Noti mpya zazua hofu ya sarafu ya zamani Zimbabwe

Taifa la Zimbabwe limezindua fedha zake kwa mara ya kwanza tangu sarafu ya dola ya taifa hilo ifutiliwe mbali miaka saba iliopita kufuatia mfumuko mkubwa wa kiuchumi.

Noti hiyo yenye dhamana ambayo ina thamani ya dola moja imezua hofu kuhusu kurudi kwa matumizi ya dola ya taifa hilo.

Noti hizo ambazo zilizinduliwa kwa mara ya kwanza mnamo mwezi Mei, zimesababisha maandamano makubwa katika kipindi cha muongo mmoja dhidi ya rais Mugabe .

Serikali imesisitiza kuwa noti hizo za dhamana sio sarafu rasmi ya taifa hilo.

Imezindua noti hizo ili kukabiliana na upungufu wa fedha mabli na kusitisha matumizi ya dola ya Marekani ambayo inazidi kutolewa nje ya taifa hilo, hatua ambayo kundi la wafanyibiashara wameiunga mkono.

Fedha zenye thamani ya dola milioni 10 zitasambazwa katika noti za dola mbili na tano.