Kijiji ambacho kuoana mkiwa dini tofauti ni kifo

Muda wa kusoma: Dakika 5

Mauaji ya wanando wa imani tofauti ya dini kumeshtua kijiji kidogo katika jimbo la Uttar Pradesh kaskazini mwa India ambapo wakazi wameishi kwa amani kwa miaka mingi.

Miili ya Kajal mwenye umri wa miaka 19, Mhindu, na Mohammad Arman mwenye umri wa miaka 27, Mwislamu, ilipatikana ikiwa imezikwa karibu na ukingo wa mto nje kidogo ya kijiji cha Umri mnamo Januari 21.

Polisi walisema walipigwa hadi kufa, ikidaiwa waliohusika ni ndugu watatu wa Kajal, ambao wamekamatwa. Kwa kuwa wako kizuizini hawakutoa maoni yao kuhusu tuhuma hizo.

Mauaji hayo yameleta ukimya wa wasiwasi katika Umri, kijiji kilicho karibu na Delhi ambako familia za Wahindu na Waislamu kwa muda mrefu zimeishi kwa amani.

Kijiji hicho kina takriban familia 400 kutoka jamii za Wahindu na Waislamu, na wakazi kadhaa waliiambia BBC kuwa wamekuwa na uhusiano mzuri bila historia ya migogoro ya kidini.

Naibu inspekta jenerali wa polisi wa jimbo Muniraj G aliiambia BBC kwamba polisi wanaamini kuwa ni kesi ya "kuua kwa heshima" - mauaji yanayofanywa na jamaa au wanajamii ili kuwaadhibu wanawake kwa kupendana au kuoa nje ya tabaka au dini yao.

Ofisi ya Kitaifa ya Kumbukumbu za Uhalifu ya India ilianza kurekodi mauaji ya heshima mwaka wa 2014, ilipoorodhesha visa 18 kote nchini. Ripoti yake ya hivi karibuni ya kila mwaka ilirekodi visa 38 kama hivyo mwaka wa 2023.

Hata hivyo, wanaharakati wanasema idadi hiyo ni kubwa zaidi, kwa mamia kila mwaka - kwani visa vingi hurekodiwa kama mauaji tu.

Umri iko katika wilaya ya Moradabad ya Uttar Pradesh, ambayo inajulikana kwa viwanda vyake vya ufundi wa chuma. Eneo hilo kwa kiasi kikubwa ni la vijijini, ambapo uongozi imara wa kijamii unaendelea kuathiri maisha ya kila siku. Ndugu zake Kajal walifanya kazi kama waashi katika mji wa Moradabad.

Uhusiano wa Kajal na Arman "ulikuwa kesi ya kwanza [ya uhusiano wa kidini]" katika kijiji chao, anasema mkazi Mahipal Saini.

Wakazi wa Umri waliozungumza na BBC kwa sharti la kutotajwa majina walisema Kajal na Arman walikuwa majirani ambao waliishi umbali wa mita 200 hivi kutoka kwa kila mmoja. Waliwaelezea kama watu wasio na marafiki wengi.

Kajal alifundisha katika shule binafsi huko Umri, huku Arman akirudi kijijini yapata miezi mitano iliyopita baada ya kutumia miaka minne huko Saudi Arabia ambapo alifanya kazi katika duka la chakula. Jamaa zake walisema alirudi kwani hakupata pesa nyingi huko na amekuwa akifanya kazi na mkandarasi wa mpasua mawe wa eneo hilo tangu aliporudi.

Haijulikani walikutana vipi na walikuwa wameishi pamoja kwa muda gani, lakini polisi wanasema kwamba "wawili hao walikuwa karibu".

Wanasema mauaji hayo yanadaiwa yalitokea nyumbani kwa Kajal usiku wa Januari 18 na 19, wakati kaka zake walipomkamata Arman wakimtembelea. Ndugu hao, Rajaram, Satish na Rinku Saini, wako gerezani na hawajasema chochote cha kuwatetea hadi sasa.

Baba yao, Ganpat Saini, aliambia BBC kwamba yeye na mkewe hawakuwa nyumbani wakati wa mauaji hayo. Alisema walikuwa wamelala kwenye kibanda nje kidogo ya kijiji ambapo kwa kawaida hulala usiku kulinda mifugo yao. Aliongeza kuwa alikuwa akimomboleza binti yake.

Kaka mkubwa wa Arman, Farman Ali, alisema kwamba kaka yake aliondoka nyumbani baada ya chakula cha jioni tarehe 18 Januari, akisema angerudi na dawa kwa ajili ya wazazi wao. Alipokuwa hajarudi asubuhi iliyofuata na simu yake ikiwa imezimwa, familia yake ilianza kuingiwa na hofu na kwenda polisi. Hii ilisababisha operesheni ya utafutaji kijijini.

Polisi wanadai kwamba ndugu za Kajal walijaribu kuwapotosha kwa kutoa malalamiko ya kutokuwepo kwake tarehe 20 Januari, wakimtuhumu Arman kwa kumteka nyara.

Wanasema walihoji familia zote mbili na kugundua tofauti katika taarifa za ndugu za Kajal.

Uchunguzi zaidi uliwaongoza hadi mahali ambapo miili ilizikwa, polisi walisema.

Ganpat Saini anasema kwamba yeye na mkewe waliporudi nyumbani asubuhi ya tarehe 19 Januari, hawakuweza kumpata Kajal nyumbani. Anasema alipata habari kuhusu mauaji hayo baada tu ya miili kupatikana.

Hata hivyo, hakujibu alipoulizwa kama yeye au mtu yeyote katika familia yake alijua kwamba Kajal na Arman walikuwa kwenye uhusiano.

Familia ya Arman inasema hawakujua uhusiano wake na Kajal.

"Hakutuambia chochote," kaka Farman Ali anasema. "Baada ya kutokumpata kwa siku nzima, baadhi ya marafiki zake walituambia kwamba alikuwa akimwona Kajal kwa takriban miezi miwili."

Wanakijiji wanasema kwa kawaida hutatua migogoro kwa msaada kutoka kwa viongozi wa baraza la kijiji waliochaguliwa. "Kama familia [ya Kajal] ingechukua hatua kwa busara zaidi, wazee katika kijiji wangeweza kusaidia kuisuluhisha," anasema mwanakijiji Mahipal Saini.

Polisi wanasema wamewatuma wafanyakazi ili kuhakikisha hakuna vurugu za kidini. Na wanakijiji wanasema maisha yao yanarudi polepole katika utaratibu.

Mauaji hayo, wengine wanasema, yamelazimisha tafakari isiyoeleweka.

"Hatukuwahi kufikiria kitu kama hiki kinaweza kutokea hapa," anasema Arif Ali, mkazi mwingine wa Umri. "Sio kwamba wanaume na wanawake katika kijiji hicho wameanza ghafla kuhisi hawana usalama. Lakini kuna ukimya unaotuzunguka."

Mauaji ya Umri ni tukio kwenye orodha ndefu ya visa vinavyoshukiwa vya "mauaji yanayochochewa na tofauti ya dini" vilivyoripotiwa kote India kwa miongo kadhaa.

Zaidi ya 93% ya ndoa nchini India "zinapangwa" na familia ndani ya tabaka na imani zao na wanandoa wanaopotoka kutoka kwa mila hiyo hulazimishwa kutafuta ulinzi kutoka kwa polisi au mahakama.

Sheria ya India inaona haya kama mauaji na mahakama zimethibitisha mara kwa mara kwamba chaguo la mtu mzima la mwenzi kwa ridhaa linalindwa kikatiba.

Mnamo 2018, mahakama kuu ya nchi hiyo iliamuru serikali za majimbo kuanzisha nyumba salama katika kila wilaya ili kuwalinda wanandoa wa imani tofauti na wa tabaka tofauti kutokana na unyanyasaji.

Hata hivyo, visa vya vurugu vinaendelea kuripotiwa kutoka majimbo yote.

Utafiti unaonyesha Wahindi wengi wanapinga ndoa za imani tofauti, na sheria zenye utata dhidi ya ubadilishaji dini zinazotekelezwa katika majimbo kadhaa mara nyingi huwaweka wanandoa kama hao katika hali ngumu.

Mtengenezaji wa filamu Nakul Singh Sawhney, ambaye alitengeneza makala kuhusu mada hiyo mwaka wa 2012, anasema data rasmi kuhusu mauaji ya misinigi ya dini haitoshi.

"Kesi nyingi hazifikii kwenye data rasmi isipokuwa nia imetajwa wazi katika hatua ya kwanza ya ripoti za polisi. Na katika visa vingi mtazamo wa mauaji hayo hujitokeza baadaye sana wakati wa uchunguzi," anasema Sawhney.

Mwanaharakati wa haki za binadamu Kavita Srivastava anasema kutotambua ukubwa wa kile kinachoitwa uhalifu huo huchangia kutojali kwa serikali. "Tatizo lisipoonekana, halifanyiwi kazi," anasema.

Wanawake wanapozidi kudai haki yao ya kuchagua wapenzi wao, Srivastava anaongeza, mara nyingi hukabiliwa na upinzani kutoka kwa kile anachokielezea kama "mfumo wa kijamii unaorudi nyuma sana".

Amri za mahakama, anasema, pekee haziwezi kuzuia "uhalifu" isipokuwa mitazamo mipana ya kijamii ikikabiliwa.