "Siku zote huwa namtazama," Trump alisema, akiongeza kuwa Omar "anamchukia kila mtu. Na nadhani ni mtu asiye na uwezo."

    "Kuniandama kwake kunatisha," Omar alisema katika chapisho katika mtandao wa kijamii. "Natumai atapata msaada anaohitaji."

    fg

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Trump pia amemkosoa Ilhan Omar, Mmarekani mwenye asili ya Somalia ambaye anawakilisha Minnesota katika Bunge la Congress m

    Idara ya Uhamiaji ya Marekani (ICE) imeagizwa na utawala wa Trump kuwalenga wahamiaji wa Kisomali wasio na vibali katika Twin Cities, mtu anayefahamu mipango hiyo ameliambia shirika la habari la CBS News siku ya Jumanne.

    Mamia ya watu wanatarajiwa kulengwa operesheni itakapoanza wiki hii, afisa huyo alisema. Gazeti la New York Times liliripoti kwa mara ya kwanza operesheni hiyo.

    Kulingana na viongozi wa eneo hilo, kuna takriban watu 80,000 wanaoishi huko ambao asili yao ni kutoka Somalia, na wengi wao ni raia wa Marekani.

    Utawala wa Trump umezidisha msako kwa wahamiaji kufuatia kupigwa risasi kwa wanajeshi wawili wa Jeshi la Kitaifa huko Washington DC wiki iliyopita, Sarah Beckstrom, 20, aliyefariki na kumjeruhi vibaya Andrew Wolfe, 24.

    Mshukiwa, ambaye amekamatwa na kushtakiwa kwa mauaji, anatoka Afghanistan.

    Pia unaweza kusoma:

  15. Mazungumzo ya Urusi na Marekani yashindwa kuleta maafikiano

    o

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Mazungumzo ya saa tano kati ya Rais wa Urusi Vladimir Putin na mpatanishi mkuu wa Rais wa Marekani Donald Trump yanaonekana kushindwa kuleta mafanikio katika kupatikana kwa makubaliano ya amani ya Ukraine.

    Msemaji wa Kremlin amesema mkutano wa Moscow ulikuwa "wa kujenga," lakini baadhi ya sehemu za mpango huo hazikubaliki kwa Urusi.

    Mjumbe maalum wa Trump, Steve Witkoff na mkwe Jared Kushner walihudhuria mazungumzo hayo ya kumaliza vita vya Ukraine. Timu ya Marekani haijatoa maoni yoyote tangu ilipoondoka Moscow.

    Mapema Jumanne, Putin alisema mabadiliko yaliyopendekezwa na Kyiv na Ulaya katika rasimu ya mpango wa amani unaoungwa mkono na Marekani hayakubaliki, akiongeza ikiwa Ulaya "inataka kuingia vitani, tuko tayari hivi sasa."

    Mpango huo, ambao ulionekana kuwa mzuri kwa Urusi baada ya kufichuliwa kwa vyombo vya habari mwezi Novemba, umefanyiwa mabadiliko kadhaa katika wiki za hivi karibuni.

    Alipoulizwa kuhusu pendekezo hilo baada ya mkutano wa Moscow, msaidizi mkuu wa Putin Yuri Ushakov amesema Kremlin "inakubaliana na baadhi ya vipengele ... lakini baadhi ya mambo tumeyakosoa." Aliongeza: "Bado hatujapata maelewano...kuna kazi kubwa iko mbele."

    Vipengele vyenye mvutano zaidi kati ya Moscow na Kyiv ni pamoja na Ukraine kukubali kuachia eneo inaloendelea kulidhibiti na dhamana ya usalama inayotolewa na Ulaya.

    Akizungumza kabla ya mazungumzo hayo, Putin aliwasuta viongozi wa bara hilo ambao wameunga mkono juhudi za kujihami za Kyiv tangu Urusi ilipoanzisha uvamizi kamili 2022.

    Alisema viongozi wa Ulaya wanajidanganya kwamba wanaweza kuishinda Urusi kimkakati. Amesema nchi yake, "haina mpango wa kuingia vitani na Ulaya - lakini ikiwa Ulaya ghafla inataka kuingia vitani, tuko tayari sasa hivi."

    Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amesema anatazamia kufahamishwa kuhusu mazungumzo ya Kremlin na timu ya Marekani baada ya mkutano huo, ingawa haikuwa wazi kama Witkoff na Kushner watasafiri kwa ndege hadi Kyiv au miji mikuu mingine ya Ulaya kwa mazungumzo zaidi ya ana kwa ana.

    Akizungumza kabla ya mazungumzo ya Kremlin kufanyika, kiongozi huyo wa Ukraine alisema siku ya Jumanne kulikuwa na fursa ya kumaliza vita "sasa kuliko wakati mwingine wowote," lakini vipengele vya mapendekezo bado vinahitaji kufanyiwa kazi.

    "Kila kitu kinategemea majadiliano ya leo," Zelensky aliuambia mkutano na waandishi wa habari wakati wa ziara rasmi nchini Ireland.

    Zelensky alisema "hakuna suluhu rahisi", akirudia msisitizo wa nchi yake kwamba Kyiv ishiriki katika majadiliano ya amani, dhamana ya wazi ya usalama ikubaliwe, kama vile uanachama wa Nato - hatua inayopingwa kwa muda mrefu na Urusi.

    Wawakilishi wa Ukraine wamefanya duru mbili za mazungumzo ya ngazi ya juu kuhusu rasimu ya mpango huo katika wiki za hivi karibuni, ambayo yalihudhuriwa na Witkoff, Kushner na Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio.

    Wakati mazungumzo ya Jumanne yakiendelea, Trump aliliambia baraza lake la mawaziri mjini Washington kwamba mzozo huo si rahisi kuusuluhishwa.

    Pia unaweza kusoma:

  16. Hujambo na karibu

    Nakukaribisha katika taarifa zetu za moja kwa moja, leo Jumatano tarehe 3 Disemba, 2025