Kenya: Rais Kenyatta amemwandikia Rais Magufuli alivyokerwa na kauli ya Jaguar

Uhuru Kenyatta

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta
Muda wa kusoma: Dakika 2

Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta amemwandikia waraka maalum Rais wa Tanzania, John Magufuli kuelezea jinsi Serikali yake ilivyoghadhabishwa na matamshi yaliyotolewa na Mbunge wa Starehe, Charles Kanyi maarufu Jaguar.

Ujumbe huo wa maandishi umewasilishwa na Balozi wa Kenya nchini Tanzania, Dany Kazungu na kupokelewa Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa kwa niaba ya Rais Magufuli.

Kwa mujibu wa Gazeti la Mwananchi, Bw. Majaaliwa alisema: "Uhusiano kati ya Kenya na Tanzania ni wa karibu kwani kuna baadhi ya makabila yanapatikana katika nchi hizi mbili hivyo ushirikiano katika masuala mbalimbali yakiwemo ya kibiashara na ya kijamii hayawezi kukwepeka."

Ruka X ujumbe
Ruhusu maudhui? (Mitandao ya kijamii)

Mkala hii imebeba madhui yaliyotoka kwenye mitandao ya kijamii. Tunaomba ruhusa yako kabla kitu chochote hakija pakiwa, sababu wanaweza wakawa wanatumia Cookies na tekinolojia nyingine. Unaweza ukasoma sera sera ya kutumia cookies katika mitandao ya kijamii kabla ya kukubali. Kutazama maudhui haya chagua accept and continue

Onyo: Imetoka kwingine na inaweza kuwa na matangazo

Mwisho wa X ujumbe

Aliongezea kuwa siku zote Watanzania na Wakenya wamekuwa huru kuishi na kufanya kazi au biashara katika nchi za Afrika ya Mashariki na pale yalipotokea matatizo au kutokukubaliana Serikali husika zilikaa mezani na kumaliza tofauti hizo.

''Watanzania wamefurahishwa na hatua mbalimbali zilizochukulia na Serikali ya Kenya dhidi ya mbunge huyo zinazodhihirisha matamshi hayo hayakuwa msimamo wa Serikali ya Kenya wala wananchi wake bali ulikuwa ni msimamo binafsi wa mbunge huyo.'' alisema

Wiki iliyopita, Jaguar alitoa matamshi yenye utata akiwataka raia wa kigeni kutoka mataifa mbalimbali wanaofanya shughuli za kibiashara nchini Kenya wakiwemo Watanzania waondoke ndani ya muda wa saa 24 kauli iliyozua mjadala mkubwa.

Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwasihi Watanzania kuendelea kuishi kwa amani na upendo na ndugu zao wa Kenya na wageni wote kutoka nchi za EAC na duniani kwa ujumla ambao wapo nchini wakifanya shughuli mbalimbali kwa mujibu wa sheria za nchi.

"Mambo yetu yote katika nchi za Afrika Mashariki hasa ya biashara na ya kiuchumi kwa ujumla yataenda vizuri endapo tutalinda na kudumisha amani, bila amani tutaogopana na tutashindwa kabisa kushirikiana," alisema Bw. Majaliwa.

Jaguar, mbunge wa Kenya aliyetoa kauli za chuki alikamatwa na kufukishwa mahakamani

Chanzo cha picha, CHARLES KANYI/FACEBOOK

Maelezo ya picha, Jaguar, mbunge wa Kenya aliyetoa kauli za chuki alikamatwa na kufukishwa mahakamani

Waziri Mkuu ameahidi kuwa Serikali ya Tanzania haitafumbia macho kauli iliyo na viashiria vya uchochezi dhidi ya nchi jirani ili kuunga mkono juhudi mbalimbali za ushirikiano wa kisiasa na kiuchumi zinazofanywa na viongozi wakuu wa Mataifa ya Afrika.

Kwa upande wake, Balozi Kazungu amemshukuru Waziri Mkuu Majaliwa kwa kuwatuliza Watanzania kupitia kauli yake aliyotowa Bungeni wiki iliyopita na kuwaomba wasitilie maanani matamshi ya Jaguar kwani sio msimamo Serikali ya Kenya au Wakenya wenyewe.

Balozi Dan Kazungu, aliongeza kuwa siku zote msimamo wa Rais Kenyatta umekuwa ni kuwapokea na kuwakubali ndugu zao wote wanaotoka nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki walioamua kuishi au kufanya biashara nchini Kenya.

Mbunge huyo ailikamatwa na kufikishwa mahakamani na kesi dhidi yake inaendelea.