Drake ndiye mwanamuziki aliyeuza zaidi duniani 2016

Mwanamuziki Drake ndiye aliyeuza nyimbo na video nyingi zaidi miongoni mwa wasanii duniani mwaka 2016.

Kwa mujibu wa Shirikisho la Kimataifa la Nyimbo, nyimbo zake iwe ni katika kuchezwa moja kwa moja mtandaoni, kuuzwa kama kanda, kuuzwa mtandaoni au kupakuliwa mtandaoni, ndizo zilizoongoza.

David Bowie alikuwa wa pili naye Coldplay wa tatu.

Adele, mwanamuziki aliyeuza zaidi 2015, alikuwa wa nne katika orodha ya mwaka 2016 baada ya albamu yake ya 25 kusalia kuwa maarufu mwaka huo wote.

Orodha ya shirikisho hilo, ambayo huangazia nyimbo zote za mwanamuziki badala ya wimbo mmoja pekee au albamu moja pekee, pia inajumuisha Justin Bieber, katika nambari tano, ambaye yupo mbele ya Twenty One Pilots na Beyonce.

Rihanna, Prince na The Weeknd wanakamilisha orodha ya 10 bora.

Ufanisi wa Drake unatokana na mauzo ya albamu yake ya nne, Views, ambayo aliichomoa mwaka jana.

Ilikuwa ndiyo albamu ya kwanza nyimbo zake kuchezwa mara bilioni moja katika Apple Music.

Wimbo wa One Dance, ulikuwa wimbo wa kwanza kabisa kuchezwa mara bilioni moja katika Spotify.

David Bowie alikuwa wa pili, sana kutokana na mafanikio ya albamu yake ya 25 kwa jina Blackstar.

Albamu hiyo ilichomolewa siku mbili kabla ya kifo chake Januari 2016.

Washindi wa awali ni pamoja na One Direction na Taylor Swift.