Fahamu mfumo wa utawala wa Iran

Muda wa kusoma: Dakika 5

Kiongozi wa kidini (Supreme Leader)

Yeye ndiye mtu mwenye mamlaka makubwa zaidi nchini Iran, nchi ambayo imewahi kuwa na viongozi wa kidini wawili tu tangu mapinduzi ya Kiislamu ya mwaka 1979; Ayatollah Ruhollah Khomeini (mwanzilishi wa Jamhuri ya Kiislamu) na mrithi wake, Ayatollah Ali Khamenei.

Khomeini alianzisha nafasi hii katika uongozi wa kisiasa wa Iran baada ya kuipindua utawala wa Mohammad Reza Pahlavi.

Kiongozi wa kidini ndiye kamanda mkuu wa vikosi vya ulinzi vya Iran na anadhibiti vyombo vyote vya usalama. Pia humteua mkuu wa mahakama, nusu ya wajumbe wa baraza lenye nguvu la waangalizi(Guardian Council), maimamu, pamoja na wakuu wa mashirika ya televisheni na redio za serikali.

Ayatollah Ali Khamenei alikuwa kiongozi wa kidini baada ya kifo cha Ayatollah Ruhollah Khomeini mwaka 1989, na tangu wakati huo ameendelea kuwa imara katika uongozi wake licha ya kukabiliana na changamoto nyingi.

Rais

Rais ndiye afisa wa juu zaidi anayechaguliwa na wananchi na anashikilia nafasi ya pili baada ya kiongozi wa kidini. Rais ana ushawishi mkubwa katika sera za ndani na masuala ya nje, lakini kiongozi wa kidini ndiye mwenye uamuzi wa mwisho katika mambo yote ya dola.

Rais wa Jamhuri ya Iran huchaguliwa kwa muhula wa miaka minne na haruhusiwi kuhudumu zaidi ya mihula miwili mfululizo.

Katiba inamtaja kama afisa wa pili katika ngazi ya uongozi wa Iran,na mwenye jukumu la kuhakikisha majukumu ya kikatiba yanatekelezwa.

Wizara ya mambo ya ndani, ambayo inaripoti kwa Rais, inasimamia jeshi la polisi la taifa. Hata hivyo, kamanda wake huteuliwa na kiongozi wa kidini na huwajibika moja kwa moja kwa kiongozi huyo, kama ilivyo kwa makamanda wa Islamic Revolutionary Guard Corps (IRGC) na kundi la polisi la Basij.

Bunge pia linaweza kufuatilia na kudhibiti mamlaka ya rais kwa kutunga sheria mpya.

Raia wa Iran walimchagua Masoud Pezeshkian kuwa mrithi wa Ebrahim Raisi, aliyefariki baada ya ndege yake kuanguka mwezi Mei, 2024.

Bunge

Bunge la Iran linawabunge 290, ambao huchaguliwa na kura ya wananchi kila baada ya miaka minne.

Bunge lina mamlaka ya kutunga sheria, kuunda bajeti ya kila mwaka, na kuwateua au kuwaondoa mawaziri pamoja na rais. Hata hivyo, sheria zote zinazopitishwa na bunge lazima ziidhinishwe na baraza la waangalizi(Guardian Council).

Baraza la waangalizi (Guardian Council)

Baraza la waangalizi ni mojawapo ya taasisi zenye nguvu kubwa zaidi nchini Iran.

Linaidhinisha miswada yote inayopitishwa na bunge na lina mamlaka ya kukataa iwapo mswada huo unakinzana au unaenda kinyume na katiba au sheria ya kiislamu.

Pia linaweza kuwazuia wagombea kushiriki katika uchaguzi wa ubunge, urais, na baraza la wataalamu (Assembly of Experts).

Ahmad Jannati kwa sasa anahudumu kama Katibu wa baraza la waangalizi la Iran.

Baraza lina jumla ya wanachama 12; wanasheria sita wa dini, wanaoteuliwa na kiongozi wa kidini, na wataalamu sita wa sheria wanaopendekezwa na mahakama na kuidhinishwa na bunge.

Baraza la wataalam wa uongozi.

Baraza hili lina wanachama 88 ambao ni wanasheria wa dini, na lina jukumu la kumteua kiongozi wa kidini na kufuatilia utendaji kazi wake.

Ikiwa itadhibitishwa kiongozi wa kidini hawezi kutekeleza majukumu yake, baraza hili lina mamlaka ya kumfuta kazi.

Movahedi Kermani kwa sasa anashikilia nafasi ya mwenyekiti wa baraza la wataalam.

Ikiwa kiongozi wa kidini atafariki au kushindwa kutekeleza majukumu yake, uchaguzi wa siri hufanywa ambapo mrithi wake huchaguliwa.

Uchaguzi wa kuwateua wanachama wa baraza hili hufanyika kila baada ya miaka minane.

Baraza la Kutoa maamuzi ya maslahi ya taifa.

Baraza hili humshauri kiongozi wa kidini na lina mamlaka ya mwisho ya kutatua migogoro yoyote juu ya sheria kati ya bunge na baraza la waangalizi.

Kiongozi wa kidini huteua wanachama wake 45, ambao ni viongozi mashuhuri wa dini, kijamii, na kisiasa. Rais wa sasa wa baraza hili ni Ayatollah Sadeq Larijani, aliyekuwa mkuu wa mahakama..

Mahakama

Kiongozi wa kidini wa Iran, hufanya uteuzi wa jaji mkuu na anaripoti kwake.

Mahakama na majaji wake huhakikisha utekelezaji wa sheria ya Kiislamu.

Mkuu wa sasa wa Mahakama ya Iran ni Gholamhossein Mohseni Ejei.

Mahakama, kwa kushirikiana na vyombo vya usalama na ujasusi vimekandamiza vikali upinzani nchini humo, na wanaharakati wa haki za binadamu mara nyingi hukosoa mahakama kwa kutoa maamuzi yasiyo ya haki kwa watu wanaokabiliwa na mashtaka ya kuhatarisha usalama wa taifa.

Vikosi vya ulinzi

Vikosi vya ulinzi vinajumuisha Islamic Revolutionary Guard Corps (IRGC) na jeshi la kawaida.

Islamic Revolutionary Guard Corps (IRGC) ilianzishwa baada ya mapinduzi ili kuilinda serikali ya kiislamu.

Jeshi hilo lina vikosi vyake vya ardhini, vya majini na vya angani.

Makamanda wote wa ngazi ya juu wa Islamic Revolutionary Guard Corps na viongozi wa jeshi katika jeshi la kawaida la Iran huteuliwa na Kiongozi wa kidini, ambaye ndiye kamanda mkuu wa vikosi vya ulinzi, na wanawajibika kwa yeye peke yake.

Baraza la mawaziri

Wanachama wa baraza la mawaziri, au serikali, huchaguliwa na rais. Wanaochaguliwa lazima waidhinishwe na bunge, ambalo pia linaweza kuwaondoa mawaziri.

Baraza la mawaziri linaongozwa na rais au makamu wa kwanza wa rais, ambaye ana jukumu la kusimamia masuala ya baraza la mawaziri.

Polisi wa maadili

Polisi wa maadili ni kitengo cha jeshi la polisi la taifa.

Nafasi hii ilianzishwa mwaka 2005 ili kudumisha maadili ya kiislamu na sheria zinazohusiana na mavazi "sahihi," ambazo zilianzishwa baada ya mapinduzi ya kiislamu ya mwaka 1979.

Inakadiriwa kuwa kuna askari wa polisi wa maadili takriban 7,000 wa kiume na wa kike wenye mamlaka ya kutoa onyo, kutoa faini, au kuwakamata washukiwa.

Revolutionary Guard

Islamic Revolutionary Guard Corps ni shirika kuu nchini Iran la kudumisha usalama wa ndani.

Jeshi la hilo pia lina tawi la nje linaloitwa Quds Force, na vinadhibiti pia vikosi vya Basij.

Imetafsiriwa na Beldeen Waliaula