Vurugu zilizoripotiwa katika uchaguzi DRC

    • Author, Didier Lando
    • Nafasi, BBC News

Wapiga kura katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo bado walikuwa wakipiga kura siku ya Alhamisi, huku upigaji kura ukiongezwa muda hadi siku ya pili katika baadhi ya vituo.

Hii ilitokana na kasoro kadhaa na hitilafu za vifaa, ambayo yameshutumiwa na waangalizi na wagombea wa upinzani, na pia kutambuliwa na Ceni [Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi].

Hapa matukio ya kila aina yalinakiliwa katika muda wa saa 48 zilizopita, kulingana na waangalizi kutoka Synergie des Missions d'Observation Electorale (SYMOCEL) na misheni ya pamoja ya uangalizi ya Kanisa Katoliki - Kanisa la Kristo nchini DR Congo.

Uvamizi wa vituo vya kupigia kura na mashambulizi dhidi ya mawakala wa uchaguzi

Vituo vingi vya kupigia kura vilivamiwa katika baadhi ya maeneo nchini na wapiga kura waliokuwa wakiandamana kupinga masuala mbalimbali.

Huko Ituri, kundi la wakimbizi wa ndani walivishambulia vituo vya kupigia kura katika mji mkuu wa jimbo hilo, Bunia.

Hawakuweza kwenda katika vijiji vyao vya Djugu na hawakuweza kupiga kura katika mji wa kwao pia.

Inadaiwa pia waliwashambulia waangalizi, wakiwemo wale wa kundi la waangalizi la Symocel, kuharibu mashine za kupigia kura na vibanda vya kupigia kura.

Mwandamanaji mmoja pia alijeruhiwa, kulingana na Dieu Merci Udongo, mwandishi wa habari wa Radio Canal Révélation, mshirika wa redio ya BBC.

Awali tume ya uchaguzi ilikuwa imeahidi kuwa kituo cha kupigia kura kingefunguliwa kwa ajili ya watu waliokimbia makazi yao ili kuwawezesha kupiga kura.

Wakati hawakuweza kufanya hivi, watu waliokimbia makazi yao walijitokeza, wakitaka haki zao za kutekeleza wajibu wao wa kiraia zilindwe.

Mvutano ulipozidi, kulikuwa na jaribio la kushambulia kituo kingine cha kupigia kura katika mtaa wa Ndibekudu. Lakini polisi waliingilia kati kuzuia ghasia hizo.

Kulingana na Kanisa Katoliki, katika kituo cha Kole huko Sankuru, vifaa vya uchaguzi vya baadhi ya vituo vilichukuliwa na wakazi wa eneo hilo ambao walitaka kuwapigia kura wagombea wao.

Milio ya risasi pia ilisikika katika kituo cha kupigia kura cha Sadilayi Lomami huko Mwene Ditu, mji ulioko kusini mwa Mkoa wa Lomami.

Uharibifu wa vifaa vya uchaguzi

Katika maeneo mengine, waandamanaji walishambulia mashine za kupiga kura.

Walichoma mashine kadhaa, jambo ambalo lilisababisha upigaji kura kufutwa.

Kwa mfano, katika kijiji cha Bweta huko Lubero eneo la Kivu Kaskazini, upigaji kura haukufanyika baada ya zaidi ya mashine kumi za kupigia kura kuchomwa moto.

Wapiga kura walikasirishwa na kuchelewa kufunguliwa kwa vituo vya kupigia kura, ambavyo vingine vilifunguliwa saa sita baadaye badala ya vile ilivyopangwa.

"Huko Mousimba, vifaa vilifika kwa kuchelewa sana. Kuandamana, vijana ambao hawakuwa na subira ya kupiga kura waliwashambulia mawakala wa tume ya uchaguzi, kuharibu vituo vya kupigia kura na kuchoma moto mashine za kupigia kura," anasema Joseph Malikidogo Mutchuva, mshauri wa jumuiya ya kiraia.

"Katika kituo cha Lubero, vijana ambao walishuku kuwa mtawa mkuu wa shule ya msingi alinyakua mashine za kupigia kura ili kumchagua mgombea wake, waliharibu majengo na kuchoma mashine moja", asema Bw Mutchuva.

Jaribio la udanganyifu

Katika maeneo mengine, baadhi ya wagombea walipatikana wakijaribu kufanya udanganyifu.

Jimbo la Kwilu, Bandundu, mgombea ubunge alipatikana asubuhi na mapema akiwa na karatasi za kupigia kura zikiwa tayari zimejazwa na kuwekwa alama.

Kisa kingine kama hicho kiliripotiwa katika mji wa Kisangani, ambapo polisi walimkamata mgombea ubunge akiwa na vifaa vya kupigia kura.

Pia uanaweza kusoma:

Imetafsiriwa na Ambia Hirsi na kuhaririwa na Maryam Dodo Abdalla