Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Kiongozi mkuu wa Iran 'huenda alijeruhiwa vibaya', huku mashambulizi yakiathiri uwezo wa Tehran kutengeneza silaha zaidi - Marekani

Waziri wa Ulinzi Pete Hegseth amesema Marekani itaanzisha mashambulizi ya kiwango cha juu zaidi dhidi ya Iran, huku ikiendelea "kuliangamiza" jeshi la Iran.

Moja kwa moja

Na Asha Juma & Abdalla Seif Dzungu

  1. Marekani yalegeza vikwazo dhidi ya ununuzi wa mafuta ya Urusi

    Bei ya mafuta ilipanda hadi zaidi ya $100 kwa pipa siku ya Alhamisi kutokana na mzozo unaoendelea, ikiwa ni pamoja na vitisho vya kusafirishwa kwa meli katika Mlango-Bahari wa Hormuz, njia yenye shughuli nyingi zaidi za usafirishaji wa mafuta duniani.

    Marekani imelegeza vikwazo dhidi ya ununuzi wa mafuta ya Urusi na mafuta ya petroli ambayo tayari yamepakiwa kwenye meli baharini, ili kujaribu kupunguza athari za kiuchumi duniani.

    Katibu wa Hazina Scott Bessent alisema msamaha huo wa muda wa siku 30 "hautaipatia serikali ya Urusi manufaa makubwa ya kifedha", ambayo ilisema ina takriban mapipa milioni 100 ya mafuta yanayosafirishwa kwa sasa.

    Kremlin ilifuatia habari hiyo na kusema Urusi inaona hatua za Marekani kama "kujaribu kuleta utulivu katika masoko ya nishati" na kwa hivyo maslahi ya nchi zote mbili yanawiana.

    Lakini waziri wa nishati wa Uingereza Michael Shanks aliambia BBC mapema kwamba Uingereza haitalegeza vikwazo dhidi ya mafuta ya Urusi "kabisa", akionya Vladimir Putin atapata fursa ya kuwekeza zaidi katika vita vya Ukraine.

  2. Habari za hivi punde, Wanajeshi wanne wafariki baada ya ndege ya Marekani ya kujaza mafuta kuanguka nchini Iraq

    Wanajeshi wanne kati ya sita wahudumu wa ndege ya kijeshi ya Marekani inayoongeza mafuta wamethibitishwa kufariki baada ya kuanguka magharibi mwa Iraq, Kamandi Kuu ya Marekani (Centcom) imesema.

    Juhudi za uokoaji zinaendelea baada ya kupotea kwa ndege hiyo aina ya KC-135, ilisema, ikiongezea kwamba kwamba ndege hiyo haikushambuliwa kimakosa.

    Ndege hiyo ya mafuta ilikuwa imehusika katika operesheni zinazoendelea za Marekani dhidi ya Iran na ilikuwa mojawapo ya ndege mbili zilizohusika katika tukio hilo.

    Ndege ya pili ilitua salama. Ndege hizo zinazotengenezwa na Boeing zina uwezo wa kujaza ndege nyengine mafuta zikiwa angani na kwa kawaida huwa na jukumu kubwa katika operesheni za kijeshi za Marekani.

    Zilitumiwa sana katika Vita vya kwanza vya Ghuba kupanua safu ya ndege za kivita na washambuliaji

  3. Miili ya wanamaji 84 wa Iran waliouawa katika shambulizi la torpedo la Marekani kurejeshwa makwao

    Miili ya wanamaji 84 wa Iran waliouawa katika shambulio la torpedo na manowari ya Marekani wiki iliyopita katika Bahari ya Hindi inatarajiwa kurejeshwa nyumbani siku ya Ijumaa, wizara ya ulinzi ya Sri Lanka imesema.

    Wanamaji hao walikuwa miongoni mwa 130 wanaodhaniwa kuwa ndani ya meli ya kivita ya Iran, Iris Dena, ilipozama tarehe 4 Machi takriban kilomita 40 kutoka ufukwe wa kusini mwa Sri Lanka.

    Polisi wakisindikiza miili yao hadi Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mattala Rajapaksa siku ya Ijumaa asubuhi kwa ajili ya kurejeshwa nchini Iran, baada ya kuhifadhiwa kwenye jokofu mbili katika Hospitali ya Kitaifa ya Galle.

    Sri Lanka ilisema wanamaji 32 waliokolewa na jeshi lake la majini baada ya shambulio la torpedo "watasalia Sri Lanka", kulingana na shirika la habari la AFP.

    Hakimu mmoja katika mji wa Galle nchini Sri Lanka aliamuru miili 84 iachiliwe kwa ubalozi wa Iran.

    Waziri wa Ulinzi wa Marekani Pete Hegseth alisema muda mfupi baada ya kuzama kwamba meli ya kivita ya Iran ilikufa "kifo cha kimya".

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araghchi alisema Marekani "imefanya ukatili baharini, maili 2,000 kutoka pwani ya Iran", na kuongeza kuwa "Marekani itakuja kujutia vikali mfano ilioweka".

    Video iliyotolewa na Wizara ya Ulinzi ya Marekani baada ya tukio hilo ilionyesha meli hiyo ikishambuliwa kabla ya kulipuka.

  4. Trump anasema anaamini kuwa kiongozi mpya wa Iran yuko hai lakini "amejeruhiwa"

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema katika mahojiano na Fox News kwamba kiongozi mpya wa Iran "aliumizwa" na mashambulizi ya Marekani na Israel katika siku ya kwanza.

    Kuhusiana na jeraha la Mojtaba Khamenei, Bw. Trump alisema: "Nadhani pengine ndivyo hivyo, nadhani amejeruhiwa, lakini nadhani pengine yuko hai kwa namna fulani."

    Hili ni jibu la kwanza la Rais wa Marekani baada ya kuchapishwa kwa ujumbe ulioandikwa na kiongozi mpya wa Jamhuri ya Kiislamu.

    Rais wa Marekani pia aliandika katika chapisho kwenye mtandao wa kijamii wa Truth Social: "Tutauangamiza kabisa utawala wa kigaidi wa Iran kijeshi, kiuchumi n.k." Aliendelea, akikosoa ripoti ya New York Times: "Jeshi la wanamaji la Iran limetoweka, jeshi lao la anga halipo tena, makombora yao, ndege zisizo na rubani na kila kitu kingine kinaharibiwa, na viongozi wao wametoweka kutoka kwa uso wa dunia."

    "Tuna vifaa vya mashambulizi visivyo na kifani, risasi zisizo na kikomo, na muda mwingi," alisema.

    Bw. Trump aliandika: “Wamekuwa wakiua watu wasio na hatia duniani kote kwa miaka 47 na sasa mimi, kama Rais wa 47 wa Marekani, ninawaua.

    Ni heshima kubwa iliyoje kufanya hivi!”

    Hapo jana Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu alisema kwa kejeli hatua za nchi yake dhidi ya Mojtaba Khamenei, kiongozi mpya wa Jamhuri ya Kiislamu na Naim Qassem, kiongozi wa Hizbullah: "Lau ingekuwa juu yangu, nisingewapa bima ya maisha."

    Siku ya Jumatatu, Baraza la Wataalamu lilimtambulisha Mojtaba Khamenei kama kiongozi wa tatu wa Jamhuri ya Kiislamu.

    Ujumbe wake jana ulikuja huku wasiwasi kuhusu afya yake na hali yake ya mwili ukiendelea kugonga vichwa vya habari kwenye vyombo vya habari, ambapo Alireza Salarian, balozi wa Iran nchini Cyprus, awali aliliambia gazeti la The Guardian la Uingereza kwamba "Nimesikia kuwa miguu, mikono na mikono yake imejeruhiwa... nadhani yuko hospitali kwa sababu amejeruhiwa" na "Sidhani kama yuko katika hali nzuri kutoa hotuba

  5. Mbunge wa Iran: Mojtaba Khamenei amenusurika kifo mara mbili

    Mjumbe wa Bunge la Iran amesema kuwa Mojtaba Khamenei, kiongozi mpya wa Jamhuri ya Kiislamu, hadi sasa "amenusurika" mashambulizi mawili.

    Kwa mujibu wa shirika la habari la serikali la IRNA, Mohammad Reza Rezaei Kochi, mwakilishi wa Jahrom katika bunge la Iran, alisema kuwa Mojtaba Khamenei "alikuwa na Ayatollah Seyyed Ali Khamenei wakati wa shambulio dhidi ya makazi ya Kiongozi Mkuu, lakini alinusurika kuuawa."

    Bwana Kochi aliendelea, "Shambulio pia lilifanywa katika hospitali wakati kiongozi wa tatu wa utawala alikuwepo, lakini kwa shambulio hili, Marekani na Israel hazikufikia lengo lao."

    Mbunge huyo hakutaja hospitali wala eneo lilipotokea shambulio hilo. Rais wa Marekani Donald Trump alisema katika mahojiano na Fox News kwamba kiongozi mpya wa Iran "aliumizwa" na siku ya kwanza ya mashambulizi ya Marekani na Israel.

    Kuhusu jeraha la Mojtaba Khamenei, Bw. Trump pia alisema: "Nadhani pengine ni sawa, nadhani amejeruhiwa, lakini nadhani pengine yuko hai kwa namna fulani."

    Jana, ujumbe wa kwanza kutoka kwa kiongozi mpya wa Jamhuri ya Kiislamu ulichapishwa.

    Haya yanajiri licha ya kwamba takriban wiki moja baada ya kuteuliwa kwake, hakuna taswira wala sauti ya Mojtaba Khamenei iliyotolewa, na wasiwasi kuhusu afya yake na hali yake ya kimwili umekuwa ukigonga vichwa vya habari kwenye vyombo vya habari.

    Hapo awali, Alireza Salarian, balozi wa Iran nchini Cyprus, aliliambia gazeti la The Guardian la Uingereza kwamba "Nilisikia kwamba miguu, mikono na mikono yake imejeruhiwa... nadhani yuko hospitalini kwa sababu amejeruhiwa" na "Sidhani angekuwa na raha kutoa hotuba [chini ya hali yoyote ile]."

  6. Habari za hivi punde, Milipuko yasikika huku Israel ikianzisha mashambulizi mapya dhidi ya Iran

    Israel imeanzisha mashambulizi mapya kuelekea mji mkuu wa Iran.

    Katika chapisho kwenye Telegram, Jeshi la Ulinzi la Israeli linasema "limeanza tu wimbi kubwa la mashambulizi yanayolenga miundombinu ya utawala wa kigaidi wa Iran kote Tehran".

    Milipuko mingi imeripotiwa ndani na karibu na jiji.

  7. Sala yasitishwa katika maeneo matakatifu ya Yerusalemu

    Wizara ya mambo ya nje ya Israel imesema mapema kwamba maombi katika maeneo matakatifu mjini Yerusalemu yamesitishwa kwa muda kutokana na vitisho vya makombora vya Iran.

    Taarifa ilisomeka: "Mmoja wao alishambulia mita mia chache kutoka Jiji la Kale, Ukuta wa Magharibi, Msikiti wa Al-Aqsa na Kanisa la Kaburi Takatifu."

    Matokeo yake, wizara ya mambo ya nje imesema maombi katika "maeneo yote matakatifu" yamesitishwa kwa muda ili kulinda maisha na usalama wa waumini.

    Baadhi ya sehemu muhimu zaidi za ibada zinazohusiana na imani za Kiyahudi, Kiislamu na Kikristo ziko katika jiji hilo.

    Soma zaidi:

  8. Trump asema vita vya Iran "vinabadilika kwa kasi mno"

    Rais Donald Trump alizungumzia kwa kifupi kuhusu Iran wakati wa hafla ya Ikulu ya White House kuadhimisha Mwezi wa Historia ya Wanawake.

    Trump alisema hali Mashariki ya Kati "inabadilika kwa kasi mno" na "inaendelea vizuri sana".

    Aliendelea kuita Iran "taifa la ugaidi na chuki", na kusema kwamba nchi hiyo "inalipa gharama kubwa hivi sasa".

    Trump amerudia kusema vita vya pamoja vya Marekani na Israel dhidi ya Iran ni operesheni ya muda mfupi lakini hajasema tarehe maalum ya lini operesheni hizo zinaweza kumalizika.

    Soma zaidi:

  9. Vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran: Tunachokijua kufikia sasa

    Kupitia ukurasa huu wa matangazo yetu mubashara: fahamu yaliyofanyika hadi kufikia sasa katika vita vya Marekani na Israeli dhidi ya Iran.

    • Jeshi la Marekani lilithibitisha kuwa ndege ya kujaza mafuta ilianguka magharibi mwa Iraq, baada ya "ajali" iliyohusisha ndege mbili. Kamandi Kuu ya Marekani ilisema "tukio hilo lilitokea katika anga rafiki wakati wa Operesheni Epic Fury", na kwamba sio matokeo ya mashambulizi ya adui wala operesheni ya kirafiki. Shughuli za uokoaji zilikuwa zikiendelea, maafisa walisema.
    • Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron alitangaza kwamba mwanajeshi mmoja wa Ufaransa ameuawa wakati wa shambulio la ndege isiyo na rubani katika eneo la Erbil nchini Iraq, huku wengine kadhaa wakijeruhiwa. Hiki ni kifo cha kwanza kutoka kwa wanajeshi wa nchi hiyo tangu vita vianze.
    • Israel imesema "imeanzisha wimbi kubwa la mashambulizi yanayolenga miundombinu" huko Tehran, mji mkuu wa Iran. Kabla ya hapo, pia ilianzisha mashambulizi zaidi dhidi ya Hezbollah kusini mwa Lebanon na Beirut.
    • Hapo awali, kiongozi mkuu mpya wa Iran Mojtaba Khamenei alisema Iran itaendelea kuzuia njia ya usafirishaji ya Mlango-Bahari wa Hormuz katika taarifa iliyosomwa kwenye TV ya serikali - ingawa bado hajaonekana ana kwa ana tangu shambulio lililomuua baba yake Ayatollah Ali Khamenei, na kuna wasiwasi juu ya afya yake.
    • Mtawala huyo mpya pia alipendekeza Iran itaendelea kulenga kambi za Marekani katika nchi jirani, wakati huo huo Waziri wa Ulinzi wa Uingereza John Healey anasema Uingereza ilidungua ndege mbili zisizo na rubani kutoka kambi moja nchini Iraq usiku kucha.

    Soma zaidi:

  10. Israel yashambulia 'vituo vya kutoa amri' vya Hezbollah

    Jeshi la Israel linasema limeanzisha "mawimbi kadhaa" ya mashambulizi huko Beirut na kusini mwa Lebanon likilenga "miundombinu ya Hezbollah".

    Taarifa mpya kupitia Telegram, Jeshi la Ulinzi la Israeli (IDF) linasema lilishambulia "vituo kadhaa vya kutoa amri" vilivyotumika kuendeleza mashambulizi dhidi ya Israeli.

  11. Marekani yalegeza vikwazo vya mafuta vya Urusi

    Marekani imeidhinisha nchi kununua mafuta ya Urusi yaliyowekewa vikwazo ambayo kwa sasa yanapakiwa kwenye meli baharini katika jaribio la kupunguza athari za kiuchumi za vita vya Marekani na Israeli dhidi ya Iran.

    Waziri wa Fedha wa Marekani Scott Bessent alisema ni hatua ya muda tu "kuendeleza utulivu katika masoko ya nishati duniani" wakati wa vita. Idhini hiyo itatekelezwa hadi tarehe 11 Aprili.

    "Hatua hii ya muda mfupi inatekelezwa tu kwa mafuta ambayo tayari yanasafirishwa na hayatakuwa na faida kubwa ya kifedha kwa serikali ya Urusi," Bessent alisema.

    Mashambulizi dhidi ya meli na miundombinu ya nishati katika eneo la Ghuba na kufungwa kwa njia muhimu ya usafirishaji mafuta ya Hormuz kumetikisa masoko ya nishati duniani.

    Bei ya mafuta ilipanda hadi dola 100 kwa pipa siku ya Alhamisi na masoko ya hisa yalishuka baada ya meli tatu zaidi za mizigo kushambuliwa katika eneo la Ghuba na kiongozi mpya mkuu wa Iran ameapa kuendelea kuzuia kutumika kwa njia hiyo.

    Karibu moja ya tano ya mafuta duniani kwa kawaida hupita kwenye njia hiyo nyembamba ya baharini.

    Awali, Marekani ilisema itaanza kusindikiza meli zake kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz "mara tu itakapowezekana kijeshi".

    Uhitaji wa kusindikizwa kijeshi "ulikuwa katika mipango yetu kila wakati", aliambia Sky News.

    Alipoulizwa kama hilo linaweza kuanza katika siku zijazo, Bessent alisema "haraka iwezekanavyo kuhakikisha usafirishaji salama".

    Soma zaidi:

  12. Mbunge wa Marekani azungumzia ajali ya ndege ya mafuta

    Wabunge wa Marekani waanza kuzungumzia ajali ya ndege ya Marekani ya kujaza mafuta iliyotokea magharibi mwa Iraq.

    Mbunge wa chama cha Democratic, Jim Himes, ameiambia BBC Newsnight kwamba bado ni "mapema sana" kubaini kilichosababisha tukio hilo, akiongeza kuwa anatumai wafanyakazi waliokuwa ndani ya ndege hiyo wako salama.

    "Hii ni sehemu ya gharama isiyoepukika ya vita. Hata jeshi bora haliendeshi shughuli zake bila kupata ajali na hilo ndilo lililoonekana kutokea sasa," amesema.

    "Tunaomba usalama wa wafanyakazi, lakini hii ndiyo gharama ya kulipia wakati taifa linapoingia vitani."

    Soma zaidi:

  13. Mwanajeshi mmoja wa Ufaransa auawa nchini Iraq, kadhaa wamejeruhiwa, asema Macron

    Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ametangaza kuwa mwanajeshi mmoja wa Ufaransa ameuawa wakati wa shambulio la ndege zisizo na rubani katika eneo la Erbil nchini Iraq, huku wengine kadhaa wakijeruhiwa.

    Alimtaja Afisa Mkuu wa Waranti Arnaud Frion kama kifo cha kwanza cha kijeshi cha Ufaransa tangu vita nchini Iran vianze mwishoni mwa mwezi uliopita.

    "Kwa familia yake, ndugu zake, nataka kuelezea upendo na mshikamano wote wa taifa," Macron aliandika kwenye mitandao ya kijamii.

    "Wanajeshi wetu kadhaa wamejeruhiwa. Ufaransa iko pamoja nao na wapendwa wao."

    Macron amelaani mashambulizi dhidi ya vikosi vya Ufaransa vinavyopigana dhidi ya Islamic State katika eneo hilo kama "yasiyokubalika".

    "Uwepo wao nchini Iraq ni sehemu ya mfumo madhubuti wa vita dhidi ya ugaidi. Vita nchini Iran haviwezi kuhalalisha mashambulizi kama hayo."

    Wanajeshi wa Ufaransa wajeruhiwa nchini Iraq

    Awali, ilitangazwa kuwa wanajeshi sita wa Ufaransa wamejeruhiwa katika shambulizi la ndege isiyo na rubani katika eneo la Erbil nchini Iraq, mashirika ya habari yakiwemo Reuters na AFP yanaripoti.

    Walipelekwa katika kituo cha matibabu kilicho karibu, Reuters imesema, ikinukuu jeshi la Ufaransa.

    Eribil, katika eneo la Kurdistan lenye kijitawala kwa kiasi fulani, liko takriban kilomita 115 magharibi mwa mpaka na Iran.

    Soma zaidi:

  14. Jukumu la ndege hizi vitani ni lipi?

    Hatujui ni nini kiliangusha ndege hii ya KC-135 inayojaza mafuta lakini uwezekano mmoja ni mgongano wa angani.

    Meli hizi za mafuta zina jukumu muhimu katika vita, zikihakikisha ndege za kivita na mabomu zina mafuta ipasavyo kwa ajili ya mapigano wakati ndege hizo zinapolazimika kupaa umbali mrefu ili kufika kwenye eneo linalolengwa.

    Ni operesheni kubwa ikiwa na ndege nyingi angani kwa wakati mmoja, kila moja ikihitaji mafuta.

    Kujaza mafuta kunahusisha kupaa karibu sana na meli ya mafuta, kabla ya kifaa cha kupima uzito kutoka kwa meli kupanuliwa na kushushwa.

    Rubani wa ndege anayepokea ndege hupaa hadi kwenye chombo na, kwa kutumia mfumo wa taa chini ya meli ya mafuta, hujiweka upya ili chombo kiweze "kuunganishwa" kwenye ndege.

    Mawasiliano yanafanyika kwa mtu mmoja, na mafuta huhamishwa katika mchakato ambao unaweza kuchukua dakika kadhaa.

    Wakati huu wote ndege iko umbali wa futi moja kutoka kwenye meli kubwa ya mafuta - katika shughuli ambazo mara nyingi hufanyika usiku.

    Mara tu zinapofikiana, mafuta huhamishwa katika mchakato ambao unaweza kuchukua dakika kadhaa.

    Wakati huu wote ndege iko umbali wa futi moja kutoka kwenye meli kubwa ya mafuta - katika shughuli ambazo mara nyingi hufanyika usiku.

    Inahitaji ujuzi mkubwa kwa rubani kudumisha mawasiliano na chombo, au katika baadhi ya matukio kifaa kinachotumika katika kujaza mafuta angani katika mazingira ambapo kunaweza kuwa na ndege nyingine nyingi karibu.

    Na wakati wa misheni za kujaza mafuta, taa za ndege zinaweza kuzimwa kabisa ili kuepuka kugunduliwa na adui.

    Jeshi Kuu la Marekani lilisema hili lilitokea Iraq lakini hatujui lilikuwa umbali gani kutoka nchi jirani ya Iran.

    Kwa kawaida KC-135 ina wafanyakazi watatu - rubani mmoja, rubani msaidizi na mtaalamu wa filamu

    Kamandi ya Uhamaji wa Anga, kulingana na USAF, ina karibu meli 400 za mafuta katika meli zake.

    Soma zaidi:

  15. Ndege ya Marekani ya kubeba mafuta ya ndege yaanguka nchini Iraq

    Tunachokijua kufikia sasa

    • Ndege ya kijeshi ya Marekani aina ya KC-135 iliyojaa mafuta imeanguka magharibi mwa Iraq
    • Ndege mbili zilihusika katika ajali hiyo, na ya pili ilitua salama
    • Tukio hilo "halikutokana na mapigano ya uadui au ya kirafiki", Kamandi Kuu ya Marekani inasema

    Juhudi za uokoaji zinaendelea

    Tusichokifahamu

    • Je, kulikuwa na watu wangapi ndani ya ndege hiyo na je, kuna majeruhi wowote?
    • Tukio hilo lilitokea lini - na shughuli za uokoaji zinafanyika wapi hasa?
    • Ni nini kilisababisha ndege kuanguka?

    Soma zaidi:

  16. Hujambo msomaji wetu. Karibu katika matangazo yetu mubashara ya tarehe 13/03/2026.