Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Marekani: Mkulima ajikata mguu kwa kisu ili kuokoa maisha yake
Mkulima mmoja aliamua kujikata mguu wake na kisu mara baada ya kukwama katika trekta ya kulimia.
Kurt Kaser mwenye umri wa miaka 63 alilazimika kujikata mguu wake kwa kisu kidogo chenye ncha ya sentimita 7.6 na kufanikiwa kutambaa mpaka eneo ambalo simu yake ilikuepo ili kuomba msaada.
Mkulima huyo alikaa hospitalini kwa wiki kadhaa kwa matibabu kabla hajaruhusiwa kurudi nyumbani.
"Sikuwa na njia nyingine ya kujiokoa" Mkulima huyo alieleza na kuongeza kuwa kama asingechukua maamuzi hayo basi angeweza kufa ndio maana aliamua kuchukua kisu alichokuwa nacho kwenye mfuko na kujikata mguu.
Mkulima huyo alikuwa anafanya kazi mwenyewe katika shamba la heka 1,500 wakati ajali inatokea.
Baada ya kushindwa kuiona simu yake ili aombe msaada, bwana Kaser akiwa anashuhudia mguu wake umenasa kwenye mashine na kumsababishia maumivu makali.
Mkulima huyo aliamua kuchukua kisu kilichokuepo kwenye mfuko wake wa suruali na kumalizia kuukata goti lake ambalo mguu ulikuwa umenasa katika mashine ya kulimia ili kujiokoa.
Alipofanikiwa kukata mguu wake Kaser alitambaa kwa hatua mia moja ili kupata simu iliyokuwa karibu naye na kumpigia mtoto wake ambaye aliweza kuja baadae kumpeleka hosptali kwa ajili ya matibabu.
Bwana Kaser anasema anajilaumu mwenyewe kwa kushindwa kurekebisha mashine yake mpaka ikamletea madhara.
Lakini anaelewa kuwa ndio maana huwa kuna ajali kazini.