Uchaguzi Uganda 2021: Mambo muhimu unayopaswa kujua

Face masks showing presidential candidates in Uganda - Bobi Wine, left, and Yoweri Museveni, right

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Bobi Wine, kushoto, ni miongoni mwa wagombea wanao wanaompinga kiongozi - wa muda mrefu Yoweri Museveni, kulia
    • Author, Na Markus Mpangala
    • Nafasi, Mchambuzi, Tanzania

Kinyang'anyiro cha nafasi ya urais nchini Uganda ndicho chenye mvuto zaidi kuliko kingine kikiwa kimebeba hekaheka nyingi, ufuasi mkubwa, matumaini, na hamasa miongoni mwa wapigakura kote nchini humo.

Uganda ni taifa la pili la Afrika mashariki kufanya uchaguzi mkuu wake wa Januari 14 mwaka 2021 baada ya Tanzania iliyokamilisha uchaguzi wake Oktoba 28 mwaka huu, huku Kenya likiwa taifa lingine linatakalofuatia katika mlolongo huo ifikapo mwaka 2022.

Nchini Uganda jumla ya wagombea 11 wanachuana kwenye nafasi ya urais huku wakifanya mikutano ya kampeni katika Kaunti 353, sawa na wilaya 134, majiji 8 pamoja na mji mkuu wake wa Kampala kwa muda wa siku 60 pekee, lakini taswira ya uchaguzi huo imekuwa yenye kuashiria hali hasi na chanya.

Matukio ya kukamatwa wagombea wa upinzani, hamasa ya wapigakura, kuibuka kwa wagombea binafsi nafasi ya urais, kampeni zilizojaa vitisho na matumizi makubwa ya vyombo vya dola.

Kifo cha muungano wa upinzani pamoja na mgomo wa vyombo vya habari kurusha matangazo ya mikutano ya kampeni ya mgombea wa chama cha NRM Yoweri Museveni ni miongoni mwa mambo yanayoangaziwa katika kukua ama kudidimia kwa siasa za vyama vingi nchini Uganda.

Ajenda za wagombea wa urais nchini humo zimejikita katika rushwa, umasikini, miundombinu, kuboresha huduma za jamii, kuzalisha ajira kwa vijana,kusimamia uhuru wa kujieleza, kulinda usalama wa raia na mali zao.

Na haya ni mambo ya kuzingatia yenye athari katika uchaguzi huo:

Kiongozi anayetaka kusalia madarakani kwa miaka 40

Rais Museveni ni mmoja wa marais waliosalia madarakani kwa muda mrefu barani Afrika. Aliingia madarakani kupitia chama chake cha National Resistance Movement mwaka 1986 at baada ya kumalizika kwa vita vya miaka mitano na ameongoza Uganda kutoka wakati huo.

Wafuasi wake wanampongeza kwa kuleta amani nchini, na hususan sera yake ya afya. Alisaidia kudhibiti kusambaa kwa virusi vya HIV, na hivi karibuni kuweka amri ya kutotoka nje- iliyosababisha shule na biashara kufungwa, kupiga marufuku usafiri wa magari ya umma na utumizi wa lazima wa barakoa katik amaeneo ya umma mwezi Mei- anapongezwa kwa kukabiliana vikali na virusi vya corona.

Kulingana na Chuo Kikuu cha Johns Hopkins, Uganda imethibitisha visa vichache vya maamukizi chini ya 40,000 na vifo karibu 300 kutokana na ugonjwa huo.

President Yoweri Museveni of Uganda wearing a hat on a visit to France

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Akishinda uchaguzi huu rais Museveni ataelekea kuwa madarakani kwa miaka 40

Licha ya kwamba wakati mmoja alipongezwa na nchi za magharibui kuwa kuwa kizazi kipy acha viongozi wa Afrika, wakosoaji wake wanamlaumu kwa kugeuka kuwa kiongozi wa kiimla .

Bw. hana mrithi katika chama chake, na mwaka 2017 alitia saini sheria ya kutoa ukomo wa miaka 75 kwa mgombea urais hatua iliyomwezesha kugombea tena urais.

Utawala wake umepingwa kwa miaka kadhaa, hususana na kiongozi wa upinzani Kizza Besigye, ambaye alikamatwa mara kadha japo aliamua kutogombea tena urais mwaka 2021.

Japo Bw. Museveni bado anafurahia uungwaji mkono mkubwa, hasa katik amaeneo ya vijijini, anakabiliwa na upinzani kutokana ana ongezeko la ukosefu wa usawa na udhibiti wake mkali wa nchi.

1px transparent line
Maelezo ya video, Uchaguzi wa Uganda 2021:Mambo matano unapaswa kufahamu kuhusu uchaguzi huu
1px transparent line

Mwenendo wa vyombo vya dola na vikundi vya kisiasa

Matukio mbalimbali yanaonesha kuwa vyombo vya dola hasa Jeshi la Polisi nchini Uganda limekuwa likivuruga mikutano ya kampeni ya wagombea wa upinzani.

Matukio kama vile ya kuzuia kufanya mikutano ya hadhara na kumkamata mgombea wa Robert Kyagulanyi, ambaye aliwekwa rumande katika kituo cha polisi cha Nalufenya , vurugu zilizotokea kati ya Novemba 18 na 19 jijini Kampala ambapo polisi walivuruga mikutano ya kampeni ni mambo ya kufuatiliwa.

Mgombea mwingine Patrick Amuriat ameripotiwa kukutana na vizuizi vya vyombo vya dola wakati anaingia katika jiji la Arua kupitia mji wa Lemerijoa, ambako idadi kubwa ya askari walizingira njia za kuingia na kutoka maeneo hayo.

Wagombea wa urais nchini Uganda

  • Taaluma: Mhandisi, Mwanasiasa
  • Umri: 57
  • Mwaka 1994, Patrick Oboi Amuriat aliwania ubunge. Kati ya 2001 na 2016, alikuwa mbunge wa alikuwa mkosoaji mkubwa kuhusu kuondolewa kwa ukomo wa muhula wa urais.
  • Amuriat amesoma Chuo Kikuu cha Makerere ambapo alipata shahada yake ya kwanza na ya pili katika Uhandisi wa Ujenzi. Amefanya kazi na makampuni kadhaa ya uhandisi nyumbani na ugenini, mashirika ya maenedeleo ya kijamii pamoja na kuwa mtumishi wa umma kama mhandisi wa wilaya.
  • Alikuwa miongoni mwa jopo la bunge ambalo liliunda chama cha Forum for Democray (FDC). Ni rais wa tatu wa chama cha FDC.
  • Taaluma: Mwandishi wa michezo, mchungaji
  • Umri: 48
  • Joseph Kiza Kabuleta ni kiongozi wa vuguvugu la Kupigania taifa na raia (ROCK)
  • Ukosoaji wake wa utawala wa chama tawala cha NRM ulimfanya kufungwa jela 2019. Alisema kwamba mateso aliopitia katika mikono ya vyombo vya usalama akiwa jela yalimfanya kumpinga rais Museveni katika kinyang’anyiro cha urais mwaka huu.
  • Kabuleta alifanya kazi kwa muda mfupi kama msimamizi katika majengo mjini kampala na ana cheti cha diploma katika uhandisi alichokipata baadaye miaka ya tisini, kisha alibadilisha taaluma na kuanza kuwa mwandishi wa michezo na alifanya kazi kama mwandishi katika kampunu ya The Crusader, kabla ya kujiunga na gazeti la The New Vision ambapo alikuwa mwandishi maarufu wa safu.
  • Baada ya kuondoka katika chumba cha habari 2016, alikuwa mchungaji kiongozi katika kanisa la watchman Ministries.
  • Taaluma: Mwandishi wa habari, Mtaalamu wa masuala ya fedha
  • Umri: 40
  • Nancy Linda Kalembe ndiye mwanamke wa pekee anayewania urais katika uchaguzi wa mwaka 202.
  • Ahadi yake kuu ya kampeni ni kuimarisha maisha ya wanawake, uchukuzi, miundo mbinu na biashara za jamii.
  • Nancy kalembe ana Shahada ya Sayansi katika masuala ya Idadi ya Watu kutoka Chuo Kikuu cha Makerere.
  • Taaluma: Hana ajira
  • Umri: 24
  • John Katumba ni mgombea mwenye umri mdogo zaidi katika kinyang'anyiro cha urais nchini Uganda. Ameweza kugombea baada ya kuondolewa kwa umri wa urais kufuatia marekebisho ya kikatiba yaliofanywa mwaka 2017.
  • Alifuzu kutoka chuo kikuu cha Makerere kitivo cha biashara mwezi Januari 2020 akipata shahada ya uchukuzi na mipangilio.
  • Ijapokuwa bado hajatoa ilani ya uchaguzi, Katumba ameahidi kuangazia ukosefu wa ajira na kuwawezesha wanawake.
  • Taaluma: Wakili, Mwanasiasa
  • Umri: 53
  • Norbert Mao amehudumu kama mbunge aliyechaguliwa katika jimbo la Gulu kwa awamu mbili kati ya 1996 na 2006.
  • Baadaye, alikua mwenyekiti wa mojawapo ya mabaraza katika wilaya ya Gulu ambapo ni wakati alipohusishwa kuwa mpatanishi kati ya waasi wa kundi la wapiganaji wa LRA na serikali ya Uganda. Alipigania sheria ya kutoa msamaha kama sheria muhimu ambayo ingesaidia katika kusitisha vita hivyo kwa amani kaskazini mwa Uganda.
  • Mwaka 2010, kufuatia kuchaguliwa kwake kuwa rais wa chama cha Democratic Party, Mao alipigania urais wa Uganda katika uchaguzi wa 2011.
  • Mao ana shahada ya Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Makerere ambapo alihudumu kama rais wa chama cha wanafunzi.
  • Taaluma: Mhandisi, Mtaalamu wa kilimo
  • Umri: 33
  • Mwaka 2016, Willy Mayambala alipigania kiti cha ubunge kwa tiketi ya chama cha Forum for Democratic Change na kupoteza.
  • Ana Shahada ya Sayansi na Teknolojia kutoka Chuo Kikuu cha Kyambogo aliyoipata 2010. Baada ya kupata shahada, Mayambala alijiunga na mmoja ya wanafunzi wenzake kuanzisha kampuni ya Kamol Engineering Services Ltd na baadaye kuondoka miaka michache baadaye ambapo aliunda kamapuni yake binfasi JohnSemp Ltd.
  • Baba yake ambaye ni marehemu John Ssempala alikuwa alikuwa ni moja ya wapiganaji wa vita vya msituni vya 1980 hadi 1985 ambavyo vilimpatia madaraka rais Museveni.
  • Taaluma: Meja Jenerali Mstaafu , Mwanasiasa
  • Umri: 62
  • Meja Jenerali mstaafu Gregory Mugisha ndio rais na mgombea wa urais wa chama cha Alliance for National Transformation.
  • Muntu alikuwa mwanachama wa zamani wa kundi la waasi la NRA na alihusika pakubwa katika ufanisi wake kutokana na sifa yake ya kujitolea , utiifu na uwajibikaji.
  • Kufuatia ushindi wao 1996, Muntu alianza kwa kuongoza kitengo cha ujasusi wa kijeshi. Alikuwa kamanda wa kitengo maalumu cha jeshi 1989. Alishikilia wadhfa huo kwa miaka tisa hadi alipotofautiana na mkuu wa majeshi yote rais Yoweri Museveni 1989.
  • Ijapokuwa alimpatia wadhifa wa uwaziri Muntu alikataa wadhifa huo.
  • Alikuwa mbunge katika Bunge la Katiba la 1994-1995 ambalo lilijadili katiba ya Uganda. Mwaka 2021 Muntu alichaguliwa kuwa kamammoja ya wawakilishi wa Uganda katika bunge la Afrika Mashariki.
  • Taaluma: Rais wa Uganda
  • Umri: 76
  • Yoweri Kaguta Tubuhrburwa Museveni amekuwa rais wa Uganda tangu 1986 kufuatia uasi wa miaka mitano alioongoza dhidi ya uatawala wa awamu ya pili wa Apollo Milton Obote.
  • Aliahidi kuongoza kwa miaka minne pekee lakini sasa amefanya mabadiliko ya kikatiba mara mbili ili kumsaidia kusalia madarakani. Mara ya kwanza alihusika katika kubadilisha katiba 2005 ili kuondoa kikomo cha urais ili kumwezesha kuwania tena urais 2006 licha ya kuahidi hadharani 2001 kwamba hangewania urais tena.
  • Harakati zake za kuwania urais 2021 ziliwezeshwa kupitia marekebisho ya kikatiba mwaka 2017 kuondoa umri wa kikomo cha kuwania urais ambapo maafisa kutoka kikosi chake cha ulinzi walivamia bunge na kuwatoa nje viongozi waliokuwa wakipinga marekebisho hayo hadi pale yalipopitishwa.
  • Kabla ya sheria hiyo kupitishwa raia wa Uganda walio chini ya umri wa miaka 18 ama wale walio na zaidi ya umri wa miaka 75 walikuwa hawawezi kuwania urais.
  • Taaluma: Mchungaji
  • Umri: 38
  • Fred Mwesigye ameshikilia wadhifa wa mchungaji na mchungaji mshiriki katika kanisa la House of God Worship Ministry International, kanisa la God World Missions huko Kamwokya, Kampala na mchungaji kiongozi katika eneo la Kitoro mjini Entebe ambalo alilianzisha 2017.
  • Mwaka 2019, aliamua kujiunga na siasa ili kuitikia 'wito wa Mungu' kuiokoa Uganda kutoka kwa matatizo kwa kile ambacho anakiita enzi mpya ya mapenzi.
  • Ahadi yake kuu ni kuongeza mishahara ya walimu na madaktari pamoja na kuzuia kuparaganyika kwa taifa hilo 'kunakosababishwa' na chama tawala cha NRM, mathalan anataka kupunguza wilaya kutoka 135 hadi 62.
  • Taaluma: Mwanamuziki, mjasiriamali
  • Umri: 38
  • Robert Kyagulani Ssentamu, kwa jina maarufu Bobi Wine, ni mwanamuziki maarufu, msanii na mjasiriamali. Alianza kufanya muziki mapema miaka ya 2000 na kujitofautisha katika muziki wake aina ya dance hall kwa kuuchanganya na jumbe za masuala yanayokumba jamii.
  • Juni 2017, alipigania ubunge katika uchaguzi mdogo na kushinda kwa wingi wa kura dhidi ya chama tawala cha NRA na chama cha Forum for Democratic Change FDC.
  • Ijapokuwa kwa sasa anaongoza chama cha National Unity Platform (NUP), Kyagulani bado ni maarufu na na kundi la Nguvu ya Umma, vuguvugu aliloanzisha kupitia kampeni ya kutoondolewa kwa sheria ya ukomo wa umri wa kuwania urais.
  • Kyagulani katika siku za hivi karibuni amepata umaarufu mkubwa akionekana kuwa mpinzani mkuu wa rais Museveni katika uchaguzi wa urais wa 2021.
  • Taaluma: Wakili, Luteni Jenerali mstaafu
  • Umri: 61
  • Luteni Jenerali mstaafu Henry Tumukunde ni wakili ambaye aliipata Shahada ya Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Makerere 1981. Pia ana stashahada katika usimamizi wa mafuta na gesi kutoka Chuo cha Geneva.
  • Ni mbunge wa zamani wa chama tawala cha NRA tangu mwaka 1996, amehudumu kama katibu na mwambata wa kijeshi katika ubalozi wa Uganda nchini Uingereza , mkurugenzi wa mipango na usimamizi katika jeshi, mkuu wa idara ya ujasusi jeshini, kamanda wa kitengo cha nne cha jeshi kaskazini mwa Uganda na mkurugenzi mkuu wa shirika la usalama wa ndani.
  • Mwaka 2015, Tumukunde alistafaishwa kutoka jeshini akiwa katika wadhifa wa Luteni Jenerali na akarudishwa kuhudumu kama waziri wa masuala ya usalama kati ya 2016 na 2018.

Aidha, jambo lingine ni kuibuka kwa vikosi vinavyofanya fujo dhidi ya vyama vya upinzani au chama tawala.

Vikundi hivyo vimetajwa na duru za usalama kuwa vinafanya kazi ya kuvuruga mikutano ya kampeni ya wapinzani wao.

Kama ilivyokuwa kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba 28 mwaka huu kwa jirani zao Tanzania, nako nchini Uganda mabango yenye matangazo ya wagombea wa nafasi mbalimbali kutoka vyama vya upinzani yamekuwa yakiondolewa na askari hali ambayo imelalamikiwa kuwa ni ukiukwaji wa haki za binadamu pamoja na kutokuwa na mizani sawa ya kufanya shughuli za kampeni za uchaguzi mkuu.

Mabango yaliyolengwa zaidi ni yale ya mgombea wa NUP, Robert Kyagulani.

Mgomo wa vyombo vya habari

Mpinzani mkuu wa rais Yoweri Musevei
Maelezo ya picha, Bobi Wine

Ingawaje haikutarajiwa lakini imeripotiwa kuwa vyombo vya habari nchini Uganda vimegoma kutangaza habari za kampeni za mgombea wa chama cha NRM.

Hili ni jambo ambalo limeleta gumzo kubwa nchini Uganda, ambapo msimamo wa vyombo hivyo ni kushinikiza uwanja sawa katika kampeni za uchaguzi nchini humo.

Mijadala kupitia mitandao ya kijamii, tovuti, vyombo vya habari vya ndani na nje vimeripotiwa kugoma kurusha matangazo ya moja kwa moja (Live) ya redio na runinga mikutano ya kampeni ya mgombea wa NRM, Yoweri Museveni.

Hatua ya vyombo vya habari kugoma kurusha matangazo hayo ni kutokana na kukamatwa kwa mgombea wa upinzani Robert Kyagulanyi na baadaye kuachiliwa huku baadhi ya wafuasi na wananchi wengine wakijeruhiwa wakati wa zoezi hilo.

Baadhi ya raia wa Tanzania wanaoishi na kusoma vyuo mbalimbali nchini Uganda wamemwambia mwandishi wa makala haya, "kulikuwa na jambo la kushangaza, televisheni zinarusha vipindi vya muziki wakati Museveni alikuwa akihutubia watu kule Moroto.

Unajua hapa Uganda wagombea wanafanya kampeni wilaya 134 sawa na majimbo 353, kote huko ni ndani ya siku 60 za kampeni.

Sasa fujo hizi wanazofanyiwa wapigakura na wanasiasa kunaswa na vyombo vya dola ni mtihani kwa wanahabari na mwelekeo wa taifa lenyewe. Wamezima kabisa mikutano ya Museveni,"

Uganda bila muungano wa upinzani wa mwaka 2016

Rais Yoweri Musevei

Nguvu kubwa ya ushindi wa Museveni imetajwa kutoka ufalme wa Buganda katikati ya taifa hilo.

Kulinda na kuheshimu utawala wa kifalme wa Buganda ni miongoni mwa eneo muhimu linalotengeneza nguvu ya Museveni licha ya madai kuwepo mzozo baridi baina ya pande hizo mbili.

Upande wa kambi ya upinzani nguvu zao zilitegemea umoja wao. Kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2016, muungano wa vyama vya upinzani ulimuunga mkono mgombea Amama Mbabazi ambaye alionekana kuwa na nguvu zaidi wakati wa uchaguzi huo.

Kwenye uchaguzi huo Mbabazi aligombea baada ya kuachana na chama cha NRM, lakini uchaguzi wa mwaka 2021 mwanasiasa mwenye nguvu amejijenga binafsi kupitia muziki.

Lakini kuelekea uchaguzi wa mwaka 2021, mwanasiasa mwenye nguvu ni Robert Kyagulanyi maarufu kwa jina la Bob Wine.

Mwanasiasa huyu anazidi kumpa changamoto Museveni kuliko wakati wowote wa uchaguzi wa Uganda.

Uhuru wa Tume ya Uchaguzi na Mahakama

Kizza Besigye

Kama zilivyo nchi zingine linapofika suala la uchaguzi mkuu, Uganda nayo imekuwa ikishuhudia malumbano makali juu ya uaminifu wa Tume yao (EC).

Tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa kumekuwa na uhaba wa uhuru katika tume yeneywe na miongoni mwa viongozi wake. Taswira waliyonayo baadhi ya wapigakura na wanasiasa kwa ujumla ni mashaka juu ya mwenendo wa tume kusimamia uchaguzi huru na haki.

Wakati wa uchaguzi wa mwaka 2016 asilimia 89 za kura za maoni zilitaka mabadiliko katika Tume na michakato yote ya uchaguzi mkuu.

Aidha, tume hiyo imekuwa ikikabiliwa na ukata kutokana na bajeti hafifu,udanganyifu wa majina ya wapigakura na vituo vya kupigia kura na uhesabuji wake.

Uchaguzi huo unahusisha wagombea 11 walioanza kampeni tangu Novemba 19 mwaka huu; John Katumba, Robert Kyagulanyi Ssentamu, Mugisha Muntu,Henry Tumukunde, Norbet Mao, Joseph Kabuleta Kiiza, Patrick Amuriat Oboi, Fred Mwesigye, Nancy Linda Kalembe, Willy Mayambala na Yoweri Museveni.

Mwaka 2001, Kizza Besigye alishindwa kufurukuta katika Mahakama ya Rufani baada ya jaribio la kupinga ushindi wa Yoweri Museveni.

Mwaka 2006, 2011 kesi nyingine ya kupinga ushindi wa Museveni ilifunguliwa, licha ya Mahakama kukiri dosari kwenye baadhi ya taratibu za uchaguzi, lakini haikufuta matokeo ya uchaguzi.

Msuguano wa mwaka 2016 ndani ya mhimili huo wa dola unatajwa kuwa huenda ukawa chachu ya kufanya uamuzi wa kupingwa matokeo ya uchaguzi mwaka huu ikiwa utatokea.

Hofu ya ugonjwa wa corona

Kampeni za uchaguzi mkuu zinafanyika huku kukiwa na tishio la ongezeko la maambukizi ya ugonjwa wa Corona, ambapo Mkurugenzi wa Shirika la Afya barani Afrika, Dk. Matshidiso Moeti akibainisha kuwa ugonjwa huo unatarajiwa kusambaa zaidi kutoka na mikusanyiko ya kampeni na kuelekea sikukuu za mwisho wa mwaka kama vile krismasi.

Virusi vya corona

Chanzo cha picha, Getty Images

Mtandao wa gazeti la kila siku la Daily Monitor umeripoti kuwa baada ya miezi 8 kupitia serikali ya Uganda imeruhusu safari za Mabasi kutoka nchi hiyo kwenda nchini Tanzania.

Vilevile limeripoti taarifa ya kijana Baroda Kayanga Watongola mwenye umri wa miaka 27 kuwania ubunge jimbo la Kamuli huku kukiwa na kumbukumbu ya mzazi wake Hajat Rehema Watongola kufariki kwa ugonjwa wa corona mnamo Novemba 14 mwaka huu.

Baroda ameomba kugombea nafasi hiyo kuziba pengo la mzazi wake ambaye alikuwa na ndoto za kuwania jimbo hilo.

Tafsiri yake ni kwamba ipo hofu ya ugonjwa wa corona ambayo imesababisha Tume ya uchaguzi nchini humo kutoa angalizo kwa viongozi wote wa timu za kampeni kuzingatia masuala muhimu ya kuepukana na ugonjwa huo.