Maandamano Kenya 'yavamiwa na wahalifu'

Maandamano dhidi ya serikali nchini Kenya yamegeuka kuwa ya vurugu huku wahalifu wakiyateka maandamano hayo.

Muhtasari

  • Idadi ya waliofariki katika maandamano ya Kenya yafikia 39 - Tume ya Haki za Kibinadamu ya Kenya
  • Mtu mmoja afariki dunia huku kimbuga Beryl kikipiga eneo la Caribbean
  • Jumanne nyingine ya maandamano Kenya licha ya serikali kuahidi kupunguza matumizi ya fedha
  • Hali ya wasiwasi yaendelea kushuhudiwa kati ya Somalia na Ethiopia
  • Ndege yaelekezwa Brazil baada ya ‘msukosuko mkali’ kujeruhi 30
  • Euro 2024: Ureno na Ufaransa zafuzu kwa robo fainali ya Euro
  • Biden asema uamuzi juu ya Trump unadhoofisha utawala wa sheria
  • Israel yawaamuru Wapalestina kuondoka eneo la kusini mwa Gaza baada ya mashambulizi ya roketi

Moja kwa moja

Asha Juma

  1. Habari za hivi punde, Maandamano Kenya: Afisi ya jinai yatoa video za wahalifu wakati wa Maandamano

    Afisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) imetoa onyo kali kwa vyombo vya uhalifu vinavyotumia maandamano ya nchi nzima dhidi ya serikali kama kisingizio cha kufanya uhalifu.

    Katika taarifa kwenye X siku ya Jumanne, DCI ilichapisha kanda za video zikionyesha wizi huo wa mchana, zikiangazia magenge ya wahalifu waliojihami wanaoendeleza uhalifu huo.

    "Maafisa wa afisi hiyo sasa wameagizwa kuwafuata wafuasi wa magenge waliorekodiwa na wananchi wanaohusika wakiwaibia Wakenya wasio na hatia barabarani, huku wakichukua fursa ya maandamano yanayoendelea," ilisema afisi ya DCI.

    Wakati huohuo Mfanyabiashara mmoja mjini Mombasa aliyeripotiwa kuwatimua waandamanaji katika eneo la Ganjoni wakati wa maandamano yanayoendelea dhidi ya serikali amekamatwa.

    Afisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), katika taarifa iliyotolewa Jumanne, imesema mmiliki wa Hoteli moja mjini Mombasa aliwapiga risasi na kuwajeruhi watu wawili mwendo wa mchana.

    Mfanyabiashara huyo alikuwa akijaribu kulinda biashara zake dhidi ya waandamanaji

    Afisi ya DCI imesema kuwa mtu huyo kwa sasa anazuiliwa na maafisa wa polisi.

  2. Maandamano Kenya 'yavamiwa na wahalifu'

    Maandamano

    Maandamano dhidi ya serikali nchini Kenya yamegeuka kuwa ya vurugu huku wahalifu wakiteka nyara maandamano hayo.

    Waandishi wa BBC wameshuhudia uporaji na uharibifu wa mali katika viunga vya Nairobi na katikati mwa jiji.

    Mwanaharakati Boniface Mwangi na wengine kadhaa wamewataka vijana (GenZ,) kurudi nyumbani.

    Mjini Mombasa, watu wawili wanadaiwa kuuawa na mwanaume anayedaiwa kuwa mfanyabiashara akitetea mali yake dhidi ya waporaji.

    Rais Ruto alitupilia mbali mipango mipya ya ushuru, lakini maandamano yanaendelea kupinga ukatili wa polisi na uongozi wake.

    Polisi walitumia gesi ya kutoa machozi na maji ya kuwasha jijini Nairobi, huku maandamano madogo yakiendelea Mombasa na Kisumu.

    Unaweza pia kusoma;

  3. Usalama Msumbiji: Rais Nyusi azishukuru Tanzania, SADC,

    Rais wa Msumbiji, Filipe Nyusi na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan

    Chanzo cha picha, Ikulu Tanzania

    Rais wa Msumbiji, Filipe Nyusi ameishukuru Tanzania pamoja na ujumbe wa kulinda amani Msumbiji SAMIM kutoka nchi wanachama wa jumuiya ya maendeleo kusini mwa Afrika SADC, kwa kusaidia kurejesha amani nchini mwake dhidi ya ugaidi ulioibuka mwaka 2021.

    Amewaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Tanzania wakati wa ziara yake ya siku tatu nchini humo kuwa imefanyika kazi kubwa kurejesha amani kwani hali ilikuwa mbaya wakati ugaidi ulipoibuka.

    “Napenda kutumia fursa hii kwa niaba ya watu wa Msumbiji kuishukuru Tanzania na SAMIM, hawa watu hawana fedha lakini wanajibana kutusaidia. Tunakumbuka mwaka 2021 hali ya ugaidi ilivyokuwa mbaya, lakini kwa usaidizi wa SAMIM kuna matokeo mazuri, watu wamerejea katika shughuli zao. Vita hivi ni vigumu sana kwa sababu wapiganaji wanahamahama, tunaishukuru sana Tanzania na wenzetu wa Rwanda” alibainisha Rais Nyusi aliyekuwa kizungumza kwa lugha ya Kireno huku mkalimani akitafsiri.

    Kiongozi huyo anayemaliza muda wake wa vipindi viwili vya jumla ya miaka 10 tangu alipochaguliwa mwaka 2014, amesema waafrika wanapaswa kuleta majibu ya matatizo yao huku akisisitiza kuwa watu wa Msumbiji hawatausahau mchango wa Tanzania wakati wa mapambano ya kupigania uhuru ambayo yalianzia Kongwa mkoani Dodoma katikati mwa nchi hiyo.

    “Kizazi cha sasa kinapaswa kuelewa mapambano ya wakati huo na hata ya sasa” alisisitiza.

    Rais Samia Suluhu Hassan pia amelizungumzia suala la usalama katika maeneo ya mpaka wa Tanzania na Msumbiji akisema kuna changamoto ya mpaka baina ya nchi mbili hizo kuwa mrefu sana hivyo kuwepo umuhimu wa kushirikiana kukabiliana na uharamia.

    Rais wa Msumbiji, Filipe Nyusi na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan

    Chanzo cha picha, Ikulu Tanzania

    Kuhusu biashara na uwekezaji, Rais Samia amesema kuna umuhimu wa kuimarisha eneo hilo kwani bado lipo katika kiwango cha chini.

    “Kwa hadhi tuliyo nayo katika ushirikiano wa kisiasa, ushirikiano wa kibiashara bado upo chini. Tumekubaliana kuanzisha kituo kimoja cha forodha kule Mtambaswala kitakachohamasisha biashara. Mwaka juzi 2022 biashara ya Tanzania na Msumbiji ilikuwa ya thamani ya milioni 57.8 dola (za Marekani) lakini mwaka jana (2023) tumeshuka kwa hiyo tumekubaliana kuangalia ni sababu gani labda usalama ulizorota bishara zilikuwa hazipitiki, vile vichochoro wanamopita kufanya boashara tulifunga na inawezekana baadhi ya miamala inayofanyika kibiashara haipatikani rasmi, kwa hiyo mwaka jana ilikuwa dola milioni 20.1, kwa hiyo hapa imetushtua sote na tumesema tupangalie vizuri. Lakini kwenye uwekezaji, nchini Msumbiji kuna wawekezaji wawili wa Msumbiji ambão wamewaajiri watanzania 650 na huko Msumbiji kuna wawekezaji wa Tanzania kampuni 16 hivyo huko kuna ajira zaidi na uwekezaji ni mkubwa zaidi” alisisitiza.

    Viongozi hao pia wamekubaliana kushirikiana katika kuendeleza na kuimarisha uchumi wa bluu (bahari) na sekta ndogo ya gesi ikizingatiwa kuwa Msumbuji ina hifadhi ya gesi iliyothibishwa futi za ujazo trilioni 100 wakati Tanzania ina futi za ujazo trilioni 57. Maeneo mengine ni nguvu za umeme, miundombinu ya barabara, anga na reli pamoja na kuunda umoja katika mazao ya kilimo Afrika hasusan Korosho ili kupambana kupata masoko bora na bei nzuri.

    Rais Nyusi anatarajiwa kuwa mgeni rasmi wakati wa ufunguzi wa maonesho ya kimataifa ya kibiashara maarufu sabasaba.

    Unaweza kusoma;

  4. Maandamano ya kuipinga serikali Kenya: Katika picha

    Muandamanaji
    Gesi ya kutoa machozi
    Waandamanaji
    Vijana waandamanaji
    Muandamanaji
    Muandamanaji
    Askari wakiwa wameshika doria
    Muandamanaji
    Waandamanaji
    Askari wakiwa wamemkamata muandamanaji
  5. Waandamanaji nchini Kenya waweka majeneza barabarani

    Maandamano ya kuipinga serikali yametikisa miji mikubwa nchini Kenya, huku vijana waandamanaji wakieleza kutoridhishwa na serikali ya Kenya Kwanza.

    Saa 11:00 asubuhi, waandamanaji waliingia barabarani katika eneo la katikati mwa jiji la Nairobi wakiwa wamejihami kwa mabango na kuimba nyimbo za kupinga serikali.

  6. Mabomu ya machozi yarushwa dhidi ya waandamanaji wanaoipinga serikali Kenya

    Moshi wa vitoa machozi unavyoonekana katikati mwa jiji la Nairobi

    Chanzo cha picha, Reuters

    Polisi wa Kenya wamefyatua gesi ya kutoa machozi katika mji mkuu Nairobi kutawanya maandamano ya kuipinga serikali.

    Katikati ya jiji biashara nyingi zimefungwa.

    Waandamanaji pia wameingia katika mitaa ya miji mingine ikiwemo Mombasa na Kisumu.

    Mashirika ya kutetea haki za binadamu yanasema tangu maandamano ya kupinga muswada wenye utata wa fedha kuanza wiki mbili zilizopita watu 39 wameuawa na vikosi vya usalama.

    Rais William Ruto tangu wakati huo ametupilia mbali mapendekezo ya nyongeza ya ushuru, lakini maandamano yamebadilika na kuwa wito wa kujiuzulu na hasira juu ya ukatili wa polisi.

    Unaweza kusoma;

  7. Takribani watu 100 wapoteza maisha katika mkanyagano wakati wa hafla ya kidini ya India

    Waliojeruhiwa walifikishwa katika hospitali iliyo karibu

    Zaidi ya watu 100 wamepoteza maisha katika mkanyagano kwenye mkusanyiko wa kidini kaskazini mwa India, maafisa wamesema.

    Kisa hicho kilitokea katika satsang (tukio la kidini la Kihindu) katika wilaya ya Hathras katika jimbo la Uttar Pradesh, afisa mkuu wa polisi alisema.

    Waathirika hao ni pamoja na idadi kubwa ya wanawake na watoto alisema na kuongeza kuwa miili bado inaendelea kutambuliwa.

    Walionusurika wameelezea jinsi maafa hayo yalivyotokea walipokuwa wakijaribu kuondoka kwenye tukio katika kijiji cha Mughalgarhi.

    Msemaji wa afisa mkuu wa polisi huko Uttar Pradesh aliiambia BBC kwamba "itachukua saa kadhaa kutoa hesabu ya mwisho", lakini alithibitisha kuwa takribani 100 walikufa.

    Video iliyosambazwa na shirika la habari la PTI ilionesha majeruhi wakipelekwa hospitalini kwa matibabu.

    "Utaratibu wa uchunguzi wa maiti unaendelea na suala hilo linachunguzwa," afisa Satya Prakash katika wilaya jirani ya Etah alisema.

    Ajali huripotiwa mara kwa mara katika matukio ya kidini nchini India, huku umati mkubwa wa watu ukikusanyika.

    Mnamo mwaka wa 2018, karibu watu 60 walipoteza maisha baada ya gari moshi kugongana na umati wa watu waliokuwa wakitazama sherehe za Dusshera, tamasha la Kihindu.

    Mnamo mwaka wa 2013, mkanyagano katika tamasha la Wahindu katika jimbo la kati la Madhya Pradesh ulisababisha vifo vya watu 115.

  8. Biden asema uamuzi wa mahakama kuhusu Trump unadhoofisha utawala wa sheria

    Biden

    Joe Biden ameelezea kama "mfano wa hatari" uamuzi wa Mahakama ya Juu unaompa Rais wa zamani Donald Trump kingadhidi ya mashtaka ya jinai.

    Rais wa sasa wa Marekani alisema hukumu hiyo inadhoofisha "utawala wa sheria" na ilikuwa "udhalilishaji mbaya" kwa Wamarekani.

    Hapo awali, Trump alisifu uamuzi wa mahakama kama "ushindi mkubwa" kwa demokrasia.

    Majaji waligundua Jumatatu kwamba rais alikuwa na kinga ya "vitendo rasmi" lakini hakuwa salama kwa "vitendo visivyo rasmi", na walirejesha suala hilo kwa jaji wa mahakama.

    Hukumu hiyo itachelewesha zaidi kesi ya jinai dhidi ya Trump kwa madai ya kujaribu kupotosha matokeo ya uchaguzi wa 2020 ambayo yalimpa ushindi Bw Biden.

    Jaji anayesikiliza kesi hiyo lazima sasa aamue ni hatua gani zilitekelezwa katika nafasi ya Trump kama rais, ambayo inaweza kuchukua miezi kadhaa.

    Kesi yoyote haitawezekana kuanza kabla ya uchaguzi wa rais wa Novemba.

    Unaweza kusoma;

  9. Maandamano dhidi ya serikali yatikisa Nairobi, Mombasa, Kisumu, Kisii, Migori nchini Kenya

    Waandamanaji

    Maandamano ya kuipinga serikali yametikisa miji mikubwa nchini Kenya, huku vijana waandamanaji wakieleza kutoridhishwa na serikali ya Kenya Kwanza.

    Saa 11:00 asubuhi, waandamanaji waliingia barabarani katika eneo la katikati mwa jiji la Nairobi wakiwa wamejihami kwa mabango na kuimba nyimbo za kupinga serikali, Citizen imeripoti.

    Maafisa wa kukabiliana na ghasia walirusha vitoa machozi karibu na Archives na Moi Avenue ili kuwatawanya waandamanaji.

    Wakati huo huo, maandamano yalianza katika barabara ya Mombasa huku waandamanaji wakifunga barabara kuu ya Emali, na kusimamisha usafiri.

    Mjini Mombasa, vijana pia wameandamana hadi barabarani kwa wingi.

    Maandamano yalianza mapema Migori huku waandamanaji wakiwasha moto na kuweka vizuizi barabarani.

    Vijana waliokasirika waliendelea na nyimbo zao huku wakizuia usafiri. Huko Kisumu, waandamanaji walishiriki maandamano ya amani huku wakiandamana na mabango dhidi ya serikali ya Rais William Ruto.

    Sehemu ya waandamanaji pia ilichukua fursa hiyo kucheza mpira kando ya barabara huku polisi wakitazama. Huko Kisii, waandamanaji waliwasha moto barabarani, na hivyo kudumaza usafiri na kusababisha biashara kufungwa.

    Unaweza kusoma;

  10. Wapalestina wakimbia Khan Younis huku wanajeshi wa Israel wakishambulia kusini mwa Gaza

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Wapalestina wamekuwa wakikimbia maeneo ya mashariki mwa mji wa pili wa Gaza wa Khan Younis baada ya Israel kutoa maagizo ya kuhama.

    Usiku kucha, walioshuhudia waliripoti mashambulio mengi ya Israel ndani na karibu na mjia wa Khan Younis. Chanzo cha matibabu cha Red Crescent cha Palestina kimesema watu wanane wameuawa na zaidi ya 30 kujeruhiwa.

    Wagonjwa na wafanyikazi wa shirika hilo pia wamekuwa wakitoka hospitali ya Gaza ya Ulaya katika eneo hilo, kwa kuwa wizara ya afya inayoendeshwa na Hamas huko Gaza iliwaambia wahame.

    Jeshi la Israel halijatoa agizo la kuhamishwa kwa hospitali hiyo.

    Shirika hilo limeripotiwa kusaidia wagonjwa katika harakati za kuhamishiwa hospitali nyingine.

    Louise Waterridge, afisa wa shirika la Umoja wa Mataifa la wakimbizi wa Kipalestina (Unrwa) huko Gaza, aliuliza ni wapi watu wanaweza kwenda huku wakilazimika kuondoka makwao kwa mara nyingine tena.

    "Katika eneo hili, watu tayari walilazimishwa kunusurika katika majengo yaliyoharibiwa vibaya na ambayo si salama kimuundo baada ya operesheni ya jeshi la Rafah," alisema.

    Kikosi cha Ulinzi cha Israel (IDF) kilitoa taarifa kuhusu operesheni yake ya hivi punde huko Gaza, kikisema kinajibu baadhi ya makombora 20 yaliyorushwa kutoka eneo la Khan Yunis kuelekea Israel siku ya Jumatatu.

    Soma zaidi:

  11. Idadi ya waliofariki katika maandamano ya Kenya yafikia 39 - Tume ya Haki za Kibinadamu ya Kenya,

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu nchini Kenya (KNCHR) imesema idadi ya waliofariki dunia imefikia 39 huku 361 wakijeruhiwa tangu kuanza kwa maandamano ya kupinga mswada wa Fedha 2024 kote nchini humo.

    ‘’Uchunguzi wa maiti kwa wengi wa waathiriwa bado haujafanywa,’’ Tume hiyo imesema.

    Tume ya KNCHR pia imesema kumekuwa na taarifa za watu kutekwa nyara na kukamatwa kiholela.

    Kuna visa ‘’32 za upotevu wa kulazimishwa au kupotea bila kukusudia na 627 za kukamatwa kwa waandamanaji,’’kulingana na Tume hiyo.

    Baadhi ya watu wanasemekana kuwa mafichoni kutokana na vitisho dhidi ya maisha yao na watu wasiojulikana.

    Katika ripoti yake, Tume hiyo imeendelea kushtumu utumiaji wa nguvu kipita kiasi dhidi ya waandamanaji na wengineo kama wafanyakazi wa afya, waandishi wa habari na kwenye maeneo salama kama vile makanisa na vituo vya dharura vya matibabu.

    Serikali haijathibitisha idadi hiyo lakini Rais William Ruto siku ya Jumapili, Juni 30, wakati wa kikao na wanahabari, alisema kufikia wakati huo waliofariki walikuwa 19.

    Rais aliongeza kuwa maafisa wa polisi walitekeleza majukumu yao kwa njia huru wakati wa maandamano hayo.

    Kulingana na vyombo vya habari vya ndani tayari maandamano yameanza katika maeneo kama vile Mombasa licha ya Rais Ruto kutangaza Jumatano iliyopita kwamba hatatia saini Mswada tata wa Fedha kuwa sheria.

    Soma zaidi:

  12. Mtu mmoja afariki dunia huku kimbuga Beryl kikipiga eneo la Caribbean

    Maelezo ya video, Kimbunga Beryl chakumba Caribbean: upepo mkali na mvua kubwa

    Takriban mtu mmoja amefariki baada ya kimbunga Beryl kukumba nchi kadhaa za Caribbean.

    Maelfu ya watu wamesalia bila umeme au wanaishi katika makazi ya muda huko St Vincent na Grenadines, Grenada na St Lucia.

    Waziri mkuu wa St Vincent na Grenadines alithibitisha angalau mtu mmoja amefariki.

    Nchi nyingine zinaendelea kujizatiti kukabiliana na kimbunga Beryl kikielekea upande wa mashariki. Kimbunga hicho kinatarajiwa kuikumba Mexico mwishoni mwa wiki.

    Baada ya Kimbunga Beryl kufika kwenye Kisiwa cha Carriacou huko Grenada, ilionekana wazi kwamba sehemu kadhaa katika njia yake zilikuwa zimeathirika sana.

    Picha kwenye mitandao ya kijamii zilionyesha nyumba zikiwa bila paa na wakazi wakiokota vifusi ili kuokoa mali zao.

    Ralph Gonsalves alipendekeza kuwa kunaweza kuwa na vifo zaidi.

    Hapo awali, viwanja vya ndege na biashara zilifungwa na wakaazi wakahamishwa kutafuta makazi kwingineko wakati dhoruba inakaribia.

    Soma zaidi:

  13. Jumanne nyingine ya maandamano Kenya licha ya serikali kuahidi kupunguza matumizi ya fedha

    th

    Chanzo cha picha, Shutterstock

    Wanaharakati nchini Kenya wamewataka waandamanaji kujitokeza tena barabarani hii le Jumanne, huku wengi wakikataa ombi la Rais William Ruto la mazungumzo kufuatia uamuzi wake wa kuondoa mapendekezo ya nyongeza ya ushuru.

    Takriban watu 24 waliuawa katika makabiliano kati ya waandamanaji na polisi wiki iliyopita, wakati bunge lilipovamiwa kwa muda mfupi na kuchomwa moto.

    Maandamano hayo ambayo yameongozwa na vijana na kuandaliwa kwa kiasi kikubwa kwenye mitandao ya kijamii, awali yalichochewa na mswada wa fedha ulionuiwa kukusanya shilingi za Kenya bilioni 346 (dola bilioni 2.69) kupitia ushuru.

    Lakini matakwa ya waandamanaji wengi yameongezeka katika muda wa wiki mbili zilizopita na kujumuisha wito wa kupambana na ufisadi na kumtaka Ruto ang'atuke, madarakani jambo ambalo linawasilisha mzozo mkubwa zaidi katika utawala wake wa miaka miwili.

    Mahojiano ambayo Ruto aliyatoa Jumapili jioni ya runinga, ambapo alitetea zaidi vitendo vya polisi na serikali yake, yalionekana kuzidisha misimamo ya waandamanaji kurejea barabarani.

    Siku ya Jumatatu, wanaharakati walikuwa wakishiriki vipeperushi kwenye mitandao ya kijamii ambavyo viliwataka watu kujitokeza katikati mwa jiji la Nairobi. Wengi walichapisha jumbe kupitia hashitagi ya #OccupyCBDDTuesday.

    Harakati za waandamanaji hazina uongozi rasmi, na haikufahamika ni kwa kiwango gani watu wangeitikia wito huu baada ya makumi ya maelfu kujitokeza wiki iliyopita katika baadhi ya maandamano makubwa zaidi nchini humo .

    Katika majukwaa ya mitandao ya kijamii, wanaharakati wamekuwa wakijadili jinsi ya kudumisha kasi na shinikizo dhidi ya serikali baada ya kufaulu kuuzima mswada wa fedha

    Unaweza pia kusoma

  14. Hali ya wasiwasi yaendelea kushuhudiwa kati ya Somalia na Ethiopia

    .

    Chanzo cha picha, SOMALIA GOVERNMENT

    Rais wa Somalia Hassan Sheik Mohamud amesema hakuna dalili za Ethiopia kujiondoa kwenye makubaliano ya bandari yenye utata ambayo yalizua mvutano kati ya nchi hizo mbili.

    Rais alikuwa akizungumza baada ya wajumbe kutoka nchi hizo mbili za Pembe ya Afrika- wakiongozwa na mawaziri wao wa mambo ya nje- kufanya mazungumzo nchini Uturuki kwa lengo la kurekebisha uhusiano wao.

    Makubaliano yasiyo ya lazima ambayo ndio msingi wa mvutano wao yaliotiwa saini mwezi Januari kati ya Addis Ababa na jamhuri iliyojitangaza ya Somaliland- yamefungua njia kwa Ethiopia isiyo na bandari kuwa na kilomita 20 za ukanda wa pwani.

    Ethiopia kwa upande wake inaweza kutambua Somaliland inayochukuliwa na Mogadishu kama sehemu ya eneo lake kama nchi huru.

    Somalia inaona makubaliano hayo kama uchokozi.

    Hakuna mafanikio makubwa yaliyopatikana katika mazungumzo hayo ambayo yalikuwa ya kwanza tangu mpango huo kutangazwa.

    Lakini ukweli kwamba yalifanyika unaonekana kama maendeleo na nchi hizo mbili zimekubaliana kukutana tena mnamo mwezi Septemba.

    Kulingana na Sheik Mohammed mazungumzo hayo yaliombwa na Ethiopia, lakini majadiliano ya moja kwa moja hayakufanyika.

    Soma zaidi:

  15. Ndege yaelekezwa Brazil baada ya ‘msukosuko mkali’ kujeruhi 30

    .

    Chanzo cha picha, @pichipastoso via X

    Ndege iliyokumbwa na "msukosuko mkali" imetua kwa dharura nchini Brazil, huku watu 30 wakiripotiwa kujeruhiwa.

    Ndege ya Air Europa Boeing 787-9 Dreamliner ilikuwa ikisafiri kutoka Madrid kwenda Montevideo wakati tukio hilo la angani lilipotokea, shirika hilo la ndege lilisema.

    Ndege ya UX045 ilielekezwa kwenye uwanja wa ndege wa Natal kaskazini-mashariki mwa Brazil ikiwa njiani kuelekea mji mkuu wa Uruguay, kampuni hiyo ya Uhispania ilisema kwenye mtandao wa X, zamani ukijulikana kama Twitter.

    Iliongeza kuwa abiria ambao walipata majeraha "wanapokea uangalizi".

    Ndege hiyo, iliyokuwa na abiria 325, ilikumbwa na msukosuko kwenye bahari ya Atlantiki ilipokuwa karibu kufika pwani ya Brazil, msemaji wa Air Europa alisema.

    Ndege ilitua kama kawaida na ilikutana na kundi la ambulansi.

    Maafisa wa uwanja wa ndege walisema baadhi ya abiria walihitaji usaidizi wa kimatibabu na walipelekwa katika hospitali ya karibu.

    Timu ya madaktari wa eneo hilo iliambia vyombo vya habari vya Brazil kwamba walihudumia angalau abiria 30 wa mataifa mbalimbali na kwamba 10 kati yao walipelekwa hospitalini.

    Wagonjwa hao walikuwa wamegonga vichwa vyao wakati wa msukosuko huo na kupata majeraha ikiwa ni pamoja na kuvunjika sehemu ya fuvu na majeraha usoni, timu hiyo iliongeza.

    Tukio hilo linatokea wiki kadhaa baada ya ndege ya shirika la ndege la Singapore kukumbwa na msukosuko mkubwa nchini Myanmar, na kusababisha makumi ya majeruhi na kifo cha muingereza.

    Msukosuko mkali ni nadra lakini tafiti za hivi karibuni zimeonyesha kuwa mabadiliko ya hali ya hewa yanaweza kuongeza hatari ya hilo kutokea.

    Soma zaidi:

  16. Euro 2024: Ureno na Ufaransa zafuzu kwa robo fainali ya Euro

    th

    Chanzo cha picha, Rex Features

    Cristiano Ronaldo alibubujikwa machozi baada ya penalti yake kuokolewa katika muda wa ziada lakini Ureno bado walifuzu hadi robo fainali ya Euro 2024 kufuatia ushindi mkubwa 3-0 kupitia mikwaju ya penalti dhidi ya Slovenia.

    Nahodha huyo nyota wa Ureno alishuhudia penalti yake ikizuiwa na kipa wa Atletico Madrid, Jan Oblak na kufarijiwa na wachezaji wenzake, huku mashabiki wakiimba jina lake uwanjani .

    Lakini alipata ahueni na kufunga penalti ya kwanza kwa nchi yake kwenye mkwaju wa penalti - ambapo kipa Diogo Costa aliokoa mikwaju yote mitatu aliyokabili - kabla ya Bernardo Silva wa Manchester City kufunga mkwaju wa ushindi.

    Ronaldo alipambana usiku kucha akitafuta bao lake la kwanza kwenye Euro 2024.

    Kabla ya penalti yake kuelekezwa kwenye lango, alipoteza nafasi nzuri katika dakika ya mwisho ya muda wa kawaida, akipiga shuti iliyoelekea moja kwa moja hadi kwa Oblak, baada ya krosi zake nyingi kupaa juu ya kichwa chake katika dakika 120 za mchezo mkali.

    th

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Bao la kujifunga la Jan Vertonghen liliipeleka Ufaransa katika robo fainali ya Euro 2024 kwa kuishinda Ubelgiji bao moja kwa nunge .

    Mchezo ambao haukuwa na ubora na msisimko kwa muda wote ulionekana kupangiwa muda wa ziada, lakini shuti lililopigwa na mchezaji wa akiba Randal Kolo Muani lilimgonga Vertonghen na kuingia kimyani zikiwa zimesalia dakika tano kuhitimisha ushindi huo kwenye Uwanja wa Dusseldorf Arena.

    Ufaransa walikuwa wamepoteza nafasi nyingi kabla ya hapo kwani kwa mara nyingine tena kupungua makali kwa timu yao kuliwaangusha, na hata nahodha Kylian Mbappe aliweka juhudi lakini alipiga nje shuti nyingi.

  17. Biden asema uamuzi juu ya Trump unadhoofisha utawala wa sheria

    ,

    Chanzo cha picha, Reuters

    Rais Joe Biden wa Marekani ameelezea kama "mfano wa hatari" uamuzi wa Mahakama ya Juu Zaidi unaompa rais wa zamani Donald Trump kinga kwa kiasi fulani dhidi ya mashtaka ya jinai.

    Rais wa sasa wa Marekani alisema uamuzi huo unadhoofisha "utawala wa sheria" na ilikuwa "udhalilishaji mbaya" kwa Wamarekani.

    Hapo awali, Trump alisifu uamuzi wa mahakama kama "ushindi mkubwa" kwa demokrasia.

    Majaji walisema Jumatatu kwamba rais alikuwa na kinga ya "vitendo rasmi" lakini hakuwa salama kwa "vitendo visivyo rasmi", na walirejesha suala hilo kwa jaji wa mahakama.

    Hukumu hiyo itachelewesha zaidi kesi ya jinai dhidi ya Trump kwa madai ya kujaribu kuvuruga matokeo ya uchaguzi wa 2020 ambayo yalimpa ushindi Bw Biden.

    Jaji wa mahakama hiyo lazima sasa aamue ni hatua gani zilitekelezwa katika nafasi ya Trump kama rais, ambayo inaweza kuchukua miezi kadhaa. Kesi yoyote haitawezekana kuanza kabla ya uchaguzi wa rais wa Novemba.

    Katika taarifa yake kwa njia ya televisheni mwishoni mwa Jumatatu, Rais Biden alisema: "Taifa hili lilianzishwa kwa msingi wa kwamba hakuna wafalme Marekani. Kila mmoja wetu ni sawa mbele ya sheria. Hakuna aliye juu ya sheria. Hata rais wa Marekani.

    "Uamuzi wa leo [wa mahakama] kwa hakika unamaanisha kuwa hakuna kikomo kwa kile ambacho rais anaweza kufanya.

    "Mtu aliyetuma kundi hilo la watu katika Bunge la Marekani anakabiliwa na hatia ya uhalifu kwa kile kilichotokea siku hiyo. Watu wa Marekani wanastahili kupata jibu mahakamani kabla ya uchaguzi ujao.

    Bw Biden alikuwa akizungumzia Trump anayekabiliwa na kesi kwa madai ya kuhusika katika kuchochea ghasia hizo.

    Soma zaidi:

  18. Israel yawaamuru Wapalestina kuondoka eneo la kusini mwa Gaza baada ya mashambulizi ya roketi

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Jeshi la Israel limewaamuru Wapalestina kuondoka katika eneo kubwa la ardhi mashariki mwa mji wa Khan Younis, kusini mwa Gaza baada ya kurusha makombora kuelekea Israel.

    Watu katika eneo hilo kwanza walipokea jumbe za sauti zikiwaambia waondoke, kabla ya jeshi la Israel kutuma ujumbe kwa Kiarabu unaorudia onyo hilo kwenye mitandao ya kijamii.

    Walioshuhudia wanasema watu wengi tayari wanakimbia.

    Haya yanajiri baada ya takriban roketi 20 kurushwa katika shambulizi zito zaidi katika kipindi cha miezi kadhaa, huku idadi kubwa ikinaswa na nyingine zikitua katika maeneo ya wazi bila kuripotiwa majeraha yoyote.

    Kundi la Jihad la Kiislamu la Palestina (PIJ) lilisema limeanzisha mashambulizi hayo kujibu "uhalifu" wa Israel.

    Agizo la hivi punde la uhamishaji linashughulikia eneo karibu na hospitali ya Ulaya kusini-mashariki mwa Khan Younis.

    Wafanyakazi wameanza kuhamisha baadhi ya vifaa muhimu katika hospitali ya Nasser huko Khan Younis na baadhi ya wafanyakazi na wagonjwa pia wameondoka, ripoti za ndani zinasema.

    Kwingineko, mapigano makali yaliendelea kwa siku ya tano huko Shejaiya kaskazini mwa Gaza na mwanajeshi wa Israel aliuawa katika eneo la kusini la Rafah.

    Siku ya Jumapili, waziri mkuu wa Israel alisema wanajeshi wake walikuwa kwenye "mapigano makali" katika eneo lote la Palestina.

    Jeshi la Israel lilianzisha kampeni ya kuiangamiza Hamas kujibu shambulio ambalo halijawahi kushuhudiwa kusini mwa Israel tarehe 7 Oktoba, ambapo takriban watu 1,200 waliuawa na wengine 251 walichukuliwa mateka.

    Zaidi ya watu 37,900 wameuawa huko Gaza tangu wakati huo, wakiwemo 23 katika muda wa saa 24 zilizopita, kulingana na wizara ya afya ya eneo hilo inayoendeshwa na Hamas.

    Jumatatu asubuhi, ving'ora vilisikika katika jamii za Waisrael karibu na uzio wa mpaka wa Gaza, ambao wengi wao wamehamishwa tangu shambulio la Oktoba 7.

    Baraza la Mkoa wa Eshkol baadaye liliripoti kwamba roketi 18 zilirushwa kuelekea maeneo inakotawala, kulingana na gazeti la Jerusalem Post.

    Mengi yalitua katika maeneo ya wazi, lakini moja ilianguka "katika eneo la uzio wa Kibbutz Holit", lilisema.

    Roketi nyingine ilinaswa na mfumo wa ulinzi wa makombora wa Iron Dome, liliongeza.

  19. Hujambo na karibu katika matangazo yetu mubashara ikiwa ni tarehe 02/07/2024