Watanzania watahadharishwa safari za Mashariki ya Kati
Serikali ya Tanzania imesema inafuatilia kwa karibu hali ya usalama inayoendelea katika eneo la Mashariki ya Kati.
Serikali kupitia Wizara yake ya Mambo ya Nje, imeshauri raia wa Tanzania wanaoishi au wanaopanga kusafiri katika eneo hilo ikiwemo Bahrain,Israel,Kuwait,Qatar na Falme za Kiarabu (UAE) kuzingatia;
- Kuepuka safari za kwenda au kutoka Mashariki ya Kati katika kipindi hiki.
- Kubaki katika makazi wanayoishi inapowezekana.
- Kufuata maelekezo yanayotolewa na mamlaka za maeneo husika na kuwa waangalifu wakati wote.
- Kuepuka maeneo yenye shughuli za kiusalama au kijeshi katika maeneo wanayoishi.
- Kutumia njia rasmi za mawasiliano na taarifa.
- Kuhifadhi pasipoti na vitambulisho vya Tanzania katika sehemu salama na vitakapopatikana kwa urahisi iwapo kutakuwa na dharura.
Taarifa ya Wizara hiyo imesema pamoja na Misheni za Kidiplomasia, itaendelea kutoa taarifa na usaidizi wa Kibalozi kadiri hali itakavyoruhusu katika maeneo husika.