Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Trump atishiwa kuuawa kwa 'mafumbo' kupitia Televisheni ya Iran

Pande zote mbili zimekuwa zikionya mara kwa mara kuhusu madhara ya shambulio lolote.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Mariam Mjahid

  1. Rekodi ya Guiness yamtambua Truphena Muthoni kwa kuukumbatia mti kwa saa 72

    Mwanamazingira kutoka Kenya, Truphena Muthoni, amepokea uthibitisho rasmi kutoka rekodi ya dunia ya Guinness (GWR) kwa kukumbatia mti kwa saa 72, zaidi ya mwezi mmoja baada ya kufanikisha rekodi hiyo.

    Truphena mwenye umri wa miaka 22 alishiriki rekodi hiyo kuanzia Jumatatu, Desemba 8, hadi Alhamisi, Desemba 11, 2025, nje ya ofisi ya gavana wa Nyeri, nchini Kenya, Mutahi Kahiga, akitumia jitihada hiyo kulalamika dhidi ya ukataji miti na kushirikisha utunzaji wa mazingira.

    Hii ilikuwa jitihada yake ya pili ya kuvunja rekodi, baada ya hapo awali kuweka rekodi ya saa 48 mnamo 2025.

    Katika chapisho la Facebook lililosomwa na BBC Swahili, Guinness ilieleza kuwa lengo la Truphena lilikuwa kukuza utunzaji wa miti na kuheshimu hekima za jadi za mazingira.

    "Shindano refu zaidi ya kukumbatia mti — saa 72 na @truphena_muthoni. Lengo la Truphena katika jitihada hii ya rekodi lilikuwa kuinua na kutetea ulinzi wa miti ya kienyeji na kuheshimu hekima za watu wa asili. Aliivunja rekodi yake mwenyewe ya saa 48, iliyowekwa awali mnamo 2025," ilisema taarifa hiyo, ikifuatana na video yake akiukumbatia mti.

  2. India, EU zatarajiwa kutangaza makubaliano ya kibiashara ya kihistoria

    India na Umoja wa Ulaya (EU) zimekamilisha makubaliano ya kihistoria ya biashara, amesema Waziri Mkuu wa India, Narendra Modi, Jumanne, huku pande zote mbili zikijaribu kujikinga dhidi ya uhusiano usiokuwa thabiti na Marekani.

    Baada ya takriban miongo miwili ya mazungumzo yasiyo thabiti, makubaliano hayo yatafungua njia kwa India kuwekeza na kufungua soko lake kubwa na lililolindwa sana, ambalo ni soko lenye idadi kubwa ya watu duniani, kwa biashara huru na Umoja wa Ulaya wa nchi 27, mshirika wake mkubwa wa kibiashara.

    “Jana Jumatatu ya 26 Januari, makubaliano makubwa yalisainiwa kati ya Umoja wa Ulaya na India,” alisema Modi.

    “Watu duniani kote wanayaita haya kama ‘makubaliano ya kihistoria.’ Makubaliano haya yataleta fursa kubwa kwa watu bilioni 1.4 wa India na mamilioni ya watu wa Ulaya,” alisema.

    Inatarajiwa kuwa Modi na Rais wa Tume ya Ulaya, Ursula von der Leyen, watatoa tangazo la pamoja katika kilele cha Mkutano wa India–EU mjini New Delhi, sambamba na maelezo ya kina ya makubaliano hayo, baadaye leo.

    Soma Pia:

  3. Trump asema Iran inataka makubaliano na Marekani - Axios

    Rais wa Marekani, Donald Trump, ameiambia Axios kwamba Iran inatafuta makubaliano na Washington huku Marekani ikituma nguvu kubwa za kijeshi kuelekea eneo hilo.

    Trump alisema: “Meli kubwa zenye nguvu zimeegeshwa karibu na Iran, lakini Tehran inataka kuzungumza. Wanataka kufanya makubaliano. Najua hivyo. Wametuita mara nyingi.”

    Afisa mmoja wa ngazi ya juu wa Marekani alithibitisha kwa waandishi habari kupitia simu kwamba Washington iko tayari kufanya makubaliano ikiwa Wairan wanataka kuwasiliana.

    Ripoti ya Axios, iliyochapishwa Jumatatu na mwandishi Barack Ravid, inabainisha kuwa nguvu za kijeshi zilizoko karibu na Iran ni kubwa zaidi kuliko zile zilizoko karibu na Venezuela.

    Hata hivyo, Trump anashikilia imani kuwa Iran inataka kuzungumza na kufikia makubaliano.

    Taarifa hiyo imejitokeza wakati kundi la meli ya kivita Abraham Lincoln lilifika katika eneo la Kamandi kuu ya Marekani ya Kati (CENTCOM) Mashariki ya Kati, eneo linalojumuisha Iran, ikionyesha uwepo wa kijeshi wa kimkakati wa Marekani katika eneo lenye mvutano.

    Hapo awali, Trump na baadhi ya wajumbe wake walitangaza kwamba maandalizi ya mazungumzo ya moja kwa moja na Tehran yalikuwa yameanza kabla ya kuanza kwa maandamano ya Januari nchini Iran.

    Wiki iliyopita, mjumbe wake maalum kwa Mashariki ya Kati, Steve Whittaker, alitarajia kuzungumza na Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Abbas Araqchi, kando ya jukwaa la uchumi la Davos, lakini mwaliko wake ulifutwa kufuatia ukandamizaji mkali wa maandamano hayo.

    Unaweza pia kusoma:

  4. Ufaransa yaidhinisha mswada wa kupiga marufuku mitandao ya kijamii kwa watoto chini ya miaka 15

    Wabunge wa Ufaransa wamepitisha mswada ambao utawapiga marufuku vijana wa chini ya umri wa miaka 15 nchini humo kuwa katika mitandao ya kijamii.

    Mswada huo uliopitishwa katika Bunge la kitaifa sasa utapelekwa kwa Baraza la Seneti ili kupitishwa kuwa sheria.

    Rais Emmanuel Macron ameitaja kuwa hatua muhimu kuelekea kuwalinda watoto wa Ufaransa.

    Maafisa wa Serikali wanatumai kuwa mswada huo utaidhinishwa haraka kuwa sheria ili ianze kutekelezwa mwanzoni mwa mwaka mpya wa masomo nchini humo unaoanza mwezi Septemba.

    Sheria hiyo ikipitishwa,itapiga pia marufuku wanafunzi kwenda shuleni na simu za mkononi.

    Mwezi uliopita,Australia ilikuwa nchi ya kwanza kupiga marufuku mitandao ya kijamii kwa watoto walio chini ya umri wa miaka 16.

    Soma pia:

  5. Marekani yaonesha picha za ndani ya meli ya kivita Abraham Lincoln inayoelekea Iran

    Kamandi kuu ya jeshi la Marekani ya Kati (CENTCOM) imetoa picha mpya zilizopigwa ndani ya meli ya kivita ya ndege, USS Abraham Lincoln (CVN-72).

    Picha hizo zinaonesha wanajeshi wakiwa ndani ya meli, wakifanya kazi za kiufundi huku meli ikiwa safarini katika Bahari ya Hindi, Januari 26.

    Tamko hilo liliendelea kufafanua kwamba kundi la mashambulio la meli ya Abraham Lincoln limepelekwa Mashariki ya Kati ili kuimarisha usalama na utulivu katika eneo hilo.

    Hapo awali, afisa mmoja wa serikali ya Marekani alithibitisha katika mahojiano na CBS kwamba kundi la mashambulio limeingia eneo la amri la CENTCOM Mashariki ya Kati, likiwemo Iran.

    Meli hiyo iliondoka katika eneo la Pasifiki la Asia Mashariki takriban wiki mbili zilizopita, ikiwa inaelekea Bahari ya Hindi na Bahari ya Oman, kufuatia ongezeko la mvutano kati ya Iran na Marekani.

    Sifa za meli hii ni kama vile:

    • Meli hii inafanya kazi kama uwanja wa ndege unaoelea, ikiwa na uwezo wa kurusha ndege nyingi kwa dakika moja.
    • Meli inaweza kufanya mashambulio ya anga dhidi ya malengo ya ardhini, baharini, na angani.
    • Imeundwa kufanya kazi kwa kipindi kirefu bila kuhitaji mafuta, jambo linaloruhusu uwepo wa muda mrefu karibu na Iran.
    • Mnamo 2012 na 2019, meli hii ilipelekwa kupitia Kipene cha Hormuz kinachounganisha Bahari ya Oman na Ghuba ya Uajemi, chenye urefu wa maili za baharini 21.
    • Meli hii inasafirishwa pamoja na manowari ya kasi na ya kulinda meli nyingine, ikitoa ulinzi wa kisasa wa makombora pamoja na uwezo wa mashambulio.

    Soma pia:

  6. Hezbollah yatoa tamko dhidi ya Marekani

    Naim Qasim, Katibu Mkuu wa shirika la Hezbollah la Lebanon, aliwaambia wafuasi wake katika hotuba ya televisheni na mkutano wa umma wa kuunga mkono Iran: “Kama Marekani na Israel zitaanza vita na Iran, hatutakaa kimya.”

    Kiongozi wa Hezbollah wa Lebanon alisema: “Tunaona tishio la Marekani dhidi ya Iran kama tishio kwetu, na tuna nguvu kamili kuchukua hatua yoyote tunayoyaona inafaa kukabiliana nalo.”

    Hotuba ya Naim Qasim ilipeperushwa moja kwa moja kwenye Televisheni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.

    Aliongeza: “Sisi hatutaunga mkono upande wowote katika suala la Iran, na tutatangaza hatua zetu wakati unaofaa,” akionya kuwa vita vipya na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran vinaweza “kuzuka tena katika eneo lote.”

    Miezi ya hivi karibuni, kumekuwa na mvutano wa maneno kati ya maafisa wa Iran na serikali ya Lebanon kuhusu usalimishaji wa silaha wa kundi hilo.

    Soma pia:

  7. UN yasisitiza utekelezaji kamili wa makubaliano ya kusitisha mapigano Gaza

    Umoja wa Mataifa umesema ni muhimu sana kuwa makubaliano ya kusitisha mapigano Gaza yakatekelezwa kikamilifu baada ya mwili wa mateka wa mwisho wa Israeli kupatikana jana Jumatatu.

    Wanamgambo wa Hamas wamesema walisaidia katika kupatikana kwa mwili wa Ran Gvili kama sehemu ya kuonesha wamejitolea kuzingatia makubaliano kati yao na Israel.

    Umoja wa Mataifa umesema idadi kubwa inayovunja rekodi ya Wapalestina waliaachwa bila ya makazi katika Ukingo wa Magharibi mwaka jana.

    Zaidi ya watu elfu thelathini na saba walilazimika kuyahama makazi yao kwa kiasi kikubwa wakikimbia mashambulizi makali ya Israeli yaliyolenga kambi za wakimbizi kaskazini mwa Gaza.

    Soma zaidi:

  8. Afisa mkuu wa uhamiaji aondoka Minneapolis, Trump apeleka 'Tsar' wa mipaka Tom Homan eneo la tukio

    Meya wa mji wa Minneapolis, Marekani, Jacob Frey amesema amefanya mazungumzo ya tija na Rais Donald Trump na kumuomba akomeshe operesheni ya kuwasaka wahamiaji haramu inayoendeshwa na kikosi maalum cha maafisa wa uhamiaji, operesheni ambayo imesababisha kamata kamata kubwa na mauaji ya raia wawili.

    Msemaji wa Ikulu ya Rais Karoline Leavit amesema Rais Trump anataka uchunguzi kuendeshwa kikamilifu kuhusu matukio yaliyojiri Minneapolis.

    Afisa mmoja wa ngazi ya juu wa uhamiaji nchini Marekani anatarajiwa kuondoka mjini Minneapolis, hatua inayotafsiriwa kama dalili ya mabadiliko ya msimamo wa Ikulu ya Marekani kufuatia kuuawa kwa raia wa pili wa Marekani kwa kupigwa risasi na maafisa wa ICE mwishoni mwa wiki.

    Wakati Kamanda wa Doria ya Mpakani Gregory Bovino na baadhi ya maajenti wa uhamiaji wakiondoka, “msimamizi wa mipaka” Tom Homan anatarajiwa kuongoza moja kwa moja shughuli za utekelezaji wa sheria eneo la Minnesota. Hatua hii inakuja baada ya tukio la Jumamosi lililosababisha kifo cha Alex Pretti na kuongeza mvutano.

    Uamuzi huo wa Rais Donald Trump unaonekana kuashiria nia ya utawala wake kupunguza au kurekebisha matumizi ya hatua kali za shirikisho katika operesheni yake ya kitaifa ya kudhibiti uhamiaji.

    Hata hivyo, licha ya mabadiliko hayo ya kiuongozi, ufuatiliaji wa shughuli za mtandaoni unaonyesha kuwa operesheni za ukaguzi na misako ya uhamiaji bado zinaendelea katika maeneo mbalimbali.

    Soma zaidi:

  9. Trump aongeza ushuru wa bidhaa zinazoagizwa Marekani kutoka Korea Kusini hadi 25%

    Rais wa Marekani, Donald Trump, ametangaza kuwa ataongeza ushuru wa bidhaa zinazoingizwa kutoka Korea Kusini hadi kufikia asilimia 25.

    Hatua hiyo imekuja baada ya kumshutumu Seoul kwa “kutotekeleza ipasavyo” makubaliano ya biashara yaliyofikiwa mwaka jana.

    Kupitia ujumbe aliouandika kwenye mitandao ya kijamii, Trump alisema ataongeza ushuru huo kutoka asilimia 15 kwa bidhaa mbalimbali zikiwemo magari, mbao, dawa, na “ushuru mwingine wote wa kulipizana (reciprocal tariffs)”.

    Trump alisema kuwa wabunge wa Korea Kusini wamekuwa wakichelewa kuidhinisha makubaliano hayo, ilhali Marekani “imechukua hatua haraka kupunguza ushuru wake kulingana na makubaliano yaliyofikiwa”.

    Kwa upande wake, Korea Kusini imesema haijapewa taarifa rasmi kuhusu uamuzi wa kuongeza ushuru kwa baadhi ya bidhaa zake, na imeomba mazungumzo ya haraka na serikali ya Marekani juu ya suala hilo.

    Ushuru hulipwa na makampuni yanayoingiza bidhaa kutoka nje ya nchi.

    Katika hali hii, makampuni ya Marekani yatalipa kodi ya asilimia 25 kwa bidhaa wanazonunua kutoka Korea Kusini.

    Trump amekuwa akitumia mara kwa mara ushuru kama njia ya kushinikiza au kutekeleza sera zake za kigeni katika muhula wake wa pili Ikulu.

    Jumamosi iliyopita, alitishia kuiwekea Canada ushuru wa asilimia 100 endapo ingeingia makubaliano ya biashara na China.

    Siku ya Jumatatu, maafisa wa China walisema kuwa makubaliano yao ya “ushirikiano wa kimkakati” na Canada hayalengi kudhoofisha au kuathiri nchi nyingine.

    Waziri Mkuu wa Canada, Mark Carney, alisema nchi yake haifuatilii makubaliano ya biashara huria na China, na kwamba “haijawahi” kufikiria kufanya hivyo.

    Awali, Trump alisema angeweka ushuru wa kuagiza bidhaa kutoka nchi nane, zikiwemo Uingereza, ambazo zilipinga mpango wa Marekani wa kuichukua Greenland, eneo linalojitawala chini ya Ufalme wa Denmark, ambayo ni mwanachama wa NATO.

    Baadaye, Trump aliondoa tishio hilo la ushuru kuhusu Greenland, akisema kumekuwa na maendeleo kuelekea “makubaliano ya baadaye” juu ya kisiwa hicho.

    Hata hivyo, tukio hilo liliharibu uhusiano wa Marekani na Denmark pamoja na washirika wengine wa NATO.

  10. Trump atishiwa kuuawa kwa 'mafumbo' kupitia Televisheni ya Iran

    Baada ya meli ya kivita ya kubeba ndege Abraham Lincoln kuingia katika eneo la operesheni la CENTCOM Mashariki ya Kati, mvutano kati ya Tehran na Washington umeongezeka tena.

    Pande zote mbili zimekuwa zikionya mara kwa mara kuhusu madhara ya shambulio lolote.

    Shirika la Habari la Fars, ambalo liko karibu na Walinzi wa Mapinduzi ya Iran, lilitoa video kadhaa siku ya Jumatatu za mahojiano yaliyofanywa kwenye kituo cha Ofogh cha Shirika la Utangazaji la Iran.

    Katika mahojiano hayo, Mostafa Khoshcheshem, mhadhiri wa chuo kikuu na mgeni kwenye kipindi hicho, anaelezea hali ya usalama nchini Iran baada ya kuuawa kwa waandamanaji kwa wingi.

    Pia anazungumzia kwa njia ya mafumbo suala la “kuuawa” kwa Rais wa Marekani Donald Trump, akilitaja kama “mshale usioonekana” na “msaada wa Mungu.”

    Donald Trump alisema katika mahojiano ya televisheni wiki iliyopita kwamba “ataifuta Iran kabisa kwenye uso wa dunia” endapo kutakuwa na jaribio lolote la kumuua.

    Soma Pia:

  11. Hujambo, na karibu kwa matangazo yetu ya moja kwa moja ya tarehe 27/01/2026.