Uchaguzi wa Kenya 2022: Wakikuyu wagawanyika kati ya Ruto na Odinga

Supporters hold painted portraits of Kenya's President Uhuru Kenyatta (L), Azimio La Umoja Coalition presidential candidate Raila Odinga (C) and running mate Martha Karua during a campaign rally in Murang'a on July 23, 2022, ahead of Kenya's August 2022 general election

Chanzo cha picha, Getty Images

    • Author, Na Evelyne Musambi
    • Nafasi, BBC News, Nyeri

Katika jamii ya Wakikuyu wenye utajiri wa kura nchini Kenya, kuna maoni tofauti kuhusu hatua ya Rais anayemaliza muda wake Uhuru Kenyatta kumuunga mkono aliyekuwa mpinzani wake Raila Odinga, badala ya naibu wake William Ruto, kuwa mrithi wake katika uchaguzi wenye ushindani mkali unaotarajiwa kufanyika tarehe 9. Agosti.

Bw. Kenyatta - ambaye amefikia kikomo cha kikatiba cha mihula miwili madarakani - alichukuliwa kwa muda mrefu kama kinara wa kisiasa wa jami hiyo, huku wazee wake wakimtaja kwa fahari kuwa "mwana wetu".

Lakini wakati BBC ilipozuru jimbo la Nyeri - ambalo lipo katika eneo la Mlima -ilibainika kuwa uaminifu wake umepata pigo kutokana na uamuzi wake wa kumuidhinisha Bw Odinga katika kile alichokitaja kuwa jaribio la kubuni umoja wa kitaifa baada ya miongo kadhaa ya chuki za kisiasa.

Wakili Wahome Gikonyo alihisi kuwa Bw. Kenyatta amemsaliti Bw Ruto, ambaye alimsaidia kushinda uchaguzi dhidi ya Bw Odinga.

"Ruto alifanya kazi ya punda mwaka 2013 na 2017. Laiti sio yeye Uhuru hangelikuwa rais. Je hiyo ndiyo njia ya kumlipa rafiki?" Bw Gikonyo alisema alipokuwa akizungumza na BBC katika afisi yake katika mji makao makuu ya kaunti hiyo, inayojulikana kama Nyeri.

Baadhi ya wakazi, kama Mchungaji Hannah Kanyithere, alihisi Bw Kenyatta hangejiuhusisha na kinyang'anyiro cha kumtafuta mrithi wake.

"Kwanini rais anaegemea upande wowote katika uchaguzi huu? Hata kama naibu wake alikuwa mbaya, alipaswa kuw ana msimamo wa wastani," aliongeza.

Lakini dereva wa teksi Hassan Kahoro alikuwa na shauku sawa katika kumtetea Bw Kenyatta, akipendekeza kwamba, wakati ulikuwa umewadia kwa jamii ya Wajaluo kupata rais wao kwanza - Bw Odinga.

Hassan Kahoro

Chanzo cha picha, Peter Njoroge/BBC

Maelezo ya picha, Hassan Kahoro anasemajamii ya Wajaluo inastahili kupewa nafasi ya kuongozi

"Tunapaswa kupatia jamii ya Wajaluo nafasi ya kuongoza nchi hii. Nani alisema urais unastahili kuwa wa Wakikuyu na Wakalenjin?" Bw Kahoro alisema, huku akihutubia kundi la watu waliokuwa wamekusanyika katika soko kuu la eneo hilo.

Alikuwa anaashiria ukweli kwamba Kenya watatu kati ya marais wanne wa Kenya tangu tupate uhuru wamekuwa Wakikyu. Hayati Daniel arap Moi - ambaye alihudumu kwa muda mrefu kam rais wa Kenya (miaka24) alikuwa Mkalenjin, kama Bw Ruto.

Welder Jackson Maina pia aliridhika na hatua ya Bw Kenyatta kumuunga mkono "Baba", jina linalotumiwa ma wafuasi wake kumuita Bw Odinga mwenye umri wa miaka 77.

"Tuko imara nyuma ya rais na tuko nyuma ya Baba," alisema akiwa nje ya karakana yake.

Mji wa Nyeri umesheheni mabango ya kampeni uchaguzi mkuu unapokaribia.

Nyimbo za kuunga mkono kambi zote zinasikika.

Nyimbo moja - iliyoimbwa mwanamziki wa Kenya Ben Githae - inasema kwamba Kenya itakuwa salama mikononi mwa Bw Odinga na mgombea mwenza wake Martha Karua -waziri wa zamani wa haki na Mkikuyu anayechukuliwa kama "binti yao" kutoka Mlima Kenya.

Nyimbo nyingine - iliyoimbwa na Betty Maina - anawaasa watu kumpigia kura Bw Ruto, ambaye amemchagua Rigathi Gachagua- mwanabiashra Mkikuyu kutoka Kaunti ya Nyeri kama mgombea mwenza wake.

Naibu wa Rais William Ruto (Kulia) na mfanyabiashara Rigathi Gachagua wana matumaini ya kushinda uchaguzi

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Naibu wa Rais William Ruto (Kulia) na mfanyabiashara Rigathi Gachagua wana matumaini ya kushinda uchaguzi

Ingawa Bw Gachagua anakabiliwa na tuhuma za ufisadi, yeye ni mhamasishaji hodari na anapendwa sana na Wakikuyu wanaohangaika.

Bi Karua ni kinara wa kisiasa ambaye ana uungwaji mkono kitaifa kando na Wakikuyu - na anajulikana kwa shauku yake ya mageuzi ya mahakama na msimamo wake mkali dhidi ya ufisadi serikalini.

Lakini iwapo kura ya maoni ya hivi punde zaidi ya shirika la utafiti la Tifa itaaminika, si yeye wala Bw Kenyatta ambaye amewashawishi Wakikuyu walio wengi kumpigia kura Bw Odinga. Kura hiyo ya maoni inampa Bw Ruto uongozi kwa wingi katika Mlima Kenya - 66% dhidi ya 27% za Bw Odinga.

Katika ngazi ya kitaifa, picha ni tofauti, huku kura ya maoni ikimweka Bw Odinga mbele kwa tofauti ndogo ya 46.7% dhidi ya 44.4% - haitoshi kwake kupata urais, kwani mshindi anahitaji kura nyingi zaidi ya 50% ili kuepuka duru ya pili ya uchaguzi.

Nani yuko kwenye kinyang'anyiro cha kuiongoza Kenya ?

Fahamu zaidi kuwahusu wagombea urais wa Kenya

Chagua mgombea ili kutazama wasifu wake

Raila Amollo Odinga

Muungano wa Azimio la Umoja

  • Mgombea huyo mwenye umri wa miaka 77 ni mhandisi aliyesomea Chuo Kikuu cha Ufundi cha Magdeburg (sasa kinajulikana kama Chuo Kikuu cha Otto-von-Guericke Magdeburg) nchini Ujerumani.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya Azimio la Umoja One Kenya Coalition Party.
  • Hili litakuwa jaribio lake la tano baada ya kugombea katika: 1997, 2007, 2013 na 2017.
  • Bw Odinga alikuwa mmoja wa wapiganiaji wa demokrasia ya vyama vingi nchini Kenya. Alikamatwa, akafungwa na wakati fulani akaenda uhamishoni kwa sababu ya kupigania haki hiyo
  • Aliwahi kuwa Waziri Mkuu, kuanzia 2008-2013.
  • Odinga alihusika kufanikisha miradi mikubwa iliyotekelezwa na serikali ya Kibaki, kama vile miradi ya umeme vijijini na barabara.
  • Kuafikia ukuaji wa uchumi wa tarakimu mbili kupitia uwekezaji katika biashara ndogo ndogo na sekta ya viwanda.
  • Utoaji wa huduma bora za afya kwa wote.
  • Utoaji wa vifaa vya michezo na burudani kwa ukuaji wa kimwili, kiakili, kijamii, kimaadili na maendeleo ya watu.
  • Kufuatia jaribio la mapinduzi ya Agosti 1, 1982, Raila Odinga alikamatwa na kukabiliwa na mashtaka kadhaa, yakiwemo ya uhaini ambayo alizuiliwa bila kufunguliwa mashtaka. Tume ya Ukweli ya Haki na Maridhiano iliambiwa mwaka 2011 kwamba Odinga alikuwa na mawasiliano na mpangaji mkuu wa mapinduzi hayo. Odinga amekana kuhusika kila mara. - Makavazi ya Kitaifa ya Kenya.

William Samoei Ruto

Muungano wa Kenya Kwanza

  • Mgombea huyu mwenye umri wa miaka 55 ana Shahada ya Uzamifu/PhD katika Ikolojia ya Mimea na BSc katika Botany na Zoology kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi.
  • Anawania kiti cha urais kwa tikiti ya chama cha United Democratic Alliance ( chenye mafungamano na Kenya Kwanza).
  • Aliongoza Vuguvugu la vijana la Youth for Kanu '92 (YK'(92).
  • Wizara yake iliorodheshwa kama inayofanya bora zaidi serikalini alipokuwa Waziri wa Kilimo.
  • Alihudumu kama Naibu Rais wa kwanza wa Kenya chini ya katiba mpya ya 2010.
  • Alihudumu kama mbunge wa eneo bunge la Eldoret Kaskazini kuanzia 1997-2007.
  • Kutenga $424 milioni kila mwaka kwa biashara ndogo ndogo za kati.
  • Kuanzisha mfuko wa elimu wa kitaifa ili kukidhi gharama zisizo za masomo.
  • Tekeleza kikamilifu sheria ya usawa wa kijinsia ya thuluthi mbili katika uteuzi wa kisiasa na kutenga nusu ya baraza lake la mawaziri kwa wanawake.
  • Mnamo 2008, Mahakama Kuu ya Kenya iliamuru Naibu Rais William Ruto kusalimisha shamba la ekari 100 na kulipa $ 62,500 kwa Adrian Muteshi, mkulima ambaye alimshtaki kwa kuchukua mali hiyo baada ya uchaguzi wa 2007. - Kenya Law
  • Mnamo 2011, Bw Ruto alikabiliwa na kesi kwa makosa matatu dhidi ya binadamu: Mauaji, uhamisho wa watu kwa lazima na mateso ya watu katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu. Miaka mitano baadaye mahakama ilisitisha kesi hiyo kwa msingi kwamba - ushahidi wa upande wa mashtaka ulikuwa dhaifu. -ICC

George Wajackoyah

Chama cha Roots

  • Profesa huyo mwenye umri wa miaka 61 ana shahada ya uzamili katika sheria kuhusu maendeleo kutoka Chuo Kikuu cha Warwick na shahada ya uzamili , sheria (sheria za Marekani kutoka Chuo Kikuu cha Baltimore.
  • Bw Wajackoyah anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Roots Party.
  • Alihudumu kama Inspekta katika idara ya usalama ya Special branch wakati wa utawala wa marehemu Rais Daniel Moi kabla ya kulazimika kutorokea ng'ambo ili kuepuka kufunguliwa mashtaka na mamlaka.
  • Yeye ni mshirika katika kampuni ya mawakili aliyoianzisha mwaka wa 2018.
  • Alifunnza somo la sheria na uchumi katika vyuo vikuu vya Marekani, Uingereza na Kenya.
  • Kuhalalisha matumizi ya kiviwanda ya bangi
  • Badilisha siku za kazi hadi Jumatatu hadi Alhamisi.
  • Huduma ya afya ya bure na msaada kwa wazee, walio hatarini na wajawazito

David Mwaure Waihiga

Chama cha Agano

  • David Mwaure anawania kiti cha urais kwa tiketi ya Chama cha Agano.
  • Ni kiongozi wa Chama cha Agano.
  • Alihitimu na shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi na ana Shahada ya Uzamili katika masomo ya uongozi.
  • Yeye ni wakili mkuu na amehudumu kama mwanasheria kwa zaidi ya miongo mitatu.
  • Ana kampuni ya uwakili na amewania viti mbalimbali vya kisiasa.
  • Ilianzishwa chama cha Agano mwaka 2006.
  • Kupambana na ufisadi uliokithiri.
  • kuunda nafasi za ajira.
  • Kurejesha mali ya Kenya iliyofichwa nje ya nchi.

Pata maelezo zaidi kuhusu sera za wagombea urais hapa

Kwa hivyo pande hizo mbili zitakuwa na kibarua cha ziada kuvutia wapiga kura katika siku za mwisho za kampeni.

Uamuzi wa Bw Kenyatta kumuunga mkono Bw Odinga haikugawanja jamii yake tu bali pia familia yake.

Binamu yake Kungu Muigai aliviambia vyombo vya habari kuwa rais alienda kinyume na wazee wa Kikuyu kwa kukiuka mapatano ya 2013, yaliyoitaka jamii kuunga mkono Wakalenjin mara tu mihula miwili ya Bw Kenyatta itakapokamilika.

Mgawanyiko huo unalalamikiwa na wazee wa jamii ya Wakikuyu, kama alivyoelezea Nduhiu Njama mwenye umri wa miaka 100, na mkazi wa Tetu huko Nyeri.

"Tulipata uhuru kwa kuwa wamoja. Tunachokiona kwa sasa ni ubinafsi ambao utatugharimu," alisema huku akionyesha picha zake za zamani.

Wakikuyu hasa ni wakulima. Mashamba ya chai na kahawa, pamoja na mashamba ya maziwa, yanaenea katika Mlima Kenya.

Kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa eneo la Mlima Kenya.

Chanzo cha picha, PETER NJOROGE/BBC

Maelezo ya picha, Kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa eneo la Mlima Kenya.

Barabara za vijijini zimewekwa lami na kuwarahisishia wakulima kusafirisha mazao yao.

BBC ilitembelea wakulima karibu na mji wa Othaya, ambao ulikuwa nyumbani kwa marehemu Rais Mwai Kibaki.

Alipokuwa akiwapa lishe ng'ombe wake wa maziwa, George Wambugu alisema anamuunga mkono Bw Ruto.

"Ruto ni mkulima kama mimi na alipokuwa waziri wa kilimo alileta mageuzi ambayo yaliwafanya wakulima wa chai kupata bonasi ya juu zaidi kuwahi kutokea. Najua ataboresha sekta ya kilimo," baba wa watoto watatu mwenye umri wa miaka 40 alisema, akieleza. maoni ambayo yaliungwa mkono na baadhi ya wakulima wenzake.

Uchaguzi wa Kenya 2022: Vyama vinakuahidi nini?

Chagua suala ambalo linakuvutia

Sera za kila chama

  • Azimio La Umoja One Kenya Coalition

  • Roots Party of Kenya

  • Chama cha Agano

  • Kenya Kwanza Alliance

Mwongozo huu ni muhtasari wa sera kuu zinazotolewa na kila chama.

Pata maelezo zaidi kuhusu wagombea urais wa Kenya hapa

End of Uchaguzi wa Kenya 2022: Vyama vinakuahidi nini?
1px transparent line
.

Unaweza pia kusoma

,