Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
AFCON 2025: Mchele na pumba kuanza kujitenga leo, nani kufuzu 16 bora?
Mechi za mwisho za makundi kwenye michuano ya AFCON 2025 huko Morocco zinaanza leo Jumatatu huku nafasi za kufuzu zikiwa bado wazi kwa timu nyingi na huenda tukashuhudia maajabu ya timu zilizotarajiwa kuondolewa na zisizotarajiwa kufuza hatua ya 16 bora..
Timu tatu mpaka sasa tayari zimejihakikishia nafasi zao kwenye raundi ya 16 bora baada ya kushinda mechi zao mbili za mwanzo. Timu hizo ni Misri, Nigeria na Algeria. Kwa timu nyingine zote, mechi za mwisho za makundi zitatoa mwangaza si tu juu ya timu gani zitashika nafasi mbili za juu na kufuzu moja kwa moja, bali pia ni timu gani nne zitakazoshika nafasi ya 3 zenye matokeo bora zenyewe kutinga 16 bora.
Mechi za leo Jumatatu zitaanza kwa wakati mmoja kwa kila kundi, jambo litakaloongeza msisimko na mvutano mkubwa.
Katika kundi B, ubora wa Misri mwanzoni umewapa uhakika wa alama 6 na kufuzu, lakini bado kuna ushindani nyuma yao. Afrika Kusini wako nafasi ya pili na alama 3, wakijua kuwa ushindi dhidi ya Zimbabwe utaondoa mashaka yote, wakati Angola waliokuwa na alama 1 sawa na Zimbabwe lazima iichape Misri na kuombaea matokeo mengine yawape faida. Kwa kuwa tofauti ya mabao ni muhimu, goli moja la ziada linaweza kuamua kila kitu.
Kundi A, wenyeji Morocco wako salama wakiongoza kwa alama 4. Mali na Zambia ziko sawa kwa alama 2, huku Comoros bado wakiwa na matumaini ya alama 1 na usiku wa Jumatatu unaleta mechi mbili zinazoweza kugeuza hali ya kundi hili. Morocco wanakabiliana na Zambia, timu ambayo tayari imeonyesha inaweza kupambana kwa bidii, wakati Mali itatarajiwa kupata alama dhidi ya Comoros na kufuzu.
Kundi C na D, mechi zao zitapigwaJumanne wakati Nigeria, tayari zimefuzu kutoka Kundi C, zikicheza dhidi ya Uganda. Hii inawaachia Tunisia, wakiwa na alama 3, jukumu la kuhakikisha inaichapa Tanzania ili kufuzu, lakini kwa kuwa Tanzania na Uganda bado wana nafasi ya kufuzu, mechi hazitakuwa rahisi.
Kundi D, Senegal na DR Congo wakiwa sawa kwa alama 4, Benin wakiwa alama 3 nyuma, na Botswana wakipambana kupata alama yao ya kwanza. DR Congo wanatarajia kuwasumbua Botswana, lakini mechi ya Senegal dhidi ya Benin ina hatari kubwa, ikiwa mwenye nafasi ya kwanza, anaweza kufuzu moja kwa moja, au hata kutolewa, yote kutategemea matokeo, hakuna aliye salama.
Jumatano inaleta sura ya mwisho ya awamu ya makundi kwa mechi za kundi E na F. Algeria, tayari imefuzu kutoka kundi E, bado inaweza kuathiri nani atakayemfuata. Burkina Faso na Sudan wakiwa sawa kwa alama 3 na tofauti ndogo za mabao, mmoja anaweza kumfuata.
Kundi F, Cameroon na mabingwa watetezo Ivorycoast, wakiwa sawa kwa alama 4, huku Msumbiji ikiwa nyuma yao kwa alama 3, inafanya mechi za mwisho kuwa msisimko zaidi, ingawa Gabon tayari ni kama imeaga.