Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Wanawake wanavyokaribia kutawala dunia
Japo ni jambo ambalo linaamuliwa katika saa chache zijazo, ni jambo ambalo wengi wanasubiri kwa hamu na shauku kuu kuona iwapo litatilia.
Iwapo Bi Hillary Clinton atashinda kiti cha urais wa Marekani itakuwa ni mageuzi makubwa sana kwa Marekani na dunia nzima, na pia fahari kuu kwa wanawake.
Mwandishi wa BBC Katty Kay anachanganua:
Hii ni kwa sababu hili itamaanisha sasa shirika kuu la fedha duniani na mataifa matatu tajiri duniani yatakuwa yakiongozwa na wanawake.
hati inaendelea hivi: Uingereza Bi Theresa Mary May na Malkia Elizabeth, Ujerumani Bi Angela Merkel, na Bi Chistine Lagarde katika uongozi wa shirika la fedha duniani IMF.
Sasa katika orodha hiyo ongezea marais wa kike, wanawake wanaoongoza baadhi ya nchi zilizo na utawala wa kifalme na hata mawaziri wakuu wa kike, ndio utabainikiwa jinsi mambo yalivyobadilika katika safu ya uongozi iliyokuwa ikisheheni tu viongozi wa kiume miaka michache iliyopita!
Afrika kuna Ellen Johnson Sirleaf ambaye amekuwa rais wa Liberia. Amekuwa madarakani tangu 2006.
Bi Park Geun-hye ndiye rais wa Korea Kusini. Amekuwa madarakani tangu 2013.
Bi Kolinda Grabar-Kitarović ni rais wa Croatia na amaekuwa madarakani tangu Februari mwaka jana.
Lakini je hilo lina uzito gani hasa katika minzani ya kuboresha maisha ya kila siku ya mwanadamu.
Kuna kauli zisemazo wanawake hawatakiani mema na mifano inatolewa ya baadhi ya taasisi zilizoongozwa na akina mama wakamavu, walioelimika vyema ... ambako haikuonekana bayana kuinua maisha ya wanawake wenzao kisera wala kiuchumi licha ya kuwa wengi wa walio maskini duniani ni wanawake, vijana na watoto.
Hata hivyo utafiti mbali mbali uliofanywa na taasisi za kimataifa unaonesha kuwa wanawake wanapokuwa uongozini tatizo la mfumo dume hupungua , wasichana hupata motisha zaidi masomoni na katika kazi zao hata iwe ya ngazi ya chini kiasi gani.
Pia uongozi wa wanawake huendeleza sera za kutafuta suluhu za kidiplomasia kwa mizozo ya kisiasa kuliko kukimbilia vita - kwani wao ndio waathirika wa kwanza wakati amani inapovurugwa.
Zaidi ya hayo utafiti unaonesha ili mabadiliko ya kisawa sawa yafanyike, yakuboresha maisha ya wote kwa jumla ni sera za kuongeza idadi ya wanawake katika sekta zote za kimaisha zitekelezwe.
Na sekta zinazopaswa kupewa kipa umbele kwa hilo ni katika nyanja za kisiasa, kiuchumi, kibiashara, fani za uandishi habari, udaktari, na hata katika jeshi.
Pia tafiti hizo zaonesha mwanapopewa fursa katika upande wa usomi, kutafuta maridhiano na kuwa kielelezo cha mifano miema wanawake wengi wako mstari wa mbele kuliko wanaaume ...bila kusahau majukumu yao ya a msingi ya kuwatunza waume zao, na kuwapa watoto ulezi bora.