Rais wa Marekani Joe Biden amesema kuondoka kwa majeshi ya Marekani Afghanistan ulikuwa uamuzi bora

Rais wa Marekani Joe Biden

Chanzo cha picha, Reuters

Rais Joe Biden ametetea uamuzi wake uliokosolewa kwa kiasi kikubwa wa kuwatoa wanajeshi wa Marekani kutoka Afghanistan - tukio ambalo lilisababisha kuanguka ghafla kwa serikali ya Afghanistan na kurejea kwa wanamgambo wa Taliban wanaodhibiti nchi hiyo.

Tangu tarehe 15 Agosti, wakati mji mkuu, Kabul, ulipoanguka - operesheni ya kijeshi iliyoongozwa na Marekani ilianzishwa kuwaondoa zaidi ya watu 120,000 - raia wa Magharibi na Waafghan ambao walikuwa wakifanya kazi kwao.

Kwa hivyo Biden alisema nini juu ya uamuzi huu?

Rais Biden alisema alikubali jukumu la uamuzi wa kujiondoa, akiongeza kuwa anaamini kuwa kukaa muda mrefu haikuwa nia yao.

Ingawa vikosi vya usalama vya Afghanistan vilianguka haraka kuliko ilivyotarajiwa, Marekani ilikuwa tayari kwa hali hiyo, pia, Biden alisema

Kuhusu uokoaji, alisema "ni Marekani tu ndiyo iliyokuwa na uwezo na utashi " wa kutekeleza hilo.

Rais aliahidi kuwahamisha Wamarekani walioachwa nchini Afghanistan "ikiwa watataka". Na kwa Waafghan wenyeji ambao wanataka kuondoka, alisema, "sisi hatujamaliza"

Wakati kukiwa na ukosoaji kwamba uokoaji unapaswa kuanza mapema, Biden alisema bado kungekuwa na " hali ya kukimbilia uwanja wa ndege"

Ingawa kulikuwa na vitisho kwa Marekani kutoka kwa wanamgambo wa Kiisilamu, rais wa Marekani alisema mkakati wa Marekani ulibidi ubadilike - hakukuwa na haja ya kuwa na wanajeshi ardhini kupambana na ugaidi

Na akizungumzia washirika wa IS ambaowa walishambulia umati katika uwanja wa ndege wa Kabul - na kuua zaidi ya watu 170, 13 kati yao wanajeshi wa Marekani - Biden alionya: "ISIS-K bado hatujamalizana na wewe."