Wanawake waliopigana katika vita vya wenyewe kwa wenyewe hawataki kuona vita vingine tena

Chanzo cha picha, Abeba Amdu
Abeba Amdu mwenye umri wa miaka 22 ameona baadhi ya miaka bora ya maisha yake ikimezwa na vita na hana hamu ya kushuhudia mgogoro mwingine ukizuka katika eneo la kaskazini la Tigray nchini Ethiopia, jambo ambalo baadhi ya watu wanaogopa linaweza kutokea.
Alikwenda kwenye mstari wa mbele mwaka 2020 kama askari wa Tigray kupigana katika vita vya wenyewe kwa wenyewe dhidi ya jeshi la shirikisho, na bado anaendelea kuathirika kisaikolojia kutokana na aliyoyapitia, zaidi ya miaka mitatu baada ya kumalizika kwa mgogoro huo mkali.
"Nilipoteza kila kitu," aliiambia BBC Tigrinya.
Kabla ya vita, Abeba alikuwa nyota anayechipukia wa soka. Alicheza soka tangu akiwa na miaka saba, na hatimaye akiwa na umri wa miaka 17 akawa mshambuliaji wa timu ya wanawake ya 70 Enderta.
Alijiona kama mtetezi wa haki za wanawake, akipinga mitazamo ya kitamaduni kuhusu ushiriki wa wanawake katika michezo. Msichana huyo pia alikuwa mwanafunzi bora, akisoma Teknolojia ya Habari (IT) katika jiji kuu la Tigray la Mekelle, na alikuwa na maono kuhusu mustakabali wake.
Kisha dunia aliyokuwa akiijua ilisimama ghafla. Kwanza kulikuwepo na janga la corona, ambalo lilisababisha kusimamishwa kwa masomo yake. Kisha vita vikaanza.
"Sikuwa naamini katika vita, kwa sababu nilijua wazazi wangu walipitia nini," anasema.
Abeba alikuwa akimaanisha kwamba mama na baba yake walibeba makovu ya vita vya muda mrefu na vya kikatili vilivyomalizika mwaka 1991, wakati Tigray People's Liberation Front (TPLF) ilipomuondoa madarakani mtawala wa Ethiopia wa wakati huo, Mengistu Haile Mariam.
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
Baadaye TPLF ilitawala serikali ya shirikisho hadi mwaka 2018, wakati Waziri Mkuu wa sasa Abiy Ahmed alipoingia madarakani kufuatia maandamano makubwa dhidi ya utawala uliodaiwa kuwa wa ukandamizaji.
TPLF kisha ilirejea katika ngome yake ya Tigray, na ikapata mgogoro mkubwa na Abiy kuhusu mwelekeo wa baadaye wa nchi.
Mgogoro kati ya pande hizo mbili ulizuka mwaka 2020, huku nchi jirani ya Eritrea ikiingia vitani upande wa jeshi la shirikisho.
Vita vilimalizika miaka miwili baadaye baada ya makubaliano ya amani yaliyosimamiwa na Umoja wa Afrika (AU). Mjumbe wake, Rais wa zamani wa Nigeria Olusegun Obasanjo, alikadiria idadi ya waliokufa katika mgogoro huo kuwa takriban 600,000.
Kwa Abeba, wito wa kushika silaha haukuwa tu chaguo, ulikuwa kama urithi wa wajibu.
Alikulia katika familia iliyokuwa imejikita sana katika historia na hadithi za TPLF, akilelewa akisikiliza simulizi za kujitolea kwa baba yake aliyepigana dhidi ya utawala wa Mengistu miaka karibu 50 iliyopita. Uzalendo na kujitolea kwa nchi vilikuwa sehemu muhimu ya malezi yake.
Lakini uamuzi wake wa kujiunga na tawi la kijeshi la TPLF, Tigray Defence Forces (TDF), pia ulikuwa jibu la kukata tamaa kutokana na hofu ya kubakwa, baada ya kusikia kuhusu wanawake waliokuwa wakifanyiwa ukatili wa kingono na "adui".
"Wahalifu hawakumfuata mtu mmoja tu; ningepata hatima ileile kama waathirika wengine. Hali nzima ndiyo iliyonilazimisha kupigana."
Msisimko wa michezo ulipisha nafasi uhalisia wa vita. Kulikuwa na njaa ya mara kwa mara na ukosefu wa mahitaji ya msingi, ikiwemo sodo.
Hata hivyo, mwisho wa vita haukuleta amani ambayo Abeba alikuwa ameitarajia. Kurudi kwa familia yake na katika kazi yake kuligeuka kuwa kama uwanja mwingine wa mapambano.
"Mwili wangu na akili yangu vyote vimeathirika sana kisaikolojia."
Anajikuta akipambana na upweke na kujitenga, akihisi kuwa watu ambao hawakupitia aliyopitia hawamwelewi.
"Ni sasa ndipo ninaanza kuelewa tabia ya baba yangu, tabia ya mpiganaji huwa na hisia fulani ya hasira. Sasa natambua kwamba ilikuwa kwa sababu hakuwahi kupona kiakili."
Abeba anaelezea maisha yake kama mzunguko wa huzuni na migogoro, kubishana na wapendwa wake, kuacha kazi mara kwa mara, na kulia peke yake.
Mkusanyiko wa umakini unaohitajika katika soka la kitaaluma ulikuwa umetoweka.
Ingawa alijaribu kurudi mazoezini, uzito wa "miaka iliyopotea" ulimfanya ashindwe kurudisha kiwango chake cha zamani.
Ili kuelekeza maumivu yake katika kitu chenye manufaa, Abeba alifanya kazi kwa muda mfupi kama mwandishi wa habari, na pia alianzisha mradi wa wanawake uitwao "Wegahta", uliolenga kuwalea na kuwashauri wasichana 30 vijana wanaocheza soka.
Alitumaini kusaidia kukuza kizazi kipya cha wachezaji, lakini ukosefu wa fedha hatimaye uliifanya juhudi hiyo kusimama.
Mwisho wa yote, Abeba anaona jitihada hizi kama njia ya kutafuta mahali pa kujisitiri au kupata faraja, badala ya kuwa tu hatua ya kawaida ya kazi.
"Nafanya haya yote ili nipate mahali pa kujificha."

Chanzo cha picha, Selam Hailu
Hofu kubwa ya Abeba ni kwamba vita vinaweza kuzuka tena.
Mwishoni mwa Januari kuliripotiwa mapigano mafupi kati ya wanajeshi wa serikali ya shirikisho na wapiganaji wa Tigray, ambao wanadai kurejeshewa maeneo yaliyotekwa na mkoa jirani wa Amhara wakati wa vita.
Mashambulizi ya ndege zisizo na rubani (drones) yalipiga Tigray, na safari za ndege kwenda miji ya eneo hilo zilisitishwa kwa karibu wiki moja.
Serikali ya shirikisho pia imeishutumu Eritrea kwa kuingilia mambo katika eneo hilo, lakini safari hii ikidaiwa kuunga mkono vikosi vya Tigray. Eritrea imekanusha madai hayo.
Kwa upande wake, TPLF inaituhumu serikali ya shirikisho kwa kupeleka wanajeshi karibu na mipaka ya Tigray kama maandalizi ya mapigano mapya, wakati Waziri Mkuu Abiy Ahmed analishutumu kundi hilo kwa kuhamisha fedha za serikali ili kuendeleza vikosi vyake.
"Kwa sasa, naona hofu kila mahali, hofu ya mgogoro mwingine," Abeba anasema.
"Siamini kwamba vita ni lazima. Tumeona kwamba mwishowe, mazungumzo, si mapigano, ndiyo yanayotoa suluhisho."
Selam Hailu, mwanasheria mwenye umri wa miaka 30 na mama wa watoto wawili, pia ni mkongwe wa mstari wa mbele vitani na anaunga mkono hisia hizo.
Alijiunga na mapigano mwezi Septemba 2021 wakati tayari alikuwa mama, mtoto wake mkubwa akiwa na miaka mitano tu.
Sababu yake ilikuwa ya binafsi sana. Wazazi wake, waliokuwa wafanyakazi wa serikali waliostaafu na ambao tayari walikuwa wamejiunga na vita, walirudi nyumbani wakiwa wamechoka sana na katika hali mbaya.
Baada ya kuona mateso yao na kusikia simulizi zao kuhusu "ukatili wa kingono na mauaji ya watu wengi", Selam anasema alihisi kulazimika kuchukua hatua, na pamoja na mdogo wake, walikwenda kujiunga na vikosi vya Tigray.
Kama wanawake wengine wengi, kwanza walipata mafunzo mafupi lakini makali ya kijeshi.
Selam anasema maisha milimani katika Tigray yalikuwa magumu sana.
"Kwa upande wangu, ilikuwa vigumu hata kujisaidia porini," anasema.
Dhiki ilizidishwa na ubaguzi wa kijinsia.
"Hakuna anayeelewa tunapokuwa kwenye hedhi na tabia zetu hubadilika," Selam anaeleza.
Hata hivyo, pambano gumu zaidi lilikuwa dhidi ya uongozi wa kijeshi.
"Tatizo ndani ya jeshi lilikuwa kwamba hawakuamini kuwa mwanamke ana kipaji au uwezo," anasema.
Aligundua kwamba mpiganaji wa kike wa umri wa ujana ambaye "hakuogopa risasi, aliogopa neno la afisa au adhabu yake," na wengi wao walikaa kimya walipolazimishwa kuingia katika mahusiano.
Kwa kuwa yeye alikuwa mkubwa kidogo na pia mwanasheria, alizungumza wazi dhidi ya "mahusiano yasiyo ya kimaadili" kama hayo na akaadhibiwa kwa kuwekwa kizuizini kwa usiku mmoja.
Selam pia ana wasiwasi kwamba vita vinaweza kuzuka tena:
"Vijana wanakimbia mji kwa njia yoyote ile, halali au haramu. Tunaweza kuona hofu kwenye nyuso za kila mtu.
"Watu wanahifadhi chochote wanachoweza, wakiwa na uhakika kwamba akiba zao ndizo pekee zitakazowatenganisha na maangamizi.
"Hakuna anayehitaji amani zaidi kuliko sisi, hatuwezi kabisa kumudu tena kujitoa muhanga kwa mara nyingine."

Chanzo cha picha, Rahwa Gebremedhin
Kwa Rahwa Gebremedhin mwenye umri wa miaka 30, mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Mekelle, vita vilikuwa kama kuingilia ndoto zake badala ya kuwa sababu ya kisiasa yenye maana.
Maisha yake ya kitaaluma yalikuwa ndiyo yanaanza, na alikuwa na matarajio ya kuwa na nyumba, gari, na watoto.
Hata hivyo, alijiunga na majeshi ya Tigray kutokana na ukatili uliofanywa na "majeshi ya adui".
"Nilishtushwa na mauaji. Nilikuwa na hasira kwa sababu wanawake walibakwa na kila kitu kilikuwa kinaharibiwa."
Kama msomi, maarifa yake kuhusu jeshi yalitokana zaidi na filamu za vita.
"Ilikuwa vigumu, kujifunza mazingira ya vita, kushika silaha, na kupata mafunzo," anasema.
Madhara ya kihisia na kisaikolojia ya vita yalikuwa makubwa sana, na kurejea kwenye maisha ya kiraia imekuwa changamoto.
"Unaweza kuona dalili zote za msongo wa mawazo baada ya tukio la kutisha kwangu. Kila mwanamke alipata mshtuko wa kisaikolojia.
"Nilirudi kwenye kazi yangu ya kufundisha, lakini si kama ilivyokuwa. Sihisi chochote.
"Ninajaribu tu kuishi."














