Mapinduzi ya kijeshi yafanyika Guinea-Bissau

Milio ya risasi ilisikika katika mji mkuu huku Embaló na mpinzani wake Fernando Dias wakidai ameshindi.

Muhtasari

Moja kwa moja

Asha Juma & Rashid Abdallah

  1. Tanzania yawafutia mashtaka washukiwa 600 wa maandamano

    G

    Chanzo cha picha, Reuters

    Tanzania yawamefuta mashtaka dhidi ya watu 607 waliokamatwa wakati wa msako wa baada ya uchaguzi wa Oktoba, wengi wao wakishtakiwa kwa uhaini kufuatia maandamano mabaya.

    Katika taarifa ya video, Waziri wa Masuala ya Sheria, Juma Homera amesema watu 2,045 kote nchini walikamatwa na kushtakiwa kuhusiana na machafuko hayo.

    Homera amesema zaidi ya watu 1,400 wanaendelea kushikiliwa huku kesi zao zikipitiwa na Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP).

    "Watu 607 tayari wameachiliwa huru kufikia Jumanne... Baadhi wataachiliwa huru siku zijazo na huku wengine wakitarajiwa kubaki kizuizini kwa tathmini zaidi, na kuachiliwa huru zaidi kutategemea matokeo ya DPP," anasema Homera.

    Uamuzi wa kuondoa mashtaka unafuatia agizo lililotolewa na Rais Samia Suluhu wakati wa ufunguzi wa Bunge Novemba 14, likimuagiza DPP na vyombo vya usalama kupitia kesi hizo na kuwaachilia wale ambao hawakuwa katikati ya ghasia za baada ya uchaguzi.

    Maandamano ya wiki nzima, yaliyosababishwa wakati wa uchaguzi wa Oktoba, yalishuhudia vikosi vya usalama vikikabiliana na waandamanaji.

    Kulingana na vyanzo mbalimbali, mamia ya watu waliuawa.

    Uhaini una adhabu ya kifo nchini Tanzania, ingawa hukumu nyingi za kifo baadaye hubadilishwa kuwa kifungo cha maisha.

    Utekelezaji wa mwisho nchini wa hukumu ya kifo ni katika miaka ya 1990.

  2. Wanajeshi wa Guinea-Bissau watangaza mapinduzi

    Hh

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Kundi la maafisa wa kijeshi wamesema wametwaa udhibiti wa Guinea-Bissau huku kukiwa na ripoti kwamba rais, Umaro Sissoco Embaló, amekamatwa.

    Rais wa Guinea-Bissau Umaro Sissoco Embaló amekamatwa na watu wenye silaha siku chache tu baada ya uchaguzi wenye utata ambapo upinzani ulizuiliwa kushiriki.

    Milio ya risasi ilisikika katika mji mkuu huku Embaló na mpinzani wake Fernando Dias wakidai ameshindi.

    Vilevile, milio ya risasi imezuka karibu na makao makuu ya tume ya uchaguzi ya Guinea-Bissau Jumatano, siku moja kabla ya matokeo ya urais yenye mvutano yalitarajiwa kutangazwa.

    Nchi hiyo ya Afrika Magharibi yenye historia ya mapinduzi ilifanya uchaguzi wa rais na wabunge Jumapili.

    Kinyang'anyiro hicho kilimkutanisha Rais aliye madarakani Umaro Sissoco Embalo na mpinzani wake mkuu Fernando Dias, na pande zote mbili zinadai ushindi katika raundi ya kwanza mapema wiki hii.

    Haikuwa wazi mara moja ni nani aliyehusika katika ufyatuaji risasi, ambao ulishuhudiwa na mwandishi wa habari wa Reuters na wakazi wengine wawili.

    Msemaji wa Embalo, Antonio Yaya Seidy, aliambia Reuters kwamba watu wenye silaha wasiojulikana walishambulia tume ya uchaguzi ili kuzuia kutangazwa kwa matokeo ya kura.

    Alisema watu hao walikuwa na uhusiano na Dias, bila kutoa ushahidi. Msemaji wa Dias hakujibu ombi la kutoa maoni.

    Mmoja wa mashahidi alisema wakazi walikuwa wakikimbia kutoka eneo la tukio huku milio ya risasi ikiendelea karibu na jengo la tume ya uchaguzi.

    Dereva mmoja huko Bissau ambaye aliomba asitajwe jina alisema pia kulikuwa na milio ya risasi katika wizara ya mambo ya ndani na ikulu ya rais.

    Taifa hilo dogo la pwani kati ya Senegal na Guinea lilishuhudia angalau mapinduzi tisa kati ya 1974, lilipopata uhuru kutoka kwa Ureno, na 2020, wakati Embalo alipochukua madaraka.

    Embalo anasema amenusurika majaribio mengine matatu ya mapinduzi tangu wakati huo, ingawa wapinzani wake wamemtuhumu kwa kutengeneza migogoro kama kisingizio cha ukandamizaji - madai ambayo anayapuuza.

    Embalo alikuwa akitafuta kuwa rais wa kwanza katika miongo mitatu kushinda muhula wa pili mfululizo nchini Guinea-Bissau.

    Uchaguzi huo ulikuwa wa kwanza kufanyika bila Chama kikuu cha upinzani PAIGC, chama kilichoongoza mapambano ya uhuru kutoka kwa Ureno katika miaka ya 1960 na 1970.

    PAIGC ilizuiwa kuwasilisha wagombea baada ya mamlaka kusema iliwasilisha hati kwa kuchelewa.

  3. Mahakama yatupilia mbali kesi ya kupinga bomba la mafuta la Tanzania na Uganda

    Y

    Chanzo cha picha, AA

    Mahakama ya haki ya jumuiya ya afrika mashariki, imetupilia mbali kesi iliyowasilishwa katika mahakama hiyo kupinga mradi wa ujenzi wa bomba la mafuta, la TotalEnergies unaofadhiliwa na serikali za Tanzania na Uganda. .

    Mashirika manne ya kutetea haki za kijamii yaliwasilisha kesi katika mahakama hiyo ya Afrika Mashariki, kutaka mradi huo wa ujenzi la bomba la mafuta kutoka magharibi mwa Uganda hadi Tanga ufanyiwe ukaguzi wa kina. Makundi hayo yalidai kuwa mradi huo utakuwa na athari kubwa kwa haki za kibinadam, kimazingira na pia kuathiri mabadiliko ya tabia ya nchi.

    Mradi huo unajengwa kwa ushirikiano kati ya kampuni za Total Energies na kampuni ya kimataifa ya China CNOOC, na shirika la taifa la mafuta ya Uganda.

    Bomba hilo lenye urefu wa kilomita 1443, litakuwa bomba refu zaidi duniani na litatumiwa kusafirisha mafuta ghafi kutoka ziwa Albert magharibi mwa Uganda hadi bandari ya Tanga nchini Tanzania.

    Lakini mapema hii leo, mahakama ya Afrika Mashariki ilifuta kesi hiyo kwa misingi ya utaratibu. Mahakama ilisema kuwa kesi hiyo iliwasilishwa baada ya siku sitini nje ya muda wa kupinga uamuzi uliotolewa mwaka wa 2023.

    Asilimia sitini ya mradi huo utakaogharimu dola bilioni tano nukta sita, tayari umejengwa na umepata sifa ya kuwa mradi mkubwa zaidi wa kiuchumi kati ya Uganda na Tanzania, ambako idadi kubwa ya raia wake ni masikini.

    Mawakili wa upande wa jamii zikizoathirika wamesema kwamba uamuzi huo wa mahakama ni pigo kubwa kwa raia na pia mazingira.

    Makundi ya kuteteta haki za kibinadam yamesema kuwa zaidi ya watu laki moja wamepokonywa ardhi zao bila kulipwa fidia inayostahili, huku baadhi yao wakishurutishwa na serikali kusaini mikataba ambayo hawaielewi.

    Mwaka wa 2023, mahakama ya Ufaransa ilifutilia mbali kesi nyingine kama hii iliyokuwa imewasilishwa dhidi ya kampuni ya mafuta ya Total energies, kwa misingi ya utaratibu.

    Watetezi wa haki za kibinadam wanadai kuwa mradi huo unakiuka azimio lililoidhinishwa mwaka wa 2017, linalotaka serikali na makampuni kufanya tathmini ya kina ili kuzuia ukiukwaji wa haki za kibinadam, afya, usalama na pia uharibifu wa mazingira

  4. Pande zinazopigana Sudan haziko tayari kusitisha mapigano - mshauri wa Trump

    s

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Mshauri Mkuu wa Marekani wa Masuala ya Kiarabu na Afrika, Massad Boulos, akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu mzozo unaoendelea nchini Sudan, Abu Dhabi, Falme za Kiarabu, Novemba 25, 2025.

    Marekani imewasilisha pande zinazozozana nchini Sudan na pendekezo la kusitisha mapigano lakini hakuna upande uliokubali hadi sasa, mjumbe wa Marekani Massad Boulos alisema Jumanne.

    Wakati huo huo jeshi la Sudan, linawashutumu Rapid Suport Forces kwa kufanya mashambulizi licha ya kutangaza kusitisha mapigano.

    RSF walitangaza kusitisha mapigano siku ya Jumatatu kulingana na matakwa ya Marekani. Lakini siku ya Jumanne jeshi lilisema kuwa limezima shambulio kwenye kambi ya Babanusa katika jimbo la Kordofan Magharibi.

    Rais wa Marekani Donald Trump alisema wiki iliyopita ataingilia kati kusimamisha mzozo kati ya jeshi na RSF, uliozuka Aprili 2023 kutokana na mzozo wa madaraka na kusababisha njaa, mauaji ya kikabila na watu wengi kuyahama makaazi yao.

    Juhudi za hapo awali zikiongozwa na Marekani, Saudi Arabia, Misri na Umoja wa Falme za Kiarabu zimeshindwa kuzaa matunda.

  5. Urusi haina nia ya kushiriki mazungumzo ya amani - Mkuu wa Umoja wa Ulaya

    c

    Chanzo cha picha, EPA

    Maelezo ya picha, Mkuu wa Tume ya Ulaya aliliambia Bunge mjini Strasbourg kwamba Ulaya itaendelea kusimama na Ukraine

    Mkuu wa Tume ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen ameelezea kuwa hali ni tete nay a hatari katika vita vya Ukraine na kuishutumu Urusi kwa kutokuwa na "nia ya kweli" ya kushiriki katika mazungumzo ya amani.

    Maoni yake yamekuja muda mfupi kabla ya msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov kusema ni "mapema" kuzungumzia juu ya makubaliano ya amani.

    Von der Leyen amesema Ukraine itahitaji uhakikisho wa usalama na mashambulizi yoyote, akisema kuwa Urusi bado inashikilia msimamo wa kama baada ya Vita vya Pili vya Dunia.

    Ameyasema hayo wakati akilihutubia Bunge la Ulaya mjini Strasbourg huku Marekani ikiongeza juhudi za kupatanisha makubaliano kati ya Kyiv na Moscow.

    Mazungumzo ya wiki hii mjini Geneva na kisha Abu Dhabi yamepelekea Ukraine kukubaliana na mapatano ya amani, baada ya mabadiliko kufanywa katika mpango wa awali wenye vipengele 28.

    Katika hotuba yake kwa wabunge wa Umoja wa Ulaya, Von der Leyen amesema: "Nataka kuwa wazi tangu mwanzo: Ulaya itasimama na Ukraine na kuiunga mkono Ukraine kwa kila hatua."

  6. Vifo kutokana na mlipuko wa virusi vya Marburg Ethiopia vimefikia 6

    SD

    Chanzo cha picha, MTT

    Idadi ya vifo kutokana na mlipuko wa virusi vya Marburg nchini Ethiopia imeongezeka hadi sita, shirika la habari la serikali ya nchi hiyo limeripoti siku ya Jumatano.

    Ethiopia ilithibitisha kwa mara ya kwanza mlipuko huo Novemba 14, huku vifo vitatu vikiripotiwa siku tatu baadaye.

    "Kati ya watu 11 ambao virusi hivyo viligunduliwa, sita wamekufa, na watano wanapokea matibabu," Shirika la Habari la Ethiopia lilisema kwenye ukurasa wake wa Facebook, likitoa taarifa kutoka wizara ya afya.

    Kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, Wizara imesema watu 349 ambao walishukiwa kukutana na watu walioambukizwa walitengwa, na 119 kati yao wameruhusiwa baada ya kukamilisha uchunguzi wao.

    Marburg, kutoka familia moja ya virusi na Ebola, mara nyingi husababisha maumivu makali ya kichwa na kusababisha kuvuja damu.

    Pia unaweza kusoma:

  7. Seneta wa Marekani amtaka Trump kutofanya majaribio ya silaha za nyuklia

    p

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Seneta wa Marekani Edward Markey akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari

    Seneta wa chama cha Democratic nchini Marekani, Edward Markey Jumanne amemtaka Rais Donald Trump kutofanya majaribio ya silaha za nyuklia, akisema kuwa kufanya hivyo kunaweza kuchochea mataifa hasimu yenye nyuklia Urusi na China kufanya vivyo hivyo.

    Trump alitangaza mwishoni mwa mwezi uliopita kwenye mitandao ya kijamii kuwa anaiagiza Pentagon kuanza mara moja mchakato wa majaribio ya silaha za nyuklia baada ya kusitishwa kwa miaka 33.

    Agizo lake limesababisha mkanganyiko kwa sababu ni Kitengo cha Kitaifa cha Usalama wa Nyuklia, tawi la Idara ya Nishati, ambacho ndio kina uwezo wa kufanya majaribio ya silaha za nyuklia.

    “Hata jaribio moja dogo la nyuklia la Marekani litazipa Urusi na China mwanga wa kijani wa kufanya majaribio mengi makubwa ya nyuklia ambayo yatazisaidia katika utengenezaji wa silaha mpya za nyuklia ambazo zinaweza kuwa tishio kwa usalama wa taifa la Marekani,” Markey aliandika katika barua yake kwa Trump.

    Markey, mwenyekiti mwenza wa Kikundi cha Kudhibiti Silaha za Nyuklia, amekuwa kiongozi wa muda mrefu katika juhudi za kuzuia urutubisha wa urani kupitia Congress.

    Markey alikomosoa Trump 2020, wakati wa muhula wake wa kwanza wa urais, dhidi ya kuanza tena majaribio ya milipuko ya silaha za nyuklia.

    Ikulu ya White House ilirudia kusema siku ya Jumanne kwamba mchakato wa majaribio utaanza "mara moja" na Trump aliagiza utawala wake kufanya hivyo "kwa sababu ya programu za majaribio za nchi zingine."

    Mkurugenzi wa CIA John Ratcliffe alisema kwenye mtandao wa kijamii Novemba 3 kwamba Trump "yuko sahihi" kuhusu nchi zingine kuwa zinafanya majaribio silaha za nyuklia.

    Kwa kumjibu Trump, Rais wa Urusi Vladimir Putin aliwaamuru maafisa wake wakuu kuandaa mapendekezo ya majaribio ya silaha za nyuklia, jaribio ambalo Moscow haijalifanya tangu kuanguka kwa Umoja wa Kisovieti mwaka 1991.

    Trump amesema Urusi na China zinafanya majaribio madogo ya nyuklia ambayo ni vigumu kuyagundua.

    "Ripoti za majaribio kama hayo mwaka 2019 zinaleta wasiwasi, lakini hazijathibitishwa," Markey alisema. "Hata kama ni kweli, majaribio hayo hayawezi kuhalalisha majaribio ya nyuklia ya Marekani."

    Markey amemwomba Trump atoe ushahidi ifikapo Desemba 15 kwamba Urusi na China zinafanya majaribio ya siri ya nyuklia.

    Pia unaweza kusoma:

  8. Watoto wafungua kesi mahakamani kupinga marufuku ya mitandao ya kijamii Australia

    Z

    Chanzo cha picha, Digital Freedom Project

    Maelezo ya picha, Noah Jones na Macy Neyland wanasema marufuku hiyo inazuia haki za watoto

    Marufuku ya kutumia mitandao ya kijamii nchini Australia kwa watoto imekumbana na changamoto baada ya kesi kufunguliwa katika mahakama ya juu zaidi ya taifa hilo, huku vijana wawili wakidai kuwa sheria hiyo ni kinyume na katiba kwani inawanyima haki yao ya kuwasiliana.

    Kuanzia tarehe 10 Desemba, kampuni za mitandao ya kijamii - ikiwa ni pamoja na Meta, TikTok na YouTube - lazima zihakikishe kwamba Waaustralia walio na umri wa chini ya miaka 16 hawawezi kuwa na akaunti kwenye mitandao yao.

    Sheria hiyo, ambayo inafuatiliwa kwa karibu kote ulimwenguni, inaelezwa na serikali na wanaoiunga mkono kuwa ni muhimu ili kulinda watoto dhidi ya maudhui hatari.

    Hata hivyo, watoto wenye umri wa miaka 15 Noah Jones na Macy Neyland - wanaoungwa mkono na kundi la kutetea haki za binadamu – wamefungua kesi kuwa marufuku hiyo inapuuza haki za watoto.

    "Hatupaswi kunyamazishwa," Macy Neyland alisema katika taarifa yake.

    Baada ya habari za kesi hiyo kuibuka, Waziri wa Mawasiliano Anika Wells aliambia bunge kuwa serikali haitayumbishwa.

    "Hatutatishwa. Hatutatishwa na changamoto za kisheria. Hatutatishwa na kampuni kubwa za teknolojia. Kwa niaba ya wazazi wa Australia, tutasimama kidete," alisema.

    Kesi hiyo imewasilishwa katika Mahakama Kuu siku ya Jumatano kwa mujibu wa Kundi la Digital Freedom (DFP)

    Vijana hutegemea mitandao ya kijamii kwa habari na urafiki, na marufuku inaweza kuumiza watoto kama vile wenye ulemavu, jamii za wachache, watoto wa mashambani na wa vijijini na LGBTIQ+ - limesema kundi hilo kwenye tovuti yao.

    Hatua nyingine za kuboresha usalama mtandaoni zinapaswa kutumika badala yake, kundi hilo limebainisha.

    Ingawa inapingwa na makampuni ya teknolojia, marufuku hiyo inaungwa mkono na watu wazima wengi wa Australia, kulingana na kura za maoni.

    Pia unaweza kusoma:

  9. Hamas yarudisha mwili mwingine wa mateka wa Israel

    s

    Chanzo cha picha, Anadolu via Getty Images

    Maelezo ya picha, Wanachama wa kundi la Jihad ya Kiislamu la Palestina wakitafuta mwili wa mateka katikati mwa Gaza siku ya Ijumaa.

    Israel imethibitisha kuwa Hamas na kundi la Palestina Islamic Jihad (PIJ) wamekabidhi mwili wa mateka wa Israel Dror Or siku ya Jumanne.

    Ofisi ya Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu ilisema serikali yake "inahuzunika na familia ya Or" kufuatia kukamilika kwa uchunguzi wa kisayansi wa mwili huo na kuthibitisha utambulisho wake.

    Imesisitiza kuwa Israel inafanya kazi "bila kuchoka" kuwarejesha nyumbani mateka wawili wa mwisho waliokufa ambao bado wako Gaza na kuitaka Hamas kutekeleza ahadi zake za kukabidhi mabaki yao chini ya makubaliano ya kusitisha mapigano Gaza.

    Mwili wa Or ulikabidhiwa kwa Msalaba Mwekundu baada ya PIJ na Hamas kutangaza kuwa ulikuwa umepatikana katikati mwa Gaza siku ya Jumatatu.

    Kulingana na IDF, baba huyo wa watoto watatu mwenye umri wa miaka 48 aliuawa na PIJ nyumbani kwake huko Kibbutz Be'eri wakati wa shambulio lililoongozwa na Hamas kusini mwa Israel tarehe 7 Oktoba 2023. Mwili wake ulitekwa nyara na kupelekwa Gaza kama mateka.

    Mke wa Bw Or, Yonat, pia aliuawa wakati wa shambulio hilo, huku watoto wao wawili, Noam na Alma, wakitekwa nyara wakiwa hai. Walishikiliwa mateka huko Gaza hadi Novemba 2023, walipoachiliwa kama sehemu ya makubaliano ya kusitisha mapigano ya wiki moja.

    Hii ni awamu ya kwanza ya makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyosimamiwa na Marekani, ambayo yalianza kutekelezwa tarehe 10 Oktoba, Hamas ilikubali kuwarejesha mateka 20 wa Israel walio hai na miili ya mateka 28 waliokufa wa Israel na raia wa kigeni ambao bado wako Gaza.

    Mateka wote walio hai waliachiliwa huru tarehe 13 Oktoba badala ya wafungwa 250 wa Kipalestina na 1,718 wanaoshikiliwa kuachiliwa.

    Hadi sasa, mabaki ya mateka raia 23 wa Israel wamekabidhiwa, pamoja na wale wa mateka watatu raia wa kigeni - mmoja wao akiwa Thai, mmoja wa Nepal na mmoja Mtanzania.

    Kwa kubadilishana, Israel imekabidhi miili ya Wapalestina 330 waliouawa wakati wa vita. Inapaswa kukabidhi miili mingine 15 kama malipo ya mabaki ya Bw Or.

    Mmoja wa mateka waliobaki waliokufa ni Israel - Ran Gvili, 24 - na mwingine ni Thai - Suthisak Rintalak, 43.

    Mateka wawili waliouawa bado wako Gaza walikuwa miongoni mwa watu 251 waliotekwa nyara na Hamas na washirika wake tarehe 7 Oktoba 2023, wakati watu wengine wapatao 1,200 waliuawa.

    Israel ilijibu shambulio hilo kwa kuanzisha kampeni ya kijeshi huko Gaza, ambapo zaidi ya watu 69,770 wameuawa, kulingana na wizara ya afya ya eneo hilo inayoendeshwa na Hamas.

  10. 17 wamefariki baada ya moto kuteketeza ghorofa Hong Kong

    sd

    Chanzo cha picha, Reuters

    Takriban watu 17 wameripotiwa kufariki baada ya moto kuteketeza majengo mengi ya makazi huko Hong Kong.

    Picha zinaonyesha miali ya moto na moshi ukifuka kutoka kwenye ghorofa hizo, ambapo watu kadhaa pia wanaaminika kuwa wamenasa.

    Moto huo katika eneo la Wang Fuk ulizuka usiku kwa saa za huko, kulingana na taarifa kutoka serikali ya Hong Kong.

    Moto huo ulianza katika majumba ya Wang Fuk katika wilaya ya Tai Po kaskazini mwa Hong Kong siku ya Jumatano.

    Wazima moto ni miongoni mwa wale ambao wamejeruhiwa walipokuwa wakijaribu kuzima moto huo.

    Pia unaweza kusoma:

  11. China inaongeza maandalizi ya kijeshi kutwaa kisiwa hichi kwa nguvu, Taiwan inasema

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Taiwan Lai Ching-te ameonya kuwa China inazidisha maandalizi yake ya kijeshi ili kutwaa kisiwa hicho kwa nguvu.

    Alisema serikali yake imetenga dola bilioni 40 za ziada kwa ajili ya ulinzi dhidi ya China ili kuonyesha azma yake ya kulinda maslahi yake.

    Rais wa Taiwan alisema bajeti itatumika zaidi katika utengenezaji wa ndege zisizo na rubani, makombora na mifumo ya ulinzi.

    Bw. Lai alisema "hali hatari zaidi" sio hatua ya kijeshi yenyewe, lakini kupoteza nia ya kupinga hatua hiyo.

    Rais wa Taiwan alisema kukubali kwa sababu ya shinikizo na vitisho "kutasababisha vita tu".

    Taiwan hufanya mazoezi ya kila mwaka ili kukabiliana na uwezekano wa uvamizi wa China, unaojulikana kama mazoezi ya ‘Han Kuang’.

    Katika siku za hivi karibuni, China ilisema kuwa itachukua hatua dhidi ya uingiliaji wowote wa nchi za kigeni katika suala la Taiwan na kuonya kwamba ina nia na uwezo wa kutetea "uadilifu wa eneo lake".

    China inaichukulia Taiwan kuwa ni sehemu ya eneo lake na haijaondoa uwezekano wa matumizi ya nguvu kulirejesha.

    Pia unaweza kusoma:

  12. Bunge Italia lapitisha kwa kauli moja mswada wa mauaji ya mwanamke kuwa uhalifu

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Wabunge nchini Italia wamepiga kura kwa kauli moja kutambulisha uhalifu wa mauaji ya wanawake - mauaji ya mwanamke, yanayochochewa na jinsia - kama sheria inayojisimamia ambayo hukumu yake itakuwa kifungo cha maisha.

    Katika hatua ya kuashiria jambo fulani, mswada huo uliidhinishwa siku iliyowekwa kwa ajili ya kutokomeza unyanyasaji dhidi ya wanawake duniani kote.

    Wazo la kutunga sheria juu ya mauaji ya wanawake lilikuwa limejadiliwa nchini Italia hapo awali lakini mauaji ya Giulia Cecchettin na mpenzi wake wa zamani ni tukio lililoshtua nchi na kuchochea kuchukuliwa kwa hatua hiyo.

    Mwishoni mwa Novemba 2022, mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 22 aliuawa kwa kuchomwa kisu na Filippo Turetta, ambaye kisha aliufunga mwili wake kwenye mifuko na kuutupa kando ya ziwa.

    Pia unaweza kusoma:

  13. Mama ahukumiwa kifungo cha maisha jela kwa kuua watoto wake New Zealand

    .

    Chanzo cha picha, TVNZ

    Mama mmoja New Zealand aliyewaua watoto wake wawili na kuficha miili yao kwenye masanduku amehukumiwa kifungo cha maisha jela.

    Hakyung Lee, ambaye alipatikana na hatia mnamo mwezi Septemba ya mauaji ya kushtua ya Yuna Jo mwenye umri wa miaka minane na Minu Jo mwenye umri wa miaka sita, inabidi akae gerezani kwa angalau miaka 17 kabla ya kustahiki msamaha.

    Lee, 45, alidai kwamba alikuwa mwendawazimu wakati wa mauaji hayo mnamo mwaka 2018, ambayo yalitokea mara tu baada ya mumewe kufariki. Jaji wa Mahakama Kuu Geoffrey Venning alisema afya ya akili ya Lee ilichangia katika kesi hiyo, lakini matendo yake yalipangwa.

    Mabaki ya watoto hao yaligunduliwa tu mnamo mwaka 2022 na wanandoa ambao walishinda mnada.

    Baada ya mauaji hayo, Lee alibadilisha jina lake na kuondoka New Zealand. Alikamatwa nchini Korea Kusini - alikozaliwa - Septemba mwaka 2022, na kurejeshwa New Zealand baadaye mwaka huo.

  14. Mjumbe wa bodi BBC aliyejizulu amtupia lawama Mwenyekiti wa bodi

    .

    Mjumbe wa zamani wa Bodi ya BBC, Shumeet Banerji, ambaye alijiuzulu wiki iliyopita, amekupitia barua yake ya kujiuzulu na BBC News, amefafanua kwa undani matukio yaliyosababisha kuondoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa BBC na Mkurugenzi Mtendaji wa habari. Banerji amekosoa namna mgogoro wake ulivyoghughulikiwa na Mwenyekiti wa bodi

    Shumeet Banerji alijiuzulu siku ya Ijumaa, akitaja "masuala ya utawala" lakini sababu kamili hazijajulikana hadi sasa.

    Katika barua yake, alisema kiongozi wa kitengo cha habari Deborah Turness aliambiwa kwamba "wajumbe wengi wa bodi hahaakua na imani naye".

    Lakini, Banerji aliandika, "hakuitwa kwenye kikao chochote ambacho suala la umuhimu kama hilo lilikuwa linajadiliwa".

    Maelezo ya barua hiyo yanajitokeza siku moja baada ya mwenyekiti wa bodi wa shirika hilo, Samir Shah, kuiambia kamati ya bunge kwamba anaamini kuwa kulikuwa na mawasiliano na Banerji, na wawili hao walikuwa na mazungumzo ya "simu ya dakika 26".

    Banerji aliiambia BBC News siku ya Jumanne kuwa, alikuwa amefuatilia majadiliano kwenye kamati hatua kwa hatua.

    Aliongeza: "Barua yangu ya kujiuzulu inaweza kufafanua sababu zangu za kujiuzulu. Inaweza pia kuarifu juu ya taarifa potofu ambazo zinaweza kutokea kwa wanakamati na watazamaji."

    Kujiuzulu kwa Davie na Turness kulitokana na kipindi cha Panorama kilichoripoti sehemu za hotuba ya Rais wa Marekani mwaka 2021, Donald Trump, iliyohaririwa kwa namna imeleta tafsiri tofauti na Trump kutishia kufungua mashtaka.

    Mgogoro huo ulizuka baada ya kumbukumbu iliyofichuliwa kweye bodi iliyoandikwa na mshauri wa zamani wa nje, Michael Prescott.

    Tangu wakati huo, mashaka yameibuka baadhi ya maeneo kuhusu jinsi bodi ya BBC inavyofanya kazi. Bodi hiyo ina jukumu la kusimamia na kupanga mikakati ya shirika.

    Katika barua yake, Banerji aliandika: "Siwezi kuonekana kama mshiriki katika uamuzi wa bodi ambao sikushirikishwa au ambao, kwa mtazamo wangu, haukuwa na mjadala wa kutosha."

    Jumatatu, Shah aliulizwa moja kwa moja na wabunge kuhusu kujiuzulu kwa Banerji na akakataa madai yake kwamba hakushirikishwa kuhusu matukio yaliyopelekea kujiuzulu kwa Turness na Davie.

    "Nasikitika na kushangazwa na kile anachosema," Shah alijibu mbele ya kamati hiyo, akisema: "Nachoweza kusema alishirikishwa."

    Hata hivyo, barua ya kujiuzulu ya Banerji inasema tofauti. Aliandika kuwa mikutano miwili ya bodi ilifanyika kujadili mgogoro katika shirika baada ya kumbukumbu ya Prescott kufichuliwa.

    Alishindwa kuhudhuria kikao cha kwanza, lakini katika kikao cha pili alishangazwa kujua kuwa Turness tayari alikuwa amejulishwa kuwa "wajumbe wa bodi wengi hawakuwa na imani naye".

    Soma zaidi:

  15. Umaarufu unapunguza miaka ya kuishi kwa wanamuziki, utafiti umegundua

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Umaarufu unaweza kupunguza maisha ya mwanamuziki kama vile kuvuta sigara mara kwa mara, utafiti mpya umegundua, baada ya kulinganisha data kati ya waimbaji maarufu na wasanii wasiojulikana sana.

    Umaarufu unaweza kufupisha maisha kwa miaka 4.6, kulingana na utafiti uliochapishwa katika Jarida la Epidemiology & Community Health.

    Kutalii, uigizaji na mitindo ya maisha ya rock'n'roll hapo awali ulibainika kupunguza miaka ya kuishi kwa wanamuziki.

    Utafiti mpya unaonyesha uhusiano wa moja kwa moja kati ya umaarufu na kifo kwa mara ya kwanza.

    Watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Witten Herdecke chenye makao yake huko Witten, Ujerumani, walichunguza data ya waimbaji 648, nusu yao wakiitwa mashuhuri na nusu nyingine sio maarufu sana. Hizi ni pamoja na mchanganyiko wa wasanii wa kujitegemea, waimbaji wanaoongoza bendi na wale wa nyuma ya bendi.

    Nyota maarufu walichaguliwa kutoka kwa wasanii 2,000 bora wa Wakati Wote, orodha iliyokusanywa na tovuti ya Muziki Unaovuma.

    The Beatles, Bob Dylan, na Rolling Stones, David Bowie, na Bruce Springstein wanatoa majina matano bora yanayotambulika zaidi kwenye tovuti.

    Wasomi walilinganisha kila mwimbaji maarufu na asiyejulikana sana, aliyeoanishwa kulingana na sifa zao kama vile jinsia, utaifa na aina ya muziki.

    Waligundua kuwa waimbaji mashuhuri waliishi hadi umri wa wastani wa 75 huku waimbaji wasio maarufu waliishi hadi umri wa miaka 79.

    "Hatari inayoongezeka ya kifo inayohusishwa na umaarufu inalinganishwa na hatari zingine za kiafya zinazojulikana kama vile kuvuta sigara mara kwa mara," waandishi waliandika.

    Kwa kuondoa umaarufu kama kipengele cha hatari, utafiti unaonyesha kupata umaarufu kunaweza kuwa "mabadiliko" katika kuleta wasiwasi mkubwa wa kiafya.

    Wasanii wa kujitegemea pia walikuwa katika hatari kubwa ya kifo, utafiti uligundua, ikilinganishwa na waimbaji ambao wangeweza kugeuka kuwa wa bendi kwa kuzingatia "kihisia na vitendo".

    Kupoteza faragha, uchunguzi mkali wa umma, na shinikizo la utendakazi vyote ni sababu zinazochangia, ingawa utafiti unabainisha kuwa hauhusiani kabisa.

    "Kuwa maarufu ni jambo muhimu linaloathiri maisha marefu na inasisitiza hitaji la hatua zinazolengwa ili kupunguza athari zake mbaya kwa maisha marefu."

    Utafiti huo hata hivyo ulikuwa na mwelekeo wa kijinsia, 83.5% wanaume hadi 16.5% wanawake.

    Pia unaweza kusoma:

  16. Bolsonaro kuanza kutumikia kifungo cha miaka 27 jela kwa njama ya mapinduzi

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Mahakama ya Juu Zaidi nchini Brazil imeamuru kuwa rais wa zamani wa mrengo wa kulia Jair Bolsonaro aanze kutumikia kifungo chake cha miaka 27 na miezi mitatu kwa kupanga mapinduzi baada ya kushindwa katika uchaguzi uliopita.

    Jaji Alexandre de Moraes siku ya Jumanne aliamua kwamba kesi hiyo ilikuwa imefikia uamuzi wake wa mwisho na kwamba hakuna rufaa zaidi inayowezekana kuwasilishwa.

    Bolsonaro, 70, alipatikana na hatia ya kuongoza njama iliyolenga kumuweka madarakani baada ya kushindwa katika uchaguzi wa 2022 na mpinzani wake wa mrengo wa kushoto, Luiz Inacio Lula da Silva.

    Ataanza kutumikia kifungo chake katika gereza la serikali kuu la polisi katika mji mkuu, Brasilia, ambako amezuiliwa tangu Jumamosi baada ya kuonekana kuwa katika hatari ya kutoroka na kuondolewa kizuizi cha nyumbani.

    Pia unaweza kusoma:

  17. Wanafunzi 24 wa Nigeria waliotekwa nyara waachiliwa huru

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Watoto wa shule 24 waliotekwa nyara katika jimbo la magharibi la Kebbi wiki iliyopita wameachiliwa huru, kulingana na mamlaka ya Nigeria.

    Katika taarifa yake, Rais wa Nigeria Bola Ahmed Tinubu alikaribisha kuachiliwa kwa wanafunzi 24 wa shule waliotekwa na watu wenye silaha Jumatatu iliyopita.

    Aliahidi kuimarisha usalama katika maeneo yaliyo hatarini kuzuia utekaji nyara zaidi.

    Serikali ya Nigeria imekuwa ikikosolewa pakubwa kwa kushindwa kuimarisha hali ya usalama.

    Msemaji wa haki za binadamu wa UN alilaani kutekwa nyara kwa watoto zaidi ya 300 kutoka shule ya Katoliki katika jimbo la Niger Ijumaa iliyopita, akitoa wito wahusika kuwajibishwa.

    Utekaji nyara ni sehemu ya wimbi jipya la utekaji nyara wa watu wengi kaskazini na kati Nigeria.

    Kumekuwa na ukosoaji kama huo kutoka kwa wanaharakati, mashirika ya Kikristo, na Marekani.

    Mapema mwezi huu, Rais Donald Trump alitishia kuchukua hatua za kijeshi, akishutumu viongozi wa Nigeria kwa kushindwa kuwalinda Wakristo kutokana na mashambulio kutoka kwa wanamgambo wa Kiisilamu - kitu ambacho serikali inakanusha vikali.

    Wachambuzi wanasema Wakristo na Waislamu wamekuwa waathiriwa wa matukio ya utekaji nyara.

    Pia unaweza kusoma:

  18. Hatua ya Trump kupunguza misaada ya kigeni imeua watu na kuwaacha mamilioni bila dawa - UNAIDS

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Umoja wa Mataifa imesema juhudi za kimataifa za kupambana na ukimwi zimepitia hali ngumu kutokana na kupunguzwa kwa ufadhili kimataifa.

    Nchi maskini na zenye raia wa kipato cha kati ndizo zimeathiriwa zaidi.

    Mkurugenzi wa shirika la kimataifa la Umoja wa Mataifa la kupambana na ukimwi UNAIDS Winnie Winnie Byanyima amezungumza juu ya kupunguzwa kwa kiwango kikubwa cha ufadhili kulikotangazwa na Rais wa Marekani Donald Trump baada ya kushinda uchaguzi na kurejea madarakani.

    "Kukosa fedha kwa muda mrefu na hatari kubwa zinazokabili mapambano ya kimataifa ya UKIMWI zina athari kubwa na za kudumu juu ya afya na ustawi wa mamilioni ya watu ulimwenguni pote", shirika la UNAIDS lilisema Jumanne katika ripoti iliyoitwa "Kushinda Msukosuko".

    "Idadi isiyo julikana ya watu wamefariki dunia kutokana na UKIMWI na milioni 2.5 wamepoteza ufikiaji wa dawa ya kukinga," Ripoti hiyo iliongeza.

    Nchi nyingine pia zimepunguza msaada kwa kiasi kikubwa na kusababisha hatari ya kusambaratika kwa huduma za kuzuia maambukizi ya HIV, hali ambayo inaweza kusababisha ongezeko la maambukizi.

    Winnie Byanyima alisema ahirika hilo linashirikiana na takriban nchi 30 kuboresha ufadhili wa ndani ili kuondokana na utegemezi wa wafadhili wa kimataifa.

    Lakini alisema pengo la ufadhili haliwezi kuzibwa mara moja, na changamoto kubwa bado zipo.

    UNAIDS inasema watu milioni 40.8 duniani kote wanaishi na VVU, huku maambukizi mapya milioni 1.3 yakiripotiwa mwaka 2024.

    Soma zaidi:

  19. Ukraine yasema 'imefikia maelewano' na Marekani juu ya mpango wa amani

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Ukraine imesema "maelewano ya pamoja" yamefikiwa na Marekani kuhusu makubaliano ya amani yenye lengo la kumaliza vita na Urusi.

    Pendekezo hilo linatokana na mpango wenye vipengele 28 uliowasilishwa kwa Kyiv na Marekani wiki iliyopita, ambao maafisa wa Marekani na Ukraine waliufanyia kazi wakati wa mazungumzo ya mwishoni mwa wiki huko Geneva.

    Katika chapisho kwenye mtandao wa kijamii, Rais wa Marekani Donald Trump alisema mpango wa awali "umefanyiwa marekebisho, na maoni ya ziada kuzingatiwa kutoka pande zote mbili".

    Aliongeza: "Nimemwagiza Mjumbe wangu Maalum Steve Witkoff akutane na Rais Putin huko Moscow na, wakati huo huo, Waziri wa Jeshi Dan Driscoll atakutana na Waukraine."

    Mkuu wa wafanyikazi wa Rais Zelensky alisema anatarajia Driscoll kuzuru Kyiv wiki hii.

    Soma zaidi:

  20. Hujambo. Karibu katika matangazo ya leo ikiwa ni tarehe 26/11/2025.