Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Bunge la Seneti Marekani lashindwa kudhibiti nguvu za kivita za Trump huku Iran ikiishambulia Israel

Hatua hiyo ingesitisha hatua za kijeshi za Marekani nchini Iran bila idhini ya bunge.

Moja kwa moja

Na Ambia Hirsi

  1. Mamlaka ya Hali ya Hewa Kenya yatoa tahadhari ya mafuriko

    Wakenya wameshauriwa kujiandaa kwa mvuu kubwa itakayonyesha katika maeneo tofauti nchini hadi Jumamosi.

    Kulingana na taarifa iliyotolewa kwa umma na Idara ya utabiri wa hali ya hewa mvua itakayozidi milimita 20 itaendelea kunyesha katika maeneo tofauti nchini ndani ya saa 24 zijazo.

    Maeneo yatakayoshuhudia mvua kubwa ni pamoja na Kanda ya Ziwa Victoria, Magharibi mwa Kenya, nyanda za juu na kati pamoja na nyanda za chini kusini.

    Maeneo ya Pwani yanatarajia kupata mvua kubwa hadi tarehe tisa mwezi Machi.

    Wakaazi wa maeneo yaliyotajwa wametahadharishwa kwamba mvua hizo huenda zikasababisha mafurika.

    Kwa mujibu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa mafurika yanaweza kushahudiwa hata katika maeneo ambayo hayatakuwa na mvua kubwa.

    Mvua kubwa ikiandamana na nguromo za radi imekuwa ikinyesha katika maeneo tofauti ya nchi katika wiki za hivi karibuni hasa nyakati za usiku.

    Msimu wa mvua wa wa mwezi Machi na Mei umeanza katika maeneo ya Nyanda za Juu Magharibi mwa Bonde la Ufa, Bonde la Ziwa Victoria, maeneo ya kati mwa nchi na kusini mwa bonde la ufa.

    Wakenya wameombw akuwa makini msimu huu wa mvua na kutoendesha magari katika barabara zilizofurika maji.

    Pia unaweza kusoma:

  2. Uhispania yajibu tishio la Trump la kusitisha biashara kwa 'kupinga vita'

    Waziri Mkuu wa Uhispania Pedro Sánchez amepinga vikali tishio la Rais wa Marekani Donald Trump la kusitisha biashara na nchi hiyo kwa kurejelea msimamo wake dhidi ya vita na kile alichokiita "ukiukaji wa sheria za kimataifa".

    Katika hotuba yake kwa njia ya televisheni ya dakika 10, Pedro Sánchez aliangazia vita vya Ukraine na Gaza, pamoja na Vita vya Iraq zaidi ya miaka 20 iliyopita, na kusema msimamo wa serikali ya Uhispania ni "la kwa vita".

    Trump alitishia kuiwekea vikwazo Uhispania vya kibiashara kwa kukataa ombi la Marekani kutumia vituo vya pamoja vya Moron na Rotafor kuishambulia Iran.

    "Uhspania imekuwa mbaya," Trump alisema wakati wa mkutano na Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz Jumanne.

    "Tutasitisha biashara yote na Uhispania. Hatutaki kufanya lolote naUhispania," aliongeza.

    Merz baadaye alisema kuwa alimwambia Trump waziwazi kwamba angeweza kufanya makubaliano ya kibiashara na Ujerumani au Ulaya yote lakini sio na Uhispania.

    Soma pia:

  3. Qatar yawahamisha wakaazi karibu na Ubalozi wa Marekani mjini Doha

    Qatar imeanza shughuli ya kuwahamisha wakaazi wanaoishi karibu na Ubalozi wa Marekani mjini Doha kama hatua ya tahadhari ya muda, kwa mujibu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Qatar.

    "Malazi yanayofaa yametolewa kwao kama sehemu ya hatua muhimu za tahadhari," Wizara ilisema katika taarifa kwa mtandao wa kijamii wa X.

    Hii inakuja baada ya balozi za Marekani nchini Saudi Arabia na Kuwait, na ubalozi mdogo wa Marekani mjini Dubai, kushambuliwa na ndege zisizo na rubani wiki hii.

    Mapema wiki hii Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ilitoa witio kwa kwa raia wa Marekani kuondoka haraka iwezekanavya Mashariki ya Kati hata kama safari nyingi za ndege kutoka eneo hilo zimesitishwa au kuahirishwa.

    Serikali ya Marekani imekuwa ikihangaika kutafuta ndege za kukodi kwa raia wa Marekani katika Umoja wa Falme za Kiarabu, Saudi Arabia na Jordan, na kutaka kuwasaidia watu waliokwama kwingine kukata tikiti za ndege za kibiashara.

    Afisa wa wizara ya mambo ya nje ya Marekani alisema tangu tarehe 28 Februari, takriban raia 17,500 wamerejea nyumbani kutoka Mashariki ya Kati.

    Maelezo zaidi:

  4. Habari za hivi punde, Iran yakanusha kurusha makombora dhidi ya Uturuki

    Maafisa wakuu wa Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran wamesema katika taarifa yao kwamba nchi hiyo "inaheshimu mamlaka ya nchi jirani na rafiki yake Uturuki na inakanusha kurusha kombora lolote kuelekea ardhi ya nchi hiyo."

    Wizara ya Ulinzi ya Uturuki ilitangaza jana kuwa kombora la balistiki lililorushwa kutoka Iran lilibadili mkondo kuelekea anga ya Uturuki baada ya kupita katika anga za Iraq na Syria, na kuzuiwa na kuharibiwa na mfumo wa ulinzi wa anga wa NATO, wenye makao yake mashariki mwa Mediterania.

  5. Tazama: Kiwango cha uharibifu Iran kufuatia mashambulizi ya Marekani na Israel

    Video zilizorekodiwa kote nchini Iran zinaonyesha milipuko mikubwa katika miji kadhaa huku mgogoro katika eneo hilo ukifikia siku yake ya tano.

    Marekani na Israel ziliishambulia Iran siku ya Jumamosi na kumuua Kiongozi Mkuu Ayatollah Ali Khamenei.

    Kanda za video zilizowekwa kwenye mitandao ya kijamii - zilizothibitishwa na BBC na mashirika ya habari - siku chache zilizopita zinaonyesha milipuko na uharibifu mkubwa kote nchini.

    Marekani pia imetoa video ambayo inasema inaonyesha jinsi kambi za kijeshi zilivyopigwa.

    Iran imejibu hatua hiyo kwa wimbi la mashambulizi katika eneo zima la Mashariki ya Kati.

  6. Urusi yaishutumu Ukraine baada ya meli yake kuzama katika bahari ya Mediterania

    Meli ya Urusi ya kusafirisha gesi ya kimiminika (LNG) imezama katika bahari ya Mediterania kati ya Libya na Malta baada ya kukumbwa na mlipuko na kuwaka moto, maafisa wa bandari ya Libya wamesema.

    Urusi imeishutumu Ukraine kwa kuishambulia Arctic Metagaz kwa "ndege zisizo na rubani" zilizorushwa kutoka pwani ya Libya.

    Idara ya usalama ya serikali ya Ukraine SBU haijatoa kauli yoyote kuhusiana na madai hayo huku mamlaka ya bandari ya Libya imesema chanzo cha moto kwenye meli hiyo hakijabainika.

    Raia wa Libya wanasema meli hiyo ilikuwa imebeba takriban tani 62,000 za LNG kabla ya kukumbwa na milipuko na kwamba ilizama takriban maili 130 (240km) kaskazini mwa bandari ya Sirte nchini Libya.

    Wizara ya uchukuzi ya Urusi ilisema Warusi 30 walikuwa ndani ya Arctic Metagaz.

    Waziri wa Mambo ya Ndani wa Malta Byron Camilleri alisema wote walipatikana wakiwa "salama katika boti ya uokozi" wakati wa operesheni ya uokoaji ya vikosi vya jeshi vya Malta.

    Picha ambazo hazijathibitishwa zilizoibuka mitandaoni zinaonekana kuonyesha meli hiyo ikiwaka moto baada ya shambulio hilo la Jumanne.

    Maelezo zaidi:

  7. Zelensky tayari kuzisaidia nchi za Ghuba kukabiliana na mashambulizi ya droni

    Rais Volodymyr Zelensky amesema kwamba Ukraine inaandaa mipango ya kupeleka wataalamu katika eneo la Ghuba kusaidia washirika walinda nchi zao dhidi ya ndege zisizo na rubani na makombora ya Iran.

    Anasema alizungumza na wenzao katika Falme za Kiarabu UAE na Qatar hapo jana, na Jordan na Bahrain hii leo.

    Baada ya kujadili mzozo wa Mashariki ya Kati na mawaziri na makamanda, aliwaomba kubuni mkakati wa kuwasaidia washirika - bila kudhoofisha ulinzi wa Ukraine yenyewe.

    Katika chapisho kwenye mtandao wa kijamii wa X, Rais Zelensky alisema: "Ukraine inaweza kusaidia kulinda maisha na kuleta utulivu..."

    Aliongeza: "Jeshi letu lina uwezo unaohitajika. Wataalamu wa Ukraine watafanya kazi mashinani, na timu tayari zinaratibu hili. Tuko tayari kusaidia kulinda maisha, kulinda raia, na kuunga mkono juhudi za kweli za kuleta utulivu wa hali hiyo na kurejesha urambazaji salama katika eneo hilo."

    Soma pia:

  8. EPL: Arsenal yatamba, City wapata sare huku Man United ikipoteza

    Arsenal walinusurika pambano kali dhidi ya Brighton na kuendeleza uongozi wao kileleni mwa Ligi ya Premia hadi pointi saba.

    Brighton walikuwa timu bora kwa muda mrefu - lakini bao la Bukayo Saka lililofungwa mapema lilitosha kukipa kikosi cha Mikel Arteta ushindi wa hali ya juu huku wapinzani wao Manchester City wakilazimishwa sare ya 2-2 nyumbani na Nottingham Forest.

    Usiku wa Arsenal nusura uanze kwa njia ya janga katika sekunde za mwanzo wakati kipa David Raya alipompatia mpira kimakosa Carlos Baleba, lakini jaribio lake la kupangua lilikuwa dhaifu, na kumruhusu Gabriel kurudi nyuma na kuokoa shambulizi lake.

    Baadaye bahati ya The Gunners ilisimama baada ya dakika tisa wakati shuti la kawaida la Saka lilipomtoka Baleba na kupita kwenye miguu ya kipa wa Brighton Bart Verbruggen, ambaye hakuwa na jibu.

    Wakati huohuo Nattingham ambao walikuwa wanacheza ugenini dhidi ya Man City walikaa nyuma na kulinda lango la huku City ikitawala katika kipindi kirefu cha mchezo kabla ya Antoine Semenyo kufunga bao la kwanza na kutoa onyo kwa wageni.

    Wenyeji waliweka presha yao baada ya nusu saa wakati Rayan Cherki alipozamisha krosi ndani ya eneo la hatari na aliyesajiliwa Januari Semenyo akafunga bao lake la saba tangu ajiunge na City.

    Vilevile Manchester United ililazimika kukubali matokeo baada ya kufungwa 2-1 na wachezaji 10 wa Newcastle ugenini.

    Hatahivyo Michael Carrick hakuitupa timu yake tofauti na mtangulizi wake Ruben Amorim ambaye mara nyengine alinukuliwa akisema : "hii labda ni timu mbaya zaidi katika historia ya Manchester United", wakati alipokuwa akitoa maoni hayo zaidi ya mwaka mmoja uliopita baada ya kushindwa nyumbani na Brighton.

    Lakini Carrick anajua siku 11 kati ya kichapo cha 2-1 kutoka kwa Newcastle katika uwanja wa St James' Park na ziara ya Aston Villa Old Trafford mnamo Machi 15 zinaweza kuwa muhimu zaidi msimu wake.

    Pia unaweza kusoma:

  9. Hezbollah 'haitajisalimisha' asema kiongozi wake huku mashambulizi ya Israel yakiongezeka

    Kiongozi wa Hezbollah Naim Qassem amesema Kundi hilo linaloungwa mkono na Iran "halitajisalimisha" huku vita na Israel vikiendelea kuongezeka.

    Katika hotuba yake ya kwanza ya hadhara tangu mzozo wa kikanda kuenea nchini Lebanon siku ya Jumatatu, Qassem alisema Hezbollah ilizingatia makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyofikiwa mwishoni mwa 2024, lakini Israel "haikuzingatia masharti yake yoyote".

    "Tulikubaliana na suluhisho la kidiplomasia tukiliona kuwa ni fursa kwa serikali kuchukua jukumu lake, lakini tumekuwa tukisema mara kwa mara 'kuna mipaka ya uvstahamilivu'," alisema katika hotuba ya runinga.

    "Chaguo letu ni kukabiliana nao hadi kufikia hatua ya kujitolea kabisa, kwa mipaka ya mbali zaidi, na hatutasalimu amri," alisema.

    Hezbollah ilirusha roketi na ndege zisizo na rubani kuelekea Israel siku ya Jumatatu baada ya Kiongozi Mkuu wa Iran Ayotollah Ali Khamenei kuuawa katika mashambulizi ya Marekani na Israel.

    Israel imejibu mashambulizi ya anga na kupeleka wanajeshi kusini mwa Lebanon, huku maelfu ya raia wakilazimika kutoroka makaazi yao.

    Maelezo zaidi:

  10. Bunge la Seneti la Marekani lashindwa kudhibiti mamlaka ya vita ya Trump dhidi ya Iran

    Azimio la pande mbili linalolenga kudhibiti uwezo wa Rais Donald Trump wa kuanzisha vita nchini Iran limeshindwa katika Bunge la Seneti la Marekani, huku mgogoro ukiendelea kuongezeka Mashariki ya Kati.

    Hatua ya mamlaka ya vita ilikataliwa kwa kura 53 dhidi ya 47 ambayo kwa kiasi kikubwa kilipigwa kwa misingi ya chama. Ingesitisha hatua za kijeshi za Marekani nchini Iran bila idhini ya bunge.

    Wabungue wa chama cha Democratic wanasema kuwa Trump alichukua hatua ya kuishambulia Iran bila idhini ya Congress kwa kutoa sababu zinazobadilika za vita. Baadhi ya wa Republican wanasema watazuia azimio hilo, lakini wanaweza kubadilisha msimamo wao ikiwa vita vitaongezeka.

    Huku hayo yakijiri Jeshi la Israel limefanya mashambulizi mengine dihdi ya mkuu wa Iran Tehran.

    "IDF imeanza wimbi la ziada la mashambulizi yanayolenga miundombinu ya kijeshi ya utawala wa Iran kote Tehran," Jeshi la Ulinzi la Israel linasema katika taarifa.

    Jeshi hilo halikutoa maelezo zaidi kuhusu eneo mahususi, lakini inasema maelezo zaidi yatafuata.

    Shirika la habari la AFP linaripoti kuwa waandishi wake walishuhudia mlipuko mkubwa katika mji mkuu Jumatano usiku.

    Hapo awali, jeshi la Israel lilitangaza kuwa jeshi lake la anga lilikuwa limekamilisha "mashambulio makubwa" dhidi ya kambi ya mashariki ya Tehran yenye vituo vya amri na maafisa wa usalama wa ndani.

    Soma zaidi:

  11. Karibu katika matangazo ya moja kwa moja.