Kufumbwa macho na kupigwa vibaya: Wanaume sita Wapalestina wanasimulia jinsi walivyowekwa kizuizini kwa mwezi mmoja Israeli

Five of the six men who say they were badly beaten sit and stand in a Rafah hospital
Maelezo ya picha, Wanaume watano kati ya sita ambao wanasema walipigwa vibaya wanaonekana kuchoka baada ya karibu mwezi mmoja katika kizuizi cha Israeli
    • Author, Adnan El-Bursh
    • Nafasi, BBC Arabic
    • Akiripoti kutoka, Rafah, Gaza

Wanaume sita wa Kipalestina kutoka Gaza wanasema walipigwa vibaya na jeshi la Israel kwa takriban mwezi mmoja wakiwa kizuizini.

Mmoja wa watu hao anasema wanajeshi wa Israel walimpiga risasi kwenye mguu wake wa kulia, ambao ulikatwa wakati yeye na wengine wakishikiliwa.

Chini ya sheria za vita, wafungwa wote wanatakiwa kutendewa utu.

Msemaji wa Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) aliambia BBC kwamba haikuwa na taarifa za kutosha kuchunguza madai ya mtu huyo ambaye mguu wake ulikatwa.

Msemaji huyo pia alisema Israel inaheshimu sheria za kimataifa.

Three of the men show the bruises on their wrists and legs
Maelezo ya picha, Mikono ya wanaume hao ilikuwa na michubuko huku wengine wakionyesha vidonda

Israel iliwaachilia wanaume hao siku ya Alhamisi, 14 Desemba katika mpaka wa Kerem Shalom unaovuka kutoka Israel hadi Gaza.

Wanaume hao kisha walitafuta matibabu katika hospitali ya Martyr Mohammed Yusuf al-Najjar huko Rafah kusini mwa Gaza.

Makumi ya wafungwa wa zamani walikuwepo. Jumla ya wanaume saba walikubali kuzungumza nami.

Wanaume wanne walikaa kwenye mstari kwenye kitanda cha hospitali, mtu wa tano alisimama kando yao.

Wote walikuwa wamevalia nguo za rangi ya kijivu na kunyoosha viganja vyao vilivyo na michubuko, huku wengine wakiwa wamefura midomo iliyokuwa na vidonda.

Wengine walikuwa bado wamevalia pingu nyeupe za plastiki zilizotumiwa na Israel kuwaweka kizuizini.

A deep wound and sore on one of the men's wrists
Maelezo ya picha, A deep wound and sore on one of the men's wrists

Mohammed Dawood alisema alizuiliwa alipokuwa akifuata amri ya Israel ya kuhamia kusini.

"Tulitoka Beit Lahia kaskazini na tulikuwa tunahamia kusini kupiti njia salama iliyotolewa," aliniambia.

"Walitukamata (IDF) kutoka huko. Walituhoji. Je! nyinyi ni Hamas? Je, ninyi ni wanamgambo wa kundi la Islamic Jihad?"

Alisema alizuiliwa kwa siku 26 na hatimaye kuachiliwa kwa sababu "hawakuweza kupata chochote kutoka kwetu".

Mohammed Dawood doing a TV interview with the BBC at a Rafah hospital
Maelezo ya picha, Mohammed Dawood aliweza kusimama wima alipokuwa akizungumza na BBC

Tarehe 14 Novemba IDF ilitangaza kufunguliwa kwa muda kwa njia za kuwahamisha Wapalestina kuelekea kusini kutoka kaskazini mwa Gaza.

Israel ilielezea kama "njia salama" kwa maslahi ya kibinadamu kwenye barabara kuu ya Salah al-Din.

Kulikuwa na ripoti za wanaume kuchunguzwa na IDF na kuwekwa kizuizini.

"Nilifungwa kamba na macho yangu yalikuwa yamezibwa kama wanaume wengine wote," alisema Mohammed Dawood.

“Walitunyanyasa, walitutemea mate na kutudharau, sote tulipigwa.

"Iwapo mtu yeyote atawaambia kuwa ni mgonjwa au mguu wao umekatwa, wao (askari wa Israeli) wangejibu, 'Kufia hapa'.

"Na wangewafunga kwa pingu zao."

Four of the men confirmed and corroborated what Mohammed Dawood told the BBC
Maelezo ya picha, Wanaume wanne kati ya hao walithibitisha kile ambacho Mohammed Dawood aliambia BBC

Msemaji wa IDF alikana madai haya.

"Kuhusu michubuko kutokana na kufungwa pingu wafungwa, tunafafanua kwamba wafungwa wanafungwa pingu kulingana na kiwango cha tishio walichonacho na afya zao," IDF ilisema katika taarifa.

"Hawaning'inizwi kutoka kwa mikono yao kwenye kituo wakati wowote."

Mohammed alisema walikuwa na blanketi moja tu kati yao na waliwekwa nje kwenye mvua, huku wakipewa chakula kidogo au maji.

Kwa mara nyingine, IDF ilikataa hili na kusema wafungwa wanapewa milo mitatu kwa siku, maji na huduma za matibabu.

Hakuna anayejua ni wanaume wangapi wamezuiliwa na jeshi la Israel huko Gaza au wanazuiliwa wapi.

Suala hili limekuwa gumzo tangu video kutoka Beit Lahia ilipoibuka mapema mwezi huu.

Ilionyesha makumi ya wanaume wa Kipalestina wakiwa wamevuliwa nguo zao za ndani na kuketi pamoja huku wanajeshi wa Israel wakiwalinda.

Mahmoud Abu Husein, who is missing his right leg, was attended to by medics in the hospital corridor
Maelezo ya picha, Mahmoud Abu Husein, ambaye amepoteza mguu wake wa kulia, alihudumiwa na madaktari katika korido ya hospitali.

Mtu wa sita, Mahmoud Abu Husein, alikaa kwenye kiti kwenye korido ya hospitali.

Alikuwa na mvi na mguu wake wa kulia haukuwepo, na dalili za damu kwenye sehemu ya chini ya nguo yake .

"Nilikuwa nyumbani kwangu, niliwaambia kuwa ninaumwa, mimi ni mzee, mwenye umri wa miaka 62," aliambia BBC, akiongeza kuwa anatoka kambi ya al-Shati kaskazini mwa Gaza.

"Waliniambia hapana, unahitaji kutujulisha Hamas iko wapi na mateka wako wapi.

“Nilipowaambia sijui walinipiga risasi mguuni, baadaye wakanikata mguu.

"Walinifanya nisaini karatasi iliyosema kuwa mguu wangu ulikuwa na tatizo."

IDF ilisema haikuwa na taarifa za kutosha kuchunguza tukio hili.

Mahmoud Abu Husein said Israeli soldiers shot him in the leg when he said he didn't know where Hamas and the hostages were
Maelezo ya picha, Mahmoud Abu Husein alisema wanajeshi wa Israel walimpiga risasi mguuni aliposema hajui walipo Hamas na mateka.

Madaktari katika hospitali hiyo ambao hawakutaka kutajwa majina walisema watu hao walifika hospitalini wakiwa katika hali mbaya. Walisema wawili kati ya wanaume hao wangali wanapokea matibabu, akiwemo Bw Husein.

Mzee mwingine, Mohammed Yusuf Ali Abu Shamla, naye alikuwa akisubiri kuhudumiwa kwenye hospitali hiyo. Anatokea kitongoji cha Zeitoun, mashariki mwa mji wa Gaza.

Bw Shamla, mwanamume wa saba ambaye BBC ilizungumza naye, alikuwa amevalia suti ya rangi ya kijivu sawa na wengine, lakini alionekana kuzuiliwa na Israel baadaye.

Mohammed Yusuf Ali Abu Shamla was also seated as he spoke to the BBC
Maelezo ya picha, Mohammed Yusuf Ali Abu Shamla pia alikuwa ameketi alipokuwa akizungumza na BBC

"Tinga lilianza kuharibu nyumba yangu nikiwa ndani. Watu wengine karibu watu 40 pia waliharibiwa nyumba zao ," aliiambia BBC. "Wanawake walikuwa wakipiga kelele. Tuliondoka nyumbani tukiwa tumeinua mikono juu."

Alisema aliwekwa kizuizini pamoja na watu wengine sita: wanawe watatu, wapwa wawili na kaka mmoja.

"Walitutaka tuvue nguo, unamaanisha nini tuvue nguo zetu, tuliona aibu lakini tukafuata mashati," alisema.

"Waliendelea kutuamuru tuvue zaidi zaidi. Tulivua hadi nguo zetu za ndani."

IDF ilisema inahitaji kuwavua nguo wafungwa ili kuangalia ikiwa wamevaa mkanda wa vilipuzi au wamebeba silaha.

The men appeared lost and traumatised after their ordeal
Maelezo ya picha, Wanaume hao walionekana kuwa na kiwewe baada ya mateso yao

Bw Shamla alisema walizuiliwa huko Gaza kwa siku tatu na kisha kupelekwa Israel.

Alisema alikuwa akijaribu kuitafuta familia yake kwani aliachiliwa peke yake.

"Sijui wengine wako wapi. Ninajijua tu."

Imetafasiriwa na Yusuf Jumah na kuhaririwa na Ambia Hirsi