Mgahawa wa Java House wabomolewa Kileleshwa, Nairobi

Muda wa kusoma: Dakika 1

Jengo lililo na mgahawa maarufu wa Java House katika mtaa wa Kileleshwa, Nairobi umebomolewa katika shughuli ya bomoa bomoa ambayo imeanza mapema leo asubuhi.

Shughuli hiyo inadaiwa kuendeshwa na Mamlaka ya Taifa ya Mazingira (Nema) na kulenga maeneo yaliyotengewa chemchemi za maji na kingo za mito.

Kituo cha mafuta cha Shell ambacho kinapatikana hapo karibu pia kimefungwa.

Mgahawa huo umeandika kwenye Twitter kwamba tawi lake la Kileleshwa limefungwa "kutokana na sababu zisizoepukika."

Shughuli ya bomoa bomoa imekuwa ikiathiri watu wengi na sana wafanyabiashara wadogo ambao wamejenga vibanda vyao kando mwa barabara.

Maelfu ya wakazi katika mtaa wa Kibera, Nairobi pia waliathiriwa na ubomoaji ambao ulilenga kuondoa nyumba zilizojengwa katika eneo lililotengewa barabara ya mchepuko ya kuunganisha barabara za Langata na Ngong.