Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Ethiopia Airline yasitisha safari za Boeing 737 Max 8, Mkurugenzi aeleza
Mkurugenzi wa shirika la Ndege la Ethiopia ametaka kusitishwa kwa ndege aina ya Boeing 737 Max 8 mpaka itakapothibitishwa kuwa ziko salama kuruka
Nchi nyingi tayari zimesitisha kurusha ndege hizo baada ya ajali ya siku ya Jumapili iliyogharimu maisha ya watu 157.
Tewolde Gebremariam ameiambia BBC kuwa ingawa sababu ya ajali hiyo haijajulikana bado, kuna ufanano na ile ajali ya ndege ya Lion Air mwezi Oktoba mwaka jana.
Lakini maafisa nchini Marekani wanasema ndege hiyo ni salama.
Mamlaka ya anga nchini Marekani imesema ''hakuna tatizo lolote katika ufanyaji wake kazi'' na kuwa hakuna sababu ya msingi ya kusitisha safari zake.
'Kusitisha safari za ndege ni hatua nzuri'
Bwana Tewolde amesema Boeing na mamlaka ya anga nchini Marekani FAA wanaweza kuwa na sababu ya kusema kuwa 737 Max 8 ni salama.Lakini ''tahadhari kubwa'' ilihitajika na wale waliositisha kuruka kwa ndege hiyo bila shaka wana sababu ya kufanya hivyo.''
Ndege zote zilikua mpya na ndege zote zilianguka dakika chache baada ya kuruka alieleza
Mamlaka za anga ikiwemo za Umoja wa Ulaya,Hong Kong,Singapore,China na Australia, zimesitisha ndege za 737 Max kuruka kwenye anga zake
Bwana Tewolde amesema mamlaka hizo zina sababu nzuri ya kufanya hivyo kwa kuwa usalama ni jambo muhimu na ''kusitisha safari ni jambo la jema''.
Wakati hayo yakijiri, wanasiasa kadhaa wa Marekani wametoa wito kwa FAA kusitisha safari za ndege aina hiyo kwa muda mpaka pale itakapothibitishwa .Lakini FAA imesema mamlaka zingine hazijatoa data zinatakazofanya Marekani ichukue hatua hiyo
Boeing imesema kuwa ina uhakika kuwa ndege ilikua salama kuruka.
Shirikisho la wafanyakazi wa ndege CWA limetaka kusitishwa kwa ndege 737 MAX kwa '' tahadhari'' Umoja wa marubani umesema wanachama ambao wanawasiwasi kuhusu usalama hawatalazimishwa kurusha ndege hizo.
Southwest Airlines na American Airlines wanaendelea kutumia ndege hizo.