China kuchimba mawe kwa mara ya kwanza mwezini tangu miaka ya 1970

Chanzo cha picha, Getty Images
China itatafuta mawe kwa mara ya kwanza kutoka kwenye mwezi tangu miaka ya 1970.
Chombo chake kisichokuwa na rubani kitarushwa Jumanne na kutarajiwa kurejea na mawe na michanga kidogo kusaidia kuelewa zaidi kuhusu chimbuko la mwezi na jinsi ulivyojitengeneza.
Mara ya mwisho kwa safari ya aina hii, Luna 24, ilikuwa ni mwaka 1976 iliyosimamishwa na Muungano wa Usovieti.
Ikiwa chombo hiki kitafanikiwa, China itakuwa nchi ya tatu kupata michanga kutoka kwenye mwezi baada ya Marekani na Muungano wa Sovieti.
Chombo cha China kinachotumika kilipewa jina kutokana na miungu ya China ya zamani ya kwenye mwezi - na kitarushwa kwa kutumia roketi nzito, ndefu ya kisasa inayofahamika kama Long March 5.
Chombo cha China kitajitahidi kupata kilo mbili za mchanga katika eneo la mwezi ambalo halijawahi kufikiwa.
Ikilinganishwa na awali, chombo cha mwaka 1976 kilichopata gramu 170 na kile cha Apollo kikifanikiwa kupata kilogramu 382 za mawe na mchanga.

Chanzo cha picha, Getty Images
Wataalamu wanaimani kuwa chombo hicho kitasaidia katika ufafanuzi wa kina zaidi kuhusu kipindi ambacho mwezi ulisalia katika mlipuko wa volkeno na ni wakati gani ugasumaku inakuwa muhimu kulinda maisha yoyote yale kutoka kwa mionzi ya jua.
China ilifanikiwa kufika mwezini kwa mara ya kwanza mwaka 2013 na kuanza mipango ya kuchimba mchanga na mawe kutoka kwa sayari ya Mihiri ndani ya mwongo mmoja.












