Juma Duni Haji: Safari yake ya kisiasa ndani na nje ya gereza

    • Author, Rashid Abdallah
    • Nafasi, Mchambuzi, Tanzania

Haji

Chanzo cha picha, ACT WAZALENDO

Juma Duni Haji ama 'Babu Duni' anavyojulikana kwa wafuasi wake, ni mwanasiasa mtiifu wa upinzani. Enzi za uhai wa Seif Sharif Hamad (almaarufu Maalim Seif) hadi anafariki, hakukushuhudiwa mvutano wa hadharani kati ya Babu Duni na Maalim.

Yuko kwenye siasa za upinzani kwa takribani miongo mitatu sasa. Ameshika nafasi mbalimbali za ndani ya Chama cha Wananchi (CUF); Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Mkurugenzi wa Uchumi na Fedha Taifa, Makamu Mwenyekiti, na Mjumbe wa Baraza Kuu la Uongozi Taifa.

Kuhama Vyama

Mwenyekiti huyo mpya wa ACT Wazalendo taifa, alianza safari yake ya kisiasa muda mrefu. Tangu akiwa mwanafunzi katika skuli ya sekondari ya Gamal Abdul Nasir, (sasa inaitwa Beit el Ras), alipokuwa mwenyekiti wa umoja wa vijana wa Afro-Shirazi Party (ASP).

Alifanya kazi kwa miaka mingi katika sekta ya elimu Zanzibar akiwa Mwalimu na kushika nyadhifa mbalimbali katika taasisi tofauti. Hizo zilikuwa ni nyakati akiwa ndani ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ).

Juma Duni Hajj

Chanzo cha picha, ACT WAZALENDO

Baada ya kuunganishwa ASP na TANU Februari 5, 1977, na kupatikana Chama cha Mapinduzi (CCM), wanachama wa vyama hivyo viwili wakawa wanachama wa chama kipya kilicholeta muungano wa kivyama kati ya Tanganyika na Zanzibar.

Duni aliihama CCM baada ya mfumo wa vyama vingi kurejeshwa kisheria Julai Mosi,1992. Kulikuwa na kundi la waasi wengine walioikimbia CCM, ambao baadaye wakawa viongozi wa ngazi ya juu wa Civic United Front (CUF), akiwemo Seif Sharif Hamad.

Amekuwa mgombea mwenza wa nafasi ya urais mara nne upande wa Muungano wa Tanzania katika chaguzi za 1995, 2005 na 2010 akiwa na Profesa Ibrahim Lipumba. Mara zote CCM ikatangazwa mshindi.

Juma Duni Haji

Chanzo cha picha, ACT WAZALENDO

Wakati wa vuguvugu la Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), Duni alihamia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa muda mfupi. Alikuwa mgombea mwenza kwa mara ya nne katika uchaguzi wa 2015 WA Muungano, akiwa na Edward Lowassa.

Ilipopatikana Serikali ya Umoja wa Kitaifa , Zanzibar baada ya uchaguzi wa 2010. Akiwa katika Baraza la Wawakilishi, aliteuliwa kuwa Waziri wa Afya. Mbadiliko madogo ya baraza hilo 2014 yalimhamisha na kumpeleka Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano.

Ulipovuma upepo wa kisiasa wa 'shusha tanga pandisha tanga,' kufuatia mzozo mkali ndani ya CUF wanachama wa CUF walikihama chama hicho wakiongozwa na Maalim Seif na kuhamia ACT Wazalendo, Machi 2019. Juma Duni Haji alikuwa miongoni mwa waliohamia ACT.

Mfungwa wa Kisiasa

Novemba 1997, siku ya mwisho ya kampeni za uchaguzi mdogo katika jimbo la Mkunazini, Unguja. Wafuasi kadhaa wa CUF walikamatwa. Kamatakamata iliendelea hadi 1998, ambapo Duni naye alitiwa mikononi mwezi Mei mwaka huo. Tuhuma zikawa ni kutaka kupindua serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Shirika la kutetea haki za binaadamu la Amnesty International lilieleza wasiwasi wake katika ripoti kuwa wafungwa 18 wako ndani kutokana na maoni yao yasiyo ya vurugu na shughuli zao za kisiasa. Ripoti hiyo ya Januari 2000 iliwaita wafungwa hao ni wa kisiasa.

Tuhuma zilizowakabili zilisababisha kufunguliwa kesi ya uhaini. Duni alikaa gerezani kwa miaka miwili na nusu, na baadhi ya wafuasi walikaa miaka mitatu huku kesi ikiendeshwa na Jaji Garba Tumaka wa Nigeria.

WAZALENDO

Chanzo cha picha, ACT WAZALENDO

Maelezo ya picha, Mkutano wa ACT Wazalendo

Hatimaye Rais wa wanne wa visiwa hivyo aliyetawala kutoka 1990 - 2000, Salmin Amour aliamuru waachiwe huru kabla ya uchaguzi mkuu 2000. Ifahamike pia kuwa mwaka huo huo wa 2000 Mahakama ya Rufaa Tanzania ilitamka kupitia uamuzi wake kuwa Zanzibar hakuwezi kutendeka kosa la uhaini kwani Zanzibar si Dola (Sovereign State) bali ipo chini ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Duni alishikiliwa tena baada ya maandamano ya Januari 27, 2001, yaliyofanywa na wafuasi wa CUF, Unguja na Pemba, (chama kikuu cha upinzani wakati huo). Msingi wa maandamano hayo ni kutoridhishwa na matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2000.

Mara hii kesi ya Duni ilikuwa ni tuhuma za kuua Askari. Mwenyewe anaeleza ajabu ya kesi hiyo; ni kutuhumiwa kumuua Askari aliyeko kisiwani Pemba wakati siku ya tukio Haji Duni alikuwa kisiwani Unguja.

Oktoba 15, 2001 Juma Duni Haji aliachiwa huru baada ya mahakama kufuta kesi hiyo. Pia makumi ya wafuasi wengine waliokamatwa katika maandamano walikuwa tayari wameachiwa huru miezi ya nyuma. Hatua hiyo ilikuja kufuatia mazungumzo ya kisiasa kati ya CCM na CUF.

Historia ya siasa za Zanzibar ni za panda-shuka, viatu mkononi. Duni amepita katika milima na mabonde ya siasa hizo. Mwenyewe anaeleza hana tena cha kupoteza na kukaa kwake gerezani kumemuongezea ujasiri.

Mwanzo wake

Juma Duni Haji alizaliwa Novemba 1950, katika kijiji cha Kibeni, Mkoa wa Kaskazini Unguja. Elimu yake ya msingi aliipata katika Skuli ya Mkwajuni, Unguja, kati ya mwaka 1958 hadi 1965.

Elimu ya sekondari aliipata katika skuli ya Gamal Abdel Nassar na Lumumba. Kisha alijiunga na chuo kikuu cha Dar es Salaam, mwanzoni mwa miaka ya 70 kwa shahada ya kwanza ya Ualimu wa masomo ya sayansi.

Safari yake ya kusaka elimu ilimfikisha katika vyuo vikuu vya Uingereza. Chuo cha Reading miaka ya 1978-1979. Alirudi tena Uingereza katika chuo Kikuu cha Manchester 1993 hadi alipohitimu shahada ya pili.

Amekusanya elimu katika masomo ya ualimu wa sayansi, biashara na usimamizi wa rasilimali watu. Maisha ya kifamilia ya mwanasiasa huyo daima yamebaki kuwa jambo binafsi.

Unaweza pia kusikiliza:

Maelezo ya sauti, Maalim Seif Sharif Hamad: na viongozi wenzake kukabidhiwa uanachama ACT Wazalendo