Vita vya Israel na Hamas: Onyo la Iran kuchukua hatua mara moja lina ukweli kiasi gani?

Huku kukiwa na hofu ya Israel kuanzisha operesheni ya ardhini huko Gaza wakati wowote, Iran imeonya kuwa huenda ikachukua hatua za 'tahadhari'.

Ufyatulianaji risasi wa hapa na pale pia unaendelea kwenye mpaka wa Israel kati ya kundi la itikadi kali la Lebanon- Hezbollah linaloungwa mkono na Iran na jeshi la Israel.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Amir Abdullahiyan alisema katika mahojiano Jumatatu usiku kwamba 'hatua za tahadhari kutoka kwa wapinzani wa Israel' zinaweza kuchukuliwa katika saa chache zijazo.

Kauli hii ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran inachukuliwa kuwa kauli kali zaidi hadi sasa kuhusu Israel.

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu alipokuwa akizungumza bungeni aliionya Iran na Hezbollah.

Aliionya Hezbollah na Iran inayoiunga mkono , "Msitujaribu, mtaumia sana."

Kwa mujibu wa kituo cha habari cha serikali ya Iran Press TV, kiongozi mkuu wa kidini wa Iran Ayatollah Ali Khamenei amesema iwapo mashambulizi ya Israel yataendelea hakuna atakayeweza kuwazuia Waislamu.

Khamenei alisema, "Iwapo uhalifu huu utaendelea, Waislamu na vikosi vya waasi vitakosa utulivu na basi hakuna atakayeweza kuwazuia."

Khamenei alisema, "Ni ukweli kwamba hata Israel ifanye nini, haitaweza kufidia aibu iliyokumbana nayo" ya mashambulizi kutoka kwa Hamas.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema kuwa Hezbollah inaweza kuanzisha mapambano dhidi ya Israel.

Amir Abdullahiyan alisema, "Njia zote zinazowezekana na uwezo upo kwa Hezbollah.

Katika hesabu zao, kila hali imetathminiwa kwa usahihi na viongozi wa upinzani hawataruhusu nguvu ya Kiyahudi (Israel) kuchukua hatua yoyote katika eneo hilo. "Hatua zinazowezekana za tahadhari zinaweza kuchukuliwa na upinzani katika saa chache zijazo."

Alikuwa akimaanisha Lebanon kufungua mkondo mpya katika mzozo wa Israel na Gaza.

Vile vile alisema viongozi wote wa upinzani (Hezbollah) wanaamini kwamba iwapo kutapatikana suluhu la kisiasa la mgogoro wa Gaza, watatoa nafasi hiyo, lakini, 'Ikiwa utawala wa Kiyahudi utaendelea kufanya uhalifu wa kivita dhidi ya raia, basi hakuna hatua itakayochukuliwa.

Kwa mujibu wa kituo cha habari cha serikali ya Iran IRNA, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran alisema kuwa ‘upinzani una uwezo wa kupigana vita vya muda mrefu na adui na iwapo mzozo unaoendelea utaenea zaidi, utabadilisha ramani ya Israel.'

Iran inatafuta uungwaji mkono

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amekutana na viongozi na wanadiplomasia katika nchi kadhaa za Mashariki ya Kati katika wiki iliyopita. Akitoa mfano huu, amesema kwamba ikiwa 'chaguo chache zinazopatikana kwa Umoja wa Mataifa kusimamisha vita hazitatumika, basi kufungua mstari mpya dhidi ya Israel ni jambo lisiloepukika.'

Amir Abdullahiyan alisema, "Ikiwa hatutalindi Gaza leo, tutalazimika kulinda hospitali za watoto wa nchi yetu dhidi ya mabomu haya ya fosforasi kesho."

Siku ya Jumatatu yenyewe, Rais wa Iran Ebrahim Raisi alikuwa amesema kwamba muda unazidi kuyoyoma kutafuta suluhu la kisiasa kwa mgogoro wa Gaza. Raisi pia alionya kuwa mzozo wa Israel na Hamas unaweza kuenea katika maeneo mengine katika eneo hilo.

Huku mzozo kati ya Israel na Hamas, mashambulizi dhidi ya Israel kutoka Lebanon na mashambulizi ya kukabiliana na mabomu kutoka Israel pia yanaendelea.

Siku ya Jumanne pia, Hezbollah ilirusha kombora la kukinga tanki kuelekea Israel. Kulingana na ripoti za vyombo vya habari vya Israeli, Waisraeli watatu wamejeruhiwa katika shambulio hili.

IDF pia imetoa video kadhaa za mashambulizi dhidi ya malengo ya Hezbollah nchini Lebanon.

IDF sasa inajiandaa kwa awamu inayofuata ya operesheni yake huko Gaza. Jeshi la Israel linaweza kushambulia Gaza wakati wowote.