Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Meli za kubeba ndege za kivita za Marekani zaonekana zikielekea Mashariki ya kati

Tunatumia zana zinazopatikana kufuatilia safari za ndege kama Flightradar24 ili kuangalia mienendo ya hivi punde ya ndege za kijeshi za Marekani huku Washington ikiendelea kuimarisha vikosi vyake katika Mashariki ya Kati.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma & Abdalla Seif Dzungu

  1. Wanasheria walaani hukumu 'hafifu' dhidi ya wanajeshi wa Cameroon waliowaua raia 21

    Wanajeshi watatu wa Cameroon wamehukumiwa kifungo jela kwa kuhusika katika mauaji ya takriban raia 21 katika eneo lenye matatizo la lugha ya Kiingereza nchini humo.

    Vifungo vya jela kwa uhalifu huo, ambao ulifanyika miaka sita iliyopita katika eneo la Kaskazini Magharibi, ni kati ya miaka mitano hadi 10 kwa kila mtu.

    Mahakama ya kijeshi hapo awali iliwapata wanajeshi hao na hatia ya mauaji, uchomaji moto na uharibifu - jambo ambalo ni nadra sana katika nchi ambapo wanajeshi ni nadra kuhukumiwa kwa uhalifu dhidi ya raia.

    Hata hivyo, mawakili wa waathiriwa waliambia BBC kuwa wamesikitishwa na urefu wa vifungo vya jela vilivyotolewa siku ya Alhamisi, na kuwaita "isiyo na maana".

  2. Meli ya kivita ya USS Gerald R Ford imeonekana ikipitia Mlango-Bahari wa Gibraltar

    BBC Verify imethibitisha picha zilizopigwa leo asubuhi na kuchapishwa kwenye X zinazoonyesha shehena ya ndege ya Marekani USS Gerald R Ford ikipitia Mlango-Bahari wa Gibraltar.

    Picha hizo - zilizochukuliwa kutoka Gibraltar - zinaonyesha meli kubwa zaidi ya kivita duniani ikiwa inaelekea mashariki kutoka Atlantiki hadi Mediterania.

    Pia tumethibitisha kwa kutumia ufuatiliaji wa meli kwamba moja ya meli katika kundi la meli za kubeba ndege za kivita za Ford, USS Mahan, ilipitia njia hiyo.

    Katika picha hii ya kwanza meli ya kubeba ndege za kivita inaonekana kwa mbali ikipita karibu na milima ya.

    Tulitumia ufuatiliaji wa meli ili kuthibitisha meli nyingine mbili kwenye picha pia zilikuwa katika eneo hilo wakati huo.

  3. Urusi na Iran katika mazungumzo kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran

    Wizara ya Mambo ya Nje ya Russia ilitangaza Ijumaa (tarehe 20 Februari) kupitia chaneli yake ya Telegram kwamba Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi Sergei Lavrov amezungumza na mwenzake wa Iran, Abbas Araghchi kuhusu mpango wa nyuklia wa nchi hiyo.

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi alisema jana kuwa shambulio la Marekani dhidi ya Iran litakuwa na madhara makubwa.

    Pia alisema: "Ninafuatilia kwa karibu hisia za nchi za Ghuba ya Kiarabu katika eneo hilo.

    Hakuna anayetaka kuzidisha mvutano. Kila mtu anajua kwamba hii ni kucheza na moto."

    Kwa mujibu wa Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi, kushadidi mivutano hiyo kunabatilisha hatua chanya zilizopigwa katika miaka ya hivi karibuni, ikiwa ni pamoja na kuboresha uhusiano wa Iran na nchi jirani hususan Saudi Arabia.

  4. Waziri wa Mafuta wa Iran: Ushirikiano wa mafuta na gesi na Marekani unawezekana

    Waziri wa Mafuta wa Iran amesema "kila kitu kinawezekana" kuhusiana na uwezekano wa ushirikiano kati ya Tehran na Washington katika nyanja za mafuta na gesi.

    Katika mahojiano na Shirika la Habari la ILNA, Mohsen Paknejad hatahivyo hakutaja muda wa kuanza kwa ushirikiano huo.

    Hamid Ghanbari, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran katika masuala ya kiuchumi pia siku chache zilizopita alisema: "Maslahi ya pamoja katika nyanja za mafuta na gesi, nyanja za pamoja, uwekezaji wa madini na hata ununuzi wa ndege yamejumuishwa katika mazungumzo na Marekani."

    Pia alisema kuwa Marekani haikunufaika kiuchumi katika makubaliano ya awali ya nyuklia, lakini "wakati huu, ili makubaliano hayo yawe endelevu, ni muhimu Marekani pia iweze kunufaika katika maeneo yenye faida kubwa na za haraka kiuchumi."

  5. Mbunge wa Tunisia afungwa miezi minane jela kwa kumdhihaki rais

    Mahakama ya Tunisia imemhukumu mbunge mmoja kifungo cha miezi minane jela kutokana na kuchapisha mitandao ya kijamii akimkejeli Rais Kais Saied kufuatia mafuriko yaliyosababisha vifo vya hivi karibuni.

    Ahmed Saidani alikamatwa mapema mwezi huu baada ya kuchapisha kwenye mitandao ya kijamii kuhusu ziara za Saied katika maeneo yaliyokumbwa na mafuriko, akimtaja kuwa "kamanda mkuu wa usafi wa mazingira na mifereji ya maji ya mvua".

    Alifungwa gerezani siku ya Alhamisi kwa mashtaka ya kuwatusi wengine kupitia mitandao ya mawasiliano, afisa wa mahakama alisema.

    Wakili wa Saidani, Houssem Eddine Ben Attia, aliliambia shirika la habari la AFP kwamba mteja wake anafunguliwa mashitaka chini ya sheria ya mawasiliano dhidi ya "kuwadhuru wengine kupitia mitandao ya kijamii", kosa ambalo linaweza kuadhibiwa hadi miaka miwili jela.

    Mashirika ya kutetea haki za binadamu yamekosoa kile wanachoeleza kuwa ni kukithiri kwa ukandamizaji wa Saied dhidi ya wapinzani tangu aliposimamisha bunge la Tunisia mwaka 2021 na kuanza kutawala kwa amri.

    Saidani, ambaye aliwahi kuwa mfuasi wa uimarishaji wa mamlaka ya Saied na kukamatwa kwa viongozi wa upinzani, hivi karibuni amegeuka kuwa mkosoaji mkubwa wa rais.

    Katika chapisho lake la Facebook, mbunge huyo alimkejeli rais kwa "kuchukua hobby ya kupiga picha na maskini " wakati akizuru maeneo yaliyofurika katika mji mkuu, Tunis na maeneo mengine ya nchi.

  6. Ndege zaidi za Kijeshi za Marekani zaonekana zikielekea mashariki ya kati

    Tunatumia zana zinazopatikana hadharani za kufuatilia safari za ndege kama Flightradar24 ili kuangalia mienendo ya hivi punde ya ndege za kijeshi za Marekani huku Washington ikiendelea kuimarisha vikosi vyake katika Mashariki ya Kati.

    Rais Donald Trump ameitaka Iran kuafikiana kuhusu mpango wake wa nyuklia na kuonya kwamba vinginevyo "mambo mabaya yatatokea".

    Hii ni picha ya skrini kutoka Flightradar24 inayoonyesha ndege sita za kijeshi za Marekani zikiingia na kutoka Mashariki ya Kati mwendo wa saa 10:00 GMT siku ya Ijumaa.

    Pamoja na safari za ndege za jeshi la anga pia nimeona ndege mbili za upelelezi za Jeshi la Wanamaji la Marekani P-8 Poseidon juu ya Mediterania - moja ikielekea magharibi kuelekea Gibraltar na nyingine nje ya pwani ya Crete.

    Tumekuwa tukifuatilia hatua za kijeshi za Marekani katika eneo hilo kwa siku kadhaa sasa na tutatumia tulichonacho kujua kuhusu ukubwa wa jeshi la Marekani katika eneo hio.Marekani inaweza kuisaidia Iran? Wairan wenyewe wanasemaje?

  7. Mpandaji milima Austria apatikana na hatia baada ya mpenzi wake kuganda hadi kufa kwenye mlima

    Mpanda mlima mmoja kutoka Austria amepatikana na hatia ya mauaji ya uzembe baada ya mpenzi wake kuganda hadi kufa kwenye mlima mrefu zaidi nchini Austria mwaka jana.

    Mwanamume huyo, aliyetajwa kwa jina la Thomas P pekee kwa mujibu wa sheria za faragha za Austria, amepewa kifungo cha miezi mitano ya adhabu ya mahakama ambayo haitumiki isipokuwa uhalifu mwingine umefanywa ndani ya kipindi maalum na kutozwa faini ya €9,600 (£8,400).

    Mpenzi wake, Kerstin G, alifariki kutokana na hypothermia (dharura ya matibabu inayotokea wakati mwili unapoteza joto kwa kasi zaidi kuliko inavyoweza kuzalisha), wakati wa safari ya kupanda mlima Grossglockner mnamo mwezi Januari mwaka 2025.

    Katika taarifa iliyotumwa kwa BBC, mahakama ilisema inachukulia rekodi safi ya awali ya Thomas P na kupotea kwa mtu wa karibu naye "kuwa sababu za kupunguza ukali wa kesi" hiyo.

    Ilisema pia ilizingatia "mjadala wa umma kwenye mitandao ya kijamii, ambao ulikuwa unamtia hatiani mshtakiwa".

    Jaji, Norbert Hofer, ambaye mwenyewe ni mpandaji milima mwenye uzoefu ambaye anafanya kazi na timu za uokoaji milimani na helikopta huko Tyrol, alisema Thomas P alikuwa Mpanda milima mzuri, lakini mpenzi wake hakuwa na uzoefu kama wake.

    Alisema wanandoa hao walipaswa kurudi nyuma kwani Kerstin G hakuwa na uzoefu wa kutosha katika hali ya baridi kali.

    Mahakama pia ilisikiliza kutoka kwa Andrea B, mpenzi wa zamani wa Thomas P, ambaye alielezea jinsi alivyomwacha peke yake katika ziara ya awali huko Grossglockner mnamo mwaka 2023.

    Alisema alikuwa amefika mwisho akihisi kizunguzungu na taa yake ya mbele ilikuwa imezimwa.

    Alisema alikuwa akilia na kupiga kelele ghafla alipotoweka, akitembea mbele na kumwacha nyuma.

  8. Hamas yapiga kura kumchagua kiongozi mpya wa mpito, chanzo cha habari kimeiambia BBC

    Hamas inafanya uchaguzi wa kiongozi mpya wa mpito, afisa mwandamizi wa Palestina anayefahamu masuala ya kundi hilo la waasi ameiambia BBC.

    Upigaji kura unafanyika kote Gaza, Ukingo wa Magharibi unaokaliwa na miongoni mwa wanachama wa Hamas kwingineko.

    Matokeo yanaweza kuashiria mwelekeo ambao kundi hilo inakusudia kuchukua - hasa wakati Marekani na wapatanishi wengine wanapojadili utawala wa Gaza baada ya vita, juhudi za ujenzi upya na hali ya baadaye ya vikundi vyenye silaha huko.

    Uchaguzi huo unakuja baada ya viongozi wengi wakuu wa Hamas kuuawa katika mashambulizi ya Israel kufuatia mashambulizi ya kundi hilo ya tarehe 7 Oktoba 2023 dhidi ya Israeli, ambapo takriban watu 1,200 waliuawa na wengine 251 walichukuliwa mateka.

    Watu huko Gaza tayari wamepiga kura zao kwa siri, kulingana na chanzo hicho, lakini haijulikani wazi kama mchakato huo umekamilika kwingineko.

    Kiongozi mpya atakapotangazwa, atashikilia wadhifa huo kwa mwaka mmoja.

    Hamas inatawala Ukanda wa Gaza na katika miaka ya hivi karibuni imekuwa na uungwaji mkono unaoongezeka katika eneo la Ukingo wa Magharibi, ingawa shughuli zake huko zimezuiliwa sana na jeshi la Israeli na vikosi vya usalama vya Mamlaka ya Palestina.

    Mkataba wa kusitisha mapigano unaoungwa mkono na Marekani huko Gaza ulianza kutekelezwa mnamo mwezi Oktoba, na mazungumzo yanaendelea kuhusu awamu za baadaye za makubaliano hayo.

    Soma zaidi:

  9. Chanjo moja inaweza kukulinda dhidi ya kikohozi, mafua na homa, watafiti wanasema

    Chanjo moja ya kupulizia puani inaweza kukulinda dhidi ya kikohozi, mafua, kamasi na aina yote ya homa, pamoja na maambukizi ya bakteria kwenye mapafu, na pia inaweza kupunguza mzio, wamesema watafiti wa Marekani.

    Timu katika Chuo Kikuu cha Stanford imefanya majaribio ya "chanjo yao ulimwengu wote" kwa wanyama na bado inahitaji kufanya majaribio kwa binadamu.

    Mtazamo wao unaashiria "mabadiliko makubwa" ikilinganishwa na jinsi chanjo zilivyobuniwa kwa zaidi ya miaka 200, wanasema.

    Wataalamu katika tasnia hiyo walisema utafiti huo ulikuwa "wa kusisimua sana" licha ya kuwa katika hatua za awali na unaweza kuwa "hatua muhimu kufikiwa".

    Chanjo za sasa hufunza mwili kupambana na maambukizi aina moja. Chanjo ya surua hulinda dhidi ya surua pekee na chanjo ya tetekuwanga hulinda dhidi ya tetekuwanga pekee.

    Hivi ndivyo chanjo imekuwa ikifanyakazi tangu Edward Jenner alipoanzisha chanjo mwishoni mwa karne ya 18.

    Mbinu iliyoelezwa katika jarida la Sayansi haifunzi mfumo wa kinga. Badala yake inaiga jinsi seli za kinga zinavyowasiliana.

    Inatolewa kama dawa ya puani na huacha seli nyeupe za damu kwenye mapafu yetu - zinazoitwa macrophages - zikiwa katika "tahadhari " na zikiwa tayari kuanza kufanya kazi bila kujali ni maambukizi gani yanayojaribu kuingia.

    Matokeo hayo yalidumu kwa takriban miezi mitatu katika majaribio ya wanyama.

    Watafiti walionyesha kuwa hali hii ya utayari iliyoongezeka ilisababisha kupungua mara 100 hadi 1,000 kwa virusi vinavyoingia kwenye mapafu na kuingia mwilini.

    Na kwa wale walioingia kisiri, mfumo uliobaki wa kinga ulikuwa "tayari kuwakinga hawa wa ndani kwa kasi kikubwa" alisema Profesa Bali Pulendran, profesa wa mikrobiolojia na kinga mwilini huko Stanford.

    Timu hiyo ilionyesha kuwa chanjo hiyo pia inalinda dhidi ya aina mbili za bakteria - Staphylococcus aureus na Acinetobacter baumannii.

    Pulendran aliiambia BBC: "Chanjo hii, tunayoiita chanjo ya ulimwengu wote, inatoa mwitikio mpana zaidi ambao ni kinga sio tu kwa virusi vya mafua, sio virusi vya Covid tu, sio virusi vya homa ya kawaida tu, bali dhidi ya karibu virusi vyote, na bakteria wengi tofauti kama tulivyofanya majaribio, na hata vizio."

    "Kanuni ambayo chanjo hii inafanya kazi ni mabadiliko makubwa na kanuni ambayo chanjo zote zimefanya kazi hadi sasa."

    Jinsi inavyoelekeza mfumo wa kinga kupambana na maambukizi pia ilionekana kupunguza mwitikio wa vizio vya wadudu wa vumbi la nyumba - ambavyo ni kichocheo cha pumu ya mzio.

    "Huu ni utafiti wa kusisimua sana," anasema Profesa Daniela Ferreira, profesa wa chanjo katika Chuo Kikuu cha Oxford, ambaye hakuhusika katika utafiti huo.

    Alisema inaweza "kubadilisha jinsi tunavyowalinda watu kutokana na kikohozi cha kawaida, mafua na maambukizo mengine ya kupumua" ikiwa matokeo yatathibitishwa katika tafiti za wanadamu.

    "Mojawapo ya yenye tija" katika utafiti huo ilikuwa maelezo wazi ya jinsi aina hii mpya ya chanjo inavyofanya kazi, aliongeza.

    Ferreira alisema utafiti huo "unaweza kuashiria kupigwa kwa hatua kubwa" ikitoa ulinzi dhidi ya maambukizi ambayo "yamekuwa tatizo kubwa" kwetu sote.

    Soma zaidi:

  10. Uingereza haijatoa ruhusa kwa Marekani kutumia kambi zake za kijeshi kushambulia Iran

    Serikali ya Uingereza haijatoa ruhusa kwa Marekani kutumia kambi za kijeshi za Uingereza kama sehemu ya kuunga mkono mashambulizi yanayoweza kutokea ya Marekani dhidi ya Iran, BBC inafahamu hilo.

    Siku za nyuma, Marekani ilitumia kambi ya RAF Fairford, huko Gloucestershire, na eneo la nje ya Uingereza la Diego Garcia, katika Bahari ya Hindi, kutekeleza mashambulizi katika eneo la Mashariki ya Kati.

    Gazeti la Times linaripoti kwamba ukosoaji wa hivi karibuni wa Rais wa Marekani Donald Trump kuhusu makubaliano ya Sir Keir Starmer ya kukabidhi Visiwa vya Chagos kwa Mauritius na kukodisha tena kambi ya pamoja ya kijeshi kati ya Uingereza na Marekani kulisababishwa na Uingereza kutotoa ruhusa ya kutumia kambi hizo.

    Msemaji wa serikali ya Uingereza alisema: "Kama kawaida, hatutoi maoni yoyote kuhusu masuala ya uendeshaji."

    Marekani imekuwa ikiishinikiza Iran kukubali kupunguza mpango wake wa nyuklia.

    Imetishia kufanya mashambulizi iwapo itashindwa kufanya hivyo na imepeleka meli, ndege za kivita na zana zingine za kijeshi eneo hilo kwa ajili ya maandalizi ya mashambulizi yanayoweza kufanyika.

    Wakati huo huo, hatua imeripotiwa kupigwa katika mazungumzo kati ya wapatanishi wa Marekani na Iran nchini Uswisi.

    Siku ya Alhamisi, Trump alisema dunia itajua "ndani ya siku 10 zijazo" ikiwa Marekani itafikia makubaliano na Iran au kuchukua hatua za kijeshi.

    Msemaji wa serikali ya Uingereza alisema: "Kuna mchakato wa kisiasa unaoendelea kati ya Marekani na Iran, ambao Uingereza inaunga mkono."

    "Iran haipaswi kamwe kutengeneza silaha za nyuklia, na kipaumbele chetu ni usalama katika eneo hilo."

    Sir Keir alizungumza na Trump kwa simu siku ya Jumanne, baada ya serikali ya Marekani kuunga mkono rasmi makubaliano ya Chagos.

    Soma zaidi:

  11. Interpol yafanya msako mkali dhidi ya ulaghai Afrika

    Shirika la polisi wa kimataifa Interpol limesema vyombo vya kutekeleza sheria kutoka nchi 16 za Afrika vimefanikiwa kupata zaidi ya dola milioni 4.3 na kukamata watu 651, katika msako mkali dhidi ya ulaghai wa kimataifa wa mtandaoni.

    Katika taarifa iliyotolewa Jumatano, Interpol ilisema hatua hiyo iliyopewa jina la Operesheni Red Card 2.0 ilichukua muda wa wiki nane, kuanzia tarehe 8 Desemba 2025 hadi Januari 30 mwaka huo.

    Baadhi ya nchi zilizoshiriki katika operesheni hiyo ni pamoja na Angola, Cameroon, Côte d'Ivoire, Kenya, Nigeria na Zimbabwe.

    Ikizungumzia kesi maalum, taarifa ya shirika hilo ilionyesha kuwa polisi wa Nigeria walizuia njama za mtandao wa wahalifu za kuwalaghai watu kupitia miradi ya uwekezaji yenye mavuno mengi.

    Walifuta zaidi ya akaunti 1000 za ulaghai wa mitandao ya kijamii na kugundua jengo linalotumika kama msingi wa uhalifu huo.

    Wakati huo huo, maafisa wa utekelezaji wa sheria wa Kenya na Ivory Coast walikamata mamia ya watu waliohusishwa na uwekezaji na miradi ya mikopo ya simu, wakikamata vifaa kadhaa vilivyotumika katika shughuli hizo haramu.

    "Makundi haya ya uhalifu wa mtandao yanaleta madhara makubwa ya kifedha na kisaikolojia kwa watu binafsi, biashara na jumuiya nzima kwa ahadi zao za uongo," alisema Neal Jetton, Mkurugenzi wa Uhalifu wa shirika la Interpol.

    Interpol ilisema ilichangia kwa kushirikisha wengine taarifa muhimu za kijasusi pamoja na ubadilishanaji habari kwa wakati halisi na mafunzo juu ya matumizi ya zana za uchunguzi wa kidijitali.

    Kwa ujumla, operesheni hiyo ilifichua ulaghai unaohusishwa na hasara ya zaidi ya dola milioni 45 na kubaini zaidi ya waathiriwa 1000, wengi wao kutoka Afrika.

    Soma zaidi:

  12. Andrew aachiliwa huru baada ya kukamatwa kwa kwenda kinyume na maadili ya uongozi

    Andrew Mountbatten-Windsor ameachiliwa huru huku uchunguzi ukiendelea kufuatia kukamatwa kwake kwa tuhuma za utovu wa nidhamu katika ofisi ya umma.

    Mfalme Charles III alisema "sheria lazima ichukue mkondo wake" akijibu kukamatwa kwa Andrew na kwamba anaunga mkono polisi "na kutoa ushirikiano wake kamili na wa dhati".

    Polisi hapo awali walisema walikuwa wakifikiria kumchunguza Andrew kuhusu madai yanayohusiana na uhusiano wake na marehemu Jeffrey Epstein, mhalifu wa kingono na walikuwa wakipitia madai kwamba wawili hao walishirikishana nyenzo za siri.

    Mawasiliano kati ya wawili hao yalionekana miongoni mwa sehemu ya faili zilizotolewa na serikali ya Marekani.

    Katika taarifa iliyosasishwa Alhamisi jioni, Polisi wa Thames Valley walithibitisha kwamba Andrew "ameachiliwa huru huku uchunguzi" ukiendelea. Iliongeza kuwa msako uliokuwa unafanyika huko Norfolk sasa umekamilika.

    Mwanamfalme huyo wa zamani alipigwa picha akiwa amelala nyuma kwenye kiti cha nyuma cha gari baada ya kutoka kituo cha polisi cha Aylsham.

    Pia unaweza kusoma:

  13. Mwanawe Robert Mugabe akamatwa Afrika Kusini kwa tuhuma za kujaribu kuua

    Polisi nchini Afrika Kusini wamemkamata mtoto wa mwisho wa Rais wa zamani wa Zimbabwe, Robert Mugabe, ambaye anakabiliwa na shtaka la kujaribu kuua baada ya kuripotiwa tukio la ufyatuaji risasi katika nyumba moja kwenye kitongoji cha kifahari cha Johannesburg.

    Bellarmine Mugabe, mwenye umri wa miaka 28, alikamatwa baada ya mwanaume mwenye umri wa miaka 23, anayeaminika kuwa mtunza bustani, kupigwa risasi na kujeruhiwa.

    Maafisa waliokuwa wakisaka nyumba iliyoko Hyde Park, ambapo Mugabe alikuwa akiishi, wamepata risasi lakini hakuna bunduki, polisi wamesema.

    Bellarmine Mugabe ni mtoto wa mwisho wa Robert na mkewe wa pili Grace Mugabe. Robert Mugabe, ambaye alifariki mwaka wa 2019, aliiongoza Zimbabwe kwa miaka 37 kabla ya kufurushwa madarakani akiwa na umri wa miaka 93 mwaka wa 2017.

    Mwanamume mwingine amekamatwa pamoja na Bellarmine Mugabe huku wachunguzi wakiendelea na kazi yao, msemaji wa polisi Kanali Dimakatso Nevhuhulwi alisema.

    Wawili hao wanatarajiwa kufikishwa mahakamani "hivi karibuni", kulingana na taarifa ya polisi.

    Polisi bado hawajamtaja rasmi Bellarmine Mugabe kama mmoja wa waliokamatwa, lakini waandishi wa habari waliokuwepo eneo la tukio walimwona akiwa amefungwa pingu na ametajwa sana na vyombo vya habari vya ndani.

    Mwathiriwa yuko hospitalini akiwa katika hali mbaya baada ya kupigwa risasi mara moja, msemaji huyo aliongeza.

    Katika taarifa iliyotolewa nje ya nyumba hiyo, Nevhuhulwi alisema washukiwa hao wawili "hawajatuambia bunduki hiyo iko wapi, na hawasemi chochote kuhusu bunduki hiyo".

    Pia unaweza kusoma:

  14. Dunia ina siku 10 kuona ikiwa Iran inafikia makubaliano au 'kitu kibaya kitokee' - Trump

    Rais Donald Trump amesema dunia itajua "ndani ya siku 10 zijazo" kama Marekani itafikia makubaliano na Iran au kuchukua hatua za kijeshi.

    Katika mkutano wa uzinduzi wa Bodi yake ya Amani huko Washington DC, Trump alisema kuhusu mazungumzo na Jamhuri ya Kiislamu juu ya mpango wake wa nyuklia: "Lazima tufikie makubaliano yenye tija vinginevyo mambo mabaya yatatokea."

    Katika siku za hivi karibuni, Marekani imeongeza vikosi vya kijeshi Mashariki ya Kati, huku hatua ikisemekana kupigwa katika mazungumzo kati ya wapatanishi wa Marekani na Iran nchini Uswisi.

    Wabunge wa chama cha Democrat, na baadhi ya Warepublican, wamepinga hatua yoyote ya kijeshi kuchukuliwa nchini Iran bila idhini ya bunge.

    Katika maelezo yake, Trump alibainisha kuwa Wajumbe Maalum Steve Witkoff na Jared Kushner, ambaye pia ni mkwe wa Trump, walikuwa na "mikutano yenye tija sana" na Iran.

    "Imedhihirika, kwa miaka mingi kuwa si rahisi kufanya makubaliano yenye maana na Iran," alisema. "Vinginevyo, mambo mabaya yatatokea."

    Siku moja kabla, Waziri wa habari wa Ikulu ya White House Karoline Leavitt alionya kwamba Iran itafanya la "busara sana" kufikia makubaliano na Marekani, akiongeza kwamba Trump bado alikuwa na matumaini ya suluhisho la kidiplomasia kuhusu mpango wa nyuklia wa Tehran.

    Makombora na ndege za ivita za Marekani zilishambulia vituo vitatu vya nyuklia vya Iran mnamo mwezi Juni mwaka jana, na Ikulu ya White House iliripotiwa kujadili chaguzi mpya za mashambulizi wiki hii.

    Vikosi vya Marekani vimekuwa vikiongeza uwepo wao katika eneo hilo katika wiki za hivi karibuni, ikiwa ni pamoja na kupelekwa kwa meli ya kivita ya USS Abraham Lincoln.

    Picha za setilaiti pia zimeonyesha Iran ikiimarisha vifaa vya kijeshi, na Kiongozi Mkuu wa nchi hiyo, Ayatollah Ali Khamanei, amechapisha ujumbe kwenye mitandao ya kijamii akitishia vikosi vya Marekani.

    "Rais wa Marekani husema kila mara kwamba Marekani imetuma meli ya kivita kuelekea Iran. Bila shaka, meli ya kivita ni kifaa hatari cha kijeshi," moja ya ujumbe wa Khamenei ulisema.

    Wabunge kadhaa wa Bunge la Marekani wameonyesha kupinga hatua yoyote ya kijeshi dhidi ya Iran.

    Soma zaidi:

  15. Hujambo na karibu katika matangazo yetu mubashara. Tarehe ni 20/02/2026.