Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Wasichana 21 wa Chibok 'waachiliwa huru' Nigeria
Afisa wa cheo cha juu serikalini ameiambia BBC kwamba wasichana 21 waliokuwa miongoni mwa wasichana wa shule waliotekwa na wapiganaji wa Boko Haram eneo la Chibok sasa wako huru.
Taarifa zinasema wasichana hao kwa sasa wamo mikononi mwa maafisa wa usalama katika mji wa Maiduguri, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.
Msemaji wa Rais Muhammadu Buhari amethibitisha kuachiliwa huru kwa wasichana hao.
Bw Mallam Garba Shehu ameandika kwenye Twitter: "Imethibitishwa kwamba wasichana 21 wa Chibok wameachiliwa na kwa sasa wamo mikononi mwa Idara ya Masuala ya Serikali."
Haijabainika iwapo wasichana hao walikomombolewa na wanajeshi au waliachiliwa huru na wanamgambo hao.
Jeshi la Nigeria kwa muda limekuwa likiendesha operesheni kubwa ya kijeshi katika msitu wa Sambisa, ngome ya Boko Haram.
Wapiganaji wa kundi hilo waliteka wasichana takriban 250 waliokuwa wakilala kwenye mabweni shuleni Aprili mwaka 2014.
Kisa hicho kilishutumiwa vikali na jamii ya kimataifa.
Tangu wakati huo, ni msichana mmoja pekee aliyekuwa ameokolewa.
Kundi la kujihami la wanakijiji lilimpata Amina Ali Nkeki mwezi Mei akiwa na mumewe, ambaye anatuhumiwa kuwa mwanachama wa Boko Haram, pamoja na mtoto wake.