Somalia yakatiza uhusiano na UAE na kufuta mikataba yote ya ushirikiano

Wizara ya Mambo ya Nje imeagizwa kuiarifu rasmi Umoja wa Falme za Kiarabu kuhusu uamuzi huo na kuratibu utekelezaji wake.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Somalia yakatiza uhusiano wa kidiplomasia na UAE

    .

    Somalia imetangaza kukatiza uhusiano na Umoja wa Falme za Kiarabu, na kufuta makubaliano yote ya ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

    Katika taarifa iliyotolewa baada ya kikao cha baraza la mawaziri siku ya Jumatatu, Baraza la Mawaziri limesema kuwa limebatilisha mikataba yote iliyofikiwa na UAE, ikiwa ni pamoja na ile inayohusiana na bandari, usalama na ushirikiano wa ulinzi.

    Uamuzi huo unajumuisha mipango yote inayohusisha bandari za Berbera, Bosaso, na Kismayo, pamoja na makubaliano na taasisi za serikali, mashirika tanzu na tawala za mikoa.

    Miongoni mwa mikataba iliyoathiriwa ni mkataba wa bandari ya Berbera, ambapo utawala wa Somaliland ulitia saini mkataba wa usimamizi mwaka 2016 na DP World.

    Serikali ya Somalia kwa muda mrefu imekuwa ikipinga makubaliano hayo, ikisema yalifikiwa bila idhini yake.

    Serikali ilisema hatua hiyo ilichukuliwa ili kulinda mamlaka ya Somalia, umoja wa eneo na utaratibu wa kikatiba.

    Ilisema uamuzi huo ulifuata kile ilichotaja kama ripoti za kuaminika na ushahidi wa vitendo vinavyodhoofisha uhuru wa Somalia, umoja wa kitaifa na mamlaka ya kisiasa.

    Baraza la Mawaziri lilisema vitendo hivyo vinakiuka kanuni za kimataifa za kujitawala na kutoingilia kati, kama ilivyoainishwa katika mikataba ya Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika, Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu na Jumuiya ya Nchi za Kiarabu.

    Wizara ya Mambo ya Nje imeagizwa kuiarifu rasmi Umoja wa Falme za Kiarabu kuhusu uamuzi huo na kuratibu utekelezaji wake.

    Wizara hiyo pia itawafahamisha washirika wa kimataifa na kikanda, ikiwemo Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa.

    Serikali ya Somalia ilisema bado iko wazi kwa ushirikiano wa kimataifa unaozingatia kuheshimiana, kutambua mamlaka ya Somalia, na kuzingatia kanuni za kikatiba na kimataifa.

  2. Mwamuzi na mwanafunzi miongoni mwa mamia waliouawa katika maandamano ya Iran

    .

    Chanzo cha picha, Instagram/Iran Human Rights

    Mwamuzi na mwanafunzi ni miongoni mwa mamia ya watu walioripotiwa kuuawa wakati wa maandamano makubwa ya kuipinga serikali nchini Iran.

    Kocha Amir Mohammad Koohkan, 26, alipigwa risasi tarehe 3 Januari wakati wa maandamano katika mji wa Neyriz, rafiki yake aliambia BBC Idhaa ya Kiajemi.

    "Kila mtu alimfahamu kwa wema wake", walisema, na kuongeza familia yake ina huzuni na "machungu kwa sababu aliuawa na serikali".

    Siku tano baadaye, mwanafunzi Rubina Aminian, 23, alipigwa risasi kutoka nyuma wakati wa maandamano huko Tehran, kulingana na mashirika ya haki za binadamu.

    "Alipigania mambo ambayo alijua ni sawa", mjomba yake aliiambia CNN.

    Takriban waandamanaji 500 na maafisa 48 wa usalama wameuawa katika wiki mbili za maandamano, shirika la kutetea haki za binadamu lenye makao yake makuu nchini Marekani linasema.

    Soma zaidi:

  3. Trump 'usihadaiwe' kuwa wafungwa wa kisiasa wameachiwa huru Venezuela - Ramón Guanipa

    Ramón Guanipa anasema ameruhusiwa kumtembelea babake mara moja tu tangu alipokamatwa
    Maelezo ya picha, Ramón Guanipa anasema ameruhusiwa kumtembelea baba yake mara moja tu tangu alipokamatwa

    Mtoto wa kiongozi wa upinzani wa Venezuela aliyefungwa jela amemuonya Donald Trump "kutodanganywa" na serikali ya nchi hiyo, huku shutuma zikiibuka kwamba haijatimiza ahadi yake ya kuachilia idadi kubwa ya wafungwa wa kisiasa.

    Ramón Guanipa, mtoto wa Juan Pablo Guanipa, alisema anaamini kuwa rais wa Marekani hajui kuwa ni wafungwa 40 tu kati ya zaidi ya wafungwa 800 wa kisiasa ndio walioripotiwa kuachiliwa kufikia sasa.

    Siku ya Jumamosi, Trump aliishukuru mamlaka ya Venezuela, akisema "wameanza mchakato huo vyema".

    Serikali ya Venezuela ilitangaza Alhamisi kuwa itawaachilia wafungwa wanaochukuliwa kuwa wafungwa wa kisiasa na mashirika ya kutetea haki za binadamu kama "ishara ya nia njema".

    Hatua hiyo imekuja baada ya Marekani kumkamata Rais wa Venezuela Nicolás Maduro jijini Caracas tarehe 3 Januari na kumpeleka New York, ambako amefunguliwa mashtaka ya ulanguzi wa dawa za kulevya.

    Jorge Rodríguez, kiongozi wa Bunge la Venezuela na kaka wa Rais wa mpito Delcy Rodríguez, alitangaza kwamba "wafungwa kadhaa wa Venezuela na wa kigeni" wataachiliwa "haraka iwezekanavyo".

    Miongoni mwa waliothibitishwa kuachiliwa ni viongozi kadhaa wa upinzani - huku wizara ya mambo ya nje ya Uhispania ikithibitisha kuachiwa huru kwa raia watano wa Uhispania, akiwemo mwanasheria wa haki za binadamu Rocío San Miguel.

    Pia unaweza kusoma:

  4. Iran haitaanza uchokozi, lakini iko tayari kwa vita - Waziri wa mambo ya nje

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran anasema Tehran haina mpango wa kuchukua hatua za kijeshi, lakini iko tayari kwa vita ikishambuliwa.

    Akiwahutubia mabalozi wa kigeni mjini Tehran, Abbas Araghchi alisema Jamhuri ya Kiislamu ya Iran "haitaki vita", huku akiwaonya wapinzani dhidi ya "mpango mbaya" wowote.

    Anasema Iran "imejiandaa zaidi" kuliko wakati wa mzozo wake wa siku 12 na Israeil mwezi Juni mwaka uliopita.

    Araghchi pia imetetea hatua ya "udhibiti" mtandao wa itaneti unaendelea katikati ya machafuko akiongeza kuwa hatua hiyo iitadumishwa hadi pale ''tutakapojiridhisha kuwa hakuna vitisho tena".

    Waziri wa mambo ya nje anasema machafuko ya hivi majuzi yamebadilika kutoka kwa maandamano hadi kwa kile anachotaja kama "operesheni za kigaidi", akirejelea kaulirasmi uliotolewa na vyombo vya habari vya Iran na vyombo vya usalama wiki iliyopita.

    Aidha amesema Iran iko tayari kwa mazungumzo, lakini kwa kile anachoeleza kuwa haki, heshima na masharti sawa - akisisitiza msimamo wa Tehran juu ya mazungumzo na Washington tangu mzozo wa Juni.

    Soma zaidi:

  5. Wasanii wa Nigeria watawala Tuzo za Afrima

    .

    Chanzo cha picha, Robert Okine via Getty images

    Wasanii wa Nigeria walipata msururu wa ushindi katika toleo la 9 la za All Africa Music Awards (Afrima), zilizomalizika mjini Lagos Jumapili usiku.

    Mwimbaji nyota wa kimataifa Burna Boy alishinda tuzo ya Albamu bora ya Mwaka kwa kazi yake mpya ya No Sign of Weakness. Pia alishiriki tuzo ya Ushirikiano Bora wa Kiafrika na mtani anayekuja kwa kasi Shallipopi, ambaye alishinda Wimbo Bora wa Mwaka tofauti kwa wimbo wake wa Laho, ambao ulivuma kwenye mitandao ya kijamii.

    Tukio hilo la wiki moja, ambalo liliwaleta pamoja wasanii, wataalamu wa tasnia na washikadau kutoka barani kote, lilifikia kilele kwa sherehe ambapo uwezo wa sasa wa muziki wa Nigeria ulionekana wazi.

    Aliyeongoza kwenye orodha hiyo ya jioni ni Rema, ambaye alitwaa tuzo tatu: Msanii Bora wa Mwaka, Msanii Bora wa Kiume Afrika Magharibi, na Msanii Bora wa Afrika katika muziki wa RnB na Soul.

    Washindi wengine mashuhuri wa Nigeria ni pamoja na Yemi Alade, ambaye alishinda Wimbo Bora wa Sauti katika Filamu, Mfululizo au Makala kwa wimbo wake You Are kutoka mfululizo wa vibonzo Iyanu, na rapa mkongwe Phyno, aliyetajwa kuwa Msanii Bora wa Kiafrika katika Hip-Hop ya Kiafrika.

    Tuzo hizo pia ziliwatunuku talanta chipukizi. Qing Madi alitawazwa kuwa Msanii Bora wa Mwaka, huku Chella akishinda taji la Kipenzi cha Mashabiki wa Kiafrika.

    Wakati nyota wa Nigeria walitawala, sherehe hiyo ilisherehekea talanta kutoka kote Afrika. Wendy Shay wa Ghana alishinda tuzo ya Msanii Bora wa Kike Afrika Magharibi, Nontokozo Mkhize wa Afrika Kusini alishinda Msanii Bora wa Kike Kusini mwa Afrika na Mtanzania Juma Jux alichaguliwa kuwa Msanii Bora wa Kiume Afrika Mashariki.

  6. Barcelona washinda kombe la Super Cup

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Barcelona imeishinda Real Madrid katika mchezo wa kusisimua wa mabao 3-2 katika fainali za Kombe la Super Cup la Uhispania mjini Jeddah, Saudi Arabia.

    Barcelona iliandikisha ushindi wa 16 katika timu hiyo ikiwa chini ya Hansi Flick, huku pia ikiwashinda Los Blancos katika fainali ya mwaka jana.

    Shambulio l;a mchezaji wa Brazil Raphinha dakika ya 73 liliihakikishia ushindi baada ya kumalizika kwa kipindi cha kwanza kwa msisimko.

    Mabao matatu ya haraka katika kipindi cha kwanza yaliwaweka wawili hao sawa wakati wa mapumziko baada ya Raphinha kufungua ukurasa wa mabao, kunako dakika ya dakika ya 36.

    Vinicius Jr alisawazisha dakika mbili baada ya muda wa nyongeza, akimzidi Jules Kounde kwa kasi nzuri kabla ya kuingia kwenye kona ya goli kufunga bao lake la kwanza la Real katika michezo 17, tangu Oktoba 4, 2025.

    Robert Lewandowski kisha alirejesha uongozi wa Barca dakika ya 49.

    Lakini Gonzalo Garcia alivutiwa na mpira dakika tatu baadaye baada ya mpira wa kichwa wa Dean Huijsen kugonga mwamba, huku kocha wa Barca Flick akipinga firimbi ya mapumziko ikiwa tayari imepulizwa.

    Frenkie de Jong alionyeshwa kadi nyekundu ya moja kwa moja katika dakika za mwisho baada ya kumchezea rafu Kylian Mbappe, ambaye aliingia kama mchezaji wa akiba baada ya kupona jeraha la goti.

    Nafasi za mwisho kwa pande zote mbili zilichangia fainali iliyojaa msisimko huku Marcus Rashford akipiga mpira nje ya goli, Alvaro Carreras na kisha Raul Asencio wote wakipiga moja kwa moja kwa kipa Joan Garcia.

    Lakini Barca walishikilia ubingwa wa pili mfululizo kwa mara ya kwanza tangu 2011.

    Pia unaweza kusoma:

  7. Trump: Iran imetupigia simu ikiomba mazungumzo

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Rais wa Marekani Donald Trump, akizungumza na waandishi wa habari kstik ndege ya Air Force One, amesema kuwa "Iran imetoa wito wa kufanya mazungumzo."

    "Ndiyo, ndio. Walipiga simu jana," Bw. Trump alimwambia mwandishi wa habari, bila kutoa maelezo zaidi.

    "Viongozi wa Iran wanataka kufanya mazungumzo. Nadhani wamechoka kushambuliwa na Marekani," alisema.

    Rais wa Marekani aliendelea: "Tunaweza kukutana nao, namaanisha, mkutano unapangwa, lakini tunaweza kuchukua hatua kwa sababu ya kile kilichotokea."

    Bw. Trump pia alimwambia mwandishi wa habari, kuhusu ripoti za kuenea kwa mauaji ya waandamanaji na iwapo Iran ilikuwa imevuka "mstari mwekundu," kwamba "wameua watu waziwazi, watu ambao hawakupaswa kuuawa.

    Hii ni vurugu. Sijui kama unaweza kuwaita viongozi, lakini wanaonekana kutawala kwa vurugu tu.

    Tunaangalia chaguzi ... Jeshi linaangalia chaguzi. Tunayo chaguzi kali sana."

  8. Trump asema atazungumza na Musk kuhusu kurejesha mtandao nchini Iran

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema anapanga kuzungumza na bilionea Elon Musk kuhusu kurejesha intaneti nchini Iran, ambapo mamlaka zimezima huduma kwa siku nne huku kukiwa na maandamano yanayoendelea dhidi ya serikali.

    "Yeye ni mzuri sana katika mambo hayo na ana kampuni nzuri sana," Trump aliwaambia waandishi wa habari akijibu swali kuhusu kama angeshirikiana na kampuni ya Musk ya SpaceX, ambayo hutoa huduma ya intaneti ya setilaiti inayoitwa Starlink ambayo imekuwa ikitumika nchini Iran.

    Musk na SpaceX hawakujibu mara moja ombi la kutoa maoni kutoka kwa shirika la Reuters.

    Upatikanaji wa taarifa kutoka Iran imekuwa vigumu kutokana na kuminywa kwa intaneti tangu Alhamisi huku kukiwa na maandamano makubwa zaidi dhidi ya taasisi ya makasisi nchini humo tangu 2022.

    Soma zaidi:

  9. Shambulizi la usiku kucha la Urusi lasababisha moto Ukraine - Jeshi

    Urusi imefanya shambulizi la anga usiku kucha dhidi ya Ukraine, na kusababisha moto katika moja ya wilaya za jiji hilo, jeshi la Ukraine lilisema Jumatatu.

    Timur Tkachenko, mkuu wa utawala wa kijeshi wa Kyiv, alisema kwenye Telegram kwamba vitengo vya ulinzi wa anga vya Ukraine vilikuwa vikijaribu kuzima shambulio hilo.

  10. Trump asema hakuna tena mafuta wala pesa za Venezuela kwenda Cuba

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Marekani Donald Trump siku ya Jumapili alisema hakuna mafuta wala pesa za Venezuela zitakazokwenda Cuba tena na kupendekeza kisiwa hicho kinachoongozwa na Wakomunisti kinapaswa kufikia makubaliano na Marekani na kuongeza shinikizo kwa nchi hiyo kulikosababisha maneno ya ukaidi kutoka kwa uongozi wake.

    Venezuela ndiyo muuzaji mkuu wa mafuta wa Cuba, lakini hakuna shehena yoyote iliyoondoka kutoka bandari za Venezuela hadi Cuba tangu kukamatwa kwa Rais wa Venezuela Nicolas Maduro na vikosi vya Marekani mapema Januari huku kukiwa na kizuizi kikali cha mafuta cha Marekani dhidi ya nchi hiyo ya OPEC.

    Wakati huo huo, Venezuela na Washington zinaendelea na mpango wa dola bilioni 2 wa kusambaza hadi mapipa milioni 50 ya mafuta ya Venezuela kwa Marekani huku mapato yakiwekwa katika akaunti zinazosimamiwa na Hazina ya Marekani.

    "HAKUTAKUWA NA MAFUTA AU PESA TENA ZINAZOENDA CUBA - SIFURI! Ninapendekeza kwamba wafikie makubaliano, KABLA YA KUCHELEWA," Trump aliandika kwenye jukwaa lake la Truth Social siku ya Jumapili.

    "Cuba iliishi, kwa miaka mingi ikitegemea kiasi kikubwa cha MAFUTA na PESA kutoka Venezuela," Trump aliongeza.

    Rais wa Cuba Miguel Diaz-Canel alikataa tishio la Trump kwenye mitandao ya kijamii, akidokeza kwamba Marekani haikuwa na mamlaka ya kimaadili ya kulazimisha makubaliano dhidi ya Cuba.

    Soma zaidi:

  11. Wasanii nyota waingia kwa mbwembwe kwenye zulia jekundu la Golden Globes

    Majina tajika kwenye ulimwengu wa filamu na televisheni yamejitokeza kwenye zulia jekundu kwa ajili ya Golden Globes ya mwaka huu, moja ya sherehe kuu za tuzo za Hollywood, zinazofanyika Los Angeles.

    Ariana Grande ameteuliwa kwa miaka miwili iliyopita - kwa filamu ya Wicked: For Good.

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Glen Powell, ambaye awali aliteuliwa katika kitengo cha filamu, anatambuliwa mwaka huu kwa nafasi yake katika mfululizo wa vichekesho vya televisheni wa Chad Powers.

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Jenna Ortega anatambuliwa kwa jukumu lake katika kipindi cha Wednesday katika filamu ya Addams Family

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Nyota wa Only Murders in the Building, Selena Gomez, ameingia kwenye zulia jekundu na mtayarishaji wa muziki Benny Blanco, ambaye alifunga ndoa naye mnamo mwezi Septemba.

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Mwimbaji wa Blackpink Lisa, ambaye alianza kuigiza The White Lotus, ni miongoni mwa watu mashuhuri katika tukio hilo.

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

  12. Bi na Bwana harusi wafariki siku moja baada ya fungate yao Pakistan

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Polisi wamesema wanandoa wapya wamefariki dunia wakati mtungi wa gesi ulipolipuka katika nyumba moja huko Islamabad ambapo walikuwa wamelala baada ya sherehe yao ya harusi.

    Watu wengine sita - wakiwemo wageni wa harusi na wanafamilia - waliokuwa hapo pia walifariki katika mlipuko huo. Zaidi ya watu kumi na wawili walijeruhiwa.

    Mlipuko huo ulitokea saa 07:00 kwa saa za eneo siku ya Jumapili, na kusababisha paa kuanguka.

    Watu waliojeruhiwa walinaswa chini ya vifusi na ilibidi wabebwe kwa machela na wafanyakazi wa uokoaji.

    Wafanyakazi wa dharura walisema mlipuko huo ulitokea kutokana na uvujaji wa gesi, ambao ulijaza chumba kisha kulipuka. Nyumba tatu jirani pia ziliharibiwa.

    Hanif Masih, baba wa bwana harusi, alisema mwanawe alikuwa ameoa siku iliyotangulia, na wanandoa hao wapya, pamoja na wanafamilia na wageni, walikuwa wamelala ndani ya nyumba hiyo wakati wa mlipuko huo.

    Pamoja na mwanawe, mkwewe, mke na shemeji yake wote waliuawa.

    Polisi walisema walikuwa wamezingira eneo hilo na walikuwa wakichunguza mazingira ya mlipuko huo.

    Maafisa wa uchunguzi wa kivita waliovalia suti nyeupe walitumwa kufanya uchunguzi kwenye vifusi.

    Kaya nyingi za Pakistani hutumia mitungi ya gesi ya petroli iliyoyeyushwa kwa ajili ya kupikia. Vipuri vya gesi vimehusishwa na ajali zingine mbaya zinazosababishwa na uvujaji wa gesi.

    Pia unaweza kusoma:

  13. Trump hatachukua eneo la Greenland kwa nguvu, amesema Mandelson

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Balozi wa zamani wa Uingereza nchini Marekani amesema Rais wa Marekani Donald Trump hatachukua eneo la Greenland kwa nguvu.

    Balozi huyo aliiambia BBC kwamba alivutiwa na "uwazi" wa Trump katika mazungumzo ya kisiasa lakini akaongeza kuwa yeye siyo "mpumbavu", na washauri wake watamkumbusha kwamba kuichukua Greenland kunaweza kusababisha "hatari kubwa" kwa maslahi ya kitaifa ya Marekani.

    Katika kipindi cha pili cha utawala wa Trump kumekuwa na angalizo zaidi juu ya jinsi eneo la Denmark linalojitawala kiasi linavyoendeshwa, huku Trump akisema Jumamosi kwamba Marekani inahitaji "kumiliki" eneo la Greenland ili kuzuia Urusi na China kufanya hivyo.

    Denmark na Greenland zinasema eneo hilo haliuzwi, huku Denmark ikionya kwamba hatua za kijeshi zitasababisha mwisho wa muungano wa kijeshi wa Nato.

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio atafanya mazungumzo na Denmark kuhusu eneo la Greenland wiki ijayo.

    Trump amesisitiza mara kwa mara kwamba Greenland ni muhimu kwa usalama wa taifa la Marekani, akidai bila ushahidi kwamba "ilikuwa imezungukwa na meli za Urusi na China kila mahali".

    Msisitizo wake wa kuchukua eneo hilo ulirejea baada ya wanajeshi wa Marekani kushambulia mji mkuu wa Venezuela, Caracas wiki iliyopita ambapo walimkamata rais Nicolas Maduro na mkewe na kuua watu kadhaa.

    Lord Mandelson, ambaye alidumu kwa miezi michache tu kama balozi, pia alisema: "Sote tutalazimika kukubali ukweli kwamba Aktiki inahitaji ulinzi dhidi ya China na Urusi. Na ukiniuliza ni nani atakayeongoza katika juhudi hizo za kupata usalama, sote tunajua, sivyo, kwamba itakuwa Marekani."

    Soma zaidi:

  14. Serikali ya Sudan yarejea katika mji mkuu baada ya vita vya karibu miaka 3

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Serikali inayoongozwa na jeshi la Sudan imerejea katika mji mkuu wa nchi hiyo baada ya karibu miaka mitatu ya kuendesha shughuli zake kutoka kambi zake za kivita katika mji wa mashariki wa bandari ya Sudan.

    Waziri Mkuu wa Sudan Kamil Idris aliwaambia waandishi wa habari siku ya Jumapili kwamba "serikali ya matumaini" imerejea rasmi Khartoum na itaanza juhudi za kuboresha huduma kwa wakazi wa jiji hilo walio katika hali ngumu.

    Jeshi lililazimika kuondoka kutokana na vitendo vya kikosi cha Rapid Support Forces (RSF) wakati vita vya wenyewe kwa wenyewe vilipozuka kati ya pande hizo mbili mwaka wa 2023. Jeshi lilichukua tena mji huo katika hatua muhimu mnamo mwezi Machi mwaka jana.

    Khartoum imekuwa ikiendelea kujikwamua kutokana na mapigano ya miaka mingi. Takriban watu milioni tano walikimbia mji huo wakati wa kilele cha mzozo, kulingana na Umoja wa Mataifa.

    Wale ambao hawakutaka au hawakuweza kuondoka walielezea uvamizi wa kikatili wa kundi la RSF, ambao ulijumuisha uporaji mkubwa na wapiganaji kuchukua nyumba za raia.

    Sehemu kubwa za jiji zimeharibika. Mnamo mwezi Oktoba, afisa wa Umoja wa Mataifa Ugochi Daniels aliripoti kwamba ni "vigumu kupata huduma za msingi".

    Siku ya Jumapili, Idris alisema serikali itajitahidi kuboresha umeme, maji, huduma ya afya na elimu huko Khartoum.

    Pia alitangaza kwamba mwaka 2026 utakuwa "mwaka wa amani" kwa Sudan, ambapo takriban watu 150,000 wamekufa tangu vita vilipozuka.

    Umoja wa Mataifa umeelezea hali hiyo kama janga baya zaidi la kibinadamu duniani na takriban watu milioni 12 wamelazimika kuyahama makazi yao.

    RSF na jeshi la Sudan wameshutumiwa kwa kufanya ukatili katika kipindi chote cha mzozo.

    Juhudi za kimataifa za kuleta amani zimeshindwa na pande zote mbili zinaungwa mkono na mataifa ya kigeni ambayo yamekuwa yakitoa silaha nchini humo.

    Falme za Kiarabu (UAE) inachunguzwa sana hivi karibuni kuhusu madai ya kuunga mkono RSF, ambayo inakanusha vikali.

    Soma zaidi:

  15. Watu zaidi ya 500 wafariki dunia Iran kwa maandamano, kundi la haki za binadamu

    .

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Machafuko nchini Iran yamewaua zaidi ya watu 500, kundi la haki za binadamu lilisema Jumapili, huku Iran ikitishia kulenga kambi za kijeshi za Marekani ikiwa Rais Donald Trump atatekeleza vitisho vya kuingilia kati kijeshi kwa niaba ya waandamanaji.

    Huku Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ikikabiliwa na maandamano makubwa zaidi tangu 2022, Trump ametishia mara kwa mara kuingilia kati ikiwa nguvu kupita kiasi itatumika dhidi ya waandamanaji.

    Kulingana na takwimu zake za hivi karibuni - kutoka kwa wanaharakati ndani na nje ya Iran - kundi la haki za binadamu lenye makao yake Marekani la HRANA limesema limethibitisha vifo vya waandamanaji 490 na wafanyakazi 48 wa usalama, huku zaidi ya watu 10,600 wakikamatwa katika wiki mbili za machafuko.

    Iran haijatoa idadi rasmi na shirika la habari la Reuters halikuweza kuthibitisha idadi hiyo kwa uhuru.

    Trump amepangiwa kukutana na washauri wakuu siku ya Jumanne kujadili chaguzi zilizopo kwa ajili ya Iran, afisa mmoja wa Marekani aliambia Reuters Jumapili.

    Jarida la Wall Street Journal lilikuwa limeripoti kwamba chaguzi hizo ni pamoja na mashambulizi ya kijeshi, kutumia silaha za siri za mtandao, kuongeza vikwazo na kutoa msaada mtandaoni kwa vyanzo vinavyopinga serikali.

    Spika wa Bunge la Iran Mohammad Baqer Qalibaf ameonya Marekani dhidi ya hatua hiyo akiita "kosa."

    "Tuwe wazi: katika kesi ya shambulio dhidi ya Iran, maeneo yanayokaliwa na (Israeli) pamoja na kambi na meli zote za Marekani zitakuwa shabaha yetu halali," alisema Qalibaf, kamanda wa zamani wa kikosi cha Revolutionary Guards cha Iran.

    Maandamano yanayoshuhudiwa nchini Iran yalianza Desemba 28 yakidai kupinga kupanda kwa gharama ya maisha, kabla ya kuwageukia watawala wa kidini ambao wametawala tangu Mapinduzi ya Kiislamu ya 1979.

    Mamlaka ya Iran imeshutumu Marekani kwa kuchochea fujo na kuitisha mkutano wa kitaifa Jumatatu kulaani "vitendo vya kigaidi vinavyoongozwa na Marekani na Israeli," vyombo vya habari vya serikali viliripoti.

    Kuminywa kwa intaneti nchini Iran pia kumefanya mawasiliano kuwa magumu nchini humo.

    Soma zaidi:

  16. Hujambo msomaji wetu. Karibu katika matangazo yetu mubashara ya tarehe 12/01/2026.