Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Amnesty:Burma yatega mabomu ya ardhini kuwazuia Rohingya
Amnesty International linasema lina ushahidi kuwa vikosi vya usalama Myanmar vimetega mabomu ya ardhini yaliopigwa marufuku katika mpaka na Bangladesh.
Hilo ni eneo ambako idadi kubwa ya waislamu wa Rohingya wanatoroka ghasia.
Shirika hilo la kimataifa la kutetea haki za binaadamu linasema raia wapatao watatu wamejeruhiwa kwa milipuko hiyo ya kutegwa ardhini katika wiki iliyopita, na inaarifiwa mwananmume mmoja aliuawa.
Watu walioshuhudia wameliambia shirika hilo kwamba waliwaona maafisa wa usalama wa Burma wakitega mabomu hayo.
Umoja wa mataifa unasema zaidi ya waislamu laki mbili na nusu wa Rohingya wametoroka Myanmar tangu jeshi lianze operesheni dhidi ya wanamgambo huko wiki mbili zilizopita.
Shirika la Umoja wa mataifa linalowashughulikia wakimbizi UNHCR linasema idadi hiyo imeongezeka baada ya ukaguzi wa kina wa maeneo ambayo awali hayakujumuishwa katika hesabu.
Waislamu wengi wa Rohingya wametembea kwa siku kadhaa wakipitia jangwani na milimani .
Baadhi wamepanda maboti wakivuka bahari ya Bengal.