Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Noura Hussein: Mahakama ya rufaa yafutilia mbali hukumu ya kifo
Mahakama ya rufaa nchini Sudan imefutilia mbali hukumu ya kifo dhidi ya mwanamke ambaye alimuua mumewe baada ya madai kwamba alimbaka , wakili wake amesema.
Noura Hussein mwenye umri wa miaka 19 badala yake alihukumiwa kifungo cha miaka mitano jela , wakili wake Abdelaha Mohamad alisema.
Mamake, Zainab Ahmed, aliambia BBC kwamba anafurahia kwamba maisha ya mwanawe yaliokolewa.
Watu maarufu wa kimataifa waliunga mkono kampeni ya mtandaoni, #JusticeforNoura,{ haki kwa Noura} iliotaka aachiliwe huru.
Mwezi uliopita, mahakama ya Kiislamu ilikuwa imemuhukumu kifo kwa kumnyonga , baada ya kukiri kumuua mumewe Abdulrahman Mohamed Hammad.
Bi Hussein alisema kuwa mumewe aliwatumia binamu zake ambao anadai walimshikilia kwa nguvu huku akimbaka.
Alipojaribu kurejelea kitendo hicho siku iliofuata alimdunga kisu hadi kufa.
Bi Hussein alilazimishwa kufunga ndoa akiwa na umri wa miaka 16. Mumewe ambaye alikuwa binamu yake alikuwa mkubwa wake kwa miaka 16 .
Kulingana na ripoti ya 2017 ya Umoja wa Mataifa kuhusu shirika la watoto Unicef, thuluthi moja ya watoto wa Sudan huolewa kabla ya kufikisha miaka 18.
Katika taarifa yake, shirika la haki za kibinaadamu la Amnesty International, lilitaja uamuzi huo kuwa habari nzuri, lakini likasema kuwa kifungo cha miaka mitano jela ni adhabu isiostahili.
Limeitaka nchi hiyo kufanyia marekebisho sheria zake kuhusu ndoa, ubakaji katika ndoa ili waathiriwa wasiadhibiwe.
Akizungumza na BBC , mamake bi Hussein, alisema kuwa mwanawe alikuwa amejichukia baada ya mumewe kumbaka .
''Alikuwa ameamua kujidunga kisu iwapo angembaka tena'', alisema Zainab Ahmed.
Baada ya kifo cha mumewe , Bi Hussein alitoroka hadi nyumbani kwao kusema kile kilichotokea.
Wakihofia kulipizwa kisasi, babake alichukua familia yote hadi katika kituo cha polisi ili kuwalinda-ambapo alikamatwa.
Hukumu yake jela ilizua hisia kali kimataifa huku watu maarufu kama vile Naomi Campbell na Emma Watson wakichapisha ujumbe wa Twitter kumuunga mkono Bi Hussein.