Waziri Mkuu wa Senegal apendekeza sheria kali dhidi ya wapenzi wa jinsia moja
Waziri Mkuu wa Senegal Ousmane Sonko amependekeza sheria ambayo inaweza kuongeza maradufu adhabu kwa watu wenye kujihusisha na mapenzi ya jinsia moja, na kuwafanya waadhibiwe kwa hadi miaka 10 jela.
Pendekezo hilo lilipelekwa bungeni Jumanne baada ya kuidhinishwa na baraza la mawaziri wiki iliyopita, baada ya wimbi la kukamatwa kwa watu wanaodaiwa kuwa wapenzi wa jinsia moja.
Akihutubia wabunge, Sonko alisema muswada huo utaadhibu kile kinachoelezwa kama "vitendo kinyume na maumbile" kwa vifungo vya gerezani kuanzia miaka mitano hadi 10, ikilinganishwa na adhabu ya sasa ya mwaka mmoja hadi mitano.
"Ikiwa kitendo hiki kitafanywa kwa mtoto mdogo, adhabu itakuwa ya juu zaidi," alisema, akikosolewa na watetezi wa haki za binadamu.
Mjadala kuhusu haki za LGBT umesababisha mvutano kwa muda mrefu nchini Senegal, nchi ya kihafidhina ambapo baadhi ya makundi yanasema harakati za LGBT ni uingiliaji kati wa kigeni.
Mashirika ya kidini yamekuwa yakifanya maandamano katika miaka ya hivi karibuni yakitaka adhabu kali zaidi.
Mapema mwezi huu, polisi waliwakamata wanaume 12 chini ya sheria zinazopinga LGBT. Vyombo vya habari vya ndani vinasema takriban watu 30 wamekamatwa kwa jumla mwezi huu.
Wale watakaopatikana na hatia wanaweza pia kukabiliwa na faini ya hadi CFA milioni 10 (karibu $18,000; £13,000), Sonko aliongeza.
Tarehe bado haijawekwa kwa ajili ya kura ya bunge kuhusu muswada huo, katika bunge linalodhibitiwa na chama cha Sonko cha Pastef.