Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Trump aionya Iran 'muda unayoyoma' huku jeshi la Marekani likiendelea kujikusanya eneo la Ghuba
"Natumaini Iran 'itakuja haraka kwenye meza ya mazungumzo' na kujadili makubaliano ya haki na usawa - HAKUNA SILAHA ZA NYUKLIA," Trump aliandika.
Muhtasari
- Nyota wa YouTube wa Marekani IShowSpeed kupata pasipoti ya Ghana
- Mwanamke wa kwanza athibitishwa kuwa Askofu Mkuu wa 106 wa Canterbury
- 'Waathiriwa wa mlipuko wa bomu wa 1998 Kenya, hawatafidiwa' - Mahakama
- 'Muda unakwisha', Trump aonya Iran huku jeshi la Marekani likiongezeka eneo la Ghuba
- Taiwan yaonyesha uwezo wa ndege za F-16 zikijibu kwa haraka huku mvutano na China ukiendelea
- Mke wa rais wa zamani wa Korea Kusini afungwa jela miezi 20
- Madaktari wafanikiwa kurejesha uume uliokatwa Ethiopia
- Iran yasema haikuomba kufanya mazungumzo na Marekani
- Rwanda yaomba usuluhishi katika makubaliano ya wanaotafuta hifadhi ya Uingereza yaliyofutwa
- Seneta wa Marekani atoa wito wa kuwapa silaha waandamanaji wa Iran
- Mazingira ya kifo cha Raila Odinga bado yaibua hisia Kenya
- Watumiaji wa Uingereza watashindwa kufikia 'Pornhub' kuanzia wiki ijayo
- Mbunge wa Minnesota Ilhan Omar ashambuliwa kwa 'kioevu kisichojulikana' wakati akihutubia wakaazi
- Maelfu ya Waethiopia watishiwa kuuawa Kenya waamriwa kuondoka
- Trump asema Marekani 'haitaisaidia tena Iraq' ikiwa itamchagua Maliki kama Waziri Mkuu
- Seneta wa zamani wa Ufaransa apatikana na hatia ya kumlewesha mbunge dawa za kulevya
- Zelensky alaani shambulizi mbaya la ndege zisizo na rubani za Urusi kwenye treni ya abiria
- Iran ikivamia Israel, tutajibu kwa nguvu haijawahi kushuhudiwa - Netanyahu
- Trump atangaza 'kulegeza kamba' dhidi ya wahamiaji haramu Minnesota kufuatia mauaji ya Mmarekani
Moja kwa moja
Na Mariam Mjahid & Asha Juma
Nyota wa YouTube wa Marekani IShowSpeed kupata pasipoti ya Ghana
IShowSpeed, nyota maarufu wa YouTube duniani, anatarajiwa kupokea pasipoti ya Ghana kufuatia safari yake inayotarajiwa katika taifa hilo la Afrika Magharibi.
Ghana ilikuwa kituo cha mwisho cha ziara ya moja kwa moja ya mwanasiasa huyo mwenye ushawishi wa Marekani barani Afrika, ambayo ilimalizika Jumanne.
Kufuatia ziara ya IShowSpeed, waziri wa mambo ya nje wa Ghana alitangaza kwamba ofisi yake imeidhinisha pasipoti ya Nyota huyo, ambaye alimwita "balozi stahiki".
Ziara yake kwa jina "Speed Does Africa" imetazamwa kote ulimwenguni, huku wengi wakiisifu kwa kusaidia kuvunja dhana potofu kuhusu bara hilo na kuonyesha tamaduni nyingi za Kiafrika kwa ulimwengu.
Soma zaidi:
Mwanamke wa kwanza athibitishwa kuwa Askofu Mkuu wa 106 wa Canterbury
Mwanamke wa kwanza kuongoza Kanisa la Uingereza amethibitishwa rasmi kuwa Askofu Mkuu wa 106 wa Canterbury katika sherehe iliyojaa mila za karne nyingi katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo.
Bi. Sarah Mullally ameiambia BBC kwamba amejitolea kuzungumza kuhusu chuki dhidi ya wanawake popote anapoona jambo hilo.
Mtangulizi wake, Justin Welby, alijiuzulu kufuatia shutuma kwamba hakufanya vya kutosha na taarifa alizokuwa nazo kuhusu mnyanyasaji mkubwa ili kuzuia unyanyasaji zaidi kutokea.
Katika mahojiano na BBC, Dame Sarah alisema ilikuwa sahihi kwamba kulikuwa na uchunguzi mkubwa zaidi katika rekodi yake mwenyewe katika kushughulikia ulinzi Kanisani.
Dame Sarah aliambia BBC: "Kuna hisia ya uzito wa ofisi ninayohisi, lakini pia ninafahamu uungwaji mkono mkubwa nilioupata kutoka kwa watu wanaoniandikia au ninaopishana nao mitaani."
Hapo awali afisa mkuu wa uuguzi wa Uingereza, Dame Sarah alikuwa ameanza siku hiyo kama Askofu wa London, wadhifa aliokuwa nao tangu 2018.
"Itakuwa sahihi kusema kwamba mimi, katika nafasi yangu ya kidunia, na pia katika Kanisa, wakati mwingine nimepitia unyanyasaji wa wanawake," alisema.
Ingawa Dame Sarah alikiri kwamba katika huduma yake yote alikuwa amepokea uungwaji mkono kutoka kwa wanaume wengi, alisema pia amejifunza kwamba masuala ya chuki dhidi ya wanawake yalihitaji "kuwekwa wazi", jambo ambalo atalifanya zaidi.
Soma zaidi:
‘Waathiriwa wa mlipuko wa bomu wa 1998 Kenya, hawatafidiwa’ - Mahakama
Mahakama Kuu imetupilia mbali ombi la kutaka kulipwa fidia na tume ya uchunguzi kuhusu mlipuko wa bomu wa mwaka 1998 uliotokea jijini Nairobi, ikiamua kuwa waombaji walishindwa kuthibitisha kuwa serikali ilipuuza wajibu wake wa kuzuia shambulio hilo.
Katika hukumu iliyotolewa Jumatano, Jaji Lawrence Mugambi aliamua kwamba ombi hilo, lililowasilishwa mwaka wa 2021, halina umuhimu na halikuthibitisha uwajibikaji kwa upande wa serikali.
Jaji Mugambi alisema walalamishi hao walidai kuwa serikali ilipuuza maonyo ya mara kwa mara ya awali na kushindwa kuchukua hatua kuzuia shambulio hilo, ikiwa ni pamoja na kulinda mipaka ya Kenya, licha ya tishio hilo kujulikana au lilipaswa kujulikana.
Hata hivyo, hakimu alidai kuwa walalamishi wanajukumu la kuthibitisha na wameshindwa kulionyesha.
"Wajibu uliowekwa kwa Serikali uko wazi. Serikali lazima ichukue hatua chanya kuzuia ukiukwaji wa haki ya kuishi," Jaji Mugambi alisema, akitoa mfano wa kanuni za kikatiba na viwango vya kimataifa vya haki za binadamu.
Kufuatia uamuzi huo, waathiriwa wanaweza kuwasilisha kesi yao katika mahakama ya rufaa na pia katika mahakama ya kimataifa ya makosa ya Jinai ICC.
Soma zaidi:
'Muda unakwisha', Trump aonya Iran huku jeshi la Marekani likiongezeka eneo la Ghuba
Donald Trump ameionya Iran kwamba "muda unakwisha" wa kujadili makubaliano kuhusu mpango wake wa nyuklia kufuatia ongezeko la vikosi vya kijeshi vya Marekani katika eneo la Ghuba.
Rais wa Marekani alisema "meli kubwa ya kijeshi ya Armada" ilikuwa "ikisonga mbele haraka, kwa nguvu, shauku, na kusudi kubwa" kuelekea Iran katika ujumbe alioandika kwenye jukwaa lake la Truth Social.
Mapema Jumatano, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araghchi alisema: "Kuendesha diplomasia kupitia vitisho vya kijeshi hakuwezi kuwa na ufanisi au manufaa."
Trump hapo awali alisema "atawaokoa" waandamanaji waliohusika katika ukandamizaji wa kikatili na usio wa kawaida dhidi ya maandamano nchini Iran mapema mwezi huu.
"Ikiwa wanataka mazungumzo yafanyike, lazima waache vitisho, madai mengi na kuibua masuala yasiyo na mantiki," Araghchi alisema katika hotuba za televisheni, zilizotafsiriwa na shirika la habari la AFP.
"Natumaini Iran 'itakuja haraka kwenye meza ya mazungumzo' na kujadili makubaliano ya haki na usawa - HAKUNA SILAHA ZA NUKLIA," Trump aliandika.
Iran inasisitiza kuwa mpango wake wa nyuklia ni wa amani kabisa na imekana mara kwa mara kutaka kutengeneza silaha za nyuklia.
Rais wa Marekani alisema kikosi cha wanamaji katika Ghuba kilikuwa kikubwa kuliko kile kilichotumwa Venezuela kabla ya vikosi vya Marekani kumkamata kiongozi wa zamani wa nchi hiyo Nicolás Maduro.
Soma zaidi:
Taiwan yaonyesha uwezo wa ndege za F-16 zikijibu kwa haraka huku mvutano na China ukiendelea
Jeshi la anga la Taiwan limeonyesha uwezo wake wa kujaza tena vifaa na mafuta na kurudisha ndege zake za kivita za F-16 angani katika mazoezi ya utayari siku ya Jumatano, yaliyolenga kuonyesha mafunzo ya mapigano.
Jeshi la anga la Taiwan hujitahidi karibu kila siku kufuatilia na kuonya ndege za China ambazo huruka mara kwa mara kuzunguka kisiwa hicho.
Taipei inaona uvamizi huo kama sehemu ya kampeni inayoendelea ya unyanyasaji ili kujaribu na kuwachosha wanajeshi kidogo wa Taiwan na kutoa shinikizo la kisiasa.
Rubani Shih Shun-de alisema ni muhimu kuwafahamisha watu jinsi jeshi la anga linavyoweza kuchukua hatua haraka.
"Mazoezi haya yanawezesha umma kuona matokeo ya mafunzo halisi na yenye mwelekeo wa mapigano ya jeshi la anga," alisema.
China inaiona Taiwan inayotawaliwa kidemokrasia kama eneo lake, licha ya pingamizi za serikali huko Taipei.
Soma zaidi:
Mke wa rais wa zamani wa Korea Kusini afungwa jela miezi 20
Mke wa rais wa zamani wa Korea Kusini aliyeondolewa madarakani amehukumiwa kifungo cha miezi 20 jela kwa kupokea rushwa kutoka kwa Kanisa la Unification lenye utata.
Hata hivyo, mahakama ilimsafisha Kim Keon Hee mwenye umri wa miaka 52 kwa mashtaka ya kudanganya bei ya hisa na kupokea kura za maoni bila malipo kutoka kwa dalali wa kisiasa kabla ya uchaguzi wa rais wa 2022, ambao mumewe Yoon Suk Yeol alishinda.
Yoon tayari amehukumiwa kifungo cha miaka mitano jela kwa kutumia vibaya madaraka na kuzuia haki kuhusiana na jaribio lake la mapinduzi ya kijeshi lililoshindwa mwaka 2024.
Hii ni mara ya kwanza katika historia ya Korea Kusini kwa aliyekuwa rais na mkewe kuhukumiwa wakati mmoja.
Pia unaweza kusoma:
Madaktari wafanikiwa kurejesha uume uliokatwa Ethiopia
Madaktari katika hospitali ya Alert huko Addis Ababa wamefanikiwa kurudisha uume uliokatwa wa kijana mmoja baada ya upasuaji wa saa saba.
Dkt. Abdurrezak Ali, mkuu wa Idara ya Upasuaji na Urekebishaji, aliambia BBC kwamba mgonjwa huyo alijiumiza usiku wa manane Jumamosi, Januari 24, 2026.
Alipelekwa kwanza kwenye kliniki ya eneo, ambayo baadaye iliwasiliana na hospitali ya Alert kuuliza ikiwa kuunganishwa tena kwa uume kuliwezekana.
"Tulifanya uamuzi wa kufanya upasuaji kwa sababu tuliamini kwamba uume bado unaweza kuunganishwa tena, kulingana na muda uliopita tangu kukatwa," Dk. Abdurrezak alieleza.
Uume ulikuwa umekatwa kabisa, na kuuacha bila mzunguko wa damu au oksijeni kwa muda wa saa tisa. Hata hivyo, Dk. Abdurrezak alibainisha kuwa mgonjwa huyo hakuwa akivuja damu nyingi, maumivu yake yalikuwa kidogo, na hali yake haikuwa mbaya sana alipolazwa.
Sehemu ya sentimita tano ya uume ilikuwa imehifadhiwa katika hali ya baridi, ambayo iliongeza kwa kiasi kikubwa kiwango cha kufanikiwa kwa upasuaji huo.
Madaktari wa upasuaji waliunganisha tena mishipa ya damu na neva, wakarekebisha miundo ya njia ya mkojo, na kurejesha tishu husika.
"Utafiti unaonyesha kwamba neva na mishipa ya damu inaweza kuishi hadi saa 16 baada ya kukatwa kwa sababu hakuna misuli katika uume. Katika hali hiyo, uume uliweza kuunganishwa upya baada ya saa tisa," Dk Abdurrezak alisema.
Mgonjwa, katika ujana wake, sasa anapata nafuu. Madaktari wanatarajia aanze kukojoa kawaida ndani ya wiki tatu, wakati uwezo wa kufanya ngono inaweza kuchukua takriban miezi mitatu.
"Haruhusiwi kufanya mapenzi katika kipindi hiki, kwani inaweza kuharibu urekebishaji wa neva," Dk. Abdurrezak aliongeza.
Sababu ya kujiumiza bado haijajulikana.
Unaweza kusoma:
Iran yasema haikuomba kufanya mazungumzo na Marekani
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araqchi alisema hakuwa amewasiliana na mjumbe maalum wa Marekani Steve Witkoff katika siku za hivi karibuni au kuomba kufanyika kwa mazungumzo, vyombo vya habari vya serikali viliripoti Jumatano.
Rais wa Marekani Donald Trump alisema siku ya Jumanne meli ya "armada" inaelekea Iran na kwamba anatumai Tehran itafanya mazungumzo na Washington.
Marekani ilipeleka meli za ziada za kijeshi katika Ghuba kufuatia maandamano ya kitaifa nchini Iran ambayo yalisababisha ukandamizaji mkubwa zaidi nchini humo tangu Mapinduzi ya Kiislamu ya 1979.
"Hakukuwa na mawasiliano kati yangu na Witkoff katika siku za hivi karibuni na hakuna ombi la mazungumzo lililotolewa kutoka kwetu," Araqchi aliviambia vyombo vya habari vya serikali, akiongeza kuwa wapatanishi mbalimbali walikuwa "wakifanya mashauriano" na walikuwa wakiwasiliana na Tehran.
"Msimamo wetu uko wazi, mazungumzo hayaendani na vitisho na mazungumzo yanaweza kufanyika tu wakati hakuna vitisho tena na madai mengi."
Rais wa Iran Masoud Pezeshkian alimwambia Mwanamfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman siku ya Jumanne kwamba Tehran inakaribisha mchakato wowote, ndani ya mfumo wa sheria za kimataifa, unaozuia vita.
Pia unaweza kusoma:
Rwanda yaomba usuluhishi katika makubaliano ya wanaotafuta hifadhi ya Uingereza yaliyofutwa
Rwanda imefungua kesi ya usuluhishi dhidi ya Uingereza kuhusu makubaliano ya wanaotafuta hifadhi ambayo Waziri Mkuu Keir Starmer aliyafuta mwaka wa 2024, serikali ya taifa hilo la Afrika Mashariki ilisema.
Chini ya mpango huo, uliosainiwa kabla ya Starmer kuchukua madaraka, Uingereza ilikubali kuilipa Rwanda ili kuwapokea wahamiaji waliofika kinyume cha sheria nchini Uingereza.
Ilituma watu wanne pekee waliotaka kwa hiari yao kwenda Rwanda, kwani mpango huo ulikwama kutokana na changamoto za kisheria.
Rwanda imewasilisha notisi kwa Mahakama ya Kudumu ya Usuluhishi yenye makao yake makuu Hague, ikidai kuwa Uingereza ilikiuka mipango ya kifedha ya "ushirika wa uhamiaji", serikali yake ilisema katika taarifa yake kwenye mtandao wa X siku ya Jumanne.
Iliongeza kuwa Uingereza iliiomba mwaka wa 2024 kusahau malipo mara mbili ya pauni milioni 50 (dola milioni 69) yaliyopaswa kulipwa Aprili 2025 na Aprili 2026 kwa kutarajia kukomeshwa rasmi kwa mkataba uliokuwa
Rwanda ilisema ilikuwa tayari kukubaliana, mradi tu mkataba huo unasitishwa na masharti mapya ya kifedha kujadiliwa na kukubaliwa.
"Hata hivyo, majadiliano kati ya Rwanda na Uingereza hayakufanyika na kiasi hicho kinasalia kuhitajika kulipwa chini ya mkataba," serikali iliongeza.
Baada ya Starmer kufuta mpango huo, serikali yake ilisema imepoteza pesa za walipa kodi na hakuna malipo zaidi yatakayofanywa.
Uhusiano kati ya Uingereza na Rwanda uliharibika mwaka jana, wakati London ilipositisha msaada kuhusu jukumu la Rwanda katika vita vya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Rwanda imekabiliwa na shinikizo la kimataifa kutokana na shutuma kwamba inaunga mkono kundi la waasi la M23 huko.
Kigali inakanusha kuunga mkono M23 na imewalaumu wanajeshi wa Congo na Burundi kwa mapigano mapya ambayo yamewaua maelfu ya watu huku wengine wengi wakilazimika kuhama makazi yao.
Soma zaidi:
Seneta wa Marekani atoa wito wa kuwapa silaha waandamanaji wa Iran
Ted Cruz, Seneta wa ngazi ya juu wa chama cha Republican katika Bunge la Marekani, ametoa wito wa kukabidhiwa silaha kwa waandamanaji wa Iran, ikiwa ni majibu ya hivi punde kwa ukandamizaji wa umwagaji damu dhidi ya maandamano nchini humo.
Seneta Cruz aliandika kwenye mtandao wa X Jumanne jioni: "Sisi (Marekani) tunapaswa kuwapa silaha waandamanaji sasa, ili watu wa Iran waweze kumpindua Ayatollah - dikteta ambaye daima anapiga kelele 'Kifo kwa Marekani.' Hii itaifanya Marekani kuwa salama na utulivu zaidi.
Unaweza pia kusoma:
Mazingira ya kifo cha Raila Odinga bado yaibua hisia Kenya
Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA), ambaye pia ni mtoto wa kike wa aliyekuwa Waziri Mkuu wa Kenya, Winnie Odinga, amekataa vikali madai ya mfanyabiashara Oketch Salah kwamba alikuwa pale wakati wa kifo cha marehemu baba yake, Raila Odinga.
Winnie ameyataja madai hayo kama “uongo hatari” na kuhoji nia halisi za Salah.
Akizungumza katika mahojiano na Citizen TV siku ya Jumanne, Januari 27, Winnie alisema kuwa madai ya Salah ni ya uongo na hayafai, ikizingatiwa hali ya hisia inayozunguka kifo cha waziri mkuu huyo wa zamani.
“Nimekutana na Oketch Salah, lakini napenda kuamini hakuna anayemjua kweli. Kudai ulikuwa pale wakati wa kifo cha baba yangu wakati hakuwa pale, na kuzungumzia mambo ambayo hayajatokea, ni hatari sana na kunalazimisha kuhoji nia zake,” alisema Winnie.
Kauli yake inajiri baada ya Salah kudai hadharani kuwa alikuwa na Raila Odinga tangu mwanzo wa ugonjwa wake hadi wakati wa kifo chake.
Salah alisisitiza kuwa hakutoa taarifa hizo kwa huruma au faida ya kisiasa, bali kwa sababu ni ukweli.
Aliongeza kuwa alimuuguza kihisia Raila na kushiriki katika mazungumzo binafsi wakati wa ugonjwa wake.
Mbunge Winnie Odinga pia ametoa malalamiko makali juu ya jinsi mchakato wa uongozi ndani ya Orange Democratic Movement (ODM) ulivyoshughulikiwa baada ya kifo cha kiongozi wa muda mrefu wa chama.
“Chama hakijatimiza wajibu wake kwa uwazi. Kiongozi wetu alifariki, na chama hakujawahi kuwasiliana nasi kama wanachama kutujulisha kifo chake. Wamechagua uongozi mpya, lakini bado hatujajulishwa rasmi,” alisema.
Winnie alihoji pia msingi wa kisheria uliopewa binamu yake na kaka wa Raila, Dk. Oburu Oginga, aliposimikwa kama kiongozi wa chama, akisisitiza kuwa hatua hiyo haikuzingatia katiba.
Aliongeza kuwa msimamo wake ni kulinda maadili ya chama na uongozi wake dhidi ya hatua zisizo za kikatiba, kuhakikisha chama na viongozi wake hawadhulumiwi au kudanganywa kisheria.
Soma pia;
Watumiaji wa Uingereza watashindwa kufikia 'Pornhub' kuanzia wiki ijayo
Ilani: Taarifa hi inahusisha mada za ngono.
Pornhub imetangaza itapunguza upatikanaji wa tovuti yake nchini Uingereza kuanzia wiki ijayo, ikilaumu ukaguzi mkali wa umri ulioanzishwa kwa tovuti zenye picha za ngono wazi.
Kuanzia tarehe 2 Februari, watu pekee waliojiunga na akaunti ya Pornhub awali ndio watakaoweza kufikia yaliyomo kwenye tovuti hiyo.
Aylo, kampuni kubwa ya Pornhub, ilisema kuwa marekebisho ya Sheria ya Usalama Mtandaoni ya Uingereza (Online Safety Act – OSA), yanayohitaji uthibitisho wa umri, hayajafanikisha lengo la kulinda watoto wadogo na yamepelekea trafiki ya watumiaji kuelekea sehemu zisizo za kawaida na zisizodhibitiwa za mtandao.
Mnamo Oktoba, Aylo ilisema kuwa mabadiliko ya sheria yalifanya idadi ya watazamaji kwenye tovuti hiyo kupungua kwa asilimia 77%.
Alex Kekesi, mkuu wa jamii na chapa (brand) katika Aylo, alisema uamuzi wa kupunguza upatikanaji wa Pornhub kwa watumiaji wa Uingereza ulikuwa uamuzi mgumu.
''Tovuti zetu, zinazotoa picha za ngono halali na zinazosimamiwa kisheria, hazitatumika tena kwa watumiaji wapya wa Uingereza, lakini maelfu ya tovuti zisizo wajibika bado zitakuwa rahisi kufikiwa'', alisema.
Vikwazo hivyo hivyo vitahusisha pia tovuti nyingine za ngono zinazomilikiwa na Aylo, zikiwemo YouPorn na Redtube.
Emma Drake, mshirika wa masuala ya usalama mtandaoni na faragha katika kampuni ya sheria ya Bird and Bird, alisema utafiti uliotajwa na Aylo unaonyesha kuwa watu wazima wanatafuta tovuti zenye hatari kubwa zaidi za ngono, pia umeonyesha kuwa matumizi ya tovuti za ngono miongoni mwa watu wazima yameshuka.
“Hali hiyo lazima iwe kweli pia kwa watoto,” alisema kwa BBC.
“Wale waliyo na azma watapata njia mbadala, kama kutumia VPN au tovuti mpya Aylo zilizotaja, lakini kuweka vizuizi kwenye tovuti maarufu zaidi bado kunaweza kulinda idadi kubwa ya watoto ambao wasingejitahidi kufanya hivyo.”
Soma pia:
Mbunge wa Minnesota Ilhan Omar ashambuliwa kwa 'kioevu kisichojulikana' wakati akihutubia wakaazi
Wakati huo huo,Mbunge wa chama cha Democratic Ilhan Omar ameshambuliwa na mwanamume mmoja wakati akihutubia katika hafla iliyokuwa ikifanyika katika ukumbi wa Manispaa ya Minneapolis.
Polisi wanasema mshambuliaji huyo alimmwagia bi Omar kitu cha majimaji mwilini.
"Nilidhani ni mmoja wa wasaidizi wake aliyekwenda kumkabidhi barua au kitu," Jacquelynn Goessling alisema juu ya mtu aliyemshambulia Omar kwa kitu cha majimaji, harufu ya akridi ambayo iliteketeza sehemu ya mbele ya chumba.
Hata hivyo alichomwagia hakikumdhuru na mdemocrat huyo ambaye ni mkosoaji mkubwa wa Rais Trump aliendelea na hotuba yake.
Katika taarifa yake kuhusu X, Omar alisema: "Mimi niko sawa. Mimi nimeokoka kwa hivyo mchochezi huyu mdogo hatanitisha kufanya kazi yangu. Siwaruhusu wanyanyasaji kushinda."
Mwanamume aliyemshambulia amekamatwa.
Unaweza kusoma pia:
Maelfu ya Waethiopia watishiwa kuuawa Kenya waamriwa kuondoka
Waethiopia wanaoishi katika Kaunti ya Mandera, kaskazini-mashariki mwa Kenya, wanasema wameonywa kuwa watakabiliwa na kifo iwapo hawataondoka katika eneo hilo ifikapo tarehe 5 Februari 2026.
Wakizungumza na BBC bila kutaja majina yao, wahamiaji kadhaa walieleza hali hiyo kuwa ya kutishia maisha.
Ubalozi wa Ethiopia nchini Kenya ukiongozwa na Balozi Demeke Atnafu umethibitisha kuwa unafuatilia kwa karibu hali hiyo.
Alisisitiza kuwa ni vyombo vya serikali pekee vinavyoweza kuamua hadhi ya kisheria ya wahamiaji, akisema: “Serikali haina uhusiano na hilo. Inatoa ulinzi unaohitajika.”
Mhamiaji mmoja, baba wa watoto wawili ambaye ameishi Mandera kwa miaka minane, alisema: “Tulinunua pikipiki, tukafungua hoteli na tulikuwa tukifanya kazi. Hatufahamu sababu, lakini wao (wakazi wa eneo hilo) walianza kusema Waethiopia wote waondoke.”
Wengine waliripoti kunyanyaswa, kukamatwa na kudaiwa rushwa.
“Wanakuja kwa magari ya polisi na kutuchukua kutoka kwenye teksi hadi gerezani. Tuko matatani. Hatuna mtu wa kutusaidia,” alisema mkazi mmoja, akiongeza kuwa Waethiopia wanaoishi Mandera, wanaokadiriwa kuwa takribani watu 10,000, wamekuwa wakijihusisha na shughuli za usafiri wa pikipiki na sekta ya hoteli.
Kwa mujibu wa mashuhuda, mvutano huo unatokana na malalamiko ya kiuchumi.
Wakazi wa eneo hilo wanadaiwa kuwashutumu Waethiopia kwa “kuvamia” eneo hilo na kuchukua biashara.
Wahamiaji walipotaka maelezo kutoka kwa viongozi wa serikali ya eneo hilo, waliambiwa waende kuwauliza wazee wa jamii.
Nao wazee waliwaambia: “Hatutaki kuwaona. Ondokeni katika nchi yetu.”
Mashuhuda walisema kampeni hiyo iliongezeka baada ya kuuawa kwa mhamiaji mmoja wa Ethiopia wiki moja iliyopita katika eneo linaloitwa Burabur.
Mwili wake ulizikwa hapo hapo baada ya mamlaka kukataa kurejeshwa Ethiopia.
Baada ya mazishi hayo, wakazi walianzisha kampeni ya kudai Waethiopia waondoke Mandera, wakitoa vitisho vya kupigwa mawe na kuuawa baada ya tarehe ya mwisho ya Februari.
Wahamiaji wanadai agizo hilo lilitolewa na wazee wa jamii wa kaunti na kusambazwa kupitia vipaza sauti vilivyowekwa kwenye magari.
Pia wanadai kuwa polisi wanawakamata Waethiopia na kudai hadi shilingi 20,000 ili kuwaachia huru, huku wasioweza kulipa wakifungwa gerezani.
“Hatuna chaguo jingine ila kujiandaa kuondoka,” alisema mhamiaji mmoja.
Soma Pia:
Trump asema Marekani 'haitaisaidia tena Iraq' ikiwa itamchagua Maliki kama Waziri Mkuu
Rais Donald Trump ametishia kuondoa msaada wa Marekani kwa Iraq iwapo aliyekuwa Waziri mkuu wa nchi hiyo Nouri al-Mailiki atarejea madarakani.
Bwana Maliki aliye na mafungamano na Iran ameteuliwa kuwa Waziri mkuu na muungano wa vyama vya Kishia ambavyo vina wingi wa uwakilishi bungeni.
Al Maliki alikuwa waziri mkuu wa Iraq kati ya mwaka 2006 hadi 2014.Kwa mara nyingine,Rais Trump anaonekana kuingilia mchakato wa kisiasa wa taifa jingine,baada ya kufanya hivyo katika uchaguzi wa Honduras na Argentina.
Trump alisema nchi hiyo itakuwa na nafasi "sifuri" ya kufaulu bila uungwaji mkono wa Marekani baada ya kuapa "haitaisaidia tena" nchi hiyo ikiwa Maliki atachaguliwa.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio alielezea wasiwasi wake kuhusu uhusiano wa Maliki na Iran wakati wa mazungumzo na Waziri Mkuu aliye madarakani Mohammed Shia al-Sudani siku ya Jumapili, akisisitiza "kwamba serikali inayodhibitiwa na Iran haiwezi kutanguliza maslahi ya Iraq mbele".
Soma Pia:
Seneta wa zamani wa Ufaransa apatikana na hatia ya kumlewesha mbunge dawa za kulevya
Seneta wa zamani wa Ufaransa Joel Guerriau amehukumiwa kifungo cha miaka minne jela kwa kumuwekea dawa za kulevya mbunge Sandrine Josso kwenye kinywaji chake kwa lengo la kumshambulia kingono.
Mahakama ilibaini kuwa bwana Guearriau alimuwekea bi Josso dawa aina ya ecstasy kwenye gilasi yake ya Champagne alipokuwa amemtembelea nyumbani kwake mjini Paris.
Joel Guerriau alipokea kifungo cha miaka minne jela - miezi 18 ambayo itatumikia gerezani - na, kulingana na vyombo vya habari vya ndani, aliamriwa kumlipa Sandrine Josso €5,000 (£4,348) kama fidia kwa msongo wa mawazo.
Muda mfupi baada ya uamuzi huo siku ya Jumanne, Josso alisema ilikuwa "afueni kubwa", AFP inaripoti. Wakati huo huo, mawakili wa Guerriau walisema atakata rufaa.
Soma Pia:
Zelensky alaani shambulizi baya la ndege zisizo na rubani za Urusi kwenye treni ya abiria
Rais wa Ukraine Volodomyr Zelensky amesema watu wanne wameuawa na wengine kadhaa hawajulikani waliko baada ya ndege ya Urusi isiyoendeshwa na rubani kushambulia treni iliyokuwa imebeba abiria kaskazini mashariki mwa Ukraine.
Rais Zelensky amelitaja shambulizi hilo kuwa la kigaidi akisema hakuna sababu yoyote ya kuwaua raia ndani ya treni iliyokuwa imewabeba zaidi ya watu mia mbili.
Urusi haijatoa maoni kufikia sasa.
Moscow katika miezi ya hivi karibuni imeongeza mashambulizi yake ya ndege zisizo na rubani na makombora yanayolenga miundombinu ya nishati na usafiri ya Ukraine huku nchi hiyo ikikabiliwa na msimu wa baridi kali zaidi kuwahi kutokea katika miaka iliyopita.
Mamilioni ya watu kote Ukraine wameachwa bila joto, umeme na maji baada ya mashambulio ya Urusi.
Rais wa Urusi Vladimir Putin alizindua uvamizi kamili mnamo Februari 2022, na Moscow kwa sasa inadhibiti karibu asilimia 20% ya eneo la Ukraine.
Soma pia:
Iran ikivamia Israel, tutajibu kwa nguvu haijawahi kushuhudiwa - Netanyahu
Waziri Mkuu wa Israel amesema kuwa iwapo Iran itajaribu kuishambulia nchi yake kwa shambulio la kushtukiza, ataijibu kwa nguvu kali.
Benjamin Netanyahu alisema katika mkutano na waandishi wa habari kuhusu uwezekano wa Iran kuishambulia nchi yake mapema,
“Ikiwa Iran itafanya kosa kama hilo na kuishambulia Israel, tutajibu kwa nguvu ambayo Iran haijawahi kuona hapo awali.”
Aliongeza pia kuwa serikali ya Israel imejiandaa kwa hali yoyote kwa kufuatilia kwa karibu maendeleo ya matukio, bila kujali maamuzi yatakayofanywa na Donald Trump.
Kauli za Bw. Netanyahu zilitolewa wakati mvutano ukiendelea kuongezeka kati ya Marekani na Iran, pamoja na kuwasili kwa meli ya kivita ya kubeba ndege, Abraham Lincoln, katika eneo la Kamandi Kuu ya Marekani (CENTCOM) katika Ghuba ya Uajemi.
Soma Pia:
Trump 'kulegeza kamba' dhidi ya wahamiaji haramu kufuatia mauaji ya Mmarekani
Rais wa Marekani Donald Trump amesema utawala wake utapunguza operesheni yake ya kuwasaka wahamiaji haramu mjini Minneapolis baada ya maafisa wa kikosi maalum cha uhamiaji kuwaua watu wawili katika mji huo mwezi huu.
Kitendo hicho cha maafisa wa ICE kilichochea wimbi la maandamano ya umma na shutuma kali.
Hayo yanajiri huku waziri wa usalama wa ndani Kristi Noem akikabiliwa na shinikizo la kujiuzulu kufuatia mauaji hayo ya Minneapolis.
Viongozi wa Democratic bungeni wametishia kupiga kura ya kutokuwa na imani naye iwapo Rais Trump hatamfuta kazi.
Seneta wa Republican Thom Tilisi amesema bi Noem anamfanya Rais Trump kuonekana mbaya lakini Rais Trump amesema ana imani naye akiongeza kuwa amefanya vizuri tu katika wadhifa wake.
Rais pia alizungumza kwa simu Jumatatu na Gavana wa Minnesota Tim Walz na Meya wa Minneapolis Jacob Frey, ambao wote ni Wanademokratic. Frey alisema baadaye kwamba Trump alimwambia "hali iliyopo" huko Minneapolis haiwezi kuendelea.
Soma zaidi: