Virusi vya corona: Upinzani Uganda waungana kupinga jitihada za serikali

Chanzo cha picha, HISANI
Viongozi wa upinzani nchini Uganda Robert Kyagulanyi, ambaye anajulikana kama Bobi Wine, na Kizza Besigye wana mpango wa kuandaa maandamano ya kitaifa dhidi ya serikali kupinga jinsi taifa hilo linavyokabiliana na janga la virusi vya corona.
Wamesema serikali haijaweka hatua madhubuti za kulinda na kuukomboa uchumi baada ya mlipuko huo.
Viongozi wa upinzani Uganda Kizza Besigye na Robert Kyagulanyi maarufu Bobi Wine wameunda muungano wa upinzani.
Robert Kyagulanyi wa vugu vugu la People Power kwa pamoja na Dkt. Kizza Besigye ambaye chama chake FDC kinaongozwa na Amulati, Meya wa Kampala Erias Lukwago wa chama cha DP, Rais wa chama cha CP Keny Lukyamuzi, rais wa chama cha JEEMA Asumani Bsalirwa na wengine wengi wamezindua rasmi muungano mpya wa upinzani kuwa na mshika bendera mmoja katika uchaguzi ujao mwaka 2021 dhidi ya Rais Museveni.

Chanzo cha picha, BOBI WINE
Akizindua rasmi muungano huo katika wilaya ya Wakiso, Robert Kyagulanyi ameutaja muungano huo kwa jina la 'United forces of change' na kusema kuwa kufikiwa walipo, wamepiga hatua kubwa.
''Nataka kushukuru viongozi wetu walioona njia, wakafuata njia hiyo na kutuonyesha njia,'' Kyagulanyi amesema hayo.
Aidha ameweka wazi kwamba hakuna njia nyingine zaidi ya kuungana.
''Ni lazima tushirikiane kwa manufaa ya nchi yetu.'' Kyagulanyi ameongeza hayo huku akisisitiza kuwa njia walioshika ndio sahihi.
Mwanamuziki huyo ambaye pia ni mbunge ameweka wazi kwamba wao (walioungana) sio maadui na kadiri wanavyoendelea kupigana vita wenyewe kwa wenyewe ndivyo wanavyoendelea kuchelewesha mabadilko ambayo raia wamekuwa wakisubiri kwa hamu.
Robert Kyagulanyi ameeleza kwamba kufikia wanacholenga kunaweza kufanikiwa tu kwa ushirikiano wa watu.
''Natoa wito kwa raia wote wa Uganda msilale badala yake mpaze sauti zetu,'' Kyagulanyi amesema na kusisitiza kwamba kampeni yao ni ya amani.
Katika hotuba yake, amemnukuu Malcolm X ambaye alikuwa mwanaharakati wa haki za kiraia za Waafrika-Waamerika ''Mikakati inaweza kutofautiana, hatua za kuchukua na mbinu zinaweza kutofautiana lakini lengo likawa moja.''
Viongozi wa vyama viwili vikuu vya upinzani vya Kizza Besigye na Robert Kyagulanyi wamekuwa wakikutana mara kadhaa kuandaa mikakati ya kuunda muungano huo wa "United force of change".
Wabunge wengine pamoja na wafuasi wao ni miongoni mwa waliohudhuria uzinduzi huo.
Na wale waliokuwepo walifuata kanuni ya kutokaribiana ili kuzuia usambaaji wa virusi vya corona.
Hata hivyo mkutano huo umesambaratishwa na polisi dakika za mwisho.
Pia unaweza kutazama:
Kizza Besigye ni nani?
Kanali (Mstaafu) Dkt Kizza Besigye Kifeefe alizaliwa mwaka 1956 katika wilaya ya Rukungiri, magharibi mwa Uganda.
Besigye alifuzu kama daktari baada ya kusomea Chuo Kikuu cha Makerere, mjini Kampala.
Alijiunga na chama cha Museveni cha Uganda Patriotic Movement muda mfupi baada ya kuondolewa madarakani kwa Idi Amin 1978.
Mwaka 1982, alijiunga na Museveni vitani baada ya kuzuiliwa miezi miwili katika hoteli moja mjini Kampala akituhumiwa kushirikiana na waasi.

Chanzo cha picha, Getty Images
Baada ya Museveni kuingia uongozini, alimteua Dkt Besigye, wakati huo akiwa na umri wa miaka 29, kuwa waziri wa nchi aliyesimamia masuala ya ndani na masuala ya siasa za taifa.
Dkt Besigye alipanda cheo jeshini na kufikia cheo cha kanali.
Alistaafu muda mfupi kabla ya uchaguzi mkuu wa 2001, miezi michache kabla ya kujitokeza na kutangaza kwamba angewania urais.
Alipata asilimia 28 ya kura zilizopigwa akilinganishwa na mshindi, Museveni, aliyepata asilimia 69.
Baada ya kushindwa, Besigye aliwasilisha kesi Mahakama ya Juu kupinga matokeo ya uchaguzi. Alishindwa kesi hiyo na akakimbilia uhamishoni Afrika Kusini akilalamikia kudhulumiwa kisiasa.
Alirejea Novemba 2005 na kuongoza chama cha FDC kwenye uchaguzi wa februari.
Hata hivyo alikamatwa wiki chache baadaye na kufunguliwa mashtaka kadhaa yakiwemo uhaini na ubakaji.
Aliachiliwa huru wiki mbili baada ya kuanza kwa kampeni za uchaguzi.
Besigye husifiwa sana kutokana na moyo anaoonyesha anapotoa hotuba zake na wengi wamemsifu kwa kusimama na kupinga utawala wa Museveni.
Hata hivyo, wakosoaji wake humshutumu wakisema hana uchu wa madaraka na baadhi husema hawezi kufanikisha mabadiliko yoyote kutokana na uhusiano wake wa muda mrefu na Museveni.
Bobi Wine ni nani?

Chanzo cha picha, Reuters
Nyota huyu wa mtindo wa Afrobeats aliingia katika taaluma ya muziki katika miaka ya 2000, na anaelezea kipaji chake kuwa ni cha kuelimisha na kuburudisha. Mojawapo ya vibao vyake vya awali Kadingo, inahusu usafi wa mwili.
Alizaliwa 12 Februari 1982, Bobi Wine na alikuwa na miaka minne pekee Museveni alipoingia madarakani mwaka 1986.
Jina lake rasmi Wine, ni Robert Kyagulanyi Ssentamu.
Alilelewa katika mtaa duni wa Kamwokya kaskazini mashariki mwa Kampala na alianza kujihusisha katika muziki mapema miaka ya 2000.
Nyimbo zake za mtindo wa dansi za 'Akagoma' na 'Funtula' zilikuwa maarufu sana miongoni mwa vijana.
Ana shahada ya muziki, dansi na uigizaji kutoka Chuo Kikuu cha Makerere ambapo alihitimu mwaka 2003.
Aprili 2018 alifuzu na stashahada ya masuala ya kisheria kutoka Kituo cha Maendeleo ya Sheria, Kampala.
Alichaguliwa kuwa mbunge katika uchaguzi mdogo baada ya kusimama kama mgombea huru mwaka 2017 wilayani Kyadondo mashariki, Uganda ya kati.
Aliwashinda wagombea kutoka chama tawala National Resistance Movement (NRM) na chama kikuu cha upinzani Democratic Change (FDC).
Baada ya kutangazwa mshindi, aliahidi kuangazia zaidi kuwaunganisha raia.
"Jambo langu la kwanza ninalotaka kufanya ni kufanikisha maridhiano kati ya viongozi wa Kyadondo Mashariki...Ninataka siasa zitulete pamoja... jinsi muziki ufanyavyo."
Ufuasi wa Vijana

Chanzo cha picha, AFP
Umaarufu wake miongoni mwa vijana nchini Uganda unaonekana kuwa changamoto kubwa kwa rais wa miaka mingi Yoweri Museveni.
Bobi Wine anajiita "Ghetto President" na anaungwa mkono zaidi na vijana
"Chama chake kitawaza iwapo sasa huu ni msururu. Bobi Wine sasa amemshinda Museveni na kiongozi wa upinzani Kizza Besigye mara nne'' katika uchaguzi mdogo.
"Bobi amepata ufuasi kwa nemba yake ya 'nguvu za watu', na ananuia kushinikiza na kupanga liwe vuguvugu," anaongeza.
Mchambuzi wa kisiasa Robert Kirunda anasema mvuto wa Wines unatokana na kuwepo 'pengo la uongozi' Uganda.
"Kuna vijana wengi Uganda ambao hawana haja ya kujua vita vya kihistoria vilivyoiingiza NRM uongozini, au ukaidi wa upinzani mkuu. Wengi wanataka ajira na wanahisi uchumi hauwasaidi."
Kirunda anasema Wine 'anapigia upatu sana'. "Anaweza kushinikiza watu.














