Wakenya 18 waliohadaiwa kujiunga na kikosi cha Urusi warejea nyumbani

Waliorejea nchini Kenya kutoka Ukraine wengi wao wana umri wa miaka kati ya miaka 20 hadi 30

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Mariam Mjahid

  1. Ghana yapeleka askari wake kusaidia kuijenga upya Jamaica

    xcv

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Kimbunga Melissa, kilikumba Jamaica mwezi Oktoba 2025 ambapo takriban watu 32 walipoteza maisha

    Ghana imewapeleka wanajeshi 54 nchini Jamaica kusaidia jitihada za ujenzi upya baada ya uharibifu mkubwa uliosababishwa na kimbunga Melissa nchini humo.

    Wanajeshi hao watashiriki katika ukarabati wa barabara, makazi ya muda, na miundombinu muhimu ya umma iliyoharibiwa na kimbunga hicho.

    Askari hao wanatoka katika Kikosi cha 14 cha wahandisi wa Jeshi la Ghana.

    Ujumbe huu ni sehemu ya dhamira ya Ghana ya kuimarisha ushirikiano wa kikanda, kutoa msaada wa kibinadamu, na kuonyesha mshikamano na mataifa ya Carrebian yanayoathiriwa na majanga ya asili.

    Hatua hii iliungwa mkono na serikali ya Marekani, ambayo ilitoa ndege ya kijeshi ya mizigo aina ya C-17 kuwasafirisha wanajeshi wa Ghana pamoja na vifaa vyao hadi Kingston, Jamaica.

    “Taifa letu linaelewa uchungu wa majanga ya asili na safari ndefu ya kupona. Dhamira ya leo inaimarisha kujitolea kwa Ghana katika kutoa msaada wa kibinadamu, kurejesha na kujenga upya maeneo yaliyoathiriwa na majanga, pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kusini kwa Kusini, mshikamano wa Pan-Afrika na Afro- Caribbean,” alisema Rais Mahama.

    Serikali ya Ghana tayari imetuma misaada ya kibinadamu ikiwemo mchele, blanketi, magodoro, ndoo za plastiki, na dawa kwenda Jamaica, Cuba, na Sudan.

    Kimbunga Melissa, ambacho ni cha kiwango cha tano, kilikumba Jamaica mwezi Oktoba ambapo takriban watu 32 walipoteza maisha huku maelfu wakihitaji msaada wa chakula na huduma za msingi.

    Jamaica ipo katika eneo linalokumbwa mara kwa mara na vimbunga, na kwa miaka mingi imeathiriwa na dhoruba kali zilizoharibu makazi, hospitali, na miundombinu muhimu.

    Soma zaidi:

  2. Marekani yashutumiwa kuwatumia wafanyakazi haramu katika kituo cha maombi ya ukimbizi Afrika Kusini

    xcv

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Afrika Kusini imeishutumu Marekani kwa kutumia raia wa Kenya ambao hawakuwa na vibali vya kazi katika kituo kilichokuwa kinashughulikia maombi ya hadhi ya ukimbizi kutoka kwa Waafrika Kusini weupe.

    Wakenya saba walikamatwa baada ya taarifa za kijasusi kubaini kuwa watu hao “waliingia hivi karibuni Afrika Kusini kwa viza za utalii na kisha kuajiriwa kinyume cha sheria” katika kituo hicho, kwa mujibu wa taarifa ya Idara ya Mambo ya Ndani ya Afrika Kusini.

    BBC imeiomba Wizara ya mambo ya nje ya Marekani kutoa maoni kuhusu suala hilo.

    Ingawa Marekani inajaribu kupunguza kwa ujumla viwango vya uhamiaji, inasema kuwa wanachama wa jamii ya Waafrika weupe wa Afrika na nchini Afrika Kusini wanaweza kupata hifadhi ya ukimbizi kwa madai kuwa wanakabiliwa na mateso, madai ambayo serikali ya Afrika Kusini inayapinga vikali.

    Marekani imepunguza idadi ya wakimbizi kutoka kote ulimwenguni kila mwaka kutoka 125,000 hadi 7,500, lakini inasema itawapa kipaumbele Waafrikana, ambao wengi wao ni wazao wa walowezi wa Uholanzi na Ufaransa.

    Hili ni moja ya masuala ambayo yamesababisha kuzorota kwa kasi kwa uhusiano kati ya Afrika Kusini na utawala wa Trump.

    Afrika Kusini inasema raia wa Kenya waliokamatwa katika uvamizi wa Jumanne sasa watafukuzwa nchini na watapigwa marufuku kuingia nchini kwa miaka mitano.

    Hapo awali walikuwa wamenyimwa visa za kazi lakini walipatikana "wakifanya kazi licha ya kuwa na visa vya watalii pekee, jambo ambalo lilikiuka wazi masharti yao ya kuingia nchini", taarifa hiyo ilisema.

    Afrika Kusini pia ilionesha wasiwasi kwamba maafisa wa kigeni walionekana kushirikiana na wafanyakazi wasio na vibali na kusema imewasiliana na Marekani na Kenya ili kutatua suala hilo.

    Wizara ya mambo ya ndani ilisema uvamizi huo ulionesha dhamira ambayo Afrika Kusini ilishiriki "na Marekani katika kupambana na uhamiaji haramu na matumizi mabaya ya visa katika aina zake zote".

    Soma zaidi:

  3. Nigeria kujibu kwa njia za kidiplomasia vikwazo vipya vya wasafiri

    xcv

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Wizara ya mambo ya nje ya Nigeria inasema itajibu kwa kupitia diplomasia marufuku ya usafiri iliyowekwa na Marekani.

    Msemaji wa wizara hiyo, Alkasim Abdulkadir, aliiambia BBC kwamba Nigeria inapanga kuwashirikisha maafisa wa Marekani ili kuelewa vyema uamuzi huo na kupata suluhisho.

    "Wizara itaanza kuwashirikisha wenzao ili kuelewa suala hilo na kutafuta njia ya kulitatua"

    Nigeria ilikuwa na nafasi za ubalozi zilizo wazi tangu Rais Tinubu alipoingia madarakani mwaka wa 2023.

    Mwishoni mwa Novemba, aliteua mabalozi 32, na uchunguzi wa taarifa zao unaendelea kwa sasa.

    "Tuko katika mchakato wa kuwachuja mabalozi na kuwatuma katika nchi mbalimbali na hakika Marekani ni moja ya nchi hizo ambazo zitapokea balozi wa Nigeria hivi karibuni na hiyo sasa itakuwa jukumu lake na kuhakikisha kwamba ushiriki wa kila siku wa kidiplomasia na kibalozi... utakuwa rahisi na wa kati"

    Rais wa Marekani Donald Trump ameweka marufuku ya usafiri dhidi ya raia wa Tanzania katika vikwazo vya hivi karibuni vya usafiri.

    Ikulu ya White House imesema vikwazo hivyo vinavyokusudia "kulinda usalama wa Marekani" vitaanza kutekelezwa Januari 1, 2026.

    Katika amri ya rais ililotiwa saini Jumanne tarehe 16 Disemba, utawala wa Trump uliijumuisha Tanzania katika orodha ya nchi zinazokabiliwa na vikwazo vya muda vya kuingia Marekani, akitaja uzembe wa ukaguzi, uhakiki na upashanaji habari wa mamlaka ya Tanzania kuhusu raia wao.

    Nchi nyingine za Afrika zinazokabiliwa na vikwazo hivyo ni Burkina Faso, Mali, Niger, Sudan Kusini, Syria pamoja na watu walio na pasipoti ya Mamlaka ya Palestina.

    Laos na Sierra Leone, ambazo hapo awali ziliwekewa vikwazo vya muda, sasa zimejumuishwa kwenye orodha ya nchi 15 zilizopigwa marufuku, ikiwa ni pamoja na Nigeria, Tanzania na Zimbabwe.

    Soma zaidi:

  4. Venezuela yashutumu amri ya Trump kuzuia meli, yadai ni “vitisho vya kuchochea vita”

    xcv

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Marekani Donald Trump ameamuru kuwekwa "kizuizi kamili na cha jumla" kwa meli zote za mafuta zilizoidhinishwa kuingia na kutoka Venezuela - hatua ambayo Caracas imeishutumu na kuiita ni "vitisho vinavyochochea vita".

    Trump aliandika kwamba serikali ya rais wa Venezuela Nicolás Maduro ilitangazwa kuwa shirika la kigaidi la kimataifa (FTO), ambalo pia lilihusika katika "Ulanguzi wa dawa za kulevya, na Usafirishaji haramu wa binadamu".

    Matamshi hayo yamekuja baada ya Marekani kukamata meli moja ya mafuta katika pwani ya Venezuela wiki iliyopita hatua iliyochukuliwa kuwa muhimu, ikizingatiwa Venezuela hutegemezi zaidi sekta ya mafuta kwa uchumi wake.

    Aidha Marekani hivi karibuni imetekeleza mashambulizi makali dhidi ya meli zinazodaiwa kuwa za usafirishaji haramu wa dawa za kulevya za Venezuela, na imeongeza kwa kiasi kikubwa majeshi yake baharini.

    Soma zaidi:

  5. Naveed Akram ashtakiwa kwa makosa 15 yanayohusiana na shambulizi la Bondi

    xcv

    Chanzo cha picha, Saeed KHAN / AFP via Getty Images

    Naveed Akram, mshukiwa aliyenusurika katika shambulio la risasi la Jumapili huko Bondi Beach mjini Sydney, ameshtakiwa kwa makosa 59, ikiwa ni pamoja na makosa 15 ya mauaji na moja ya kufanya kitendo cha kigaidi, polisi wa New South Wales wanasema.

    Baba yake Sajid Akram, 50, aliuawa katika makabiliano ya risasi na polisi katika eneo la tukio.

    Watu 15 waliuawa na wengine kadhaa kujeruhiwa katika shambulio hilo, ambalo lililenga jamii ya Wayahudi ya Australia katika hafla ya kuadhimisha usiku wa kwanza wa Hanukkah.

    Ulikuwa ufyatuaji risasi mbaya zaidi nchini humo tangu 1996.

    Akram pia anakabiliwa na mashtaka 40 ya kusababisha madhara makubwa ya mwili kwa nia ya kuua, pamoja na shtaka moja la kuonyeshwa hadharani nembo ya shirika la kigaidi lililopigwa marufuku.

    Alijeruhiwa vibaya wakati wa tukio hilo Jumapili, na kesi yake ilisikilizwa kwa mara ya kwanza akiwa kitandani mwake hospitalini, mahakama ya eneo hilo ya New South Wales ilisema.

    Kesi hiyo imeahirishwa hadi Aprili 2026, mahakama iliongeza.

    Soma zaidi:

  6. Mshtuko baada ya DJ maarufu wa Afrika Kusini kuuawa kwa kupigwa risasi jijini Johannesburg

    xcv

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Polisi wanasema DJ Warras alipigwa risasi na mwanaume aliyekuwa na nywele za rasta mchana kweupe.

    DJ maarufu wa redio na klabu nchini Afrika Kusini ameuawa kwa kupigwa risasi katika jiji kubwa zaidi nchini humo, Johannesburg, na kusababisha mshtuko kote katika taifa hilo linalopambana na uhalifu uliokithiri.

    Warrick Stock, maarufu kama DJ Warras, alipigwa risasi katikati ya jiji Jumanne alasiri.

    Polisi walisema mtangazaji huyo aliyekuwa na umri wa miaka 40 alifikiwa na washukiwa watatu, mmoja wao akimfyatulia risasi kabla ya kukimbia kwa miguu.

    Sababu za kutekelezwa shambulio hazijafahamika na hakuna mtu aliyekamatwa hadi sasa, polisi walisema.

    Stock alikuwa mtangazaji maarufu wa redio na televisheni pamoja na mtayarishaji wa vipindi vya podikasti nchini Afrika Kusini.

    Fred Kekana, mkuu wa polisi wa eneo hilo, alisema Stock alishambuliwa alipokuwa akitoka kwenye Jumba la Zambesi karibu na Kituo cha Carlton.

    Stock alitumia saa kadhaa katika jengo hilo akisimamia ufungaji wa mifumo ya usalama katika eneo hilo, ambalo lilikuwa limekaliwa kwa utata na watu wasiojulikana,kwa mujibu wa SABC inayomilikiwa na serikali.

    "Inadaiwa Stock alifikiwa na washukiwa watatu wasiojulikana baada ya kuegesha gari lake, na wakamfyatulia risasi kabla ya kukimbia eneo la tukio kwa miguu," Idara ya Polisi nchini Afrika Kusini (SAPS) ilifafanua katika taarifa yake.

    Soma zaidi:

  7. Mghana ashtakiwa kwa kuwalaghai wanawake wazee dola milioni 8 katika sakata ya mapenzi

    Abu Trica aliibua shaka baada ya kuonekana kwenye mitandao ya kijamii akionyesha magari ya bei ghali, kiasi kikubwa cha pesa na mali

    Chanzo cha picha, ABUTRICA/INSTAGRAM

    Maelezo ya picha, Abu Trica aliibua shaka baada ya kuonekana kwenye mitandao ya kijamii akionyesha magari ya bei ghali, kiasi kikubwa cha pesa na mali

    Mwanaume mmoja wa Ghana anayejulikana mitandaoni amekamatwa na kushtakiwa kwa kudanganya Wazee wa Marekani zaidi ya Dola milioni 8 kwa madai ya mapenzi.

    Mwanaume huyu, anayejulikana kama Abu Tricia lakini jina lake halisi ni Frederick Kumi, amekamatwa na polisi wa Ghana ili kuchunguza tuhuma kwamba aliiba zaidi ya Dola milioni nane kutoka kwa wanawake wazee kwa kudanganya kuwa anawapenda.

    Kesi ya mashtaka inasema kuwa Kumi alitumia teknolojia ya akili bandia (AI) kuunda wasifu mitandaoni ili kuvutia wanawake wazee, hasa kwenye tovuti za uhusiano.

    Mara walipomwamini, alikuwa akiwatoza pesa, na alifanya hivyo kwa watu mbalimbali.

    Kumi anashutumiwa kwa makosa mawili:

    1. Ujambazi wa kielektroniki kwa lengo la kudanganya

    2. Kuficha au kuchakatua pesa (money laundering)

    Iwapo atapatikana na hatia, anaweza kufungwa hadi miaka 20 gerezani.

    Mwanaume huyo wa miaka 31 alikamatwa Ghana katika operesheni ya pamoja kati ya Ghana na Marekani, na Marekani inapanga kuomba kuhamishiwa kwake.

    Frederick Kumi bado hajatoa maoni kuhusu mashtaka hayo.

    Soma pia:

  8. Wakenya 18 waliohadaiwa kujiunga na kikosi cha Urusi warejea nyumbani

    Katika video moja inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii, wanaume saba wanaomba usaidizi wa serikali ya India kurejea nyumbani
    Maelezo ya picha, Katika video moja inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii, wanaume saba wanaomba usaidizi wa serikali ya India kurejea nyumbani

    Kufikia sasa wakenya 18 waliokuwa wamejipata Ukraine katika mstari wa mbele kupigania Urusi wemerejea nyumbani huku wakikaribishwa na familia zao kwa shangwe.Haya ni kwa mujibu wa gazeti la Standard nchini humo.

    Wa hivi punde ni Stanley Mungai, Brian Kimutai waliotua nchini Kenya tarehe 2 Desemba naye Michael Barasa akiwasili tarehe 3 Disemba 2025.

    Baadhi yao wana majereha ambayo waliyapata walipokuwa wakipigana huko Ukraine.

    Waliorejea nchini Kenya kutoka Ukraine wengi wao wana umri wa miaka kati ya miaka 20 hadi 30.

    Raia hawa ni miongoni mwa 84 waliotafuta msaada wa kurejeshwa nyumbani katika ubalozi wa Kenya ulioko Moscow.

    Serikali ya kenya kupitia wizara ya mambo ya kigeni inayoongozwa na Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi imebatilisha leseni za kampuni 600 zilizokuwa haziafiki kanuni ambazo zainadaiwa kuwalaghai wakenya kujiunga na vikosi vya Urusi.

    Mapema mwezi huu, Waziri wa Masuala ya Kigeni wa Kenya Musalia Mudavadi alisema baadhi ya Wakenya wanaopigania Urusi ni wanachama wa zamani wa jeshi la Kenya.

    "Inakadiriwa kuwa mitandao ya kuajiri bado inafanya kazi nchini Kenya na Urusi. Ubalozi wa Kenya huko Moscow umeripoti majeraha miongoni mwa raia wa Kenya, na wengine, [ambao] wamekwama [nchini Urusi]," alisema.

    Raia wa Somalia, Sierra Leone, Togo, Cuba na Sri Lanka, miongoni mwa wengine, kwa sasa wanazuiliwa katika kambi za wafungwa wa vita nchini Ukraine, Petro Yatsenko, msemaji wa Ukraine, aliiambia BBC.

    "Wengi wa watu hawa wanatoka katika nchi maskini na wanaishia kupigania Urusi kwa njia tofauti. Wengine wanadanganywa - kuahidiwa kazi katika viwanda - wakati wengine wanajiunga na vita kwa hiari. Ni muhimu kuelewa kwamba ni wachache sana wanaokamatwa wakiwa hai; wengi wao huuawa au kujeruhiwa vibaya," aliongeza.

    Mpango wa Alabuga Start (AS) uligonga vichwa vya habari duniani hivi karibuni baada ya wanamitandao wa Afrika Kusini waliokuwa wakiutangaza kushutumiwa kwa kuhusika na usafirishaji haramu wa binadamu.

    Kwa makadirio, zaidi ya wanawake 1,000 wameajiriwa kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika kufanya kazi katika viwanda vya silaha vya Alabuga.

    Mwezi Agosti, serikali ya Afrika Kusini ilianzisha uchunguzi na kuwaonya raia wake kutojiunga na mpango huo.

    Haya yakijiri rais wa Ukraine Vlodomyr Zelensky amezitaka mamlaka za bara la Afrika kuwakanya raia wao kutojiingiza kwa vita vinavyoendelea Ukraine.

    Soma pia:

  9. Kenya: Serikali ya jimbo la Nairobi kuwapatia wanawake mapumziko wanapokuwa kwenye hedhi

    Unashauriwa kumuona daktari usipopata hedhi kwa miezi mitatu mfululizo na huna ujauzito.

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Unashauriwa kumuona daktari usipopata hedhi kwa miezi mitatu mfululizo na huna ujauzito.

    Serikali ya Kaunti ya Nairobi nchini Kenya imeidhinisha rasmi utaratibu wa kutoa siku mbili kila mwezi za kupumzika kwa sababu ya hedhi kwa wanawake wafanyakazi, kama sehemu ya mfumo wa rasilimali watu wa kaunti hiyo.

    Uamuzi huu umefikiwa baada ya kikao cha baraza la mawaziri kilichoongozwa na Gavana wa jimbo hilo Johnson Sakaja, kilichopendekeza kuingiza usaidizi wa afya ya hedhi katika sera za rasilimali watu, kwa lengo la kuboresha ustawi wa wafanyakazi na kuongeza utendakazi wawanawake kazini.

    Taarifa ya kaunti inabainisha kuwa changamoto za afya ya hedhi, hususan dysmenorrhea (maumivu makali ya hedhi), huathiri kwa kiasi kikubwa ustawi wa wanawake na utendaji wao kazini.

    Tafiti zinaonyesha kuwa kati ya wanawake 65 hadi 80 kwa mia hukabiliwa na maumivu ya hedhi, na idadi kubwa ufanisi wao kazini huathirika zaidi.

    Kwa kuwa wanawake wanajumlisha zaidi ya nusu ya wafanyakazi wa Kaunti ya Nairobi, changamoto hizi zinachangia kupungua kwa ufanisi, kuwepo kazini licha ya ugumu wa kiafya (presenteeism) na kuathiri huduma za umma.

    Hadi sasa, afya ya hedhi haikuwa imeingizwa katika sera za rasilimali watu, jambo lililowalazimisha wanawake kwenda kazini wakiwa wagonjwa.

    Sera mpya itawaruhusu wanawake kusitisha kazi kwa siku mbili kila mwezi bila kuongeza mzigo wa kifedha kwa kaunti, na hivyo kutoa msaada wa kimuundo kwa wafanyakazi.

    Kulingana na waraka wa baraza la mawaziri, sera hii imejengwa kwa msingi wa ushahidi na inalingana na ahadi za kaunti za usawa wa kijinsia, kazi yenye heshima na utawala jumuishi.

    Nchi nyingine zilizo na haki za likizo ya hedhi ni pamoja na Zambia, Japan na Korea Kusini-ambapo Sheria ya Viwango vya Kazi inawataka waajiri kutoa siku moja ya likizo ya hedhi kwa mwezi.

    Indonesia hutoa siku mbili za kisheria, zilizochukuliwa siku ya kwanza na ya pili ya hedhi wakati maumivu yanaripotiwa, wakati Uhispania ilianzisha sheria sawa mnamo 2023.

    Soma pia:

  10. China yapunguza ushuru wa uagizaji wa nyama ya nguruwe kutoka Umoja wa Ulaya

    GG

    Chanzo cha picha, Getty Images

    China imepunguza ushuru wa uagizaji wa nyama ya nguruwe kutoka Umoja wa Ulaya, hatua iliyoanza kutekelezwa leo.

    Wizara ya Biashara ya China imesema kiwango cha juu cha ushuru kwa nyama ya nguruwe ya Ulaya kitakuwa chini ya asilimia ishirini, kiwango ambacho ni chini ya theluthi moja ya ushuru uliowekwa mwezi Septemba.

    Hatua hiyo imepokelewa kwa ahueni na wazalishaji wa nyama ya nguruwe barani Ulaya, hasa nchini Hispania na Ufaransa.

    China ndiyo nchi inayoongoza duniani kwa kula nyama ya nguruwe; mnamo 2024, zaidi ya nusu ya uagizaji wake wa thamani ya dola za Marekani bilioni 4.8 ulitoka Umoja wa Ulaya.

    Wakulima wengi wa Ulaya wanategemea sana soko la China, hasa ikiwa kwamba utumbo wa nguruwe, masikio,na miguu ya nguruwe haviliwi sana katika maeneo mengine ya dunia.

    Soma pia;

  11. Mazishi ya kwanza yafanyika Australia kwa waathiriwa wa ufyatuaji wa risasi kwenye ufukwe wa Bondi

    Familia zikifika katika mazishi ya aliyeuawa katika shambulizi lililofanyika katika ufukwe wa Bondi nchini Australia

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Familia zikifika katika mazishi ya aliyeuawa katika shambulizi lililofanyika katika ufukwe wa Bondi nchini Australia

    Mamia ya watu wamekusanyika katika sinagogi nchini Australia kwa maziko ya kwanza ya waathirika wa shambulio la watu wengi katika ufukwe wa Bondi.

    Rabi Eli Schlanger alikuwa mmoja wa watu kumi na watano waliouawa wakati wa tamasha la Kiyahudi la Hannukah huko Sydney siku ya Jumapili.

    Baba mkwe wake aliongoza maziko hayo na kuitaka jamii kutoogopa kuzuru eneo hilo.

    Waziri Mkuu wa Jimbo, Chris Minns, ambaye ametoa wito wa kuwepo kwa sheria kali za umiliki wa bunduki, alihudhuria.

    Rais wa Marekani Donald Trump ametuma risala za rambirambi kwa familia zilioathiriwa na shambulio la ufukwe wa Bondi, akisema Marekani "imeungana katika maombolezo" na Australia. Trump aliyasema hayo katika tafrija ya White House Hanukkah.

    Wakati huo huo, watu 21 wamesalia katika hospitali kote Sydney, pamoja na mmoja katika hali mahututi, mamlaka ya afya inasema.

    Familia ya mmoja wa maafisa wawili wa polisi waliojeruhiwa katika mashambulizi hayo wanasema amepoteza uwezo wa kuona katika jicho moja.

    Mshukiwa aliyenusurika, Naveed Akram, anaripotiwa kutoka katika hali ya kukosa fahamu, lakini bado yuko hospitalini.

    Mshukiwa mwingine, babake, Sajid alikufa katika eneo la mashambulizi.

    Bunge la jimbo la New South Wales la Australia litakutana tena wiki ijayo kujadili sheria ya dharura kuhusu udhibiti wa bunduki kufuatia mauaji ya Bondi na kuzingatia mageuzi ya maandamano, Waziri Mkuu Chris Minns alisema Jumatano.

    G

    Chanzo cha picha, Getty Images

    g

    Chanzo cha picha, PA Media

    Soma pia:

  12. Trump aamuru kuzuiwa meli za mafuta zilizowekewa vikwazo kuingia au kutoka Venezuela

    Rais wa Marekani

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Marekani, Donald Trump, ametangaza kuanzishwa kwa mzingiro kamili na wa jumla dhidi ya meli zote za mafuta zilizo chini ya vikwazo, zinazoingia au kutoka nchini Venezuela.

    Kupitia ujumbe alioutoa kwenye mtandao wa Truth Social, Trump alisema serikali ya Rais Nicolás Maduro imetangazwa kuwa shirika la kigaidi la kigeni, akiituhumu kwa kuiba mali za Marekani pamoja na kujihusisha na ugaidi, biashara ya dawa za kulevya na usafirishaji haramu wa binadamu.

    “Kwa msingi huo, leo ninaamuru mzingiro kamili na wa jumla wa meli zote za mafuta zilizo chini ya vikwazo zinazoingia na kutoka Venezuela,” aliandika Trump.

    Tamko hilo linakuja wiki moja baada ya Marekani kukamata meli ya mafuta karibu na pwani ya Venezuela.

    Serikali ya Caracas ilijibu kwa kukataa vikali hatua hiyo, ikiitaja kuwa tishio lisilokubalika na la kichokozi.

    Katika ujumbe wake, Trump alidai Venezuela “imezungukwa kikamilifu na msafara mkubwa zaidi wa kijeshi kuwahi kukusanywa katika historia ya Amerika Kusini”, akisisitiza kuwa nguvu hiyo itaendelea kuongezwa na kwamba itakuwa hali ambayo haijawahi kushuhudiwa.

    Trump pia aliishutumu serikali ya Maduro kwa kutumia mapato ya mafuta yaliyoibwa kufadhili shughuli za uhalifu ikiwemo ugaidi wa dawa za kulevya, biashara ya binadamu, mauaji na utekaji nyara.

    Utawala wa Trump umekuwa ukiishutumu Venezuela mara kwa mara kwa kuhusika katika usafirishaji wa dawa za kulevya.

    Tangu Mwezi Septemba, jeshi la Marekani limesema limeua takribani watu 90 katika mashambulizi dhidi ya boti lilizodai zilikuwa zikisafirisha fentanyl na dawa nyingine haramu kuelekea Marekani.

    Katika miezi ya karibuni, Marekani pia imeongeza uwepo wake wa kijeshi katika eneo hilo kwa kupeleka meli za kivita.

    Venezuela, ambayo ni miongoni mwa nchi zenye akiba kubwa zaidi ya mafuta duniani, imekuwa ikiituhumu Washington kwa nia ya kunyakua rasilimali zake.

    Marekani, chini ya tawala za Trump na rais wa zamani Joe Biden, imekuwa ikiipinga serikali ya Maduro kwa muda mrefu, ikiweka vikwazo vikali kama sehemu ya juhudi za kumlazimisha aondoke madarakani.

    Wiki iliyopita, Washington iliweka vikwazo vipya dhidi ya meli sita zaidi ilizosema zilikuwa zikisafirisha mafuta ya Venezuela. Hatua hizo pia ziliwalenga baadhi ya ndugu wa Rais Maduro pamoja na kampuni zinazohusishwa na kile Marekani inachokiita serikali haramu.

    Siku moja kabla, Ikulu ya Marekani ilitangaza kukamatwa kwa meli ya mafuta iitwayo Skipper karibu na pwani ya Venezuela, ikidai ilihusika katika usafirishaji haramu wa mafuta na kwamba ingetolewa hadi bandari ya Marekani.

    Serikali ya Venezuela ililaani vikali kukamatwa kwa meli hiyo, huku Rais Maduro akidai Marekani “iliwateka nyara wafanyakazi wa meli” na “kuiba chombo hicho”.

    Kabla ya oparesheni hiyo, Marekani ilikuwa imeongeza kwa kiasi kikubwa uwepo wake wa kijeshi katika Bahari ya Caribbean, ikihusisha maelfu ya wanajeshi pamoja na manowari kubwa zaidi duniani, USS Gerald Ford, iliyowekwa katika eneo la karibu na Venezuela.

    Mbunge wa Marekani kutoka Texas, Joaquin Castro wa Chama cha Democratic, alisema mzingiro wa majini uliotangazwa na Trump “ni kitendo cha vita kisicho na shaka”. Aliongeza kuwa Bunge la Marekani linatarajiwa kupiga kura juu ya azimio litakalomuelekeza rais kusitisha uhasama dhidi ya Venezuela.

    Soma pia:

  13. Hujambo na karibu kwa matangazo ya moja kwa moja ya Jumatano tarehe 17/12/2025