Zaidi ya wafungwa 1,500 wa kisiasa wa Venezuela waomba msamaha
Jumla ya wafungwa 1,557 wa kisiasa wa Venezuela wameomba msamaha chini ya sheria mpya iliyowasilishwa Alhamisi, Rais wa Bunge la Taifa amesema. Jorge Rodríguez, kaka wa Rais wa mpito wa Venezuela Delcy Rodríguez na mshirika wa Rais wa zamani Nicolás Maduro, pia alisema "mamia" ya wafungwa walikuwa tayari wameachiliwa.
Miongoni mwao ni mwanasiasa Juan Pablo Guanipa, mmoja wa sauti kadhaa za upinzani zilizokosoa sheria hiyo kwa kuwatenga baadhi ya wafungwa.
Marekani imeitaka Venezuela kuharakisha kuachiliwa kwa wafungwa wa kisiasa tangu vikosi vya Marekani vilipomkamata Maduro katika uvamizi wa tarehe 3 Januari.
Serikali ya kijamaa ya Venezuela imekuwa ikikanusha kila mara kuwashikilia wafungwa wa kisiasa.
Katika mkutano na waandishi wa habari siku ya Jumamosi, Jorge Rodríguez alisema maombi 1,557 ya kuachiliwa huru yanashughulikiwa "mara moja" na hatimaye sheria hiyo itafikia wafungwa 11,000.
Serikali ilitangaza kwa mara ya kwanza siku chache baada ya kukamatwa kwa Maduro, mnamo Januari 8, kwamba "idadi kubwa" ya wafungwa wataachiliwa huru kama ishara ya nia njema.
Upinzani na makundi ya haki za binadamu yamesema serikali chini ya Maduro ilitumia kizuizi cha wafungwa wa kisiasa kuwakomesha wapinzani na kuwanyamazisha wakosoaji kwa miaka mingi.
Makundi haya pia yamekosoa sheria mpya. Ukosoaji mmoja unaotajwa mara kwa mara ni kwamba hautatoa msamaha kwa wale waliotaka kuingilia kati kwa silaha za kigeni nchini Venezuela, mtaalamu wa BBC Amerika Kusini Luis Fajardo anasema.
Alibainisha kuwa profesa wa sheria Juan Carlos Apitz, wa Chuo Kikuu cha Kati cha Venezuela, aliambia CNN hispania kwamba sehemu hiyo ya sheria ya msamaha "ina jina na jina la ukoo". "Kifungu hicho ni aya ya Maria Corina Machado." Haijulikani wazi kama msamaha huo utamnufaisha Machado, ambaye alishinda Tuzo ya Amani ya Nobel mwaka jana, Fajardo alisema.
Unaweza kusoma;