Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Takribani watu 21 wapoteza maisha baada ya treni mbili za mwendo kasi kugongana Hispania

Takribani watu 21 wamepoteza maisha baada ya ajali iliyohusisha treni za mwendo kasi kusini mwa Hispania, huku mamlaka zikionya kwamba idadi ya vifo inaweza kuongezeka.

Muhtasari

Moja kwa moja

Lizzy Masinga na Ambia Hirsi

  1. Chile yatangaza “hali ya janga” baada ya moto wa misituni kuua takribani watu 18

    Rais wa Chile, Gabriel Boric, ametangaza hali ya janga katika mikoa miwili ambako moto mkubwa wa misituni umesababisha vifo vya takribani watu 18.

    Zaidi ya watu 50,000 wamehamishwa kutoka kwenye makazi yao katika mikoa ya Ñuble na Biobío, iliyopo takribani kilomita 500 kusini mwa mji mkuu, Santiago.

    Rais Boric alisema idadi ya vifo inatarajiwa kuongezeka kadiri shughuli za uokoaji na tathmini zinavyoendelea.

    Moto hatari zaidi umeteketeza misitu mikavu iliyo karibu na jiji la pwani la Concepción, na kwa mujibu wa maafisa wa kushughulikia maafa, takribani nyumba 250 zimeharibiwa.

    Vyombo vya habari vya ndani vimeonesha picha za magari yaliyoungua na kubaki mabaki barabarani.

    Shirika la misitu la Chile, Conaf, lilisema kuwa zima moto walikuwa wakipambana na moto kote nchini siku ya Jumapili. Moto hatari zaidi, liliongeza, upo katika mikoa ya Ñuble na Biobío.

    Moto umeteketeza ekari 21,000 katika mikoa hiyo miwili hadi sasa.

    “Kwa kuzingatia uzito wa moto unaoendelea wa misituni, nimeamua kutangaza hali ya janga katika mikoa hiyo miwili,” Rais Gabriel Boric alisema katika ujumbe aliouandika kwenye mtandao wa X.

    Chini ya hali ya janga, majeshi ya Chile yanaweza kupelekwa kusaidia katika kudhibiti hali hiyo.

    Sehemu kubwa ya uhamishaji wa wakazi ilifanyika katika miji ya Penco na Lirquén, kaskazini mwa Concepción, miji ambayo kwa pamoja ina wakazi wapatao 60,000.

    Upepo mkali umechochea kuenea kwa moto huo, hali iliyochangiwa na joto kali la majira ya kiangazi, na hivyo kuhatarisha jamii na kuvuruga juhudi za kuzima moto.

    Sehemu kubwa ya Chile iko chini ya tahadhari ya joto kali, huku halijoto zikitarajiwa kufikia nyuzi joto 38 za Selsiasi kati ya Santiago na Biobío katika siku chache zijazo.

    Chile imekumbwa na msururu wa matukio ya moto mkubwa na mbaya katika miaka ya hivi karibuni, hali iliyochochewa zaidi na ukame wa muda mrefu.

    Miaka miwili iliyopita, moto wa misituni uliua takribani watu 120 katika mkoa wa Valparaíso, karibu na mji wa Santiago.

    Unaweza kusoma;

  2. Israel yapinga uteuzi wa Trump wa watendaji wa 'Bodi ya Amani' ya Gaza

    Kiongozi wa Israel, Benjamin Netanyahu, ameitisha mkutano na washauri wake wakuu kujadili kile Rais wa Marekani Donald Trump anachokiita “Bodi ya Amani” kwa Gaza, baada ya Israel kusema haikushirikishwa katika mazungumzo kuhusu muundo wa moja ya vyombo vya chini vya bodi hiyo.

    Marekani ilitangaza Jumamosi majina ya wajumbe wa kwanza wa Bodi ya Utendaji ya Gaza, wakiwemo Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki, afisa mmoja wa Qatar, aliyekuwa Waziri Mkuu wa Uingereza Tony Blair, pamoja na mkwe wa Trump, Jared Kushner.

    Ofisi ya Netanyahu baadaye ilisema uteuzi huo “haukuratibiwa na Israel na unakwenda kinyume na sera yake.”

    Bodi ya Amani ni sehemu ya mpango wa vipengele 20 wa Trump unaolenga kumaliza vita kati ya Israel na Hamas, na inatarajiwa kusimamia kwa muda uendeshaji wa Ukanda wa Gaza.

    Muundo kamili wa bodi hiyo, ambayo pia itasimamia ujenzi upya wa Gaza, bado haujawekwa wazi, na wajumbe wengine bado wanaendelea kualikwa.

    Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ikulu ya Marekani (White House), “Bodi ya Utendaji ya Gaza” itakuwa na jukumu la kusimamia shughuli zote za utekelezaji wa kazi zinazofanyika nchini humo kwa niaba ya chombo kingine cha kiutawala kinachoitwa Kamati ya Kitaifa ya Usimamizi wa Gaza (NCAG).

    Chombo cha pili, kinachoitwa “Bodi ya Utendaji ya Waanzilishi”, ambacho pia kinawajumuisha Jared Kushner na Tony Blair, kitakuwa na jukumu la ngazi ya juu katika masuala ya uwekezaji na diplomasia.

    Unaweza kusoma;

  3. Syria yakubali kusitisha mapigano na vikosi vinavyoongozwa na Wakurdi baada ya wiki mbili za mapigano

    Serikali ya Syria imetangaza kusitishwa mara moja kwa mapigano kote nchini kati yake na Vikosi vinavyoongozwa na Wakurdi, (SDF) hatua inayoiwezesha serikali kudhibiti karibu nchi nzima, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya serikali ya Syria.

    Makubaliano hayo ya kusitisha mapigano yanamaliza takribani wiki mbili za mapigano makali na ni sehemu ya makubaliano mapana ya vipengele 14, ambayo yataifanya SDF kuunganishwa rasmi katika jeshi la Syria na taasisi za serikali.

    Akizungumza mjini Damascus, Rais Ahmed al-Sharaa alisema makubaliano hayo yatawezesha taasisi za serikali ya Syria kurejesha mamlaka katika magavana (mikoa) mitatu ya mashariki na kaskazini, al-Hasakah, Deir Ezzor na Raqqa.

    Hatua hiyo imefuatia mkutano kati ya Rais al-Sharaa na mjumbe maalum wa Marekani kwa Syria, Tom Barrack, uliofanyika Damascus. Barrack alisifu makubaliano hayo akisema ni hatua muhimu kuelekea “Syria iliyoungana.”

    Kamanda wa SDF, Mazloum Abdi, alitarajiwa kuhudhuria mkutano huo lakini hakuwahi kusafiri kutokana na hali mbaya ya hewa, na ziara yake ikaahirishwa hadi Jumatatu, alisema Rais al-Sharaa.

    Katika hotuba ya televisheni, Abdi alithibitisha kuwapo kwa mkutano huo na kusema kwamba atatoa maelezo zaidi kuhusu makubaliano hayo kwa Wakurdi wa Syria baada ya kurejea kutoka mji mkuu.

    Akizungumza na kituo cha televisheni cha Kikurdi Ronahi, Abdi alisema makubaliano aliyofikia na Damascus yalijumuisha kusitishwa kwa mapigano ili kuepusha vita vikubwa zaidi, akisisitiza kuwa mapigano hayo “yalilazimishwa” dhidi ya SDF.

    Vikosi vinavyoongozwa na Wakurdi vilianzisha utawala wao wa wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe vya Syria, takribani miaka kumi iliyopita, kwa msaada mkubwa wa Marekani, ambayo iliwapa silaha na mafunzo SDF kama mshirika wake mkuu wa ndani katika mapambano dhidi ya kundi la wanamgambo wa Kiislamu (ISIS).

    Unaweza kusoma;

  4. Takribani watu 21 wapoteza maisha baada ya treni mbili za mwendokasi kugongana Hispania

    Takribani watu 21 wamepoteza maisha baada ya ajali iliyohusisha treni za mwendokasi kusini mwa Hispania, huku mamlaka zikionya kwamba idadi ya vifo inaweza kuongezeka.

    Zaidi ya watu 30 wanatibiwa majeraha makubwa hospitalini, waziri wa uchukuzi wa nchi hiyo, Oscar Puente alisema.

    Tukio hilo lilitokea karibu na mji wa Adamuz, karibu na jiji la Cordoba, wakati treni ya mwendo kasi iliyokuwa ikisafiri kutoka Malaga hadi Madrid ilipoacha reli na kuvuka hadi kwenye njia nyingine, mwendeshaji wa mtandao wa reli Adif alisema.

    Treni iliyoacha reli kisha ikagongana na treni nyingine ikisafiri kutoka Madrid kuelekea Huelva.

    Huduma za dharura za Andalusia zilisema takribani watu 73 walijeruhiwa katika ajali hiyo.

    Tukio hilo lilionekana kuwa "la ajabu sana", Puente aliongeza, kwa sababu treni iliacha njia moja kwa moja, ambayo ilikuwa imekarabatiwa Mei mwaka jana.

    Chanzo rasmi bado hakijajulikana. Uchunguzi kubaini kilichotokea utachukua takribani mwezi mmoja.

    Waziri Mkuu, Pedro Sánchez, alisema nchi hiyo itapitia "usiku wa maumivu makali". Iryo, kampuni binafsi ya reli iliyoendesha safari hiyo kutoka Malaga, ilisema takriban abiria 300 walikuwa ndani ya treni iliyoacha njia kwa mara ya kwanza, huku treni nyingine, inayoendeshwa na shirika la Renfe ikiwa na abiria wapatao 100.

  5. Habari za asubuhi, karibu katika taarifa zetu za leo