Msemaji wa jeshi Hamas Abu Obeida auawa

Kundi la Kipalestina la Hamas limethibitisha kuwa msemaji wake wa kijeshi, Abu Obeida, pamoja na kiongozi wa zamani wa Gaza, Mohammed Sinwar, waliuawa na jeshi la Israel.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Rashid Abdallah

  1. Msemaji wa jeshi Hamas Abu Obeida auawa

    s

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Kundi la Kipalestina la Hamas limethibitisha kuwa msemaji wake wa kijeshi, Abu Obeida, pamoja na kiongozi wa zamani wa Gaza, Mohammed Sinwar, waliuawa na jeshi la Israel.

    Kundi hilo kupitia brigedi ya Qassam ilitangaza taarifa hiyo ya kuthibitisha hilo Jumatatu. Pia zilithibitisha vifo vya Mohammed Shabanah, kiongozi wa tawi la Rafah, pamoja na viongozi wengine wawili, Hakam al-Issi na Raed Saad.

    Jeshi la Israeli lilisema mwezi Mei kwamba liliwaua Sinwar, kaka mdogo wa kiongozi wa zamani wa Hamas, Yahya Sinwar. Miezi mitatu baadaye, lilidai pia kwamba lilimuua Abu Obeida.

    Hamas imethibitisha kuwa jina halisi la Abu Obeida lilikuwa Huthaifa al-Kahlout.

    Taarifa ya mwisho ya Abu Obeida ilikuwa mwanzoni mwa Septemba wakati Israel ilipoanza hatua za awali za shambulio jipya la kijeshi kwenye Jiji la Gaza, ikitangaza eneo hilo kama kizuizi cha mapambano huku ikiharibu mamia ya majengo ya makazi na mamilioni ya Wapalestina walikimbia makazi yao.

    Abu Obeida alikuwa sauti muhimu ya Hamas huko Gaza, akitoa taarifa kuhusu hali ya mapambano, ukiukaji wa makubaliano ya kusitisha mapigano, na makubaliano ya kubadilishana wafungwa kati ya Wapalestina na Israel mwanzoni mwa mwaka huu wakati wa mapumziko ya muda mfupi ya amani, ambayo Israel iliyavunja.

    Sinwar na Abu Obeida ni wawakilishi wa hivi karibuni wa Hamas waliothibitishwa kuuawa na Israel katika miaka miwili iliyopita, ikiwa ni pamoja na viongozi wengi wa ngazi ya juu wa kijeshi na kisiasa wa Hamas, kama vile kiongozi wa kisiasa Yahya Sinwar; kamanda wa kijeshi Mohammed Deif, mmoja wa waanzilishi wa Brigedi za Qassam miaka ya 1990; na kiongozi wa kisiasa Ismail Haniyeh, aliyeuawa katika mji mkuu wa Iran, Tehran.

  2. Marekani kuipa Ukraine dhamana za usalama kwa miaka 15 – Zelensky

    s

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Marekani imeitoa dhamana za usalama kwa Ukraine kwa kipindi cha miaka 15, amesema Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky, wakati wa mazungumzo kuhusu mpango wa amani uliorekebishwa na Donald Trump huko Florida Jumapili.

    Rais wa Marekani alisema kwamba makubaliano kuhusu suala hili yamekaribia kufikiwa kwa "asilimia 95%", lakini kiongozi wa Ukraine amesisitiza kwamba angependa dhamana hizo ziwe hadi miaka 50.

    Rais Zelensky alieleza masuala ya eneo na kiwanda cha nyuklia kilichotawaliwa na Urusi huko Zaporizhzhia kama mambo ya mwisho yanayohitaji suluhu, na hatma ya eneo la Donbas lililo na utata nchini Ukraine.

    Urusi awali ilikataa sehemu muhimu za mpango huo, lakini msemaji wa Kremlini alikubaliana Jumatatu na tathmini ya Trump kwamba amani iko karibu, ripoti ya shirika la habari la Urusi Tass iliripoti.

    Akizungumza na waandishi wa habari, baada ya mkutano wa Jumapili, Zelensky alirudia imani yake kwamba makubaliano ya amani kwa jumla yamefika 90%, ni takwimu aliyotoa kabla ya ziara hiyo.

    Viongozi wa Marekani na Ukraine pia walionyesha kwamba kumekuwa na maendeleo kuhusu kizuizi kimoja muhimu, dhamana za usalama kwa Ukraine. Shirika la habari la Reuters liliripoti kwamba Zelensky anatumai dhamana yoyote ya usalama itaanza mara Kyiv itakaposaini makubaliano ya amani.

    "Pasipo dhamana za usalama, vita hivi haviwezi kuonekana vimeisha kweli. Hatuwezi kukiri kwamba vimeisha, kwa sababu tukikabiliwa na jirani kama huyu bado kuna hatari ya shambulio jipya," Zelensky alieleza, kulingana na ripoti ya AFP.

    Aliongeza kwamba anataka Marekani "kuzingatia zaidi uwezekano wa miaka 30, 40, 50".

    Marekani bado hajajibu kuhusu kuongezwa kwa muda huo. Jumapili, Trump alisema makubaliano yako karibu kufikiwa.

  3. Anthony Joshua ajeruhiwa katika ajali ya gari Nigeria, wawili wafariki dunia

    s

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Shujaa wa ngumi za uzito wa juu duniani raia wa Uingereza, Anthony Joshua, amejeruhiwa katika ajali ya gari iliyotokea leo katika barabara kuu ya Ogun–Lagos, Nigeria, ambapo watu wawili wamefariki dunia.

    Polisi wa jimbo la Ogun wamesema kuwa Joshua, mwenye umri wa miaka 36 na mzaliwa wa familia yenye asili ya Sagamu, Nigeria amepata majeraha madogo lakini yupo salama. Wengine waliokuwa wamejeruhiwa walikimbizwa hospitalini..

    Vyombo vya habari vya ndani vimeripoti kuwa Joshua alikuwa nyuma ya dereva wakati gari lake, aina ya Lexus, lilipogonga lori lililokuwa limeegeshwa. Mashuhuda walisema kuwa gari hilo lilikuwa na abiria wanne, akiwemo Joshua. Watu wake wa ulinzi walikuwa katika gari lingine lililokuwa nyuma yao kabla ya kutokea kwa ajali hiyo.

    Masaa machache kabla ya ajali, Joshua alishiriki video kwenye Instagram akiwa akicheza tenisi na mtu mwingine. Joshua alikuwa nchini Nigeria baada ya mechi yake na Jake Paul mnamo 19 Desemba, lakini haijajulikana kwa uhakika wakati na mahali video hiyo ilipigwa.

    Polisi na vyombo vya habari vya ndani vinaendelea kufuatilia hali ya Joshua na pamoja na uchunguzi zaidi wa ajali hiyo.

  4. Thailand yailaumu Cambodia kwa kuvunja makubaliano mapya ya kusitisha mapigano

    s

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Jeshi la Thailand lilaulaumua Cambodia kwa kuvunja makubaliano mapya ya kusitisha mapigano, yaliyotiwa saini baada ya wiki kadhaa za mabishano yaliyopelekea karibu watu milioni moja ykukimbia makazi yao.

    Jeshi la Thailand limesema kuwa zaidi ya ndege zisizo na rubani (UAV) 250 zilionekana zikiruka kutoka upande wa Cambodia Jumapili usiku.

    Katika taarifa, jeshi la Thailand limesema kwamba hatua ya Cambodia “ni ukiukaji wa hatua zilizokusudiwa kupunguza mvutano”, huku ikionekana kutokubaliana na masharti ya kusitisha mapigano.

    Jeshi hilo pia limesema linaweza kufikiria upya kuhusu kuachiliwa kwa wanajeshi 18 wa Cambodia waliokuwa wameshikiliwa Thailand tangu Julai.

    Cambodia bado haijatoa kauli yoyote kuhusu madai haya.

    Hii inatokea masaa machache tu baada ya Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Wang Yi, kusifu hatua ya kusitishwa kwa mapigano iliyofikiwa kwa juhudi kubwa, na Rais wa Marekani, Donald Trump

    China imesifu pia kumalizika haraka kwa mzozo na kwa haki kwa makubaliano muhimu.

  5. Trump na Netanyahu kukutana Florida kuijadili Iran na Gaza

    s

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amesafiri kwenda Florida kukutana na Rais wa Marekani Donald Trump. Netanyahu anatarajiwa kufanya mikutano tofauti leo, Jumatatu, na Rais Trump pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio.

    Hatima ya Ukanda wa Gaza na mpango wa makombora ya Iran ni miongoni mwa mambo muhimu yatakayojadiliwa katika mazungumzo kati ya Netanyahu na Donald Trump.

    Hali ya usalama nchini Lebanon pamoja na suala la kunyang’anywa silaha kwa kundi la Hezbollah pia ni masuala muhimu katika ajenda ya mazungumzo hayo.

    Hii ni ziara ya tano ya Waziri Mkuu wa Israel nchini Marekani tangu aliporejea madarakani. Mkutano huu kati ya viongozi wa Marekani na Israel unafanyika wakati ambapo kipaumbele cha Rais Trump ni kutangaza utekelezaji wa awamu ya pili ya mpango wa amani wa Gaza unaotarajiwa kuanza mwezi ujao, huku Benjamin Netanyahu akisisitiza zaidi kuzingatia kile anachokiita “tishio la Iran.”

    Awamu ya kwanza ya mpango huo, uliokubaliwa mwezi Oktoba, ilijumuisha kusitisha mapigano, kuondolewa kwa sehemu kwa wanajeshi wa Israel kutoka Ukanda wa Gaza, pamoja na kuwasilishwa kwa misaada ya kibinadamu.

    Awamu ya pili inajumuisha kuundwa kwa serikali ya kitaalamu katika Ukanda wa Gaza, kupelekwa kwa kikosi cha kimataifa cha kuimarisha usalama, pamoja na kunyang’anywa silaha taratibu kwa Hamas.

    Serikali ya Israel inasisitiza kuwa ujenzi upya wa Gaza haupaswi kuanza hadi Hamas itakaponyang’anywa silaha kikamilifu na mateka wote kuachiliwa.

    Hamas tayari imerudisha mateka au mabaki yao, lakini bado haijarudisha mwili wa Sajenti Ron Gweli nchini Israel. Baraza la usalama la Israel pia limekataa kufungua kikamilifu mpaka wa Rafah.

  6. Doumbouya anatarajiwa kushinda uchaguzi Guinea

    w

    Chanzo cha picha, Reuters

    Guinea ilipiga kura jana, Jumapili, katika uchaguzi wa rais unaotarajiwa kumrejesha Mamady Doumbouya, aliyechukua madaraka kupitia mapinduzi ya kijeshi mnamo 2021.

    Kurejea kwa Kiongozi huyo kutafanya atumikie muhula wa miaka saba, na kuhitimisha utawala wa mpito wa taifa hilo la Afrika Magharibi na sasa kurudi kwenye utawala wa kiraia.

    Doumbouya, mwenye umri wa miaka karibu 40, anakabiliana na wagombea wanne katika kinyang’anyiro hicho kinachoonekana kuwa na wagombea wengi wasio na upiinzani madhubuti.

    Rais aliyefukuzwa, Alpha Conde, na kiongozi wa muda mrefu wa upinzani, Cellou Dalein Diallo, bado wako uhamishoni.

    Idadi ya wapiga kura kuhusiana na mji mkuu Conakry ilionekana kuwa kidogo huku baadhi ya wapiga kura wakieleza uchaguzi huu kama matokeo yake tayari yameamuliwa.

    “Mambo muhimu zaidi ni kwamba nchi irudi katika hali ya kawaida. Mimi ni mtu wa kutumia akili kwa vitendo. Nimepiga kura kwa yule aliye madarakani na anayeendelea kuendeleza utendaji wa serikali,” alisema Moussa Kaba, muuzaji wa bidhaa, akizungumza na Reuters.

  7. Ronaldo asema hatastaafu soka hadi afikishe mabao 1,000

    o

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Cristiano Ronaldo alijiunga na klabu ya Al-Nassr ya Saudi Arabia 2022

    Nahodha wa Ureno Cristiano Ronaldo amesema hatastaafu kucheza soka hadi atakapofunga bao lake la 1,000.

    Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 40 alifunga mabao mawili katika ushindi wa Al-Nassr wa 3-0 dhidi ya Al Akhdoud siku ya Jumamosi na kufikisha jumla ya mabao 956 aliyofunga kwa klabu na timu ya taifa.

    Mshambuliaji huyo, ambaye alijiunga na Al-Nassr 2022, alisaini mkataba mpya wa miaka miwili na klabu hiyo ya Saudi Arabia Julai iliyopita ambao unampeleka zaidi ya siku yake ya kuzaliwa ya kutimiza miaka 42.

    Akizungumza baada ya kutajwa kuwa Mchezaji Bora wa Mashariki ya Kati katika Tuzo za Soka za Globe huko Dubai siku ya Jumapili, Ronaldo alisema: "Ni vigumu kuendelea kucheza, lakini nina motisha."

    "Shauku yangu ni kubwa na ninataka kuendelea. Haijalishi nacheza wapi, iwe Mashariki ya Kati au Ulaya. Nafurahia kucheza mpira kila wakati na nataka kuendelea."

    "Mnajua lengo langu ni nini. Nataka kushinda mataji na nataka kufikia idadi hiyo [mabao 1,000]. Nitafikia idadi hiyo bila shaka, ikiwa sitopata majeraha."

    Katika mahojiano na Piers Morgan mwezi uliopita, Ronaldo alisema anapanga kustaafu soka "hivi karibuni."

    Ronaldo amefunga mabao 13 katika mechi 14 msimu huu akiwa na Al-Nassr, na wako mbele kwa pointi nne kileleni mwa jedwali katika Ligi ya Saudi Pro.

    Ronaldo anashikilia rekodi ya kufunga mabao mengi zaidi kwa Ureno (143) na Real Madrid (450), na ndiye mchezaji pekee aliyefunga mabao zaidi ya 100 kwa vilabu vinne - Manchester United, Real Madrid, Juventus na Al-Nassr.

    Mshambuliaji huyo alisema mwezi Novemba kwamba Kombe la Dunia la 2026 nchini Marekani, Canada na Mexico litakuwa mashindano yake ya mwisho ya kimataifa.

    Alikuwa nahodha wa Ureno waliposhinda Euro 2016 nchini Ufaransa.

  8. Moto waua watu 16 katika nyumba ya wazee

    sd

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Baadhi ya wazee walihamishwa wakati nyumba yao iliposhika moto

    Watu kumi na sita wamefariki na watatu wamejeruhiwa baada ya moto kuteketeza nyumba ya wazee kaskazini mwa Indonesia, imesema serikali ya mtaa.

    Idara ya zimamoto iliarifiwa kuhusu moto katika nyumba ya wazee ya Damai katika jiji la Manado, mji mkuu wa jimbo la Sulawesi Kaskazini, Jumapili usiku.

    Waliofariki wengi walipatikana ndani ya vyumba vyao, mkuu wa zimamoto na uokoaji la jiji hilo Jimmy Rotinsulu aliliambia shirika la habari la AFP.

    Polisi bado wanachunguza chanzo cha moto huo, ambao umezimwa usiku huo huo.

    Polisi wanajaribu kuwatambua marehemu, wakiwasihi wanafamilia kuwasiliana na hospitali ambapo miili hiyo imepelekwa.

    Wengi wao walikuwa katika hali "isiyotambulika," afisa mmoja wa eneo hilo alikiambia chombo cha habari cha mtandaoni cha Detikcom.

    Mapema mwezi huu, moto katika jengo lenye ghorofa saba katika mji mkuu wa Jakarta uliwaua watu 22.

  9. Shujaa wa Bondi asimulia alivyomnyang'anya silaha mshambuliaji

    D

    Chanzo cha picha, CBS

    Mwanaume aliyemnyang'anya silaha mmoja wa watu waliowaua watu 15 huko Bondi Beach, Australia aeleza kilichotokea.

    Katika video, Ahmed al Ahmed - mmiliki wa duka huko Sydney aliyezaliwa na kukulia nchini Syria - alimkabili kutokea nyuma mmoja wa wafyatuaji risasi wawili.

    "Nilimshika kwa mkono wangu wa kulia na kuanza kusema maneno, kama kumwonya - 'dondosha bunduki yako, acha kufanya unachofanya'," baba huyo wa watoto wawili ameiambia CBS News katika mahojiano maalum.

    Ahmed, ambaye alipigwa risasi mara kadhaa na mshukiwa mwingine, anasema kitendo chake kiliokoa "watu wengi... lakini bado nawahurumia waliopoteza maisha."

    Katika mahojiano anakumbuka alipomkabili Sajid Akram, mwenye umri wa miaka 50, aliyekuwa akiwapiga risasi waliohudhuria katika tukio la Kiyahudi la Hanukkah huko Bondi Beach siku ya Jumapili tarehe 14 Desemba.

    "Lengo langu lilikuwa ni kumnyang'anya bunduki, na kumzuia asiue watu wasio na hatia."

    Watu kumi na tano walifariki wakati wa shambulio hilo - shambulio baya zaidi nchini Australia tangu 1996 - na wengine 40 walijeruhiwa. Polisi wametangaza shambulio hilo kuwa tukio la kigaidi lililolenga jamii ya Wayahudi.

    Sajid Akram alipigwa risasi na kuuawa na polisi huku mwanawe Naveed, mshukiwa mwingine ambaye alilazwa hospitalini baada ya shambulio hilo, ameshtakiwa kwa makosa 59 yakiwemo makosa 15 ya mauaji na moja ya kufanya shambulio la kigaidi.

    Siku chache baada ya kupigwa risasi, Ahmed alipewa hundi kando ya kitanda chake hospitalini ya dola milioni 2.5 (£1.24m; $1.7m) ambazo zilikusanywa kutoka maelfu ya watu walioguswa na ushujaa wake.

    Alipigwa risasi mara kadhaa begani baada ya kumkabili Sajid Akram na kufanyiwa operesheni tatu.

    Waziri Mkuu wa Australia Anthony Albanese alimtembelea Ahmed hospitalini, akimtaja kama "mtu bora zaidi katika nchi yetu" huku Waziri Mkuu wa New South Wales Chris Minns akimwita "shujaa wa kweli."

    Pia unaweza kusoma:

  10. Watu tisa, wakiwemo watoto watano, wadungwa kisu na kufa

    k

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Picha ya mtaa katika mji mkuu wa Suriname, Paramaribo

    Polisi wamesema watu tisa wakiwemo watoto watano wamedungwa kisu hadi kufa nje kidogo ya mji mkuu wa Suriname, Paramaribo.

    Polisi wa jiji wamesema katika taarifa yao mtu mzima mmoja na mtoto walipelekwa hospitalini baada ya kupata majeraha makubwa katika shambulio hilo.

    Maafisa waliitwa Jumamosi usiku, ambapo walimkamata mshukiwa mwanaume baada ya kumpiga risasi mguuni. Pia alipelekwa hospitalini kwa matibabu na yuko chini ya ulinzi wa polisi.

    Vyombo vya habari vya ndani vimedokeza kwamba mwanaume huyo alikuwa akisumbuliwa na matatizo ya afya ya akili, vikiwanukuu maafisa na wakazi, huku rais wa taifa hilo la Amerika Kusini akisema familia yake na majirani zake ni miongoni mwa waathiriwa.

    Rais Jennifer Geerlings-Simons amesema nawatakia wafiwa wote nguvu, ujasiri na faraja katika kipindi hiki kigumu kisichoelezeka.

    Suriname ni miongoni mwa mataifa yenye viwango vya chini vya vifo vya kuchomwa kisu, na kufanya matukio kama haya kuwa nadra sana.

    Hata hivyo, imepitia mapinduzi kadhaa na vita vya wenyewe kwa wenyewe tangu ilipopata uhuru wake kutoka Uholanzi mwaka wa 1975.

    Pia unaweza kusoma:

  11. Mataifa matatu yaaga mapema mashindano ya AFCON 2025

    p

    Chanzo cha picha, CAF

    Botswana, Guinea ya Ikweta na Gabon zimeondolewa kwenye Kombe la Mataifa ya Afrika la 2025 baada ya kushindwa kupata pointi hata moja katika hatua ya makundi.

    Botswana, ambayo imemaliza ikiwa ya mwisho katika Kundi D, ilishindwa katika mechi zake mbili za ufunguzi. Walifungwa 3-0 na Senegal kabla ya kupoteza 1-0 dhidi ya Jamhuri ya Benin.

    Ingawa bado wana mechi ya mwisho ya makundi dhidi ya DR Congo iliyopangwa kufanyika Jumanne, Desemba 30, matokeo mengine tayari yamethibitisha kuondolewa kwao katika mashindano hayo

    Guinea ya Ikweta katika Kundi E, imepoteza mechi zao zote tatu. Walianza kwa kichapo cha 2-1 dhidi ya Burkina Faso, wamefungwa 3-0 na Algeria, na kumaliza hatua yao ya makundi kwa kichapo cha 1-0 dhidi ya Sudan, na kuwaacha bila pointi.

    Katika Kundi F, Gabon pia wametoka mapema baada ya kushindwa mfululizo. Walianza kampeni yao kwa kupoteza 1-0 dhidi ya Cameroon kabla ya kufungwa 3-2 na Msumbiji katika mechi yao ya pili.

    Kwa pointi sifuri, Gabon iko katika nafasi ya nne katika kundi hilo na wameondolewa. Hata hivyo, watacheza mechi ya mwisho watakapokabiliana na mabingwa watetezi Ivory Coast Jumatano, Desemba 31.

    Pia unaweza kusoma:

  12. Ajali ya treni Mexico yaua watu 13 na kuwajeruhi karibu 100

    l

    Takriban watu 13 wamefariki na karibu 100 wamejeruhiwa baada ya treni kuacha njia katika eneo la kusini-magharibi mwa Mexico la Oaxaca, limesema jeshi la wanamaji la Mexico.

    Treni hiyo, iliyokuwa ikisafiri kati ya Ghuba ya Mexico na Bahari ya Pasifiki, imebeba abiria 241 na wafanyakazi tisa.

    Jumla ya watu 98 wamejeruhiwa, ambapo 36 wanatibiwa hospitalini, imesema taarifa ya jeshi.

    Treni iliacha njia yake ya reli ilipozunguka kona karibu na mji wa Nizanda.

    Mwanasheria Mkuu wa Mexico amethibitisha kuwa uchunguzi unaendelea.

    Rais wa Mexico Claudia Sheinbaum amesema watano kati ya waliojeruhiwa walikuwa katika hali mbaya.

    Picha kutoka eneo la ajali zinaonyesha wafanyakazi wa uokoaji wakiwasaidia abiria kushuka kwenye treni.

    Jeshi la wanamaji la Mexico ndilo linaloendesha safari za treni iliyokumbwa na ajali.

    Pia unaweza kusoma:

  13. Eritrea yataka Umoja wa Mataifa kuchukua hatua kwa uamuzi wa Israel kuitambua Somaliland

    ol

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Eritrea imesema hatua ya Israel kuitambua Somaliland ni juhudi za makusudi za kusababisha ukosefu wa utulivu na machafuko katika eneo hilo na duniani kote.

    Eritrea imetoa wito wa majibu makali kutoka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na wanachama wake.

    ‎Katika taarifa iliyotolewa Jumapili, Eritrea imeiomba China kuchukua hatua kwa sababu inaamini kuna kufanana kati ya hali ya Somaliland na Taiwan.

    Huku hayo yakijiri, baadaye leo jijini New York, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa litaketi kujadili eneo la Somaliland lililojitenga na Somalia - na haswa uamuzi wa hivi karibuni wa Israel wa kulitambua rasmi kama taifa huru.

    Hatua hiyo imelaaniwa na makundi ya kikanda na nchi jirani.

    Somaliland, ambayo haitambuliwi kimataifa kama taifa, ilitangaza uhuru wake mwaka 1991 baada ya Somalia kuingia katika vita vya wenyewe kwa wenyewe vya umwagaji damu kufuatia kupinduliwa kwa dikteta wa kijeshi wa Somalia Mohamed Siad Barre.

    Pia unaweza kusoma:

  14. China yafanya mazoezi ya kijeshi karibu na Taiwan kama onyo

    k

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Tangu 2022 Beijing imeongeza mazoezi ya kijeshi katika Mlango-Bahari wa Taiwan

    China inafanya mazoezi ya kijeshi kuzunguka Taiwan ikiiga kukamatwa na kuzingirwa kwa maeneo muhimu ya kisiwa hicho, kama onyo dhidi ya "vikosi vya Taiwan."

    Jeshi la ardhini, jeshi la wanamaji, jeshi la anga na kikosi cha roketi vimetumwa kwa ajili ya mazoezi hayo ambayo yanajumuisha mazoezi ya kufyatua risasi za moto, limesema jeshi la China.

    Mazoezi hayo yanafanyika siku chache baada ya Marekani kutangaza kuuza silaha kwa Taiwan zenye thamani ya dola bilioni 11 (pauni bilioni 8.2). Hatua hiyo imesababisha upinzani mkali kutoka Beijing ambayo imewekea vikwazo makampuni ya ulinzi ya Marekani.

    Taiwan kuongeza ulinzi wake mwaka huu pia kumeikasirisha Beijing, ambayo inadai kisiwa hicho kinachojitawala ni eneo lake.

    Ofisi ya rais ya Taiwan imekosoa mazoezi ya China, ikiyaita ni tatizo kwa kanuni za kimataifa.

    Wizara ya ulinzi ya Taiwan imesema imegundua ndege na meli za China zikizunguka Taiwan Jumatatu asubuhi, na wameweka vikosi vyao na mifumo ya makombora tayari ili kufuatilia hali hiyo.

    Vikosi viko "tayari" kuilinda Taiwan na "kuwalinda watu wetu", wizara hiyo imesema.

    Ingawa mazoezi ya awali yameanza, jeshi la China lilisema litafanya mazoezi makubwa kuanzia Jumanne.

    Pia unaweza kusoma:

  15. Trump asema kuna maendeleo katika mazungumzo ya kumaliza vita vya Ukraine

    sz

    Chanzo cha picha, Reuters

    Rais Donald Trump wa Marekani na Volodymyr Zelensky wa Ukraine, wamesema kuna maendeleo yamepatikana katika mazungumzo ya kumaliza vita vya Ukraine wakati wa mazungumzo ya Florida lakini rais wa Marekani amekiri kwamba tatizo la mpaka bado "halijatatuliwa."

    Akihutubia waandishi wa habari huko Mar-a-Lago, Zelensky alisema wamefikia makubaliano kuhusu "90%" ya mpango wa amani wa vipengele 20, huku Trump akisema dhamana ya usalama kwa Ukraine "imekamilika karibu 95%.

    Baadaye Zelensky alisema timu za Marekani na Ukraine zitakutana wiki ijayo kwa mazungumzo zaidi kuhusu masuala yanayolenga kukomesha vita vya Urusi vilivyodumu kwa karibu miaka minne nchini Ukraine.

    "Tulikuwa na mazungumzo muhimu kuhusu masuala yote na tunathamini maendeleo ambayo timu za Ukraine na Marekani zimepiga katika wiki zilizopita," Zelensky alisema katika taarifa ya Telegram.

    Pendekezo la kugeuza eneo la Donbas mashariki mwa Ukraine, ambalo Urusi kwa kiasi kikubwa inalidhibiti, kuwa eneo lisilo la kijeshi bado "halijatatuliwa," Trump alisema.

    Moscow kwa sasa inadhibiti takriban 75% ya eneo la Donetsk, na takriban 99% ya eneo jirani la Luhansk. Mikoa hiyo kwa pamoja inajulikana kama Donbas.

    Urusi inataka Ukraine ijiondoe kutoka sehemu ya eneo ambalo bado inalidhibiti huko Donbas, huku Kyiv ikisisitiza kuwa eneo hilo linaweza kuwa eneo huru la kiuchumi linalolindwa na vikosi vya Ukraine.

    Urusi ilianzisha uvamizi dhidi ya Ukraine Februari 2022, na kwa sasa Moscow inadhibiti takriban 20% ya eneo la Ukraine.

    Pia unaweza kusoma:

  16. Hujambo na karibu

    Nakukaribisha katika taarifa zetu za moja kwa moja, leo Jumatatu tarehe 29, Disemba 2025