Matokeo ya Uchaguzi Kenya 2022: Fahamu kiasi cha fedha anazolipwa rais mstaafu wa Kenya anapostaafu

Chanzo cha picha, Ikulu ya Rais Kenya
- Author, Abdalla Seif Dzungu
- Nafasi, BBC Swahili
Waswahili wanasema hayawi hayawi huwa, hatimaye uchaguzi mkuu wa Kenya umefanyika na naibu Rais William Ruto ametangazwa mshindi na Tume ya Uchaguzi IEBC licha ya mvutano uliokuwepo kati ya makamishna wa tume hiyo.
Makamishna wanne wa IEBC kati ya saba waliopo walipinga matokeo hayo yaliyotolewa na mwenyekiti wa tume hiyo Wafula Chebukati wakidai kwamba licha ya zoezi hilo kuendeshwa vizuri, awamu ya mwisho ya shughuli hiyo ilikumbwa na kiza kikuu.
Hatahivyo Ruto sasa anatarajiwa kumrithi rais Uhuru kenyatta kama rais wa tano wa taifa la Kenya tangu taifa hili lijipatie Uhuru iwapo mpinzani wake Raila Amollo Odinga hatokwenda mahakamani kupinga matokeo hayo.
Na baada ya William Ruto kutangazwa kuwa rais mteule, Rais Uhuru Kenyatta anatarajiwa kumkabidhi mrithi wake mamlaka na kuendelea na maisha yake ya kustaafu.

Kabla ya kustaafu kwake , kamati ya makabidhano ya mamlaka ilifanya kikao chake siku ya Ijumaa.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Joseph Kinyua, alipokuwa akihutubia wanahabari kutoka , alisema tarehe ya kuapishwa kwa rais mteule itatangazwa kuwa siku ya mapumziko
Alisema kwamba mamlaka ya kamati hiyo yataanza kufanya kazi mara tu tume ya uchaguzi itamtangaza rasmi rais mteule.
Lakini baada ya kuhudumu kwa mihula miwili, Je maisha ya rais anayeondoka madarakani Uhuru Kenyatta yatakuwaje.
Mafao ya rais anayeondoka madarakani

Rais Uhuru Kenyatta ambaye anatarajiwa kuondoka madarakani atakabidhiwa marupurupu mengi ya kustaafu, ikiwa ni pamoja na kundi la magari ya kifahari, ofisi ya kibinafsi iliyo na samani kamili na wafanyakazi kadhaa baadaye mwaka huu.
Sheria inampatia wasaidizi wawili wa kibinafsi, makarani wawili, wajumbe wanne, madareva wanne pamoja na walinzi wanne katika ofisi yake mpya na wafanyakazi wanne wa nyumbani chini ya mfumo unaosimamiwa na walipa kodi. Wafanyakazi hao watatolewa na serikali.

Vilevile wafanyakazi hao watashirikisha makatibu wa habari na maafisa wa usalama watakaolipwa na serikali. Rais Kenyatta pia atakabidhiwa magari manne ikiwemo magari mawili aina ya limousine na magari mawili aina ya sport ambayo hubadilishwa kila baada ya miaka minne.
Marupurupu
Pia atakabidhiwa marupurupu ya kila mwezi ya shilingi 300,000 , marupurupu ya mafuta ya ksh.200,000, marupupuru ya burudani ya ksh. 300,000 na marupurupu mengine ya ksh 300,000 yatakayolipa kodi ya maji na umeme pamoja na bima ya afya.
Mbali na hayo rais Uhuru Kenyatta pia atakabidhiwa ofisi yenye samani iliokamilika , takrima ya mwaka mmoja kwa kila muhula aliohudumu mbali na pensheni ya kila mwezi ya asilimia 80 ya mshahara wake aliopata katika mwezi wake wa mwisho. Mshahara rasmi wa rais ni ksh. Milioni 1.44.

Bima ya afya ya rais anayeondoka madarakani inamruhusu kupata matibabu nyumbani na ughaibuni. Bima hiyo pia inamshirikisha mkewe Margeret Kenyatta.
Mafao ya kustaafu ya marais wastaafu yamezingatiwa sana, haswa katika miaka michache iliyopita wakati mgao uliongezeka kwa kiasi kikubwa, licha ya serikali kusisitiza kuwa imeweka hatua za kubana matumizi ili kukabiliana na mishahara mikubwa ya wafanayakazi wa umma .

- MATAYARISHO:Uchaguzi Kenya 2022: Je Kenya iko tayari kwa uchaguzi mkuu?
- YA MSINGI:Uchaguzi Kenya 2022: Kwa nini uchaguzi wa Kenya mwaka huu ni muhimu?
- MIUNGANO:Uchaguzi Kenya 2022: Musalia Mudavadi kujiunga na naibu rais William Ruto itabadilisha siasa za Kenya?
- UNAYOFAA KUJUA:Uchaguzi Kenya 2022: Je Naibu wa rais wa Kenya William Ruto anakabiliwa na changamoto gani katika kumteua naibu wake wa rais?
- UCHAMBUZI:Uchaguzi wa Kenya 2022: Je hatua ya Rais Kenyatta kumuunga mkono Raila Odinga itamsaidia au kumharibia?
- WASIFU:William Ruto: Muuza kuku aliyepanda ngazi hadi kuwa naibu wa rais wa Kenya
- RAILA ODINGA:Uchaguzi Kenya 2022: Siwezi kuwa kibaraka wa mtu yeyote-Raila Odinga













