Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Kutoka kwa wachezaji densi aina ya Belly hadi wauzaji maua: Mashujaa 6 wanaopambana na janga la corona Afrika
Watu barani Afrika wanachukua majukumu ya kipekee na kusaidia wengine wakati huu wa janga la virusi vya corona.
Hizi ni simulizi sita za kutia moyo za mashujaa wa kila siku.
1) Kutoka nguo za kisasa hadi za wahudumu wa afya
Kampuni moja nchini Libya imebadilisha shughuli zake kutoka kutengeneza nguo za kisasa hadi nguo wanazovaa wahudumu wa afya wa kuwahudumia wagonjwa wa Corona.
Wanawake sita wanaoshona nguo za madaktari na wahudumu wa afya katika kiwanda kimoja cha utengenezaji nguo cha Fashion House mji mkuu wa Libya, Tripoli.
Wote wamejitolea kufanyakazi hiyo huku baadhi yao wakiamua kulala katika kiwanda hicho.
Hadi kufikia sasa wametengeneza nguo 50 na kwasasa wameanza kundi jingine la nguo hizo.
Wahudumu wa afya katika mji wa Tripoli waliwapongeza kwa juhudi zao mapema wiki hii.
"Wazo hili lilianza wakati daktari katika hospitali ya al-Jalaa Hospital mjini Tripoli alipoomba msaada kutoka kwa wafanyabiashara mbalimbali," mwanzilishi mwenza wa kampuni ya Fashion House Najwa Taher Shokriy, 26, amezungumza na mwanahabari wa BBC Rana Jawad.
Alianzisha kampuni hii mwaka mmoja uliopita lakini mipango ya kupanua kampuni hii ameiweka pembeni kidogo kukabiliana na janga hili lililosababisha matatizo makubwa katika sekta ya afya.
Yeye pamoja na mafundi wenzake wanataka kutengeneza nguo zaidi lakini changamoto ni kupata nyenzo husika za vitambaa na mashine za kushonea katika mji huo unaokumbwa na vita.
2) Jengo la kutunza wazee la pambwa
Janga hili la Corona limesababisha harusi nyingi kuahirishwa na matokeo yake maua chungu nzima yamenyauka.
Lakini kundi moja la wauza maua huko Paarl, mji uliopo katika eneo ambalo ni kitovu cha utengenezaji wa mvinyo Afrika Kusini liliungana na kupamba jengo moja.
Wakiwa na maua 600 kutoka kampuni ya maua ya Adene, walipamba nje ya jengo la zamani la wazee la Huis Vergenoegd.
Wakazi wa jengo hilo wamekuwa wakifungiwa tangu katikati ya mwezi Machi, lakini waliruhusiwa kutoka nje na kutazama kulivyopambwa kukiwa kunanukia harufu nzuri ya maua ya waridi kulingana na ukurusa rasmi wa mtandao wa Facebook wa kampuni ya maua.
"Magari mengi yalijitokeza, wapita njia wengi wakatazama - mapambo haya yalikuwa ya furaha kubwa isio na kifani," kulingana na mkuzaji mmoja wa maua.
3) 'Mmiliki wa nyumba' wateja hawatalipa kodi kwa miezi miwili
Mmiliki mmoja wa nyumba nchini Kenya amewaambia wapangaji wake 34 kwamba hawatalipa kodi ya mwezi Machi na Aprili kwasababu anaelewa kwamba janga la Corona limesababisha msukosuko wa kifedha kwa kaya nyingi.
Michael Munene anamiliki majumba 28 magharibi mwa Kenya eneo la Nyandarua ambapo kila mpangaji analipa 3,000 za kenya sawa na dola 30 au euro 23 kila mwezi.
Pia ana majengo 6 ya kibiashara ambapo wapangaji hulipa elfu 5 za Kenya kila mwezi. Ikiwa hakuna atakayelipa atapoteza zaidi ya dola 2,000.
Kupitia runinga ya NTV nchini humo, Bwana Munene amekuwa akipongezwa tangu aliposema kwamba ni kheri kitakachopatikana kilishe watoto.
Kuna wakati alikuwa mpangaji na aliwahi kufurushwa kwasababu ya kushindwa kulipa kodi ya mwezi. ameeleza.
"Wamekuwa wateja wangu kwa muda sasa na kodi wanayolipa imekuwa ikinisaidia kufanya mambo mengi," amesema.
"Kwahiyo, nimeamua kuwa huu ndio muda muafaka wa kushirikiana nao na kuwasaidia."
Gazeti moja la eneo, limemuandika kama mmiliki wa nyumba mwenye ukarimu.
4) Mchezaji densi ya belly afanya onesho mtandaoni
Mchezaji densi ya belly nchini Tunisia Nermine Sfar amekuwa akifanya onesho wakati huu ambapo raia wanatakiwa kusalia majumbani katika hilo la kaskazini mwa Afrika.
Amekuwa akifanya onesho akiwa nyumbani kwake kila usiku huku mamilioni ya watu wakimtazama kupitia video kwenye mtandao wa Facebook wiki iliyopita.
Alianza kufanya onesho kabla ya amri ya kusitisha shughuli zote kutolewa Jumapili Machi 29 nchini Tunisia - ingawa wakati huo tayari watu walikuwa wanahamasishwa kusalia majumbani.
Tukio hilo linalofanyika kwenye mtandao wa kijamii amelipa jina la: "Salia nyumbani na mimi nitacheza kwa ajili yako".
Inaonekana kana kwamba amefanikiwa lengo lake - kwasababu mamia ya maelfu ya watu wanamtazama na video moja ya wiki jana imetazamwa mara karibia milioni mbili.
5) Nyota wa muziki wa Pop atoa nyumba yake kama kituo cha karantini
Nyota wa muziki wa pop Ethiopia ametoa nyumba yake itumike na watu walio kwenye karantini.
Mwezi uliopia, serikali ya Ethiopia iliagiza kila mmoja anayewasili nchini humo kuwekwa kwenye karantini katika hoteli kwa gharama zao wenyewe kwa siku 14.
Hamelmal Abate, aliyekuwa maarufu miaka ya 1990 kwa nyimbo za Amharic na Afaan Oromo amemuarifu mwanahabari wa BBC Ethiopia, Kalkidan Yibeltal hatua hiyo ilikuwa ni kama faini kwa raia wa kigeni wenye pesa.
"Wale wanaohitajika kujitenga pia ni wetu," amesema.
"Kwa baadhi ambao wanatoka ulaya, wanaweza kumudu gharama za hoteli zilizotengwa lakini kuna wale ambao uwezo wao ni wa chini. Pia nao wanastahili kupewa huduma sawia na hiyo."
Nyumba aliyotoa Hamelmal ni mkabala na makazi yake mjini, Addis Ababa.
Ni miongoni mwa raia wa Ethiopia wanaotoa nyumba zao kuwa vituo vya karantini huku wasiwasi wa upungufu wa vituo vya wanaohitajika kujitenga ukiendelea kudhirika.
6) Kipaatoa pesa za kununua chakula kwa mashabiki wake
Mchezaji soka wa Nigeria amewapa mashabiki wake wanne pesa kuhakikisha wanapata chakula katika kipindi hiki cha mlipuko wa ugonjwa wa corona.
Mlinda lango wa Plateau United Chinedu Anozie alitoa naira 5,000 naira sawa na dola 14 au euro 11 kwa kila shabiki wake.
Huenda isionekane kuwa pesa nyingi lakini kiuhalisia wanasoka wengi nchini Nigeria wanalipwa takriban dola 88 kwa wiki (karibia $4,600 kwa mwaka), amesema mwandishi wa BBC Nduka Orjinmo mjini Lagos.
Mlinda lango huyo hajafungwa hata goli moja katika mechi 10 alizoshiriki - na timu yake inaongoza katika ligi, ingawa kwa wakati huu mechi zimesimamishwa kwasababu ya virusi vya corona.